Monday, December 25, 2017

HADITHI, MWANAUME WA KIJINI SEHEMU YA 2

SITASAHAU NILIVYOKUMBANA NA MWANAUME WA KIJINI 2

ILIPOISHIA

Nilipomtajia namba yangu aliiandika kwenye simu yake kisha akanipigia hapo hapo.

Simu yangu ilipoita aliniambia.

“Namba  yangu ndiyo hiyo, ahsante sana”

Hakurudi tena kwenye meza yake akatoka. Kwa vile mtu aliyefanya niamue kuondoka alishatangulia kutoka nikaona niendelee kukaa kidogo.

Lakini sikutimiza hata nusu saa nikainuka na kutoka. Nilirudi nyumbani kwa teksi. Nikafikia kuoga na kujilaza kitandani.
Wakati usingizi unataka kunichukua, simu yangu ikaita. Nilipoichukua na kutazama kwenye sikrini ya simu niliona namba ya yule mzungu. Nikaipokea simu yake.

“Hello!” nikasema kwenye simu.

SASA ENDELEA

“Hello! Mambo vipi?” Sauti ya yule mzungu ikasikika kwenye simu. Nilifurahi alivyoniuliza “Mambo vipi?” Niliona alikuwa mzungu aliyebobea katika lugha ya Kiswahili.

“Poa” Na mimi nikamjibu kwa kutumia lugha ile ile ya mitaani.

“Uko poa kabisa?” akaniuliza.

“Mimi niko poa, sijui wewe?”

“Mimi pia niko poa. Umesharudi nyumbani?”

Mara moja nikagundua kuwa mzungu huyo alikuwa anataka kurefusha mazungumzo.

“Nimesharudi. Hapa niko kitandani” nikamjibu.

“Samahani sana. Mimi naitwa Mr Smith, sijui mwenzangu unaitwa nani?”

“Naitwa Enjo”

“Okey. Jina lako zuri sana. Unaishi wapi?”

“Naishi Sinza”

“Unafanya kazi?”

“Hapana. Kwa sasa niko nyumbani tu”

“Okey. Mimi ni Muingreza. Ninapenda kuja Afrika Mashariki mara kwa mara kutembea. Huwa ninafikia hoteli tu”

“Ndio…ndio”

“Nimefurahi kukufahamu Enjo na ninapenda uwe rafiki yangu”

“Kuna aina nyingi za urafiki, wewe umependelea urafiki wa aina gani?”

“Urafiki wowote tu lakini tutazungumza zaidi tutakapokutana. Enjo una mchumba?”

“Sina mchumba”

“Vizuri. Unadhani tunaweza kukutana wapi kwa ajili ya mazungumzo zaidi”

“Sema wewe”

“Mimi si mwenyeji sana hapa Dar”

“Umefikia katika hoteli gani?”

“Hoteli ya Lux hapa Masaki. Niko chumba namba 35. Unaweza kufika.

Mzungu kanitajia hadi namba  ya chumba chake akidhani ningeweza kwenda kwake.

“Kwanini tusikutane mahali pengine?” nikamwambia.

“Tunaweza. Sasa sema wewe ni mahali gani”

“Ngoja, kesho nitakupigia kukufahamisha”

“Kesho saa ngapi”

Nikafikiri kidogo kisha nikamjibu.

“Kesho mchana”

“Ningefurahi zaidi kama utanitajia saa ili nisubiri simu yako”

“Tuweke saa tano”

“Sawa. Nipige mimi au utanipigia wewe?”

“Nitakupigia mimi”

“Sawa. Nitasubiri simu yako saa tano”

“Nashukuru. Usiku mwema”

“Usiku mwema na kwako”

Nikatangulia mimi kukata simu kisha nikaiweka kwenye kimeza cha mchagoni. Baadaye niliona niizime kabisa kwani sikupenda nikatishwe usingizi wangu kwa milio ya simu.

Usingizi haukuchelewa kunipitia, nikalala. Wakati niko usingizini nikaota niko kwenye ufukwe wa bahari mimi na yule mzungu tukikimbizana huku tukirushiana michanga. Sote wawili tulikuwa tumevaa mavazi hafifu ya kuogelea.

Mimi nilivaa chupi na sidiria yake na mzungu alivaa chupi peke yake. Lakini rangi ya chupi yake na yangu zilikuwa zikifanana.

Baada ya kufukuzana na kuangushana kwa dakika kadhaa tuliingia kwenye maji na kuanza kuogelea kwa pamoja. Tuliogelea hadi tukafika maji mengi.

Mimi nilikuwa nyuma, yule mzungu alikuwa mbele yangu. Ghafla tukajikuta tuko katikati ya bahari. Ule ufukwe wa bahari hatukuuona tena.


