Tuesday, August 2, 2016

HADITHI ,MWANAMKE SEHEMU YA 51

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI 0713 340572

MWANAMKE 51

ILIPOISHIA

Tukatoka tena. Tulijipakia kwenye gari tukaondoka.

Breki ya kwanza ilikuwa mbele ya hoteli moja iliyokuwa katika mtaa mwingine. Ilikuwa hoteli ndogo ya ghorofa moja, Ilikuwa imeandikwa kwa herufi kubwa. AL ASAD.

“Hii ndio hoteli ambayo nitakuachia wewe, itakuwa kama mali yako kwani tutakuwa tunagawana faida kila mwezi na kila mwaka kama utapenda kuendelea kubaki Somalia” Abdi aliniambia tukiwa bado tupo kwenye gari.

Alipoona nilikuwa nikiiangalia angalia ile hoteli, aliniambia.

“Tushuke uione vizuri”

Tukashuka.

Tuliingia ndani ya ile hoteli. Kwa kweli ilikuwa imechangamka.

“Sasa nani anaiendesha kwa hivi sasa?” nikamuuliza.

“Yuko mtu lakini nitamuondoa”

“Sasa ni kwanini umuondoe?”

“Lengo langu ni kukunufaisha wewe rafiki yangu au nimefanya kosa?’

“Hapana. Ni vizuri”

Abdi alinitembeza hoteli nzima kisha tukaingia katika ofisi ya meneja.

Meneja mwenyewe alikuwa mtu mzima. Kichwa chake kilishaanza kutoka mvi.

SASA ENDELEA

Walizungumza kwa kisomali huku meneja huyo akinikodolea macho.

Walizungumza kwa karibu robo saa kisha tukatoka.

“Yule ndiye meneja aliyeko sasa” Abdi aliniambia wakati tunatoka nje ya hoteli hiyo.

“Utamuhamishia mahali pengine au unammuondoa kabisa?’ nikamuuliza.

“Nitamfikiria”

“Umeshamwambia?”

“Nilitaka kwanza nikubaliane na wewe”

“Mimi nimeshakubali”

“Una uzoevu wa kuendesha hoteli?”

“Kwa kweli sina uzoefu huo”

“Utajifundisha hapa hapa. Ninaamini hutaweza kushindwa”

“Nitajaribu”

“Kazi yako itakuwa kuongoza na kukagua. Kuna kijana ambaye amesomea uendeshaji wa hoteli yuko pale atakusaidia”

“Nafikiri nitaweza. Usiwe na wasiwasi”

Baada ya hapo hatukuzungumza tena. Mwenzngu alikuwa amenyamaza, sikujua alikuwa akiwaza nini. Mimi nilikuwa na mawazo ya kubaki Somalia kuendesha shughuli ya hoteli.

Kikubwa kilichonipa tamaa ni kuwa kazi ya umeneja wa hoteli ni ya heshima na aliniambia kuwa angenipa ile nyumba pamoja na gari. Isitoshe tungegawana mapato ya hoteli..

Nilijiambia kama ningeweza kuchuma pesa pale Somalia na kurudi kwetu nikiwa na utajiri kama alivyoniahidi Abdi, sikuona haja ya kung’ang’ania kurudi Tanga ambako sikuwa na hakika kama nisingefukuzwa kazi kutokana na kutoonekana kazini kwa kipindi kirefu bila taarifa yoyote.

Abdi akanipeleka nyumbani kwake. Ilikuwa nyumba nzuri ya ghorofa moja iliyokuwa ndani ya geti. Mlinzi wake alitufungulia geti. Gari la abdi likaingia.

Kulikuwa na banda la magari lakini Abdi alilisimamisha gari hilo mbele ya mlango wa nyumba yake ya kifahari.

Tukashuka. Abdi alikwenda kufungua mlango akaniambia.

“Karibu kaka”

Tukaingia ndani. Alikuwa na sebule ya kupendeza iliyokuwa imepambwa vizuri kwa fanicha za thamani. Wakati tunaingia kulikuwa na msichana mmoja aliyekuwa akifanya usafi kwa kutumia kufaa maalum cha kuondoa vumbi.

“Karibu ukae” Abdi aliniambia huku naye akikaa. Akaongeza.

“Jisikie uko nyumbani. Hapa ndio kwetu bwana”

Nikawa natupa macho huku na huko kuiangalia sebule.

“Asante. Nimefurahi kupafahamu nyumbani kwako”

“Utakunywa kahawa?” Abdi akaniuliza.

“Hapana”

“Tangu uje Somalia sijakuonesha nyumbani kwangu. Hii nyumba ni yangu na mimi ninaishi hapa” Abdi aliendelea kuniambia kisha akaongeza.

“Unaweza kuona nyumba iko kimya kwa sababu watoto hawapo”

“Wako wapi?”

