Sunday, February 8, 2015

YALIYONIKUTA TANGA (13)

HADITHI
 
YALIYONIKUTA TANGA (13)
 
ILIPOISHIA TOLEO LILILOPITA
 
Sote tukasimama. Kila polisi akachukua bunduki yake.
 
Tulishindwa hata kujibu, tukawa tunatazamana.
 
“Vipi jamani, mbona mmelala hapa” Inspekta Amour akatuuliza tena.
 
Polisi mmoja akaeleza kilichotutokea. Polisi hao waliokuja wakashangaa.
 
Waliusogelea mwili wa Sajenti Erick na kuutazama.
 
“Huyu ndiye Sajenti Erick” Amour akasema baada ya kuutazama mwili huo. Akaongeza.
 
“Sasa nini kilitokea?”
 
“Ni miujiza mitupu” nilijibu mimi.
 
“Hiyo nyumba imetowekaje?”
 
“Hatujui. Muda huu tunazinduka tunaona nyumba haipo”
 
“Ilikuwa kwa wapi”
 
“Sisi tulikuwa uani mwa hiyo nyumba. Lile gari tulilokuja nalo lilikuwa mbele ya nyumba” polisi mwingine alijibu.
 
SASA ENDELEA
 
“Kwa hiyo nyumba ilikuwa hapa katikati?”
 
“Ndiyo. Ilikuwa kati ya sisi na lile gari” nikajibu.
 
“Sasa wale watu mnaosema mliwaona, wako wapi?”
 
“Hawapo tena, tumezinduka hatuwaoni” koplo akajibu yeye.
 
“Walikuwa ni watu wa aina gani?”
 
“Wale si watu, wale ni majini” nikasema na kuongeza.
 
“Wale ndio wamemuua Sajenti Erick. Yule mwanamke ndiye tuliyemkamata siku ile kwa tuhuma za kukutwa na madawa ya kulevya”
 
“Lakini yule mwanamke alikufa?” Amour akasema.
 
“Kwa kweli tumemuona na ndiye aliyetupungia mkono, sote tukapotewa na fahamu” Koplo akaeleza.
 
Inspekta Amour akaguna na kutupa mcho huku na huku.
 
“Yule binti yake ambaye aliwatoroka alikuwa pamoja naye?” akatuuliza tena.
 
“Walikuwa wote pamoja na mwenzao mwingine mwanaume” nikasema.
 
Nilitupa macho chini nikayaona yale magazeti ambayo niliyachukua mle chumbani. Nikainama na kuyachukua.
 
“Haya magazeti yana habari ya yule mwanamke, niliyakuta katika chumba alichochinjwa Erick”
 
Nilikunjua gazeti mojawapo nikampa Inspekta Amour. Amour alilichukua na kulitazama. Nilimpa na lile gazeti jingine nalo akalitazama.
 
“Itakuwa ni yeye kweli” alisema baada ya kusoma vile vichwa vya habari.
 
Pembeni na eneo hilo kuliwa na watu wamesimama wakitutazama. Inspekta Amour alimuita mtu mmojawapo. Mtu huyo alikuja kwa uoga akasimama kando ya Inspekta Amour.
 
“Wewe ni mwenyeji wa eneo hili?” Amour alimuuliza.
 
“Sisi tunaishi kule kando, hapa tunapita njia tu” Mtu huyo alijibu huku akionesha kuwa na wasiwasi
 
“Eti hapa mahali pana nyumba?”
 
“Hili ni eneo la makaburi tu, hakuna nyumba” Mtu huyo akamjibu.
 
“Hujawahi kuona nyumba mahali hapa jana au juzi?”
 
“Sijawahi kuona nyumba”
 
“Sisi tulikuta nyumba tulipokuja usiku” Koplo akasema.
 
“Eneo hili ni la makaburi tu” Yule mtu alisisitiza.
 
“Kwani jana usiku ulifika hapa?” Amour aliendelea kumuuliza.
 
“Jana sikuwahi kufika, nilipita leo alfajiri nikaona hawa polsi wamelala hapa, nikaona na ule mwili umekatwa kichwa…”
 
Alionesha mwili wa Sajenti Erick.
 
“Nani aliyepiga simu polisi?’
 
