Tuesday, February 6, 2018

UNA SIKU CHACHE ZA KUISHI SEHEMU YA 44

HADITHI

UNA SIKU CHACHE ZA KUISHI 44

ILIPOISHIA

Zainush alikuwa akitabasamu.

“Usimpe kero mama” Omar akamwambia Zainush.

“Namkera kwa ajili yako. Hutaki kunisikiliza mimi. Unamsikiliza mchumba wako aliyeko Ujerumani” Zainush akamwambia.

“Umar una mchumba Ujerumani?” Sauti ya Ummi Mariam ikasikika kutoka upande wa pili wa pazia.

“Nilikuwa naye lakini nimeamua kuachana naye”

“Afadhali uachane naye. Zainush atakusumbua na anaweza kumdhuru”

“Sitamuoa tena. Kwanza baba yake ndiye huyo rais wetu anayetaka kuniua”

“Mwache kabisa. Wewe kuwa na Zainush. Utakubali kumuoa Zainush?”

Omar hakujibu.

“Jibu sasa. Utakubali kunioa?” Zainush akamuuliza.


SASA ENDELEA


“Nitakubali” Omar akajibu.

“Mwache aseme kwa hiyari yake, usimlazimishe” Ummi Mariam akasema.

“Amesema amekubali”

“Eti Omar unakubali kwa hiyari yako?”

“Nimekubali” Omar akasema.

“Sawa. Sasa mtapanga wenyewe siku ya kuoana”

“Kwani ni lazima tuoane huku huku?” Omar akauliza.

“Ni hiyari yenu. Mtakavyoamua wenyewe”

“Basi tutapanga na Zainush”

“Sawa”

“Lakini unavyoona, ninaweza kuja kuwa rais?”

“Utakuwa lakini kwa sharti moja”

“Sharti gani?”

“Sharti hilo ni kwamba wakati wote ukuwa kwenye harakati zako uwe sambamba na Zainush” Ummi Mariam alimwambia Omar.

“Nakubaliana na hilo” Omar alimwambia huku akimkubalia kwa kichwa.

“Zainush ni mjanja na anaweza kujigeuza sura za watu mbalimbali. Naamini kwamba atakusaidia sana”

“Mara nyingi anapenda kujigeuza kama mimi na kwa kweli amenisaidia sana”

“Na ataendelea kukusaidia. Yeye anapenda sana uwe rais na yeye awe mke wako”

“Ameshaniambia hivyo”

“Halafu waangalie sana watu walio karibu yako. Baadhi yao ni watu waliopachikwa kukuhujumu wewe na kuhujumu chama chako”

“Mimi sitaweza kuwajua wote lakini nikiwa na Zainush nitaweza kuwajua”

“Usimtegemee  Zainush kwa kila kitu. Zainush ni kiumbe kama wewe. Kuna mambo mengine uwe makini nayo wewe mwenyewe. Umenielewa?”

“Nimekuelewa. Umesema sawa”

“Vile vile mtegemee Mungu”

“Ni kweli”

Pakapita kimya cha sekunde kadhaa kabla ya sauti ya Ummy Mariam kusikika tena.

“Sasa utarudi lini nyumbani kwako?”

Omar akamtazama Zainush.

“Eti Zainush utanirudisha lini?”

“Tutakwenda kupanga sasa hivi, inawezekana ikawa kesho au keshokutwa” Zainush akasema.

“Kwanini unamchelewesha?” Ummi Mariam akamuuliza.

“Ni kwa sababu ya usalama wake. Omar bado anatafutwa”

“Sawa lakini usimuweke sana huku, ukiona hali imekuwa shwari mrudishe haraka”

“Sawa maa”

“Umar urudi salama kwenu” Ummy Mariam alimuaga.

“Asante mama na wewe ukae salama”

“Mimi naitwa Ummy Mariam, mama yake Zainush”

“Nimefurahi kukufahamu”

“Na mimi pia nimefurahi kukufahamu. Ishaallah tutaonana tena”

“Panapo majaliwa”

“Haya Zainush, nendeni. Usiku mwingi, mwenzako anataka kulala” Ummy Mariam alimwambia Zainush.

