HADITHI na Faki . A . Faki 0713 340572 , 0655 340572
MWANAMKE ALIYENICHUNUKA 8
Kutoka siku ile yule jini
hakunifuata tena, nikawa nimefurahi. Lakini baada ya kupita juma moja nilianza
kuota ndoto za ajabu ajabu, nyingine zikiwa za kutisha.
Kusema kweli hazikuwa ndoto
za kawaida kwani zilifululiza kama mkanda wa
sinema, ikimalizika hii inakuja hii. Wakati mwingine ninaota nipo kwenye
majabali marefu nikiwa na msichana ambaye ghafla huanza kunilaumu kuwa
nimemgeuka. Lakini mara sura yake hubadilika na kuwa ya yule msichana wa
kijini. Hapo huanza kumkimbia na kila ninavyokimbia yule msichana hutokea mbele
yangu.
Wakati mwingine huzinduka
usingizini lakini usingizi unaponijia tena, ile ndoto huendelea. Inapoendelea
hujikuta nimefika kingoni mwa jabali ambapo yule msichana hunisukuma, nikajiona
naanguka kutoka juu ya jabali refu huku ninapiga kelele.
Inapomalizika ndoto hii
inakuja nyingine. Huota nipo kwenye maeneo ya makaburi. Ghafla miili ya watu
waliokufa hutoka katika makaburi na kunifuata ikiwa mifupa mitupu. Ninatoka
mbio lakini najiona ninavutwa kwa nyuma kama
ninayevutwa kwa sumaku hadi ile mifupa inanikaribia na kunigombania na ndipo
ninapozinduka.
Ndoto za namna hiyo
ziliniandama karibu kila siku. Mwisho nilirudi tena kwa yule Mchungaji
kumueleza, akanifanyia maombi tena lakini ndoto hazikukoma. Nilipoona hali
inazidi kuwa mbaya nikahamia kwa rafiki yangu Juma.
Kwa Juma pia sikupata nafuu
yoyote. Ndoto ziliendelea kuniandama huko huko. Siku moja niliota nachinjwa
nikapiga ukulele uliomuamsha Juma. Alipoamka aliniuliza.
“Una nini Alfred?”
Jasho lilikuwa linanitoka na
moyo ulikuwa unanienda mbio kama ulitaka
kutoka. Nikaketi kitandani na kumueleza nilivyoota Hata yeye aliogopa. Siku ile
hatukulala tena hadi asubuhi.
“Uende kwa mganga” Juma
akaniambia asubuhi. Alinielekeza kwa mganga mmoja aliyekuwa akikaa kitongoji
cha Amboni. Kitongoji hicho kipo umbali wa kilometa 10 hivi kutoka jiji la
Tanga.
Akaniambia kaka yake alikuwa
na tatizo kama langu la kuota ndoto za kutisha lakini alipokwenda kwa mganga
huyo tatizo hilo
likamalizika.
“Huyo mganga anaitwa nani?”
“Anaitwa Mtemi Wembe”
“Nitakwenda Amboni
kumuulizia”
“Ningekupeleka lakini ndiyo
hivyo ninakwenda kazini na kurudi ni jioni”
“Hakuna tatizo, kwa vile
umeshanielekeza nitakwenda mwenyewe”
Juma alipoondoka kwenda
kazini kwake na mimi niliondoka kwenda huko Amboni. Nilikwenda stendi nikapanda
daladala za kwenda Amboni. Nilipofika Amboni nilimkuta mtu mmoja akichoma
mahindi ya kuuza palepale kwenye kituo cha daladala. Nikamuuliza kama anamfahamu
mganga Mtemi Wembe.”
“Ni maarufu” akanijibu na
kuongeza..
“Kamata barabara hii, nenda
moja kwa moja. Mbele kule utakuta njia mbili, moja inaelekea kulia na nyingine
kushoto. Fuata ile ya kushoto, ukienda mbele utakuta mbuyu. Ukiupita mbuyu
utakata tena kushoto. Nyumba utakayoikuta mbele yako ndiyo hiyo ya Mtemi Wembe”
Ilikuwa kama alivyonielekeza
Juma. Nikamshukuru yule mtu kisha nikafuata ile barabara aliyonielekeza hadi
nikauona ule mbuyu. Nilipokata kona kushoto nikaiona ile nyumba. Nikaenda
Nilikuta watu kadhaa wakiwa
nje wameketi kwenye gogo la mnazi wakisubiri zamu ya kuingia. Na mimi nikaenda
kujiunga nao. Kulikuwa na watu wengine waliokuja nyuma yangu. Sote tukawa
tunasonga taratibu kuelekea kwenye mlango wa nyumba ya mganga.
Ghafla nilisikia harufu ya
manukato makali puani mwangu, nikageuza uso wangu na kumtazama msichana
aliyekuwa ameketi kushotoni kwangu. Nikashituka nilipoona ni yule msichana wa
kijini. Alikuwa ameketi sambamba na mimi. Wakati namtazama na yeye alikuwa akinitazama.
