Sunday, July 17, 2016

HADITHI MWANAMKE SEHEMU YA 44

SIMULIZA ZA FAKI A FAKI 0655 340572
 
MWANAMKE 44
 
ILIPOISHIA
 
Kwa sababu ya njaa niliyokuwa nayo nilikula sana mpaka nikahisi kwammba ningevimbiwa. Pilau ilikuwa nyingi hatukuimaliza.
 
Nilimuacha Mapama akiendelea kula.
 
“Ukiwa katika hali ya baridi unatakiwa ule sana” Mapama aliniambia.
 
Tonge zake zilikuwa kubwa na nilihisi alikuwa akimeza bila kutafuna.
 
Alipotosheka na yeye aliiacha. Akairudisha sinia kwenye kabati.
Baada ya kuosha mikono Mapama alinipa maji ya kunywa nikayanywa. Na yeye akanywa.
 
“Sasa baridi hatutaisikia. Tunaweza kuendelea na safari” Mapama akaniambia.
 
Tukakaa na kuendelea kuzungumza. Mara moja moja alikuwa akitazama mitambo. Nilikuwa nimejifunza kwamba boti haikuwa ikiendeshwa kama gari.
 
Haihitaji kushikiliwa sukani wakati wa kuendesha. Unaweza kuweka muelekeo wako na ukaiacha iende yenyewe.
 
Ndivyo Mapama alivyokuwa akifanya. Hatimaye Mapama alianza kusinzia. Alikuwa akisinzia huku akishituka.
 
“Nikuache uangalie, mimi najinyoosha kidogo” akaniambia.
 
Nikajua kuwa pilau aliyokuwa ameila kwa wingi ilikuwa imemlewesha.
 
“Wewe lala, baadaye nitakuamsha” nikamwambia.
 
Mapama akajitupa chini. Baada ya muda kidogo nilimsikia akikoroma.
 
Huku boti ilikuwa ikiendelea na safari. Masaa yalipita. Saa yangu ilikuwa imesimama kutokana na kuingia maji ya chumvi, sikuweza kujua ilikuwa saa ngapi.
 
SASA ENDELEA
 
Mawazo yangu yalikuwa ni kurudi kwetu salama. Nilijiambia Zena alikuwa amenifikishia mkasa wa kutatanisha sana ambao sikutegemea kama ungenitokea.
 
Niliamini kuwa siku zangu za kufa bado zilikuwa mbali, vinginevyo ningelikwishakufa.
 
Kama nisingekufa kwenye ile ajali ya meli, ningekufa wakati Zena ananikokota baharini. Na kama nisingekufa baharini, ningekufa kwenye kile kisiwa chenye majoka na baridi.
 
Lakini bado, japo nilinusurika kote, wale washenzi wenye ile boti wangeniua kama walivyowaua wale polisi waliowatosa. Na kama hawakuniua ningeuliwa na lile joka lililowaua watu wote na kumbakisha Mapama na mimi. Mpaka muda ule nilishindwa kujua joka lile lilitoka wapi na pia nilishindwa kujua jinsi nilivyonusurika.
 
Kusema kweli niliona kunusurika kwangu kulikuwa kwa ajabu sana.
 
Wakati nikiwa kwenye mchanganyiko huo wa mawazo huku macho yangu yakitazama mbele tunakoelekea, niliona kitu kama kimulimuli kikielekea upande wetu. Nikashituka na kuangaza macho vizuri.
 
“Nini kile?” nikawa najiuliza kimoyo moyo.
 
Baadaye kidogo niligundua kuwa ilikuwa boti iliyokuwa na kimuli muli na ilikuwa na maandishi yaliyosomeka POLISI KENYA.
 
“Mama yangu we!”
 
Kwa haraka nikamuamsha Mapama.
 
“Hebu amka uone!”
 
“Nini?” Mapama aliniuliza akiwa bado amefumba macho.
 
“Polisi. Kuna boti ya polisi inatuufuata. Amka!” nikamwambia.
 
“Polisi?”
 
“Tunafuatwa na boti ya polisi!”
 
Mapama akainuka.
 
“Iko wapi?” akaniuliza.
 