Itaendelea kesho hapahapa kuwa nami

Saturday, December 23, 2017

SITASAHAU NILIVYOKUTANA NA MWANAMKE WA KIJINI (1 )

SITASAHAU NILIVYOKUMBANA NA MWANAUME WA KIJINI

Nilichozoea kusikia ni kwamba kuna majini wanawake wanaojigeuza binaadamu na kuwatongoza wanaume.

Wengi wa majini hao hutaka kuishi na  binaadamu kama mke na mume jambo ambalo baadhi ya watu linawavutia kutokana na tamaa ya kupata utajiri.

Lakini nimekuja gundua kuwa hawapo majini wanawake pekee,  bali pia wapo majini wanaume ambao huwatongoza wanawake wa kibinaadamu na kutaka waishi nao kama mume na mke.

Hilo ndilo lililonitokea mimi na kuniingiza katika mkasa uliyoyatatanisha maisha yangu. Nilifikia mahali sasa nilitamani kufa.

Jina langu naitwa Enjo, ukipenda Engle. Ni mtoto wa tatu katika familia ya mzee Sabastian Chacha. Wa kwanza alikuwa mwanaume. Jina lake ni Raymond au Ray kama marafiki zake walivyozoea kumuita.

Yeye anafanya kazi Uingreza. Ameshaoa na ana watoto wawili. Wa pili alikuwa mwanamke kama mimi, anaitwa Miriam. Anaishi Dar ninapoishi mimi, naye pia ameshaolewa na ana mtoto mmoja.

Kwa wanaomkumbuka mzee Sabastian Chacha aliwahi kuwa mkuu wa wilaya ya Handeni kisha akawa mbunge wa jimbo la Kibaha iliko nyumba yetu.

Mzee Chacha alifariki dunia miaka michache iliyopita kwa ajali ya gari. Miaka miwili baadaye mama yetu naye alifariki ghafla katika hospitali ya Muhimbili kutokana na shinikizo la damu.

Baada ya masomo yangu ya chuo kikuu nilipata kazi wizara ya afya. Haikutimia hata miaka miwili nilifukuzwa kazi kutokana na sababu ambayo haikuelezwa wazi.

Lakini nilijua kuwa nilitofautiana na bosi wangu aliyekuwa akinitaka kimapenzi nikamkataa. Yeye ndiye aliyenisingizia madai ya kuwa mzembe hadi nikafukuzwa kazi.

Kulikuwa na mwanaume Mzanzibari ambaye nilikuwa na matarajio naye sana kwamba angekuja kunioa. Yeye alikuwa akisoma huko Uingreza. Kwa vile alikuwa na ndugu zake huko ambao walikuwa wakijiweza, alikuwa akinitumia pesa mara kwa mara.

Wakati ule nafanya kazi nilipangisha nyumba huko Sinza. Hiyo nyumba tulichangia watu wawili. Upande mmoja alipangisha mtu mmoja aliyekuwa na familia yake na upande mwingine nilipangisha mimi lakini tulikuwa tunatumia mlango mmoja.

Siku moja nilikuwa nimealikwa katika hafla moja iliyokuwa ikifanyika katika hoteli moja kule Masaki.

Watu tulikuwa tumekaa kwenye viti tukipata vinywaji. Katika meza ya pembeni kwangu aliketi mzungu mmoja aliyekuwa akinitazama sana.

Mzungu huyo alikuwa amevaa suti iliyokuwa imempendeza sana na alikuwa amejifunga kikuba cha rangi nyekundu shingoni. Jinsi alivyokuwa amezichonga vyema ndevu zake alionekana kama muungwana na mtu aliyejistahi sana.

Alikuwa akinywa kinywaji chake taratibu huku jicho lake likiwa  upande wangu.

Sikuweza kujua ni kwanini alikuwa akinitazama sana. Kwanza nilidhania pengin e alikuwa amenifananisha na  mtu aliyekuwa anamfahamu au aliniona mahali fulani na alikuwa akijaribu kunikumbuka.

Lakini nilipomuangalia ili niweze kumuelewa vyema alikuwa akikwepesha macho yake na kutazama upande mwingine. Na ninapogeuza uso wangu anaanza tena kunitazama bila kujua kuwa nilikuwa nikimtazama kwa pemebeni mwa macho yangu.

Kusema kweli alinikosesha raha. “Kama amenipenda angeniambia tu kuliko kunitazama vile” nikajiambia kimoyo moyo nikiwa nimekasirika.

Kwa vile muda ulikuwa umepita sana niliona bora niondoke nirudi nyumbani. Lakini kama aliyekuwa amesoma mawazo yangu aliinuka haraka akanifuata nilipokuwa nemeketi na kuniambia.

