Sunday, January 4, 2015

KISIWA CHA HARISHI (25)


HADITHI
 
KISIWA CHA HARISHI (25)
 
Nikamwambia Yasmin “Tusifungue hii chupa tuone nini kitatokea”
 
“Wewe achana naye, kama akitoka mwenyewe na atoke, potelea mbali!”
 
Nilikuwa nimesimama kando ya lile kabati. Yasmin alisimama karibu na kitanda. Macho yetu sote yalikuwa kwenye ile chupa.
 
Ingawa nilikuwa nimejikaza kiume, hofu ilikuwa ikitambaa kwenye mishipa yangu. Yasmin hakuonesha kuwa na hofu hata chembe. Nilishangaa kuona msichana ambaye siku zote nilimuona dhaifu, siku ile alikuwa amejaa ujasiri usio kifani. Hapo niliamini kweli kuwa Yasmin alikuwa amejitolea kufa kupona.
 
Ile sauti ya Harishi iliyokuwa ikitoka kwenye chupa ilipotea lakini ule moshi uliendelea kuonekana. Kwanza ulionekana moshi wa rangi nyeusi kisha ukabadilika na kuwa wa rangi nyeupe. Baada ya muda kidogo ulibadilika tena na kuwa wa rangi nyeusi.
 
Mawazo yangu yote yalikuwa kwenye kifo kibaya kilichokuwa kinatungoja.
 
. Nilijua kuwa Harishi angekizibua mwenyewe kile kizibo na kutoka. Hapo hasira zake zisingekuwa na kifani. Nilipata wazo la kumwambia Yasmin tukimbie lakini nikajiuliza tutakimbilia wapi usiku ule? Na ni wapi ambapo Harishi hataweza kufika?
 
Muda uliendelea kupita. Tuliona Harishi hatoki kwenye ile chupa kama ilivyo kawaida yake. Aliendelea kututaka tukifungue kizibo kwa sauti ya upole akiahidi kwamba hatamuua yeyote.
 
Nikahisi inawezekana kwamba kitendo kile cha kuwahi kukifunga kile kizibo cha cha chupa wakati Harishi yumo ndani ya chupa ile akiwa katika umbile la moshi, kilikuwa kimemzuia kutoka na hakuwa na uwezo tena wa kutoka mwenyewe.
 
Hapo hapo nikazikumbuka simulizi za wazee wa zamani ziizosema kwamba majini walikuwa wakifungiwa ndani ya chupa na kutoswa baharini pindi wanapofanya makosa.
 
Kumbe ni kitu kinachowezekana kweli, nikajiambia.
 
“Sisi tunaiondoa hii chupa!” nikasema kwa sauti ili kusikia Harishi atajibu nini.
 
“Usiiondoe. Nataka mnifungulie niende zangu” Sauti ya Harishi ikasikika kutoka kwenye ile chupa.
 
“Hakuna atakayekufungulia muuaji wewe”Yasmin akamwambia.
 
“Nifungulie nitakurudisha kwenu”
 
“Mbona siku zote hukunirudisha?”
 
“Nakwambia kweli kabisa. Ukinifungulia nitakurudisha kwenu Comoro”
 
“Kwenda zako, mimi si mjinga wa kukufungulia wewe.. Bora ubaki humo humo. Siku zako zimeshafika”
 
Yasmin akanigeukia mimi na kuniambia.
 
“Twende tukaizike hii chupa”
 
“Hapana.. hapana. Msiizike!” Sauti ya Harishi ikalalamika.
 
“Mimi naona tukaizike baharini” nikamwambia Yasmin.
 
“Hapana…hapana. Msiitose baharini!” Ilikuwa sauti ya Harishi lakini hatukuipatiliza.
 
“Niliwahi kusikiakule kwetu kwamba majini wanafungiwa kwenye chupa na kutoswa baharini” nikamwambia Yasmin.
 
“Tukiitosa baharini itaelea na kisha itarudishwa ufukweni na mawimbi”
 
“Labda tuifunge kamba na jiwe ili izame chini”
 
“Nyinyi msifanye hivyo. Mimi nimeshwambia sitawaua. Nifungulieni niende zangu” Harishi akatuambia.
 
“Basi tutaifunga na jiwe tizamishe” Yasmin akasema.
 
“Hamsikii hivi ninavyowambia. Nyinyi mnataka mfe?” Sauti ya Harishi ikasikika kutoka kwenye chupa.
 
“Utakufa wewe, mbona huwezi kutoka !” Yasmin akamwambia.
 
“Tusubiri kuche” nilimwambia Yasmin.
 
“Linaweza likatoka!”
 
“Usiku huu hatutaweza kwenda baharini”
 
“Basi tusubiri”
 
Tukasubiri. Harishi sasa alikuwa amenyamaza. Sauti yake haikusikika tena. Lakini ule moshi uliendelea kuonekana ndani ya ile chupa. Ulikuwa unabadilika rangi kila mara.
 
Nipoona kunaanza kupambazuka nilijaribu kuishika ile chupa. Ilikuwa nyepesi kama chupa tupu.
 
Yasmin alileta kapu. Akaniambia tuitie kwenye kapu.
 
“Tutapata wapi kamba?” nikamuuliza.
 
“Twende nayo, tutapata kamba huko huko”
 
Tukatoka nje ya lile jumba. Mimi ndiye niliyeshika lile kapu. Kulikuwa na baridi kali lakini tulijikaza hivyo hivyo. Wakati tunaelekea baharini tuliokota kipande cha kamba na jiwe tukavitia kwenye kapu.
 
Tulipofika ufukweni mwa bahari tuliitoa ile kamba tukaifunga kamba kisha ile kamba tukaifunga na jiwe.
 
Tulimsikia Harishi akisema maneno ndani ya ile chupa lakini sauti yake ilikuwa ya chini kiasi kwamba hatukuelewa anasema nini.
 
Mimi na Yasmin tulijitosa kwenye maji. Tukatembea kwa miguu hadi tulipofika kwenye maji mengi tukaanza kuogelea kwenda mbali zaidi tukiwa na ile chupa tuliyoifunga jiwe.
 
“Tuizamishe hapa hapa” Yasmin akaniambia.
 
Nikaiachia ile chupa, ikazama ndani ya maji taratibu. Hatukuiona tena.
 
“Sasa turudi. Zama za Harishi zimekwisha” Yasmin akaniambia.
 
Tukaogelea kurudi ufukweni. Tulipofika ufukweni nilimwambia Yasmin.
 
“Sidhani kama atatoka tena”
 
“Hawezi kutoka. Labda atokee mtu aifungue ile chupa”
 
“Na huyo mtu atatokea wapi?”
 
“Labda wavuvi”
 
“Wavuvi ni watu wanaojua. Wakiona chupa chini ya bahari hawaifungui. Na pia hakuna wavuvi wanaofika huku”
 
“Lakini ni kitu cha ajabu. Ujanja wote ule alionao ameshindwa kujitoa kwenye chupa!”
 
“Ndio maana tunaambiwa kiumbe hakukamilika kwa maumbile wala kwa ujuzi. Mkamilifu ni Mungu peke yake”
 
“Tungejua mapema tungemfungia tangu tulipofika, tungesalimika sote”
 
“Hatukujua. Hata mimi ningeweza kumfungia. Sasa nimeshajua sababu ya kunisisitiza kila siku kuwa niweke mbali kile kizibo na nisiifunge hata siku moja”
 
ITAENDELEA KESHO,USIKOSE MTU WANGU NIKO TAYARI KUPOTEZA MUDA WANGU UPATE KILE UNACHOPENDA

No comments:

Post a Comment