“Mama naye! Kwani amekwambia ana usingizi?”

“Kwani mpaka aniambie, yeye ni binaadamu usiku analala, si jini kama wewe”

“Omar nyanyuka twende zetu” Zainush akamwambia Omar.

Omar akanyanyuka.

Wakatoka. Wakati wanarudi Zainush akamwambia Omar.

“Vipi unajisikia njaa?’

“Hapana, sihitaji kula saa hizi”

“Au unataka ugali uliouzoea kwenu?”

“Hapana, lile bokoboko nililokula bado nalisikia tumboni”

“Sasa unaonaje tukatembee kidogo?”

“Tukatembee usiku huu?’

“Huku kwetu harakati zinaendelea usiku na mchana”

“Tutakwenda kutembea wapi?”

“Twende gulioni. Nataka nikanunue asali”

“Ni mbali sana”

“Si mbali sana”

“Twende”

 Wakaenda. Kwa vile walikuwa wakitembea huku wakizungumza walikwenda mwendo mrefu bila Omar kujua. Omar aliona barabara za ujinini. Walipishana na punda waliobebeshwa mizigo. Zainush alimwambia Omar punda hao walikuwa wakitoka kwenye gulio.

Pia walipishana na watu mbalimbali weusi na weupe waliokuwa wamevaa mashuka kama waarabu na wengine wako na madevu hadi chini.

Kitu ambacho kilimshangaza Omar ni kuwa kila waliyepishana naye alikuwa na ndevu ndefu zilizokaribia kufika chini.

Zainusha alimtambulisha Omar kuwa hao walikuwa majini wakiwa kwenye harakati zao. Lakini majini hao hawakuwa wakizungumza. Kila mmoja alikuwa akiendelea na hamsini zake kimya kimya.

Hatimaye walifika hapo kwenye gulio. Ulikuwa uwanja ulioonekana kama jangwa. Kulikuwa na mkusanyiko mkubwa wa majini uliokuwa umeshamiri kelele.

Majini walikuwa wakinadi bidhaa zao na wengine wakiuza na kununua. Palikuwa na mitindo tofauti ya biashara, kuanzia ule wa kuuza kwa mnada, kuuza kwa kupatana bei na kuuza kwa kubadilishana vitu, toa mali upewe mali.

Zainush alimwambia Omar pesa zilizokuwa zinatumika ni za falme za  kiarabu, pesa ya India, Ujerumani na China.

“Kwanini zinatumika pesa hizo tu?” Omar akamuuliza.

“Kwa sababu majini hupenda kutembelea katika nchi hizo kununua vitu”

“Una maana bidhaa na vitu ninavyoviona hapa vimetoka katika nchi ulizotaja?”

“Baadhi yake si vyote, vingine vimetoka hapa hapa”

Kulikuwa na vyombo vya kaure na vilivyofinyangwa kwa udongo kama vile sahani, mabakuli, vyungu na mitungi.

Pia kulikuwa na ngozi za wanyama zilizokaushwa, mabusati, miswala, mazulia na vitu vingine ambavyo Omar hakufahamu matumizi yake.

Baada ya kuzunguka pande zote wakiwa wamefuatana pamoja, walitokea kwenye mnada wa asali na uyoga. Zainush akanunua kibuyu cha asali kwa real ya Oman yenye thamani ya shilingi elfu moja.


Wakati wanaondoka Omar alimuona mnunuzi akinunua ndama wa mbuzi kwa kutoa kuku wanne.

Kitu ambacho kilimchusha Omar ni harufu za majini hao ambazo Omar hakuwa amezizoea. Kama vile Zainush aliyaelewa mawazo ya Omar akamuuliza.

“Unasikia harufu tofauti?”

Omar akacheka kidogo.

“Kwanini umeniuliza hivyo?”

