HADITHI
YALIYONIKUTA TANGA (23)
ILIPOISHIA TOLEO LILILOPITA
Hata hivyo nilikuwa
nikijiuliza bangi ilikuwa inatumikaje katika uganga wakati kilikuwa kilevi
kisichokubalika? Sikupata jibu la swali hilo.
Yule mtu aliyetumwa bangi
hakuchelewa sana
akarudi akiwa na bangi yake mkononi. Nikahisi kwamba bangi ilikuwa ikiuzwa sana pale kijijini.
Nikakumbuka zamani
nilishuhudia kesi ya mvuta bangi mmoja aliyedai kuwa akivuta bangi huwa anapata
nguvu ya kulima. Nikajiambia huenda
zilitumika pale kijijini kwa sababu hiyo.
Ile bangi ilipoletwa
ilichanganywa na vile vitu vingine vilivyoletwa kwanza, yaani ule mchanga wa
kaburini na kile kinyesi cha nguruwe.
Baada ya vitu hivyo
kuchanganywa vilitiwa kwenye chungu na kuwekwa kwenye jiko. Baada ya sekunde
chache vilianza kuungua na kutoa moshi. Yule mganga alikuwa ameshika mwiko
akivigeuza huku na huku.
Vilikuwa vikitoa harufu mbaya
iliyokuwa inaumiza kichwa. Mama yangu alipiga chafya mara mbili.
“Kama
unasikia vibaya toka nje” Mganga huyo akamwambia mama.
Mama akatoka nje. Mganga
aliendelea kuvichoma vile vitu mpaka vikaungua na kuwa vyeusi. Aliepua kile
chungu na kukiweka kando ya jiko.
SASA ENDELEA
Alisubiri chungu hicho
kilipopoa akaanza kuvisaga vile vitu alivyokuwa amevichoma kwa kutumia aina
fulani ya jiwe lililokuwa na rangi ya kahawia.
Vitu hivyo vilisagwa na kuwa
unga unga mweusi ambao aliutoa kwenye chungu hicho na kuutia kwenye karatasi
nyeupe. Akaanza kuutabania maneno ya kiganga huku akiugeuza geuza kwa kidole
chake.
Alipomaliza kuutabania
aliuchota kidogo akautia kwenye kile kisanduku akauchnganya changanya na yale
mapambo ya dhahabu. Ule unga uliobaki aliufunga kwenye ile karatasi akanipa.
“Utakuwa unachota kisdogo na
kutia kwenye maji ya kuoga kama ulivyofanya
jana. Utaoga asubuhi na jioni kwa siku saba” akaniambia.
Ili nipate uhakika wa alichoniagiza nikamuuliza.
“Umeniambia niioge hii dawa
kidogo dogo kwa siku saba asubuhi na jioni?”
“Ndio. Usipitishe hata siku
moja”
Nikabaki kumtazama yule
mganga wakati akiniambia hivyo. Sikumtazama kwa sababu nilikuwa namsikiliza.
Nilimtazama kutokana na mawazo yaliyokuwa yakipita akilini mwangu.
Nilikuwa nikijiambia, yaani
niende nikaoge bangi na mavi ya nguruwe kwa siku saba!
Uganga wa kienyeji unahusisha
mambo mengi machafu!
Licha ya kuona kinyaa,
niliona sikuwa na budi kutekeleza vile nilivyoambiwa ili kusalimisha maisha
yangu na pia nipate zile dhahabu ambazo nazo zilitiwa ile dawa.
“Ukioga dawa hiyo shetani
hatakufuata hata siku moja. Atakupitia mbali sana na hizo dhahabu hatazitaka tena kwa
sababu zimeshanajisika na wewe mwenyewe pia unapata najisi ukioga dawa hiyo”
Mganga aliniambia.
“Hata zikipita hizo siku saba
hao majini hawatanifuata?” nikamuuliza ili nipate ufafanuzi.
“Ukishaioga kwa siku saba, inakuwa
ni basi. Hawatakufuata tena”
“Sawa, nimekuelewa”
Kule kwetu ni mwiko kwa
mganga kukwambia nataka kiasi fulani cha pesa isipokuwa mteja mwenyewe ndio
unamkadiria kutokana na kazi aliyokufanyia.