“Inakuja, imewasha kimulimuli. Simama uione”
 
Mapama akainuka na kuitazama ile boti kwenye kioo. Nilidhani angeanza kubabaika kama nilivyokuwa nikibabaika mimi. Badala yake nilimuona akiizima boti na kujipekua mifukoni. Alitoa burungutu la pesa za Kenya akalishika mkononi.
 
“Usiogope” akaniambia na kuongeza.
 
“Watakwenda zao sasa hivi”
 
Ile boti ya polisi ikatufikia. Ikawa ubavu kwa ubavu na boti yetu. Mapama akalirusha lile burungutu la noti kwenye ile noti. Polisi mmoja akalidaka. Hapo hapo nilimsikia akisema.
 
“Safari njema”
 
Mapama akaiwasha boti. Tukaendelea na safari. Ile boti nayo ikaelekea upande mwingine.
 
“Wale wanataka pesa tu” Mapama akaniambia na kuongeza.
 
“Kila tunapokuja huku tajiri wetu anatupa pesa maalum kwa ajili ya kuwapa polisi wa Kenya wanaofanya doria baharini. Wao wenyewe wanajua, wakiiona hii boti wanafuata pesa tu. Hawakagui kitu”
 
“Mimi nilikuwa na wasiwasi sana. Nilijua tutaishia polisi”
 
“Hapana. Hizi ni kazi zetu za kila siku, lazima tujuane na polisi. Huwezi kuvuka kwenda Somalia bila kukupamba nao”
 
“Kile kimulimuli kilinitisha kweli”
 
“Ile ni mikwara tu ya kutaka pesa. Hebu iangalie kama utakiona tena kimulimuli”
 
Nikatazama upande ule ilikoelekea ile boti. Sikuona kimulimuli wala sikuiona boti yenyewe.
 
“Boti yenyewe haionekani tena”
 
“Ni kwa sababu wamekizima kimulimuli”
 
“Huko Somali itakuwaje sijui?”
 
“Hakuna tatizo. Huyo tunaempelekea huu mzigo ni mtu mzito sana. Serikali pia inamjua”
 
Baada ya hapo tukabaki kimya.
 
Hatimaye aflfajiri ilianza kuchomoza. Sikuona dalili yoyote ya kufika Somalia. Usingizi ukaanza kuniuma.
 
“Uliniambia tutaingia Somalia wakati wa alfajiri” nikamwambia Mapama.
 
“Bado kidogo, usiwe na wasiwasi”
 
“Nasikia usingizi” nikamwambia.
 
“Lala kidogo”
 
Nikajilaza pale chini. Usingizi ukanichukua hapo hapo.
 
Mpaka nakuja kuzinduka lilikuwa jua la utosi. Mapama ndiye aliyeniamsha. Boti ilikuwa imesimama na kulikuwa na boti nyingine kubwa iliyokuwa imesimama kando ya ile boti tuliyokuwamo. Ilikuwa boti kubwa na nzuri.
 
“Tumeshafika?” nikamuuliza Mapama.
 
Sikujua kabisa kuwa Mapama angenigeuka na kunisaliti kwa magaidi..
 
Bila shaka, zile boti ndio zilikuwa zimekutana. Ile boti ya pili ilikuwa ndiyo ile ambayo Mapama aliniambia tutakutana nayo tutakapoingia Somallia ili ifaulishe ule mzigo wa pembe za ndovu.
 
Wakati ule namuuliza Mapama kama tumeshafika, niliona mtu mmoja akitoka katika boti ile ya pili na kuingia katika boti ya Mapama. Alikuwa kijana. Ingawa alikuwa mwembamba alionekana kunawiri na alivaa mavazi yalliyompendeza japo shati alilovaa lilionekana kubwa kutokana na wembamba wake.
 
Alikuwa Msomali mweusi mwenye nywele za singa. Mkono mmoja alikuwa ameshika kichanga cha mirungi aliyokuwa akitafuna na mkono mwingine alishika sigara iliyokuwa ikifuka moshi.
 
Katika kiganja cha mkono wake wa kushoto alivaa pete kubwa iliyokuwa inang’ara.
 