“Nimejua kuwa ni lazima utakuwa unasikia harufu ambayo hukuizoea”

“Ni kweli”

“Na wenzako pia wanakusikia wewe una harufu tofauti na wao. Wanakugundua wewe ni binaadamu kwa harufu yako ingawa wewe mwenyewe hujisikii”

“Una maana wameshanigundua kuwa si mwenzao?”

“Wameshakugundua lakini wanakuona uko na mwenyeji wako”

“Unilinde wasije wakanidhuru”

“Hakuna kitu kama hicho”

“Naona umetoa real, umeipata wapi?” Omar akayabadili yale mazungumzo.

“Umeishangaa ile? Mbona nina pesa nyingi za nchi za kiarabu”

“Unazipata wapi?”

“Kote huko ninafika. Wakati mwingine nikiishiwa ninaiba”

“Unaiba? Unaibaje?”

“Ninaiba benki usiku. Ninaingia bila kuonekana na kutoka na pesa”

“Kumbe unafanya hivyo?”

“Lakini mama yangu hajui na sipendi ajue. Unataka kuonja kidogo?”

Zainush alikuwa akiramba ile asali.

“Hebu nipe”

Zainush akampa Omar kile kibuyu cha asali. Omar naye akaionja.

“Tamu kweli”

Hapo hapo kibuyu kikaporwa juu kwa juu. Aliyekipora alikimbia nacho.

Je ni nani aliyekipora kibuyu hicho na nini kitatokea? Usikose toleo lijalo

Monday, December 25, 2017

HADITHI, MWANAUME WA KIJINI SEHEMU YA 2

SITASAHAU NILIVYOKUMBANA NA MWANAUME WA KIJINI 2

ILIPOISHIA

Nilipomtajia namba yangu aliiandika kwenye simu yake kisha akanipigia hapo hapo.

Simu yangu ilipoita aliniambia.

“Namba  yangu ndiyo hiyo, ahsante sana”

Hakurudi tena kwenye meza yake akatoka. Kwa vile mtu aliyefanya niamue kuondoka alishatangulia kutoka nikaona niendelee kukaa kidogo.

Lakini sikutimiza hata nusu saa nikainuka na kutoka. Nilirudi nyumbani kwa teksi. Nikafikia kuoga na kujilaza kitandani.
Wakati usingizi unataka kunichukua, simu yangu ikaita. Nilipoichukua na kutazama kwenye sikrini ya simu niliona namba ya yule mzungu. Nikaipokea simu yake.

“Hello!” nikasema kwenye simu.

SASA ENDELEA

“Hello! Mambo vipi?” Sauti ya yule mzungu ikasikika kwenye simu. Nilifurahi alivyoniuliza “Mambo vipi?” Niliona alikuwa mzungu aliyebobea katika lugha ya Kiswahili.

“Poa” Na mimi nikamjibu kwa kutumia lugha ile ile ya mitaani.

“Uko poa kabisa?” akaniuliza.

“Mimi niko poa, sijui wewe?”

“Mimi pia niko poa. Umesharudi nyumbani?”

Mara moja nikagundua kuwa mzungu huyo alikuwa anataka kurefusha mazungumzo.

“Nimesharudi. Hapa niko kitandani” nikamjibu.

“Samahani sana. Mimi naitwa Mr Smith, sijui mwenzangu unaitwa nani?”

“Naitwa Enjo”

“Okey. Jina lako zuri sana. Unaishi wapi?”

“Naishi Sinza”

“Unafanya kazi?”

“Hapana. Kwa sasa niko nyumbani tu”

“Okey. Mimi ni Muingreza. Ninapenda kuja Afrika Mashariki mara kwa mara kutembea. Huwa ninafikia hoteli tu”

“Ndio…ndio”

“Nimefurahi kukufahamu Enjo na ninapenda uwe rafiki yangu”

“Kuna aina nyingi za urafiki, wewe umependelea urafiki wa aina gani?”

“Urafiki wowote tu lakini tutazungumza zaidi tutakapokutana. Enjo una mchumba?”

“Sina mchumba”

“Vizuri. Unadhani tunaweza kukutana wapi kwa ajili ya mazungumzo zaidi”

“Sema wewe”

“Mimi si mwenyeji sana hapa Dar”

“Umefikia katika hoteli gani?”

