HADITHI
YALIYONIKUTA TANGA (24)
ILIPOISHIA
“Wewe unafanya kazi gani?”
“Mimi ni polisi upande wa
upelelezi”
“Unafanya kazi mkoa gani”
“Kwa sasa nimehamishiwa
Tanga”
“Kwa hiyo ukishanioa
tutakwenda kuishi Tanga?”
“Ndiyo”
“Sawa. Sasa uje ujitokeze kwa
wazazi wangu”
“Nitafanya hivyo katika siku
chache zijazo”
Baada ya kuzungumza na Mage,
msichana niliyechaguliwa na mama yangu na ambaye mimi mwenyewe pia nilimpenda
nilimuita mama nikamwambia kuwa nimeshazungumza naye.
“Mmeshakubaliana”
“Ndiyo, tumekubaliana”
“Basi ngoja nimsindikize
arudi kwao”
Mama akatoka na yule
msichana.
SASA ENDELEA
Aliporudi aliniuliza kama nimempenda yule msichana.
“Nimempenda” nikamjibu.
“Sasa una mawazo gani ya
kumuoa?”
“Nilikuwa sijapanga kuoa kwa sasa…”
“Nimekuonesha yule msichana
ili kukutia mawazo ya kuoa. Umeshafikia umri wa kuwa na mke”
“Ni kweli, kwa hiyo mama
unanishauri nimuoe yule msichana”
“Tena tuwaozeshe haraka
iwezekanavyo, ukimaliza likizo yako uondoke na mke wako”
“Itawezekana mama?”
“Kwanini isiwezekane. Harusi
za vijijini usizifananishe na harusi za mijini”
“Sasa la muhimu ni kupeleke
barua ya uchumba kwa wazazi wake tusikie watatujibu nini”
“Kama
msichana mwenyewe amekubali na wazazi wake watakubali tu. Hilo halina tatizo.
Niliandika barua ya uchumba
siku ile ile baada ya mama kunitia mawazo ya kuoa. Barua ilipelekwa na siku ya
pili yake majibu yakarudishwa.
Nilifurahi kwa kukubaliwa
uchumba wangu na Mage. Nilitajiwa mahari iliyokuwa inatakiwa pamoja na ada
nyinginezo kwa mujibu wa mila zetu.
Siku ile tulikaa kikao cha
ndugu tukaijadili ile barua na kukubaliana na kila kilichoandikwa. Baada ya
siku tatu nilipeleka mahari pamoja na ada zote.Tukatakiwa tutoe siku ya kwenda
kuoa.
Tulikaa tena kikao cha ndugu
tukapanga siku ya kwenda kuoa. Tulipokubaliana juu ya siku hiyo tukatoa taarifa
upande wa pili. Mipango ya harusi ikafanyika kwa pande zote mbili na siku
ilipowadia nikaoana na Mage.
Nilikaa na Mage nyumbani
kwetu kwa wiki mbili tu kabla ya kuondoka kurudi Tanga, kwani likizo yangu
ilikuwa ikikaribia kwisha.
Nilipoondoka nilikichukua
kile kisanduku changu cha dhahabu na kuondoka nacho. Nilipofika Tanga
nilimtambulisha mke wangu kwa polisi wenzangu tuliokuwa tunakaa kambini.
Polisi wenzangu walitupongeza
kwa uamuzi wetu wa kufunga ndoa lakini pia walinilaumu kwa kutowaarifu kuwa
ninaoa.
Siku mbili baada ya kufika,
Tanga nilitoa mkufu wa dhahabu, bangili mbili na vipuli na kumpa mke wangu
avae.
Usiku wa siku ile nilikwenda
kutembea mjini na mke wangu ili kumuonesha mji. Tulirudi nyumbani karibu saa
sita usiku. Tukafikia kulala.
Usiku ule ulikuwa balaa!
Hatukulala. Mke wangu alikuwa akipiga kelele usiku kucha akidai kuwa kila
alipofumba macho alikuwa akiona msichana anampiga bakora akimwambia avue zile
dhahabu alizovaa.
Mwisho wake ilibidi mke wangu
atii na kavua zile dhahabu nilizokuwa nimempa na hapo ndipo alipopata usingizi.
Kulipokucha asubuhi
nilikichukua kile kisanduku nikakitia kwenye begi na kumpa polisi aliyekuwa
jirani yangu.
“Tafadhali nihifadhie hili
begi langu nitalichukua kesho” nikamwambia.
Kwa vile yule polisi alikuwa
rafiki yangu akalichukua begi hilo
na kunihifadhia chumbani kwake. Nikaenda zangu kazini.
Niliporudi kutoka kazini mke
wangu akaniuliza maswali mengi kuhusu zile dhahabu nilizokuwa nimempa ambazo
zilikuwa zimemtia wasiwasi mkubwa.
Nikamdanganya kwamba dhahabu
hizo nilizinunua kwa sonara na kwamba nilishazirudisha.
“Sasa kwanini nilikuwa naota
ile ndoto ya kuchapwa?” akaniuliza.
“Sijajua lakini nimemueleza
sonara huyo ameniambia alikosea akaniuzia dhahabu za majini lakini kwa vile
nimezirudisha hakutakuwa na tatizo.” Nikaendelea kumdanganya ili kumtoa
wasiwasi.
ITAENDELEA KESHO, peruzi www.tangakumekucha.blogspot.com kila wakati kwa habari na matuiko ya papo kwa papo na motomoto.
No comments:
Post a Comment