Friday, June 10, 2016

HADITHI, MWANAMKE SEHEMU YA 16


MWANAMKE 16 na Faki A Faki 0655 340572
 
ILIPOISHIA
 
Nikanyanyuka kwenye kiti na kumfuata haraka. Wale vijana walikuwa wameshafika barabarani wakaelekea upande wa Chumbageni kwa mwendo wa kasi.
 
“Wamepora mkoba wako?” nikamuuliza.
 
“Basi waache tu, huwezi kuwafanya kitu” Zena alisema. Sauti yake ilikuwa tulivu lakini ilionesha ghadhabu.
 
“Wale vijana walikuwa wamekaa muda mrefu nyuma yetu, kumbe walikuwa na lao wanalongojea”
 
“Hakuna tatizo”
 
Nilikuwa nafuatana naye kuelekea kwenye lango la kutokea kwenye bustani hiyo.
 
“Dah!....”
 
“Usijali, waache tu. Mimi nakwenda zangu”
 
Ile teksi iliyomleta Zena ikatokea tena na kusimama mahali pale pale pa mwanzo.
 
Zena akaifuata na kujipakia. Teksi ikaondoka. Niliisindikiza kwa macho hadi ilipokata kona.
 
“Majini pia wanapanda teksi!” nikajisemea moyoni mwangu kisha nikaanza kutembea kwa miguu kurudi nyumbani.
 
SASA ENDELEA
 
Kile kitendo cha wale vijana kilikuwa kimefadhaisha akili yangu.
 
Sikurudi nyumbani moja kwa moja, nilikwenda nyumbani kwa kaka. Aliponiona tu akaniuliza.
 
“Ulifika huko Uhuru Park?”
 
“Nimefika na nimekutana naye”
 
“Enhe amekueleza nini?”
 
“Kwanza amenirudishia hiki kitabu changu nilichokuwa nimemuazima siku ile kisha akaniomba msamaha kwa usumbufu wowote ambao niliupata kutokana na yeye”
 
“Enhe…?”
 
“Baada ya hapo akanithibitishia  mwenyewe kwamba yeye ni jinni. Akaniambia kwamba nisimuogope kwani hatakuwa na madhara na mimi. Lakini la msingi aliloniambia ni kuwa anataka niwe mume wake…”
 
“Mume wake kivipi?”
 
“Nafikiri anataka tuoane”
 
“Eh…utamuweza kweli mke wa kijini? Kumbe ana makubwa!”
 
“Nimemuuliza kwani majini wanaoana na binaadamu? Akaniambia niende nikamuulize bibi mzaa baba, eti baba yangu baada ya kumuacha yeye alioa mke gani?”
 
“Alikuwa na maana gani?”
 
“Ameniambia nikamuulize tu halafu nije nimpe jibu”
 
“Kumbe anamjua pia bibi yetu?”
 
“Ameniambia amekuwa na mimi tangu nikiwa mdogo lakini hakuwa amejitokeza, kwa hiyo familia yetu atakuwa anaijua”
 
“Itakubidi hayo maneno ukamueleze mama”
 
“Nitakwenda kumueleza”
 
“Twende kwake sasa hivi”
 
Tukatoka na kaka kwenda nyumbani kwa mama. Tulienda kwa miguu. Njiani tulikuwa tukiendelea kuzungumza.
 
“Ameniambia kama nitaoana naye atanipa utajiri”
 
“Hilo si tatizo, tatizo ni kuwa na mke jini” Kaka akaniambia.
 
Nikajua suala hilo lilikuwa limemshitua na yeye.
 
Tulipofika nyumbani kwa mama, nikamueleza mazungumzo yote tuliyozungumza na Zena. Mama naye akashituka.
 
“Hebu nenda ukamuulize bibi yako kuhusu huyo babu yako usikie atakueleza nini lakini nakushauri usikubali kuoana na huyo mwanamke hata kama atakupa utajiri” Mama akaniambia.
 
“Mimi sijakubali, bado niko kwenye utafiti”
 
“Wewe ni binaadamu huwezi kuishi na mwanamke ambaye ni jini” Mama aliendelea kunisisitizia.
 
“Nitazingatia ushauri wako na nitakwenda kwa bibi hapo kesho” nikamwambia.
 
Bibi mwenyewe alikuwa akiishi Mwambani, mwendo wa kama kilometa kumi kutoka Tanga mjini. Kitongoji hicho kipo upande wa Kaskazini mwa jiji la Tanga katika barabara inayoelekea wilaya ya Pangani.
 
Siku ya pili yake nikaenda huko Mwambani kwa kutumia pikipiki yangu. Nilipofika nilimkuta bibi yuko barazani mwa nyumba yake akisuka ukili wake. Ingawa alikuwa kikongwe sana lakini bado alikuwa akijiweza kiasi kwamba alikuwa anaweza kusuka ukili wake.
 
Nilikuwa nimemnunulia kilo tano za sukari, nikampa.
 
Baada ya kuulizana hali nilimwambia licha ya kwenda kumsalimia pia nilikuwa na shida yangu.
 