“Hoteli ya Lux hapa Masaki. Niko chumba namba 35. Unaweza kufika.

Mzungu kanitajia hadi namba  ya chumba chake akidhani ningeweza kwenda kwake.

“Kwanini tusikutane mahali pengine?” nikamwambia.

“Tunaweza. Sasa sema wewe ni mahali gani”

“Ngoja, kesho nitakupigia kukufahamisha”

“Kesho saa ngapi”

Nikafikiri kidogo kisha nikamjibu.

“Kesho mchana”

“Ningefurahi zaidi kama utanitajia saa ili nisubiri simu yako”

“Tuweke saa tano”

“Sawa. Nipige mimi au utanipigia wewe?”

“Nitakupigia mimi”

“Sawa. Nitasubiri simu yako saa tano”

“Nashukuru. Usiku mwema”

“Usiku mwema na kwako”

Nikatangulia mimi kukata simu kisha nikaiweka kwenye kimeza cha mchagoni. Baadaye niliona niizime kabisa kwani sikupenda nikatishwe usingizi wangu kwa milio ya simu.

Usingizi haukuchelewa kunipitia, nikalala. Wakati niko usingizini nikaota niko kwenye ufukwe wa bahari mimi na yule mzungu tukikimbizana huku tukirushiana michanga. Sote wawili tulikuwa tumevaa mavazi hafifu ya kuogelea.

Mimi nilivaa chupi na sidiria yake na mzungu alivaa chupi peke yake. Lakini rangi ya chupi yake na yangu zilikuwa zikifanana.

Baada ya kufukuzana na kuangushana kwa dakika kadhaa tuliingia kwenye maji na kuanza kuogelea kwa pamoja. Tuliogelea hadi tukafika maji mengi.

Mimi nilikuwa nyuma, yule mzungu alikuwa mbele yangu. Ghafla tukajikuta tuko katikati ya bahari. Ule ufukwe wa bahari hatukuuona tena.


Itaendelea kesho hapahapa kuwa nami

Saturday, December 23, 2017

SITASAHAU NILIVYOKUTANA NA MWANAMKE WA KIJINI (1 )

SITASAHAU NILIVYOKUMBANA NA MWANAUME WA KIJINI

Nilichozoea kusikia ni kwamba kuna majini wanawake wanaojigeuza binaadamu na kuwatongoza wanaume.

Wengi wa majini hao hutaka kuishi na  binaadamu kama mke na mume jambo ambalo baadhi ya watu linawavutia kutokana na tamaa ya kupata utajiri.

Lakini nimekuja gundua kuwa hawapo majini wanawake pekee,  bali pia wapo majini wanaume ambao huwatongoza wanawake wa kibinaadamu na kutaka waishi nao kama mume na mke.

Hilo ndilo lililonitokea mimi na kuniingiza katika mkasa uliyoyatatanisha maisha yangu. Nilifikia mahali sasa nilitamani kufa.

Jina langu naitwa Enjo, ukipenda Engle. Ni mtoto wa tatu katika familia ya mzee Sabastian Chacha. Wa kwanza alikuwa mwanaume. Jina lake ni Raymond au Ray kama marafiki zake walivyozoea kumuita.

Yeye anafanya kazi Uingreza. Ameshaoa na ana watoto wawili. Wa pili alikuwa mwanamke kama mimi, anaitwa Miriam. Anaishi Dar ninapoishi mimi, naye pia ameshaolewa na ana mtoto mmoja.

Kwa wanaomkumbuka mzee Sabastian Chacha aliwahi kuwa mkuu wa wilaya ya Handeni kisha akawa mbunge wa jimbo la Kibaha iliko nyumba yetu.

Mzee Chacha alifariki dunia miaka michache iliyopita kwa ajali ya gari. Miaka miwili baadaye mama yetu naye alifariki ghafla katika hospitali ya Muhimbili kutokana na shinikizo la damu.

