HADITHI
YALIYONIKUTA TANGA (25)
ILIPOISHIA
Usiku ule ulikuwa balaa!
Hatukulala. Mke wangu alikuwa akipiga kelele usiku kucha akidai kuwa kila
alipofumba macho alikuwa akiona msichana anampiga bakora akimwambia avue zile
dhahabu alizovaa.
Mwisho wake ilibidi mke wangu
atii na kavua zile dhahabu nilizokuwa nimempa na hapo ndipo alipopata usingizi.
Kulipokucha asubuhi
nilikichukua kile kisanduku nikakitia kwenye begi na kumpa polisi aliyekuwa
jirani yangu.
“Tafadhali nihifadhie hili
begi langu nitalichukua kesho” nikamwambia.
Kwa vile yule polisi alikuwa
rafiki yangu akalichukua begi hilo
na kunihifadhia chumbani kwake. Nikaenda zangu kazini.
Niliporudi kutoka kazini mke
wangu akaniuliza maswali mengi kuhusu zile dhahabu nilizokuwa nimempa ambazo
zilikuwa zimemtia wasiwasi mkubwa.
Nikamdanganya kwamba dhahabu
hizo nilizinunua kwa sonara na kwamba nilishazirudisha.
“Sasa kwanini nilikuwa naota
ile ndoto ya kuchapwa?” akaniuliza.
“Sijajua lakini nimemueleza
sonara huyo ameniambia alikosea akaniuzia dhahabu za majini lakini kwa vile
nimezirudisha hakutakuwa na tatizo.” Nikaendelea kumdanganya ili kumtoa
wasiwasi.
SASA ENDELEA
Nilidhani kwa kuhamisha kile
kisanduku kwa mwenzangu ndio ningemaliza yale matatizo ya majini lakini
nilikuwa nimejidanganya.
Yapata saa nane usiku wakati
nimelala, yule polisi niliyempa lile begi lenye kisanduku anihifadhie
alinibishia mlango.
Nilipofungua mlango nilimuona
amesimama mbele ya mlango akiwa na lile begi mkononi.
“Chukua hili begi lako,
linaniletea miujiza chumbani kwangu” akaniambia huku uso wake ukiwa
umetaharuki.
“Miujiza gani tena?”
“Kuna joka linatoka ndani ya
hili begi halafu linazunguka chumbani kwangu”
Nikajifanya nashangaa.
“Joka?”
“Ndio joka. Tena joka kubwa sana. Linazunguka
chummbani kisha linarudi kwenye hili begi linapotea”
“Mh! Unanieleza habari ya
ajabu sana”
“Kwani umeweka nini humu
ndani”
“Sijui kilichomo humo ndani. Hilo begi alilisahau mtu
mmoja aliyekuja hapa nyumba kuomba maji ya kunywa” nikamdanganya.
“Mh! Basi lichukue. Siwezi
kuliweka kwangu”
Nikalichukua lile begi. Yule
polisi akarudi nyumbani kwake. Na mimi nikapatwa na kizungumkuti. Nilikuwa
sijui nikaliweke wapi. Yale maelezo ya polisi mwenzangu yalinitisha.
Nilipoona nimekosa pa
kuliweka nililiweka chini ya meza pale sebuleni. Nikafunga mlango wa chumbani
ili kama kuna joka linalotoka lisiingie
chumbani mwetu.
Wakati ule mke wangu alikuwa
amelala. Hakuwa akijua kilichokuwa kinaendelea. Nilishukuru kwa hilo. Laiti angekuwa macho
akasikia yale niliyokuwa nikiyazungumza na yule polisi, ingekuwa taabu.
Wakati nimejilaza kitandani
nikiwaza, nilijiambia kuwa ule uganga niliofanyiwa na yule mganga wa kijijini
kwetu haukufaa kitu, sasa vituko vilikuwa vinanijia nyumbani kiasi kwamba mimi
mwenyewe nilikuwa nimeshapata uoga na nilikuwa sijui la kufanya.
Nikajiambia tamaa yangu ya
kumiliki zile dhahabu sasa inaniponza.
Wakati niko kwenye lindi la
mawazo nikapitiwa na usingizi ghafla, nikaota nimeamka saa kumi na mbili
asubuhi, nikatoka na lile begi na kwenda kule magomeni kwenye yale mkaburi.
Nilipofika nikakitoa kile kisanduku na kukiweka juu ya kaburi mojawapo. Hapo
hapo nikaona kinatitia chini na kupotea kabisa.
Baada ya hapo nilizinduka usingizini
nikatazama saa na kuona ilikuwa saa kumi na mbili kasorobo, nikavaa nguo na
kutoka chumbani. Nilikwenda kuosha uso na kusukutua maji. Nikalichukua lile
begi na kutoka nalo bila hata kumuaga mke wangu.
Nilikwenda kupanda daladala
nikaenda Magomeni. Nilifika kule makaburini nikakitoa kile kisanduku na
kukiweka juu ya kaburi kama vile nilivyoota
usiku. Hapo hapo nikaona kile kisanduku kinazama chini.
Kilizama hadi kikapotea
kabisa.
Nilitishika sana lakini kwa vile tukio lenyewe
nilishaliota nilijikaza.
Kile kisanduku kilipopotea,
nikajua kimerudi kwa wenyewe. Nikaondoka na kurudi nyumbani. Nilipofika
nilimkuta mke wangu bado amelala. Nikaenda kuoga. Wakati narudi kutoka kuoga
nikamkuta ameshaamka. Sikumwambia chochote.
Baada ya siku ile sikuona
tena vile vituko vya majini. Tukio hilo
licha ya kunitesa lilinipa fundisho ambalo sitalisahau. Nikawa polisi muadilifu
sana niliyefanya kazi yangu kwa misingi ya haki
na sheria na sio kama nilivyokuwa hapo mwanzo.
Hayo ndiyo yaliyonikuta
tanga’ usiache kunitumia maoni yako juu ya hadithi kupitia www.tangakumekucha.blogspot.com
No comments:
Post a Comment