“Shida gani?” akaniuliza.
 
“Nilikuwa nataka kujua eti baada ya wewe kuachana na marehemu mume wako yaani babu yangu, babu alioa mke mwingine?”
 
“Ndio alioa”
 
“Enhe niambie alimuoa nani?”
 
“Inasemekana alioa mke wa kijini, alikuwa akiitwa Zena na huyo Zena ndiye aliyefanya babu yako aniache mimi. Lakini mimi sikuwahi kumuona”
 
Nikashituka niliposikia maneno yale.
 
“Alimpata wapi huyo mke wa kijini?” nikamuuliza.
 
“Alimchunuka tu akamwambia aniache mimi amuoe yeye. Babu yako akakubali kuniacha kwa ajili ya kupata utajiri”
 
“Na ni kweli alipata utajiri?”
 
“Alipata utajiri mkubwa sana lakini siku chache kabla ya kufa kwake utajiri wote ulipotoea na huyo mke wake alitoweka pia”
 
“Wakati huo alikuwa umeshamzaa baba?”
 
“Baba yako alikuwa ameshazaliwa pamoja na kaka yake Abdul yaani baba yako mkubwa ambaye alifariki nchi za nje”
 
“Sasa baada ya babu kuoa mke wa kijini, nani aliwalea kina baba?”
 
“Aliniachia nao mimi, nikawalea hadi wakawa wakubwa”
 
Nikanyamaza kimya nikijiuliza kama Zena anayemsema bibi ndiye yule anayetaka nioane naye.
 
“Kwanini umeniuliza hivyo?” Bibi aliniuliza na kunizindua.
 
“Nimekuuliza tu bibi, kuna mzee mmoja alikuwa akifahamiana na marehemu babu, alinieleza kuhusu kisa hicho ndio nikaona nije nikuulize” nikamdanganya bibi. Sikutaka kumueleza ukweli kwamba kuna mwanamke wa kijini alinituma nimuulize.
 
“Ulikuwa huamini?”
 
“Nilikuwa siamini lakini baada ya wewe kunithibitishia sasa ninaamini”
 
“Wakati babu yako anakufa, watu walishangaa kuona mali yote aliyokuwa nayo imepotea. Na yule mke wake naye hakuonekana tena. Alitoweka wiki moja kabla ya kifo cha babu yako”
 
“Na huyo babu na mke wake walikuwa wakiishi maisha ya aina gani?”
 
“Waliishi maisha ya kawaida tu lakini mke wake alikuwa hajitokezi katika shughuli za watu”
 
“Babu alipokuacha uliona uchungu sana bibi?”
 
“Kwa kweli niliumia sana kwa sababu sikuwa nimemtenda kosa lolote na bado nilikuwa nampenda babu yako”
 
“Pole sana bibi”
 
“Oh! Wanipa pole leo wakati mambo yameshapita zamani!”
 
“Lakini bibi uliona babu alifanya jambo la busara kuoa mwanamke wa kijini?”
 
“Alilazimishwa na yule jini na aliahidiwa kupata utajiri. Kuna mganga mmoja aliniambia kama babu yako asingeniacha yule jini angeniua”
 
“Eh kumbe ni viumbe hatari kiasi hicho!”
 
“Ndivyo nilivyoambiwa, sijui kama ningeuliwa kweli”
 
Pakapita ukimya wa sekunde kadhaa. Bibi alikuwa akiendelea kusuka ukili wake na mimi nilikuwa nikiumiza kichwa kwa kuwaza. Hatimaye nikauondoa ule ukimya.
 
“Kwa mfano mimi nikipata mke wa kijini, unanishaurije nioane naye?” nikamuuliza.
 
Bibi akacheka.
 
“Bibi mbona unanicheka?”
 
“Unanichekesha. Huyo mke wa kijini utampata wapi?”
 
“Kwani babu alimpata wapi?”
 
“Yule ni mpaka akuchunuke mwenyewe”
 
“Sawa. Je akinichunuka na kuniambia anataka tuoane, nikubaliane naye?”
 
“Hayo ni mawazo yako sasa, mimi nikushauri nini?”
 
“Unaweza kunishauri kwamba nioane naye au la”
 
“Hilo sio jambo la kushauriwa, ni uamuzi wako na huyo jini kama utampata. Kwani na wewe unataka kupata utajiri?”
 
“Hakuna asiyetaka utajiri bibi”
 
“Angalia sana, utajiri mwingine una matatizo. Ni bora uishi masikini hivyo hivyo”
 
Baada ya kimya kingine kifupi nikamuaga bibi. Wakati nataka kuondoka nikampa shilingi elfu ishirini. Bibi akanishukuru.
 
“Haya bibi nakwenda” nikamuaga bibi na kupanda pikipiki yangu.
 
“Uende salama, nisalimie wenzako”
 
“Nitakusalimia”
 
JE JAMAA ATACHUKUA UAMUZI GANI? HEBU ENDELEA KUFUATILIA HADITHI HII HAPO KESHO

No comments:

Post a Comment