“Amekuja muda gani?”
nikajiuliza kimoyomoyo huku nikiwa nimepatwa na mshangao.
Ukweli ni kuwa nilipofika
hapo, msichana huyo hakuwepo. Bila shaka alikuwa miongoni mwa watu wanne
waliokuja baada ya mimi. Lakini kwa vyovyote vile kuja kwake kulikuwa kwa
kimiujiza kwani sikumuona alivyofika, nilishitukia tu yupo hapo baada ya
kusikia harufu ya manukato yake.
Kwa jinsi nilivyoshituka,
moyo wangu ulianza kunienda mbio. Sikuwa na raha tena. Nikanyanyuka ghafla na
kuondoka kama mtu ambaye nilikuwa nimeghairi
kuingia kwa mganga kwani nilihisi angenifuata humo ndani.
Nilitenbea haraka haraka
nikakata kona kwenye ule mbuyu kisha nikaanza kukimbia. Nilipokata kona
nyingine kuelekea upande wa kulia. Ghafla nikamuona yule msichana mbele yangu.
Nikasisimama ghafla. Kwa
kweli niligwaya. Nikawa namtazama na yeye akanitazama. Macho yake yalikuwa
makali kama kaa la moto na uso alikuwa
ameukunja.
“Unajisumbua bure!”
akaniambia.
Ingawa alionekana kukasirika
lakini sauti yake ilikuwa tulivu.
“Mimi sikimbiliki.
Nimeshakuzunguka pande zote. Kama unaweza
kuingia chini ya ardhi ingia, ndio sitaweza kukufuata. Lakini huku juu ya ardhi
hata kama utakimbilia Ulaya nitakufuata tu!”
akaniambia.
Nilikuwa nimenyamaza kimya
nikimtazama na kumsikiliza huku nikirudi nyuma taratibu. Pakapita ukimya mfupi.
“Ulienda kwa mganga kufuata
nini?” akaniuliza ghafla na kuongeza.
“Unadhani mganga ataweza
kunifukuza mimi? Mimi sifukuziki!”
Akaendelea kuniambia “Mimi ni
Banuna mwana wa Ziraili. Ukoo wetu ni wa wachawi. Babu yangu ni mkuu wa
wachawi! Hakuna mganga atakayeniweza mimi”
Akanyamza na kunitazama jinsi
nilivyokuwa ninahema kisha
akaendelea.
“Ni kwa sababu tu nimekupenda
ninakuruhusu urudi nyumbani. Lakini ninakupa muda mwingine mfupi ufanye maamuzi
sahihi. Ukiendelea kuniletea kisoi utajuta!”
Baada ya kuniambia hivyo
alichora msitari chini kwa mguu wake, akaniambia.
“Vuka huu msitari urudi
nyumbani”
Nilikuwa nimepatwa na hofu
isiyo na kifani. Sikuelewa alikuwa ananiambia nini,mpaka aliporudia kwa mara ya
pili.
“Nimekuambia vuka huu msitari
urudi nyumbani. Nisikuone tena kwenye nyumba za waganga!’
Nikapiga hatua haraka haraka
kuvuka ule msitari aliouchora chini kwani alikuwa amesogea kando. Nilipouvuka tu
ule msitari nikajikuta nipo mbele ya nyumba ninayoishi. Sikuwapo tena mahali pale nilipokuwa na yule
msichana wa kijini!.
Huku nikiwa nimeshikwa na
mshangao uliochanganyika na hofu, niliangalia upande wa kulia na wa kushoto.
Sikumuona tena yule msichana
Nikawa najiuliza nimefikaje
pale nyumbani? Hatua moja tu niliyopiga kuvuka ule msitari imenifikisha katika
nyumba ninayoishi? Ilikuwa miujiza mikubwa!.
Badala ya kuingia ndani
niligeuka nikaelekea nyumbani kwa Juma, Juma alikuwa yupo kazini kwake lakini
kwa vile alikuwa ameniachia ufunguo mmoja, nilifungua mlango nikaingia ndani.
Nikafikia kujilaza kitandani.
Ingawa sikuwa na yule
msichana, hofu ilikuwa imenitawala na kusababisha nijisikie kupata homa.
Siku ile sikutoka tena mle
chumbani mpaka Juma aliporudi jioni. Alikuta nilikuwa nikitetemeka kwa homa.
“Alfred unaumwa?” akaniuliza.
“Nasikia homa”
“Tangu saa ngapi?”
“Tangu asubuhi”
“Dah! Umeshakula dawa?”
“Bado. Kwanza
hebu kaa nikueleze yaliyotokea kule kwa mganga”
Huku akionekana kupata
wasiwasi, Juma alikaa kwenye kiti. Nikamueleza yale yaliyonitokea kule Amboni
na nilivyorudishwa nyumbani kimiujiza.
Juma akashangaa.
Je nini kitatokea. Endelea
kufuatilia kesho hapa hapa Tangakumekuchablog
No comments:
Post a Comment