“Samahani dada, kuna kitu nataka kukuomba” akanimabia kwa kiswahili fasaha.
Nikahisi alikuwa mzungu mwenyeji kwani alikuwa akiifahamu vyema lugha yetu.

“Bila samahani, niombe tu” nikamjibu.

“Lakini natanguliza samahani, sijui kama utaridhika”

“Niambie tu, ni kitu gani?”

“Naomba namba yako”

Nilielewa kuwa alikusudia namba yangu ya simu kwa sababu hiyo ni tabia ya wanaume wengi, lakini nikamuuliza.

“Namba yangu ya….?”

“Nilikuwa na maana namba yako ya simu”

“Kama ni hilo tu hakuna tatizo” nikamwambia.

Nikampa namba yangu. Nilimpa ili anipigie na kunieleza kile alichokuwa nacho moyoni mwake.


itaendelea kesho usikose

Tuesday, November 14, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI

HADITHI
MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI
ILIPOISHIA
Mke wa Waziri Mkuu alishaanza kushituka.
“Tukio gani tena hilo?”
“Linamuhusu yeye”
“Ndiyo ni tukio gani. Hebu nieleze”
Maria akamueleza mkasa mzima uliotokea tangu alivyomuona Sofia akimfyonza damu mwanafunzi mwenzao ndani ya choo cha shule mpaka polisi walivyofika.
“Mama yangu wee!” Mke wa Waziri Mkuu akamaka.
“Yaani mimi nilishangaa sana, sijui Sofia amepatwa na nini!”
“Huyo mwanafunzi amekufa?”
“Amekufa lakini mwili wake bado uko hospitali”
“Yesu wangu, sasa ikawaje?’
SASA ENDELEA
“Baada ya kile kitendo Sofia alipotoka chooni alikwenda kukaa chini ya mti nyuma ya shule, nikamuuliza Sofia una nini. Akaniambia anasikia kichwa kinamuuma lakini kile kitendo alichokifanya alikuwa hakijui kabisa”
Mke wa waziri Mkuu alikuwa akiguna tu.
“Wakati nazungumza naye, yule mwanafunzi aligunduliwa kule chooni. Walimu wakaenda kumuona. Mkuu wa shule akapiga simu polisi. Polisi wakafika”
“Enhe..?”
“Wanafunzi tukaulizwa nani anayejua kilichompata mwenzetu, kila mmoja akasema hajui lakini mimi sikusema kitu. Nilinyamaza kimya. Wanafunzi wanne waliokuwa wamekaa na Sofia kabla ya tukio hilo wakachukuliwa polisi pamoja na mkuu wa shule”
“Walichukuliwa kama washukiwa au…?’
“Walichukuliwa kwenda kuandikisha maelezo kisha walirudishwa”
“Sofia mwenyewe hakuulizwa kitu?’
“Hakuulizwa kwa sababu hakuonekana, niliyemuona ni mimi peke yangu na sikumwambia mtu”
“Asante sana mwanangu, ngoja nimuite baba yake naye umueleze”
Mke wa Waziri Mkuu aliondoka akaingia ndani. Baadaye kidogo alirudi akiwa amefuatana na mheshimiwa Waziri Mkuu.
“Hujambo Maria?” Waziri Mkuu akamsalimia Maria huku akiketi.
“Sijambo, shikamoo”
“Marahaba. Habari za nyumbani?’
“Nzuri”
“Wazazi hawajambo?”
“Hawajambo”
“Kumetokea nini huko shule?”
“Kumetokea mambo ya ajabu sana?’
“Enhe…hebu nieleze”
Maria akamueleza.
Uso wa Waziri Mkuu ulionesha wazi kutaharuki.
“Mbona sisi hatukupata taarifa yoyote kuhusu Sofia?” akamuuliza Maria.
“Haikufahamika kwamba Sofia ndiye aliyefanya kile kitendo. Nilimuona peke yangu na sikumwambia mwalimu yeyote”
“Huyo mwanafunzi amekufa?’
“Amekufa”
Waziri Mkuu akatikisa kichwa kusikitika.
“Una hakika kwamba uliyemuona akifanya hivyo ni Sofia?”
“Ni Sofia. Baadaye nilimuuliza lakini alionekana kama hajui alichokitenda”
“Labda amepatwa na malaria iliyompanda kichwani”
“Inawezekana kwa sababu alisema kichwa kinamuuma”
Kimoyo moyo Waziri Mkuu alikuwa akijiambia ile juhudi yote iliyofanyika usiku wa jana yake kijijini kwao ambako ngo’ombe watatu walichinjwa kwenye mzimu, hazikuwa na manufaa yoyote.