Baada ya masomo yangu ya chuo kikuu nilipata kazi wizara ya afya. Haikutimia hata miaka miwili nilifukuzwa kazi kutokana na sababu ambayo haikuelezwa wazi.

Lakini nilijua kuwa nilitofautiana na bosi wangu aliyekuwa akinitaka kimapenzi nikamkataa. Yeye ndiye aliyenisingizia madai ya kuwa mzembe hadi nikafukuzwa kazi.

Kulikuwa na mwanaume Mzanzibari ambaye nilikuwa na matarajio naye sana kwamba angekuja kunioa. Yeye alikuwa akisoma huko Uingreza. Kwa vile alikuwa na ndugu zake huko ambao walikuwa wakijiweza, alikuwa akinitumia pesa mara kwa mara.

Wakati ule nafanya kazi nilipangisha nyumba huko Sinza. Hiyo nyumba tulichangia watu wawili. Upande mmoja alipangisha mtu mmoja aliyekuwa na familia yake na upande mwingine nilipangisha mimi lakini tulikuwa tunatumia mlango mmoja.

Siku moja nilikuwa nimealikwa katika hafla moja iliyokuwa ikifanyika katika hoteli moja kule Masaki.

Watu tulikuwa tumekaa kwenye viti tukipata vinywaji. Katika meza ya pembeni kwangu aliketi mzungu mmoja aliyekuwa akinitazama sana.

Mzungu huyo alikuwa amevaa suti iliyokuwa imempendeza sana na alikuwa amejifunga kikuba cha rangi nyekundu shingoni. Jinsi alivyokuwa amezichonga vyema ndevu zake alionekana kama muungwana na mtu aliyejistahi sana.

Alikuwa akinywa kinywaji chake taratibu huku jicho lake likiwa  upande wangu.

Sikuweza kujua ni kwanini alikuwa akinitazama sana. Kwanza nilidhania pengin e alikuwa amenifananisha na  mtu aliyekuwa anamfahamu au aliniona mahali fulani na alikuwa akijaribu kunikumbuka.

Lakini nilipomuangalia ili niweze kumuelewa vyema alikuwa akikwepesha macho yake na kutazama upande mwingine. Na ninapogeuza uso wangu anaanza tena kunitazama bila kujua kuwa nilikuwa nikimtazama kwa pemebeni mwa macho yangu.

Kusema kweli alinikosesha raha. “Kama amenipenda angeniambia tu kuliko kunitazama vile” nikajiambia kimoyo moyo nikiwa nimekasirika.

Kwa vile muda ulikuwa umepita sana niliona bora niondoke nirudi nyumbani. Lakini kama aliyekuwa amesoma mawazo yangu aliinuka haraka akanifuata nilipokuwa nemeketi na kuniambia.

“Samahani dada, kuna kitu nataka kukuomba” akanimabia kwa kiswahili fasaha.
Nikahisi alikuwa mzungu mwenyeji kwani alikuwa akiifahamu vyema lugha yetu.

“Bila samahani, niombe tu” nikamjibu.

“Lakini natanguliza samahani, sijui kama utaridhika”

“Niambie tu, ni kitu gani?”

“Naomba namba yako”

Nilielewa kuwa alikusudia namba yangu ya simu kwa sababu hiyo ni tabia ya wanaume wengi, lakini nikamuuliza.

“Namba yangu ya….?”

“Nilikuwa na maana namba yako ya simu”

“Kama ni hilo tu hakuna tatizo” nikamwambia.