Niliukadiria umri wake kutozidi miaka thelathini na mitano. Alikuwa amenizidi kiumri kidogo.
 
Kijana huyo alisalimiana na Mapama aliyekutana naye nje ya kile kijichumba nilichokuwemo. Nilimshangaa Mapama kwa jinsi alivyokuwa ametaharuki kiasi kwamba alipuuza hata kunijibu nilipomuuliza kama tumeshafika. Alikuwa amebadilika kabisa. Niliona kama hakuwa mwenzangu tena.
 
Aliposalimiana na yule msomali alimuonesha ule mzigo wa Pembe. Msomali huyo aliutazama kisha akamuuliza.
 
“Wenzako wako wapi?”
 
“Nilikuja nao lakini tulipata matatizo makubwa”
 
“Matatizo gain?”
 
“Nitakueleza. Wambie jamaa wafaulishe huu mzigo”
 
Msomali huyo alitumia lugha ya kisomali kuwambia wasomali wenzake waliokuwa katika ile boti ya pili waingie katika boti ya Mapama na  kufaulisha  ule mzigo. Wasomali hao walioonekana kama wapagazi wakaingia na kuanza kazi.
 
Mapama na yule msomali niliyemdhania kuwa ndiye tajiri wa ule mzigo wakaingia katika ile boti nyingine. Sikujua walikwenda kuzungumza nini. Baada ya muda Mapama alirudi peke yake na kuniambia.
 
“Yule jamaa anataka kukuona?”
 
“Jamaa gani?” nikamuuliza.
 
“Yule msomali niliyekuwa nazungumza naye”
 
“Kwani mimi nahusikaje?”
 
“Sasa utakwenda au utaleta ubishi?” Mapama akaniuliza kwa ukali.
 
Kabla sijamjibu, Msomali mwenyewe akatokeza kwenye ile boti na kuninyooshea mkono kama ishara ya kuniita, nikaenda. Niliingia katika ile boti akanishika mkono na kuniingiza katika chumba kilichokuwa katika boti yake.
 
Chumba hicho kilikuwa kikubwa kuliko cha boti ya Mapama na kilikuwa kizuri kilichozungukwa na kuta za vioo. Ndani kilikuwa na sehemu ya kulala na makochi ya kukalia.
 
“Karibu, kaa hapo” Msomali akaniambia akinionesha moja ya makochi yaliyokuwa katika kile chumba.
 
Nikakaa.
 
“Asalaam alaykum” Msomali akaniambia huku akiketi upande wa pili wa chumba hicho.
 
“Waalaika Salaam” nikamjibu kwa sauti iliyonywea huku nikimtazama usoni kwake.
 
“Nimeelezwa na Nahodha kuhusu wewe na mkasa uliowatokea mlipokuwa mnakuja. Ameniambia kulitokea joka kama nondo na kuwaangamiza wenzake, ni kweli?”
 
“Ni kweli”
 
“Kwani walitaka  kukufanya nini?”
 
“Walitaka kuniua”
 
“Wapumbavu wale, mtu unaomba msaada wanataka kukuua. Sasa hilo joka lilitoka wapi?”
 
Nikabetua mabega yangu.
 
“Sijui”
 
“Bila shaka hilo ndilo lililokuokoa usiuawe, ungekuwa umeshatoswa na kuliwa na papa”
 
Hapo sikumjibu kitu.
 
“Wewe unaitwa Umar?” Msomali akaniuliza.
 
“Hapana”
 
“Unaitwa Amiri?”
 
“Hapana”
 
“Basi utakuwa unaitwa Amour”
 
Nikamkubalia.
 
“Ndio naitwa Amour, umejuaje?”
 
Msomali huyo akacheka. Badala ya kunijibu akaniambia.
 
“Nataka twende Somali mara moja”
 
Nikashituka na kumuuliza.
 
“Kwani hapa tuko wapi?’
 
MAMBO HAYO! PANA FUMBO GANI HAPA?
 
LEO NIMEWAPA NDEFU KWELI ILI KUTULIZA KIU YENU LAKINI ITABIDI TUKUTANE TENA KWSHO

No comments:

Post a Comment