Nilitoa shilingi elfu
ishirini nikampa. Akatuambia kwamba tunaweza kwenda zetu.
Tukaondoka.
Tuliporudi nyumbani nilikitia
kile kisanduku kwenye begi langu kisha nikampa mama begi hilo ili alihifadhi chumbani kwake.
Nikaanza kutumia ile dawa. Kila
siku nikawa ninaioga mara mbili asubuhi na jioni. Mpaka siku saba zikaisha.
Nikakaa kwa mwezi mzima, sikuona tatizo lolote. Nikaamini kwamba ile dawa
ilikuwa inafanya kazi.
Udadisi ukanifanya nipige
simu kwa mpelelezi mwenzangu aliyekuwa Tanga ili anieleze hali ilivyo.
“Tuko shwari tu” akaniambia.
“Vipi kuhusu wale majini wa
barabara nane, polisi bado wanawafuatilia?’
“Ule upelelezi ulishaachwa
waka hakuna afisa yeyote anayehoji kuhusu kesi ile”
“Huenda wameingia uoga”
“Sio huenda, wameingia uoga kweli”
Baada ya kuelezwa hivyo na
kupata picha kamili ya hali iliyokuwa huko Tanga nikapata matumaini kuwa yale
matatizo yalikuwa yamekwisha na kwamba ningefaidi zile dhahabu.
Siku moja mama yangu
alinifuata chumbani na kuniambia kuwa kuna msichana ambaye alitaka nimuoe ili
niende naye Tanga. Nikataka kumjua huyo msichana.
“Nitatuma mtu jioni amuite,
utakuja kumuona” Mama aliniambia.
“Sawa”
ILipofika jioni mama akaja
chumbani mwangu akiwa na msichana mmoja mzuri wa kihaya.
Akaniambia kwa kinyumbani.
“Nimekuletea mchumba
mwanangu”
“Ndiye huyu?” nikamuuliza
nikiwa nimemtumbulia macho.
“Ndiye yeye niliyekwambia
asubuhi, ni msichana mpole sana
na ana tabia nzuri anafaa kuwa mke wako”
Msichana akanipigia goti
kisha akanisalimia. Nikafurahi kupewa heshima za kinyumbani. Baada ya
kusalimiana naye nilimwambia aketi kwenye kiti, akakaa.
“Unaitwa nani?” nikamuuliza.
“Naitwa Mage”
“Haya zungumzeni, mimi niko
hapa ukumbini” Mama akaniambia na kutoka mle chumbani.
“Unaishi na wazazi wako?”
nikamuuliza.
“Ndiyo naishi na wazazi
wangu”
“Umesoma hadi darasa la
ngapi”
“Nimekomea kidato cha nne”
“Mwaka gani?”
“Mwaka juzi”
“Mama yangu amekupenda, kwa
hiyo uko tayari tufunge uchumba?”
“Kama
na wewe umenipenda”
“Kusema ukweli alichokipenda
mama yangu na mimi nitakipenda tu”
“Wewe unafanya kazi gani?”
“Mimi ni polisi upande wa
upelelezi”
“Unafanya kazi mkoa gani”
“Kwa sasa nimehamishiwa
Tanga”
“Kwa hiyo ukishanioa
tutakwenda kuishi Tanga?”
“Ndiyo”
“Sawa. Sasa uje ujitokeze kwa
wazazi wangu”
“Nitafanya hivyo katika siku
chache zijazo”
Baada ya kuzungumza na Mage,
msichana niliyechaguliwa na mama yangu na ambaye mimi mwenyewe pia nilimpenda
nilimuita mama nikamwambia kuwa nimeshazungumza naye.
“Mmeshakubaliana”
“Ndiyo, tumekubaliana”
“Basi ngoja nimsindikize
arudi kwao”
Mama akatoka na yule
msichana.
Je nini kitaendelea? Usikose
kuendelea na hadithi hii katika toleo lijalo kupitia www.tangakumekucha.blogspot.com
No comments:
Post a Comment