“Ni mimi. Nilipiga simu baada ya kuwaona hawa polisi wamelala hapa na pia ni baada ya kuona mtu aliyekatwa kichwa”
 
Inspekta Amour akatutazama.
 
“Huu ni mkasa mzito, huyu mtu tutamchukua kwa ajili ya ushahidi. Sasa tukibebe hiki kiwiliwili tukiingize kwenye gari”
 
Baada ya Inspekta Amour kutuambia hivyo tulikibeba kile kiwiliwili cha Sajenti Erick na kukiingiza kwenye gari tuliyokwenda nayo usiku.
 
“Tutarudi tena kwa ajili ya kulipiga picha hili eneo” Inspekta Amour akatuambia na kumuomba yule mtu aliyemuita tuende naye polisi ili akaandikishe maelezo yake na kisha angerudishwa kwa gari la polisi.
 
Baada ya hapo sote tulipanda kwenye magari tukaondoka. Kwa mbali nilihisi kichwa kikiniuma na ile hofu ya usiku bado ilikuwa ikitambaa kwenye mishipa yangu.
 
Nilijua nilipata hali hiyo kutokana na kutolala usiku kucha pamoja na lile taharuki la usiku. Lazima kichwa kiume na lazima mwili usisimke kwa hofu.
 
Tulifika kituo cha polisi tukashuka kwenye gari. Tulimkuta kamanda wa polisi na afisa upelelezi wakitusubiri. Inspekta Amour alikuwa amewapigia simu tukiwa ndani ya gari.
 
Mara tu tuliposhuka kwenye gari, maafisa hao walisogea kenye gari lililokuwa na kiwiliwili cha Sajenti Erick na kukitazama.
 
“Kichwa chake kiko wapi?” Kamanda wa polisi akauliza.
 
“Kichwa chake hakikupatikana” Inspekta Amour alimjibu.
 
Kamanda wa polisi akakunja uso.
 
“Kwani ilikuwaje? Hebu njoo huku ndani utueleze”
 
“Martin twende” Inspekta akaniambia.
 
Tukaingia ndani ya kituo. Kamanda wa polisi alituita kwenye ofisi ya mkuu wa kituo. Yeye na afisa upelelezi walikaa. Sisi tukawa wima.
 
“Hili tukio ni kubwa hebu tupeni maelezo, nini kilitokea?” Kamanda wa polisi akatuambia.
 
Inspekta Amour alieleza kwa upande wake. Alieleza nilivyompigia simu saa tisa usiku na kuomba msaada wa polisi.
 
“Alituambia yuko Magomeni na kwamba alitoroka kutoka katika nyumba moja ambako aliukuta mwili wa Sajenti Erick umekatwa kichwa. Na kwamba yeye mwenyewe pia amenusurika kukatwa kichwa na bado hayuko salama.
 
“Mimi baada ya kupata habari hii nilipata hofu kidogo nikatuma gari na askari sita muda ule ule. Ukapita muda wa kama nusu saa hivi Martin akanipigia simu tena akaniambia lile gari la polisi limempita, hawakumuona. Nikawapigia kuwajulisha kuwa wamempita Martin, warudi nyuma”
 
“Baada ya hapo kukawa kimya. Nilijaribu kupiga simu tena kuwaulizia lakini simu ikawa haipokelewi. Ilipokuwa inakaribia kuwa asubuhi mtu mmoja alitupigia simu akatuambia ameona polisi wamelala juu ya makaburi na kuna mtu mmoja amekatwa kichwa.
 
“Hapo nilichukua askari na gari na kuelekea eneo la tukio. Tulizunguka sana hadi tukafika katika eneo hilo. Tuliwakuta askari wamelala kwenye eneo la makaburi na kiwiliwili cha Sajenti Erick kipo hapo hapo”
 
Inspekta Amour aliendelea kueleza jinsi walivyotuona tukizinduka na kutuhoji maswali na sisi tukaeleza kilichotutokea.
 
Je nini kitafuata? Usikose kuendelea na hadithi hii hapo kesho.
Niko tayari kukupatia kila kinachonifikia mtu wangu muda na wakati wowote kupitia www.tangakumekucha.blogspot.com

No comments:

Post a Comment