Nikampa namba yangu. Nilimpa ili anipigie na kunieleza kile alichokuwa nacho moyoni mwake.


itaendelea kesho usikose

Tuesday, November 14, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI

HADITHI
MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI
ILIPOISHIA
Mke wa Waziri Mkuu alishaanza kushituka.
“Tukio gani tena hilo?”
“Linamuhusu yeye”
“Ndiyo ni tukio gani. Hebu nieleze”
Maria akamueleza mkasa mzima uliotokea tangu alivyomuona Sofia akimfyonza damu mwanafunzi mwenzao ndani ya choo cha shule mpaka polisi walivyofika.
“Mama yangu wee!” Mke wa Waziri Mkuu akamaka.
“Yaani mimi nilishangaa sana, sijui Sofia amepatwa na nini!”
“Huyo mwanafunzi amekufa?”
“Amekufa lakini mwili wake bado uko hospitali”
“Yesu wangu, sasa ikawaje?’
SASA ENDELEA
“Baada ya kile kitendo Sofia alipotoka chooni alikwenda kukaa chini ya mti nyuma ya shule, nikamuuliza Sofia una nini. Akaniambia anasikia kichwa kinamuuma lakini kile kitendo alichokifanya alikuwa hakijui kabisa”
Mke wa waziri Mkuu alikuwa akiguna tu.
“Wakati nazungumza naye, yule mwanafunzi aligunduliwa kule chooni. Walimu wakaenda kumuona. Mkuu wa shule akapiga simu polisi. Polisi wakafika”
“Enhe..?”
“Wanafunzi tukaulizwa nani anayejua kilichompata mwenzetu, kila mmoja akasema hajui lakini mimi sikusema kitu. Nilinyamaza kimya. Wanafunzi wanne waliokuwa wamekaa na Sofia kabla ya tukio hilo wakachukuliwa polisi pamoja na mkuu wa shule”
“Walichukuliwa kama washukiwa au…?’
“Walichukuliwa kwenda kuandikisha maelezo kisha walirudishwa”
“Sofia mwenyewe hakuulizwa kitu?’
“Hakuulizwa kwa sababu hakuonekana, niliyemuona ni mimi peke yangu na sikumwambia mtu”
“Asante sana mwanangu, ngoja nimuite baba yake naye umueleze”
Mke wa Waziri Mkuu aliondoka akaingia ndani. Baadaye kidogo alirudi akiwa amefuatana na mheshimiwa Waziri Mkuu.
“Hujambo Maria?” Waziri Mkuu akamsalimia Maria huku akiketi.
“Sijambo, shikamoo”
“Marahaba. Habari za nyumbani?’
“Nzuri”
“Wazazi hawajambo?”
“Hawajambo”
“Kumetokea nini huko shule?”
“Kumetokea mambo ya ajabu sana?’
“Enhe…hebu nieleze”
Maria akamueleza.
Uso wa Waziri Mkuu ulionesha wazi kutaharuki.
“Mbona sisi hatukupata taarifa yoyote kuhusu Sofia?” akamuuliza Maria.
“Haikufahamika kwamba Sofia ndiye aliyefanya kile kitendo. Nilimuona peke yangu na sikumwambia mwalimu yeyote”
“Huyo mwanafunzi amekufa?’
“Amekufa”
Waziri Mkuu akatikisa kichwa kusikitika.
“Una hakika kwamba uliyemuona akifanya hivyo ni Sofia?”
“Ni Sofia. Baadaye nilimuuliza lakini alionekana kama hajui alichokitenda”
“Labda amepatwa na malaria iliyompanda kichwani”
“Inawezekana kwa sababu alisema kichwa kinamuuma”
Kimoyo moyo Waziri Mkuu alikuwa akijiambia ile juhudi yote iliyofanyika usiku wa jana yake kijijini kwao ambako ngo’ombe watatu walichinjwa kwenye mzimu, hazikuwa na manufaa yoyote.
“Mwanangu umefanya jambo zuri kulifanya jambo hilo kuwa ni siri. Hakuna mtu yeyote uliyemueleza?’ mke wa Waziri Mkuu akamuuliza.
Maria akatikisa kichwa.
“Sikumueleza mtu yeyote. Nimekuja kuwaeleza nyinyi ili mjue kuwa Sofia ana matatizo”