“Shemmeji yako amekwenda kwao Kismayuu. Mama yake ni mgonjwa. Atarudi pindi mama yake akipata nafuu”

Yule msichana aliyekuwa akifanya usafi alikuwa ameshaondoka.

“Nilipomuona huyu msichana nilidhani ndiye shemeji?”

“Hapana. Yule ni mfanyakazi wangu. Kwa sasa ninaishi na wafanyakazi wangu tu”

Hatukukaa sana hapo. Abdi akainuka na kuniambia.

“Sasa acha nikurudishe kule hoteli. Nataka niende shambani kwangu. Niliambiwa baadhi ya ng’ombe wangu ni wagonjwa”

Tukatoka na kujipakia tena kwenye gari, tukaondoka.

Abdi alinirudisha hotelini akaniacha na kuondoka. Niliingia chumbani nikaketi. Mawazo ya Zena yakaanza kunijia. Sikutaka kuendelea kumuwaza mwanamke huyo wa kijini lakini mawazo yake yalinijia kwa nguvu na sikuweza kuyazuia.

Kikubwa kilichosababisha nimuwaze ni kule kujitokeza nyumbani kwa yule mzee wa kisomali na kumpiga kibao yule mzee. Mpaka muda ule tukio lile lilikuwa kama kitendawili nilichoshindwa kukitegua.

Lakini jambo moja ambalo halikuwa na shaka akilini mwangu ni kwamba Abdi na yule mzee wa kisomali walikuwa wanajua ni kwanini Zena alitokea pale.

Kama walikuwa hawajui ni lazima Abdi angeonesha mshangao wake na angenieleza kitu. Lakini hakutaka kunieleza chochote kama vile ilikuwa ni siri.

Kadhalika sikuweza kujua yule mzee alikuwa ni nani, ana uhusiano gani na Abdi na kwanini nilimuota usiku akiniingiza ndani ya kaburi?

Pia nilijiuliza kile walichokuwa wanasoma pale ni kitu gani na kwanini kuliwekwa vitu mbalimbali kama vya uganga? Kwa kweli licha ya kujiuliza mara kadhaa sikupata jibu la kuridhisha.

Kwa vile sikuweza kuelewa kitu niliona nisiumize kichwa kwa kujiuliza maswali ambayo hayakuwa na majibu. Nikayaacha mawazo yale.

Siku ile sikumuona tena Abdi hadi siku ya pili yake ambapo alikuja hoteli asubuhi kunijulia hali.

“Nyumba yako itawekewa fanicha mpya leo. Kesho utaanza kuishi kule na kesho kutwa utakwenda kuanza kazi kule hotelini. Yule meneja ataondoka leo” Abdi akaniambia.

“Sawa”

“Amour unajua kuendesha?”

“Kuendesha nini?”

“Nina maana kuendesha gari”

“Ninajua lakini sikuja na leseni yangu”

“Si tatizo. Tutakwenda studio utapiga picha kadhaa za  paspoti, baadhi yake tutazitumia kukutengezea leseni ya hapa Somalia”

“Nitaipata lini hiyo leseni?’

“Kesho tu utaweza kuipata”

“Bila mimi mwenyewe kwenda kujaribiwa?”

“Hiyo kazi niachie mimi. Hata paspoti utapata bila kwenda wewe mwenyewe”

“Lakini hiyo paspoti itakuwa ya nchi gani?”

“Wewe ulitaka ya nchi gani?”

“Ya Tanzania”

“Utaipata bila shaka yoyote. Hapa kuna mabingwa wa kugushi. Nipe wiki moja tu. Utawekewa na mihuri ya tarehe uliyoingilia hapa Somalia”

Aliponiambia hivyo nilitabasamu.

“Inaonekana wewe hushindwi na kitu hapa Somalia” nikamwambia.

“Serikali yenyewe nimeiweka mikononi mwangu. Kuna maafisa wa polisi ambao wanakuja kuchukua mishahara kwangu kila mwezi kwa ajili ya kulinda miradi yangu. Wewe umeona mwenyewe juzi meno ya tembo tulivyoyaingiza na kuyapakia kwenye meli. Usifikiri kuwa polisi hawajui, wanajua. Baadhi ya mawaziri pia ni marafiki zangu. Likitokea tatizo niwapigia simu”

“Ninakuamini. Mambo yako ni makubwa!”

Nilipomsifu Abdi alicheka akanipa mkono. Alionekana kuwa ni mpenda sifa.

Tuliondoka hapo Hoteli tukaenda studio kupiga picha za papo kwa papo. Alichukua picha zangu kadhaa za usawa wa paspoti.

Wakati ananirudisha hotelini, nilimwambia kuwa nilikuwa ninahitaji saa.

“Saa tu, twende dukani tukanunue” akaniambia.

NAAM. MAMBO YANAZIDI KUPAMBA MOTO!

TUKUTANE TENA KESHO

No comments:

Post a Comment