Saturday, July 11, 2015

HADITHI SEHEMU (5)


 
NILIJUA NIMEUA 5
 
 
ILIPOISHIA JANA
 
“Ni elfu sita”
 
“Punguza, fanya tano. Mimi ni mteja wako wa kila siku”
 
“Haya nipe”
 
Mariam akafungua pochi na kutoa noti ya shilingi elfu tano akanipa. Akafungua mlango wa teksi na kushuka.
 
Aliagana na mwenzake na kwenda kubisha mlango wa nyumbani kwao. Nami nikaanza safari ya kuelekea Kange.
 
Nilipofika Kange Nilimuuliza msichana anakwenda mtaa gani, akaniambia nikate kushoto. Nilipokata kushoto akanielekeza mtaa ambao anaoishi.
 
Nilipofika katika mtaa huo alinionyesha nyumba aliyotaka nimpeleke. Ilikuwa nyumba nzuri kuliko aliyokuwa anaishi Mariam.
 
“Unanidai kiasi gani?” Msichana akaniuliza niliposimamisha teksi.
 
“Nipe elfu kumi”
 
SASA ENDELEA
 
Msichana hakubishana. Alifungua pochi yake akatoa noti ya shilingi elfu kumi na kunipa. Akafungua mlango na kushuka.
 
Alikwenda kwenye baraza ya ile nyumba na kupiga simu.
 
Nilimsikia akisema.
 
“Asiya nifungulie mlango”
 
Nikaiondoa teksi na kumuacha hapo hapo.
 
Wakati narudi jijini nilikuta gari limeegeshwa kando ya barabara. Taa zake za nyuma zilikuwa zinawaka. Wakati nalikaribia gari hilo niliona mtu aliyekuwa kando yake akinipungia mkono kunisimamisha.
 
Wazo nililolipata kwanza ni kuwa gari hilo lilikuwa limeharibika na kwamba mtu aliyekuwa akinipungia mkono ama alikuwa anataka msaada au alikuwa anahitaji huduma ya teksi yangu.
 
Kwa vile nilikuwa kwenye mwendo wa kasi nililipita gari hilo na kwenda kusimama mbele. Hapo hapo mawazo yangu yakabadilika. Niliwaza kwamba huenda gari hilo liliegeshwa kwa hila lionekane limeharibika kumbe ni majambazi wanaosubiri magari yasimame waanze kupora watu.
 
Nilikuwa nimechelewa kufikiria hilo. Nilikuwa nimeshasimamisha teksi na jamaa aliyenisimamisha alikuwa ameshafika kwenye dirisha la teksi yangu!
 
Chini ya siti yangu ya dereva, siku zote huweka parange (sime ya kimasai) kwa ajili ya kujihami endapo kutatokea tatizo la kuvamiwa na mtu au watu wenye nia mbaya.
 
Kwa vile sikuwa na uhakika kuwa mtu huyo aliyenisimamisha alikuwa na nia mbaya au nzuri, tayari nilishapeleke mkono wangu wa kulia kuushika mpini wa parange iliyokuawa chini ya siti niliyokalia.
 
Nilikuwa nimejiweka tayari, kama atakuwa na nia mbaya niweze kukabiliana naye.
 
“Samahani bwana” Mtu huyo akaniambia. Ingawa sauti yake ilikuwa tulivu nay a kibinaadamu, ilikuwa imeficha taharuki.
 
“Unasemaje?” nikamuuliza nikiwa nimemkazia macho kusoma mawazo yake.
 
“Mimi ni daktari wa hospitali ya Bombo. Nimepigiwa simu kuitwa   hospitali, kuna mama mjamzito anahitaji kufanyiwa operesheni ya dharura sasa hivi. Kwa bahati mbaya gari langu limeharibika njiani. Naomba unipeke Bombo haraka” akaniambia.
 
“Kusema kweli nilimuelewa. Nikamuuliza.
 
“Na hilo gari lako je?”
 
“Ningeomba kama itawezekana unisaidie kulivuta niliondoe mahali hapa”
 
“Hiyo itakuwa ni kazi nyingine” nikamwambia.
 
“Naomba msaad wako kaka, sina jinsi na siwezi kuliacha hapa”
 
“Unataka nilivute hadi wapi?”
 
“Hadi Bombo. Nitaliegesha sehemu. Kutakapokucha nitajua la kufanya”
 
“Utanilipa kiasi gain?”
 
“Sema wewe”
 
“Kulivuta hilo gari lako pamoja na kukufikisha wewe Bombo utanilipa elfu ishirini”
 
“Sawa. Nitakulipa”
 
Alipokubali kima changu nilifungua mwa gari nikashuka.
 
“Una kamba?” nikamuuliza.
 
“Kamba sina’
 
Nilikuwa na kamba ya akiba kwenye boneti la teksi yangu. Nilikwenda nyuma ya gari, nikafungua boneti na kutoa kamba. Nikaiweka chini.
 
Kisha niliisogeza teksi mbele ya gari la mtu huyo lililokuwa pembeni. Nikashuka tena na kufunga ncha moja ya kamba nyuma ya gari langu na ncha nyingine nikaifunga mbele ya lile gari. Nilipomaliza nilimwambia mtu huyo ajipakie kwenye gari lake.
 
Wakati anajipakia na mimi nilikwenda kwenye mlango wa teksi nikaufungua na kujipakia. Nilitia gea na kuiondo teksi taratibu. Kamba ilinyooka na kukaza kabla ya kuanza kulivuta gari la nyuma.
 
Niliingia barabarani nikawa naendesha taratibu. Kwa vile niliendesha kwa mwendo mdogo tulifika Bombo saa kumi na mbili asubuhi.
 
Nilishuka kwenye teksi nikaifungua ile kamba na kuiweka kwenye boneti.
 
ITAENDELEA KESHO , usikode uhondo huu hapo kesho

No comments:

Post a Comment