HADITHI
YALIYONIKUTA TANGA (15)
ILIPOISHIA TOLEO LILILOPITA
Kamanda akanyamaza na kututazama.
Kikapita kimya kifupi kabla ya kukitanzua kimya hicho.
“Sasa andikisha maelezo yake,
yatawekwa kwenye faili la marehemu pamoja na maelezo yenu nyote” Kamanda
akamwambia Inspekta na kunigeukia mimi.
“Wewe utatupeleka katika hilo eneo, tutachukua
mpiga picha” akaniambia.
Wakati Inspekta anachukua
maelezo ya yule mwananchi, kamanda wa polisi na afisa upelelezi walitoka nje ya
kituo wakakikagua tena kiwiliwili cha Sajenti Erick kabla ya kuamuru kipelekwe
hospitali kwa uchunguzi zaidi.
Baada ya hapo aliitwa mpiga
picha wa polisi. Dakika chache baadaye kamanda wa polisi, afisa upelelezi,
mpiga picha wa polisi na mimi tulikuwa kwenye gari tukielekea katika eneo
lilipotokea tukio.
Nikiwa ndani ya gari nilikuwa
nimeinamisha kichwa changu kwa mawazo. Tukio hilo
lilikuwa limenitia fadhaa sana
na sikujua hatima yake ingekuwa nini.
Hofu yangu ilikuwa kuzuiwa
likizo yangu ambayo ningeianza siku mbili tu kutoka siku ile.
SASA ENDELEA
Tulipofika katika lile eneo
tulishuka kwenye gari, nikawaonesha maafande wangu mahali ilipokuwa ile nyumba.
“Nyumba ilikuwa hapa”
niliwambia.
“Kwa sasa ndiyo imeyayuka?”
Kamanda akauliza.
“Ni kama imeyayuka afande kwa
maana tulipozinduka hatukuiona tena”
“Na hilo kaburi lililokuwa na mwili wa marehemu
Erick ni lipi?”
Nikawaonesha kaburi hilo ambalo lilikuwa wazi.
“Ni hili hapa”
Kamanda akamwambia mpiga
picha wa polisi apige picha eneo hilo.
“Hili kaburi lilioko wazi
utalipiga picha peke yake” aliendelea kumueleza.
Wakati mpiga picha huyo
akiendelea kufyatua picha., afisa upelelezi alimwambia.
“Na hii sehemu inayodaiwa
ilikuwa nyumba usisahau kuipiga picha. Jaribu kupiga picha nyingi zaidi kwa
sehemu tofautu tofauti”
Tuliwa tumesimama katika eneo
hilo huku
kamanda wa polisi akiendelea kunihoji na picha zikiendelea kupigwa, watu
mmojammoja walianza kufika na kutuangalia wakiwa wamesimama kwa mbali.
Afisa upelelezi aliwaita
wakasogea karibu.
“Nyinyi ni wenyeji wa eneo
hili?” akawauliza.
“Ndio ni wenyeji wa eneo
hili” Kijana mmoja akamjibu.
“Nini kilitokea asubuhi hapa?”
“Palikuwa na polisi waliokuwa
wamelala juu ya makaburi”
“Wewe uliwaona?”
“Watu waliokuwa wakipita njia
wote waliwaona”
“Na labda mlijua polisi hao
walilala juu ya makaburi kwa sababu ya nini?”
“Hatukujua lakini polisi
wengine walifika asubuhi wakawaona”
“Eti hili eneo lina historia
gani?”
“Historia ya namna gani?”
“Inasemekana kuna miujiza
inatokea katika eneo hili ni kweli?
“Ni kweli. Siku nyingine
ukipita usiku hapa unakuta mambo ya ajabu”
“Kama
mambo gani?”
“Unaweza kukuta watu wamekaa
wanasoma wamevaa nguo nyepe tupu au unaweza kukuta mwanamke mrefu ananyonyesha
mtoto wake”
“Sasa nyinyi wenyeji wa hapa
mnayachukuliaje matukio kama hayo?”