“Mwanangu umefanya jambo zuri kulifanya jambo hilo kuwa ni siri. Hakuna mtu yeyote uliyemueleza?’ mke wa Waziri Mkuu akamuuliza.
Maria akatikisa kichwa.
“Sikumueleza mtu yeyote. Nimekuja kuwaeleza nyinyi ili mjue kuwa Sofia ana matatizo”
“Asante sana. Imekuwa vyema umemuona wewe rafiki yake, je kama angekuwa mtu mwingine ingekuwaje?” Waziri Mkuu akamuuliza.
“Angesema”
“Ingekuwa ni tatizo”
“Sasa huko alikokwenda sijui itakuwaje?” mke wa waziri Mkuu akauliza kama aliyekuwa akijiuliza mwenyewe.
Hakukuwa na aliyemjibu.
“Alipokuja hapa sisi tulimuona yuko sawa tu” Waziri Mkuu akasema na kuongeza.
“Kama tungegundua kuwa ana tatizo tusingemruhusu kuondoka”
“Tumuombee tu, atarudi salama” Maria akawambia.
“Ametutia wasiwasi sana lakini tunakushukuru wewe kwa kuja kutufahamisha hilo. Kwa hiyo kutoka sasa tutakuwa na tahadhari naye” Waziri Mkuu akasema.
“Sasa mwanangu nakusisitiza sana kuwa endelea kumfichia siri rafiki yako. Usimueleze mtu yoyote. Ujue ukimueleza mtu rafiki yako atakamatwa” Mke wa waziri mkuu akamwambia Maria.
“Sitamueleza mtu yeyote”
“Huyo aliyekufa amekufa kwa sababu muda wake ulikuwa umeshawadia” waziri Mkuu akasema.
“Ni kweli. Kila mtu anakufa kwa wakati wake”
Waziri mkuu alitia mkono ndani ya mfuko wa ndani wa koti lake akatoa kitita cha noti. Alihesabu shilingi laki moja akampa Maria.
“Mwanangu chukua hizi pesa, ni zawadi yako”
“Asante sana, nashukuru”
“Akirudi tutamwambia kuwa rafiki yako alikutembelea lakini hakukukuta”
“Ndio, mumpe salamu zangu”
“Na tutamshughulikia kumpatia matibabu”
“Itakuwa vizuri kwani ile hali inatisha”
Waziri Mkuu alitoa gari lake la binafsi pamoja na dereva wake kumrudisha maria nyumbani kwao Sinza.
Mara tu maria alipoondoka Waziri Mkuu alimwambia mke wake.
“Ule uganga aliofanyiwa haukusaidia kitu”
“Ni hasara tupu”
“Sasa tatizo linakuwa kubwa. Ameanza kufyonza wanafunzi wenzake shuleni. Atasoma vipi?”
“Itabidi tumsimamishe masomo”
“Atakubali?’
“Tutamlazimisha”
“Sawa. Sasa kesho utamzuia mwanano asiende shule hadi hapo tutakapomruhusu. Na mimi nitamtuma msaidizi wangu aende shuleni kuwapa taarifa ya kumsimamisha masomo Sofia kwa ajili ya matibabu ya afya yake” Waziri Mkuu alimwambia mke wake.
“Wakiambiwa kwamba tunamsimamisha masomo kwa ajili ya afya yake watahoji ana matatizo gani”
“Sasa tuwaambieje?”
“Waambiwe tu kuwa tunamsimamisha masomo kwa muda. Unadhani kuna atakayekuhoji?”
“Sidhani”
“Basi iwe hivyo”
Wakati wa magharibi ulikuwa umeshaingia, Sofia aliporudi nyumbani. Alimkuta mama yake sebuleni.
“Mama nimerudi” alimwambia.
“Ma mdogo wako hajambo?”
“Hajambo, anawasalimia”
Sofia akaketi kando ya mama yake.
“Sofia nataka kukuuliza, hivi shuleni kwenu kulitokea nini leo?”
“Hata sijapatiliza, niliona polisi tu. Mkuu wa shule alichukuliwa na polisi pamoja na wanafunzi watano”
 Walipelekwa wapi?”
“Walikwenda kuandikisha maelezo kisha walirudishwa”
“Walikwenda kuandkisha maelezo ya nini?”
“Nilisikia kuna mwanafunzi aliyefia chooni lakini simjui. Mwenyewe kichwa kilikuwa kinaniuma, sikupatiliza”
“Huyo mwananfunzi alikufaje?’
Sofia akabetua mabega yake.
“Sijui mama. Kwani wewe umejuaje?’
“Nimeambiwa”
“Umeambiwa na nani?”
“Baba yako alipigiwa simu akaelezwa”

itaendelea kesho hapahapa Usikose uhondo huu

Friday, November 10, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI SEHEMU YA 26


MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI 26
ILIPOISHIA
Sofia akatikisa kichwa kusikitika.
Pakapita ukimya wa sekunde kadhaa.
“Sasa wewe nenda zako kajisomee. Hao polisi wakifika utaitwa”
“Sawa baba. Watakuja muda huu?’
“Muda wowote kutoka sasa”
“Haya, mimi nakwenda”
Sofia akanyanyuka na kuondoka. Akili yake ilikuwa imeshachanganyikiwa. Tangu alipoanza kufyonza watu alikuwa akisikia harufu ya damu midomoni mwake mara tu anaporejewa na akili yake.
Alipomfyonza mpishi wa nyumbani kwao alisikia harufu ya damu midomoni mwake. Alipomfyonza dada yake alisikia harufu ya damu midomoni mwake. Alipomfyonza mwanafunzi mwenzake alisikia harufu ya damu midomoni mwake na alipomfyoza muuguzi wa hospitali ya Dk Deo pia alisikia harufu ya damu.
SASA ENDELEA
Ingawa hakuwa na kumbukumbu zozote kichwani mwake za kumfyonza mtu damu lakini hali ile ilimpa maswali mengi.
Alikuwa akijiuliza kwanini linapotokea tukio kama lile, yeye anasikia harufu ya damu midomoni mwake?
Mawazo yake yalikwenda mbali zaidi, akajiuliza ni kwanini alikatizwa masomo baada ya tukio la kufyonzwa damu kwa mwanafunzi mwenzake? Kwanini alipelekwa kijijini na kuaguliwa? Kwanini wakati fulani alipelekwa Nairobi kupimwa akili yake?
Maswali  yote hayo yalipitita akilini mwa Sofia bila kuwa na majibu.
Akaingia chumbani mwake na kuendelea kujisomea.
Baada ya saa moja makachero wawili wakawasili nyumbani kwa Waziri Mkuu.
Kachero Kembo na Inspekta Alex walikaribishwa sebuleni kwa Waziri Mkuu.
Wakaeleza dhumuni lao kuwa ni kupata maelezo kutoka kwa Waziri Mkuu, mke wake na mwanawe kuhusiana na tukio lililotokea katika hospitali ya Dk Deo, asubuhi ya siku ile.
Waziri Mkuu akawafahamisha kuwa walikuwa tayari kutoa maelezo.
Thabit Kembo alifungua jalada alilokuwa nalo mikononi akaandika tarehe ya siku ile kisha akaandika jina la Waziri Mkuu.
“Mheshimiwa tutaanza na wewe” kembo akamwambia baada ya kuandika.
“”Anza”
“Tunaomba utueleze nini kilitokea katika hospitali ya Dk Deo leo asubuhi”
“Sisi tulifika pale hospitali kumjulia hali rafiki wa mwanangu na mwanafunzi mwenzake ambaye anaumwa”
“Mwanao huyo anaitwa nani?” Kembo akamuuliza.
“Anaitwa Sofia”
“Na huyo mgonjwa mliyekwenda kumjulia hali ni nani?”
“Anaitwa Maria, ni mdogo wake Dk Deo”
“Dk Deo huyu ambaye amehusika na hili tukio?”
“Ndio”
“Endelea”
“Nataka uelewe kwamba tulikwenda pale kama raia wa kawaida kumjulia hali mgonjwa”
“Ndiyo”
Waziri Mkuu akaendelea kueleza jinsi walivyomuona mgonjwa huyo wakiongozwa na muuguzi mmoja wa hospitali hiyo ambaye hakuwa akimfahamu jina lake.
Akaendelea kueleza baada ya kumuona mgonjwa walihitaji kupata maelezo kutoka kwa daktari anayemtibu kwa vile mgonjwa mwenyewe bado hakuwa na hali nzuri na hakuweza kutoa maelezo.
“Muuguzi tuliyekuwa naye alitoka mle chumbani kwenda kumuita daktari lakini alichelea sana kurudi kiasi kwamba tuliamua kutoka kumfuata” Waziri Mkuu aliendelea kueleza.
“Wakati huo mlikuwa watu wanagapi?’
“Nilikuwa mimi, mke wangu na mwanangu Sofia”
“Endelea kueleza, baada ya kutoka nini kilitokea?”
“Tulipofika katika mlango wa ofisi ya Dk Deo, tuliukuta mlango ukiwa wazi. Tukamuona Dk Deo akiwa ndani ya ofisi yake amemshikilia yule muuguzi huku meno yake yakiwa kwenye shingo ya muuguzi huyo na pale shingoni palikuwa panatoka damu” Waziri Mkuu alieleza.