“Asante sana. Imekuwa vyema umemuona wewe rafiki yake, je kama angekuwa mtu mwingine ingekuwaje?” Waziri Mkuu akamuuliza.
“Angesema”
“Ingekuwa ni tatizo”
“Sasa huko alikokwenda sijui itakuwaje?” mke wa waziri Mkuu akauliza kama aliyekuwa akijiuliza mwenyewe.
Hakukuwa na aliyemjibu.
“Alipokuja hapa sisi tulimuona yuko sawa tu” Waziri Mkuu akasema na kuongeza.
“Kama tungegundua kuwa ana tatizo tusingemruhusu kuondoka”
“Tumuombee tu, atarudi salama” Maria akawambia.
“Ametutia wasiwasi sana lakini tunakushukuru wewe kwa kuja kutufahamisha hilo. Kwa hiyo kutoka sasa tutakuwa na tahadhari naye” Waziri Mkuu akasema.
“Sasa mwanangu nakusisitiza sana kuwa endelea kumfichia siri rafiki yako. Usimueleze mtu yoyote. Ujue ukimueleza mtu rafiki yako atakamatwa” Mke wa waziri mkuu akamwambia Maria.
“Sitamueleza mtu yeyote”
“Huyo aliyekufa amekufa kwa sababu muda wake ulikuwa umeshawadia” waziri Mkuu akasema.
“Ni kweli. Kila mtu anakufa kwa wakati wake”
Waziri mkuu alitia mkono ndani ya mfuko wa ndani wa koti lake akatoa kitita cha noti. Alihesabu shilingi laki moja akampa Maria.
“Mwanangu chukua hizi pesa, ni zawadi yako”
“Asante sana, nashukuru”
“Akirudi tutamwambia kuwa rafiki yako alikutembelea lakini hakukukuta”
“Ndio, mumpe salamu zangu”
“Na tutamshughulikia kumpatia matibabu”
“Itakuwa vizuri kwani ile hali inatisha”
Waziri Mkuu alitoa gari lake la binafsi pamoja na dereva wake kumrudisha maria nyumbani kwao Sinza.
Mara tu maria alipoondoka Waziri Mkuu alimwambia mke wake.
“Ule uganga aliofanyiwa haukusaidia kitu”
“Ni hasara tupu”
“Sasa tatizo linakuwa kubwa. Ameanza kufyonza wanafunzi wenzake shuleni. Atasoma vipi?”
“Itabidi tumsimamishe masomo”
“Atakubali?’
“Tutamlazimisha”
“Sawa. Sasa kesho utamzuia mwanano asiende shule hadi hapo tutakapomruhusu. Na mimi nitamtuma msaidizi wangu aende shuleni kuwapa taarifa ya kumsimamisha masomo Sofia kwa ajili ya matibabu ya afya yake” Waziri Mkuu alimwambia mke wake.
“Wakiambiwa kwamba tunamsimamisha masomo kwa ajili ya afya yake watahoji ana matatizo gani”
“Sasa tuwaambieje?”
“Waambiwe tu kuwa tunamsimamisha masomo kwa muda. Unadhani kuna atakayekuhoji?”
“Sidhani”
“Basi iwe hivyo”
Wakati wa magharibi ulikuwa umeshaingia, Sofia aliporudi nyumbani. Alimkuta mama yake sebuleni.
“Mama nimerudi” alimwambia.
“Ma mdogo wako hajambo?”
“Hajambo, anawasalimia”
Sofia akaketi kando ya mama yake.
“Sofia nataka kukuuliza, hivi shuleni kwenu kulitokea nini leo?”
“Hata sijapatiliza, niliona polisi tu. Mkuu wa shule alichukuliwa na polisi pamoja na wanafunzi watano”
 Walipelekwa wapi?”
“Walikwenda kuandikisha maelezo kisha walirudishwa”
“Walikwenda kuandkisha maelezo ya nini?”
“Nilisikia kuna mwanafunzi aliyefia chooni lakini simjui. Mwenyewe kichwa kilikuwa kinaniuma, sikupatiliza”
“Huyo mwananfunzi alikufaje?’
Sofia akabetua mabega yake.
“Sijui mama. Kwani wewe umejuaje?’
“Nimeambiwa”
“Umeambiwa na nani?”
“Baba yako alipigiwa simu akaelezwa”

itaendelea kesho hapahapa Usikose uhondo huu