“Hapa mahali kwa kweli kuna
majini. Wale polisi tuliowakuta wamelala hapa asubuhi bila shaka walikumbwa na
majini hao”
Mwanamke mmoja aliyekuwa
akisikiliza mazungumzo hayo aliingilia.
“Pana jini anaitwa Maimuna na
mama yake anaitwa Fatuma. Kuna siku wanaonekana lakini hawadhuru mtu”
“Hao majini wanapatikana kwa
wapi?”
“Eneo lao ndilo hili hapa
lakini huwezi kuwaona mpaka usiku”
“Usiku ndio wanaonekana?”
“Mara moja moja wanaonekana”
“Sawa. Asante sana”
Afisa upelelezi akamgeukia
kamanda wa polisi.
“Kinachonishangaza mimi ni
kuwa maelezo ya polisi waliokuja huku ni kwamba yule mwanamke waliyemuona ni yule
aliyekamatwa na kete za madawa ya kulevya na kufia mahabusi, sasa swali ninalojiuliza
muda wote je majini wanafanya biashara ya madawa ya kulevya?”
“Au si majini ni watu?”
Kamanda naye akauliza swali lake.
“Hapana ni majini kama wanavyosema hawa wenyeji wenyewe. Huyo Maimuna ndiye
yule msichana niliyewaeleza na yule mwanamke alituambia jina lake anaitwa
Fatuma kama alivyotueleza huyu msichana hapa”
nikasema.
“Kwa hiyo siku ile nyinyi
mlikamata majini?” Kamanda aliniuliza.
“Ndio, wale walikuwa majini”
nikasisitiza.
“Majini pia wanafanya
biashara ya madawa ya kulevya?’
Hapo sikuwa na jibu kwa
sababu yale madawa ya kulevya, Sajenti Erick aliwabambikia tu.
“Itabidi tufanye uchunguzi wa
kuthibitisha kama ni kweli hao majini ndio
walikuwa wakazi wa ile nyumba ya barabara ya nane alipokamatwa yule mwanamke”
afisa upelelezi akasema.
“Sasa suala la msingi ni
kutafuta ile nyumba ni ya nani na kama
tutakuta watu mle ndani wahojiwe ili watoe maelezo” Kamanda akaongeza.
“Sisi tunachofahamu ni kuwa
wanaojenga nyumba au kupangisha ni watu. Sasa kama majini pia wanamiliki nyumba
au kupangisha tutakwenda kujua vizuri” afisa upelelezi akasema.
Baada ya hapo tulirudi kwenye
gari tukaondoka. Kichwa changu kilikuwa kimevurugika sana. Ile kesi ilikuwa kama
imenilemelea mimi. Hoja za maafande wangu zilikuwa zikinitibua mtima. Nikahisi
kama vile mwisho wa siku nitakamatwa na kushitakiwa mimi.
Nilikuwa na hamu ya kuwaona
wazazi wangu na ndugu zangu huko kwetu Kagera lakini likizo yangu ilikuwa
kwenye hatari ya kufutwa kutokana na uchunguzi huo.
Sikudhani kama polisi
wangeniruhusu niende likizo wakati kulikuwa na tukio la uchunguzi kama lile
ambalo lilikuwa linanihusu sana.
Kwa kweli nilifikia mahali
nilijuta kutaka kuanzisha uhusiano na yule msichana ambaye sikuwa nikimfahamu.
Matokeo yake ndio hayo ya kukumbwa na mkasa ulioyatatanisha maisha yangu.
Nilijua kuwa kama polisi watashindwa kuyathibitisha maelezo yangu
watanihusisha mimi na mauaji ya Sajenti Erick. Na kama
nitahusishwa na mauaji hayo ni wazi kuwa nitashitakiwa mimi kwa kufunguliwa
kesi ya mauaji.
Je nini kitaendelea? Usikose
kufuatilia hadithi hii hapo kesho.
Nitahakikisha nakufikishia kila linalonifikia mtu wangu muda na wakati wowote kupitia www.tangakumekucha.blogspot.com
No comments:
Post a Comment