“Ulihisi alikuwa anamfanya nini?”
“Nilihisi kama alikuwa anamfyonza damu”
“Baada ya hapo nini kilitokea?’
“Yule muuguzi alianguka chini, ndipo nilipomuuliza Dk Deo unafanya nini? Akaanza kubabaika. Hakujua kuwa kulikuwa na watu wanamuona?”
“Baada ya kumuuliza hivyo na kubabaika, ulichukua hatua gani?’
“Nilipiga simu polisi, polisi wakafika na kumchukua”
Kembo alimaliza kuandika maelezo ya Waziri Mkuu kisha alimwambia.
“Dk Deo baada ya kuhojiwa alitupa maelezo tofauti”
“Aliwambia uongo gani?” Waziri Mkuu akamuuliza huku macho yake yakimeta kwa taharuki.
“Alitueleza kwamba, yeye hakuwako ofisini kwake lakini wakati anarudi ofisini kwake alimkuta Sofia akitoka mle ofisini…”
“Huo ni uongo mtupu, Sofia tulikuwa naye sisi” Waziri Mkuu akadakia.
“Alitueleza kwamba licha ya kwamba yeye na Sofia walikua wanajuana lakini Sofia hakumsemesha chochote, alimpita kama vile alikuwa hamjui. Alipoingia ofisini kwake ndipo alipomkuta yule muuguzi amelala chini huku damu ikitoka kwenye shingo yake…”
“Yule dakatari ni muongo sana tena hafai kabisa. Sisi tumemuona waziwazi akifanya unyama wake halafu anamsingizia mwanangu! Mwanangu alifuata nini ofisini kwake wakati tulikuwa naye sisi?” Waziri Mkuu alifoka.
“Sawa. Tutachukua pia maelezo kutoka kwa Sofia lakini kabla ya yeye ni vizuri pia tupate maelezo ya mama yake kwa vile alikuwepo katika tukio”
“Sawa”
Kembo akamgeukia mke wa waziri Mkuu.
“Tupe maelezo yako, nini ulikishuhudia hapo hospitali asubuhi”
Mke wa Waziri mkuu alieleza kama alivyoeleza mume wake. Kembo baada ya kumaliza kuandika alitaka aitwe Sofia.
Mama yake ndiye aliyekwenda kumuita. Alimkuta Sofia amepitiwa na usingizi. Akamuamsha na kumwambia kuwa maafisa wa upelelkezi wameshafika kuchukua maelezo ya tukio lililotokea katika hospitali ya Dk Deo.
“Haya mama nakuja” sofia akamwambia.
Mke wa Waziri Mkuu aliporudi sebuleni Sofia alikuwa nyuma yake.
“Kaa kwenye kochi” Waziri Mkuu alimwambia.
Sofia akakaa.
“Hujambo?” Kembo akamsalimia.
“Sijambo, habari ya kazi?’
“Nzuri, za masomo?’
“Pia ni nzuri”
“Sawa. Sisi ni maafisa wa idara ya polisi ya upelelezi. Tunahitaji maelezo yako kuhusiana na tukio lililotokea leo asubuhi kwenye hospitali ya Dk Deo. Uko tayari kutueleza nini kilitokea?’
“Niko tayari”
“Sawa, anza kutueleza”
“Kuna rafiki yangu ambaye amelazwa pale hospitali akiugua malaria. Leo asubuhi tulikwenda kumsalimia…”
“Mlikwenda nani na nani?’
“Mimi, baba na mama”
“Mlipofika mlimuona huyo mgonjwa?”
“Ndio tulimuona”
“Alikuwa na hali gani?”
“Kwa kweli hali yake haikuwa nzuri, alikuwa hawezi hata kuzungumza”
“Endelea kueleza”
“Yule muuguzi aliyetupeleka alikwenda kumuita daktari ili atupe maelezo kuhusu mgonjwa”
“Ndiyo”
Hapo Sofia alisita akawa anafikiria alivyofundishwa na baba yake.
Kitendo hicho kilimuudhi Waziri Mkuu akamkazia macho Sofia.
“Eleza kilichotokea baada ya hapo” akamwambia.
“Ndio naeleza baba. Yule muuguzi hakurudi tena” Sofia akasema huku akiendelea kufikiri.
“Mlichukua hatua gani?” Kembo akamuuliza.
“Na sisi tukatoka kumfuata daktari”
“Mlimfuata wapi?”
“Ofisini kwake”
“Je mlimkuta?”

ITAENDELEA kesho Usikose Uhondo huu hapahapa kumekucha.com

Thursday, November 9, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONIO, SEHEMU YA 24

 
MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI 24
 
ILIPOISHIA
 
Waziri Mkuu akamueleza kwamba kuna muuguzi ameuawa  na daktari wake.
“Sawa mheshimiwa, tunakuja”
Waziri Mkuu alipomaliza kuzungumza na mkurugenzi wa upelelezi alitoka nje ya hospitali hiyo akiwa amefuatana na mke wake.
Walikuta Dk Deo amepakiwa katika gari la polisi huku mmoja wa polisi hao akiwasiliana kwa radio Call na polisi wenzake.
Wasiwasi wa Waziri Mkuu na mke wake ulikuwa kwa Sofia, hawakujua lipotoka katika ofisi ya Dk Deo alikwenda wapi.
Lakini walipokwenda kwenye gari lao walimkuta amejipakia katika siti ya nyuma na alikuwa amelala. Kwenye mdomo wake wa chini alikuwa na chembechembe za damu.
SASA ENDELEA
Mke wa Waziri Mkuu alifungua mlango wa gari akajipakia. Alifungua mkoba wake akatoa kitambaa na kuifuta midomo ya Sofia kisha alikikunja kitambaa hicho na kukirudisha kwenye mkoba.
Waziri Mkuu hakuingia kwenye gari. Alibaki nje ya gari akihaha huku na huku. Baadhi ya wauguzi na madaktari walikuwa wakitoka na kuingia ndani ya hospitali hali iliyoonesha taharuki.
Hakukuwa na yeyote miongoni mwao aliyefahamu nini kimetokea.
Muda usio mrefu, magari matatu ya polisi na makachero yakawasili. Gari la kwanza lilikuwa la mkurugenzi wa Upelelezi. Gari la pili lilikuwa na mchanganyiko wa makachero na polisi na gari la tatu lilitoka kituo kikuu cha polisi baada ya polisi walokuwa wakifuatana na Waziri Mkuu kuwapigia radio call.
Polisi na makachero hao waliokuwa zaidi ya kumi walishuka na kusogea alipokuwa amesimama Waziri Mkuu.
Waziri Mkuu alimueleza Mkurugenzi wa upelelezi kuhusu tukio lililokuwa limetokea akimuhusisha Dk Deo kumshambulia muuguzi wake.
“Polisi wamemkamata, yuko kwenye hili gari” alimwambia huku akimuonesha gari hilo.
Akaongeza. “Muuguzi aliyemfanyia unyama huo yuko ofisini kwake”
Mkurugenzi wa Upelelezi alisogea kwenye gari hilo akamtazama Dk Deo kisha alimwambia atoke kwenye gari. Alipotopka alimwambia.
“Twende ukatuoneshe huyo muuguzi wako”
“Lakini mimi sijamfanyia kitendo chochote kibaya, nilimkuta ofisini kwangfu akiwa ameshajeruhiwa” Dk Deo alijitetea.
“Muongo mkubwa. Nilimuona kwa macho yangu akimpopotoa” Waziri Mkuu alisema.
Mkurugenzi wa Upelelezi akampiga kibao Dk Deo kabla ya kumwambia.
“Twende ukatuoneshe huyo muuguzi wako”
Kabla ya Dk Deo kuinua hatua alitandikwa kibao kingine na kusukumwa. Mkurugenzi wa Upelelezi alikuwa amemshika kiunoni.
Wakati Dk Deo akiwapeleka ofisini kwake, Waziri Mkuu alifuata nyuma.
Walipofika ofisini humo, Waziri Mkuu aliwaonesha yule muuguzi aliyekuwa amelala chini. Ile damu iliyokuwa ikimvuja shingoni sasa ilikuwa imeganda.
“Huyo achukuliwe apelekwe hospitali ya Muhimbili kufanyiwa
uchunguzi” akawambia.
Baada ya polisi kumkagua na kumpiga picha, walimbeba na kutoka naye. Alipakiwa kwenye gari mojawapo la polisi. Dk Deo alipakiwa kwenye gari jingine.
Makachero kadhaa pamoja na polisi walibaki pale hospitali na kuanza kuwahoji madaktari wengine na wauguzi kuhusu kilichokuwa kimempata mwenzao.
Mwili wa muuguzi huyo ulipelekwa hospitali ya Muhimbili. Dk Deo alipelekwa kituo kikuu cha polisi. Waziri Mkuu, mke wake pamoja na Sofia waliondoka na kurudi nyumbani.
Walimuacha Sofia aende akalale chumbani mwake. Waziri Mkuu na mke wake wakakaa sebuleni.
“Kama nisingetumia mbinu ile ya kumsingizia yule dakatari, leo Sofia angebainika kuwa ndiye mfyonza damu na angekamatwa kutokana na ushahidi wa yule dokta” Waziri Mkuu alimwambia mke wake.
“Angekamatwa kwa sababu ingeonekana wazi kuwa ndiye aliyemfyonza damu. Aliondoka naye kule chumbani akangoja alipoingia mle ofisini akamshika…”
“Hili sasa limekuwa balaa!”
Mke wa Waziri Mkuu akatikisa kichwa.
“Sijui kama mwanangu atarejea katika hali yake ya kawaida!” alisema na kuongeza.
“Juhudi kubwa zimefanyika lakini bado hali inatia mashaka, sijui tufanye nini?’
“Sijui mke wangu, nimechanganyikiwa! Yaani nimelazimika kuokoa jahazi kwa kumbambikia yule daktari kosa la Sofia”
“Kwani atashitakiwa?’
“Lazima ashitakiwe kwa mauaji, najua tutapambana sana mahakamani lakini nitatumia kila mbinu kuhakikisha haepuki ile tuhuma”
“Sasa Sofia tutampeleka wapi?”
“Tutamrudisha kijijini akae huko huko chini ya uangalizi. Tutakodi watu wa kuwa naye wakati wote kuhakikisha hafyonzi watu. Ile damu inaweza kumuua. Damu nyingine si salama”
Ili kumkandamiza zaidi Dk Deo, Waziri Mkuu alimpigia simu Waziri wa Mambo ya Ndani akamueleza kuhusu lile tukio akidai alimshuhudia kwa macho yake Dk Deo akimfyonza damu muuguzi wake hadi kumuua.
Baada ya kumpigia Waziri wa Mambo ya Ndani, Waziri Mkuu alimpigia Mkuu wa Jeshi la Polisi.
“Nimeshapata taarifa mheshimiwa na hivi sasa tunalifanyia uchunguzi tukio hilo” Mkuu wa Jeshi la Polisi alimwambia Waziri Mkuu mara tu alipomdokeza kuhusu tukio hilo.
“Kama mmeanza kufanya uchunguzi ni vizuri. Yule mtu ni katili sana”
“Kumekuwa na matukio ya ufyonzwaji damu hapa nchini, tutachunguza kuona kama ni yeye aliyehusika”
“Itakuwa ni yeye, wasomi wengine wanafanya kazi zao kwa kutegemea ushirikina”
“Hilo suala tunalifanyia kazi mheshimiwa”
“Tunataka haki itendeke na mhakikishe kwamba anapelekwa mahakamani mara tu uchunguzi wenu ukikamilika”
“Asante mheshimiwa”
Wakati huo hospitali ya Dk Deo ilikuwa imezingirwa na makachero na kuwekwa chini ya ulinzi wa polisi. Mwili wa muuguzi aliyefyonzwa damu na Sofia ulifanyiwa uchunguzi haraka haraka katika hospitali ya Muhimbili na matokeo ya uchunguzi huo yalitolewa kwa polisi.
Uchunguzi huo mbali ya kuthibitisha kifo cha muuguzi huyo ulieleza kuwa kifo hicho kilitokana na marehemu kufyonzwa damu nyingi mwilini mwake kupitia katika jereha lililokuwa kwenye shingo yake ambalo lilitokana na kuumwa meno ya binaadamu.
Taarifa hiyo ya madaktari ndio iliowapa polisi taharuki. Ile dhana kwamba Dk Deo ndiye mfyonza damu za binaadamu iliwafanya polisi wamng’ng’anie kama ruba.
Mbali ya hospitali yake kuwekwa chini ya ulinzi wa polisi, makachero walianza kuwahoji madaktari na wauguzi wa hospitali hiyo.
Madaktari na wauguzi wote waliohojiwa walieleza kuwa hawakuliona tukio hilo linalodaiwa kufanywa na Dk Deo.
Pia walieleza kwamba hawaamini kuwa Dk Deo anafyonza watu damu.
Baada ya kutoridhishwa na maelezo ya madaktari na wauguzi hao, makachero walianza kuwahoji wagonjwa waliokuwa wamelazwa katika hospitali hiyo.
Wagonjwa hao pia hawakuwa na maelezo ya kuwatosheleza polisi kuhusiana na tuhuma zilizokuwa zinamkabili Dk Deo. Mkurugenzi wa Upelelezi akaja na dhana nyingine. Aliwataka makachero hao kuifanyia upekuzi hospitali hiyo kwa hofu kwamba Dk Deo anaweza kuwa ananunua viungo vya binaadamu ambavyo anavitumia katika shughuli zake za kishirikina.
Upekuzi huo ulifanywa lakini hakukuwa na kiungo chochote kilichopatikana.
Dk Deo mwenyewe alihojiwa kwa saa kadhaa. Alichokuwa akikieleza kilikuwa hakikubaliwi na polisi ambao tayari walishajenga hisia kwamba Dk Deo ni mfyonza damu.
Dk Deo alieleza kwamba wakati tukio hilo linatokea hakuwepo ofisini. Lakini wakati anarudi ofisini mwake alimuona Sofia binti wa Waziri Mkuu akitoka ofisini mwake.
“Nilipoingia ofisini mwangu nikamuona muuguzi wangu akiwa chini huku akitokwa na damu shingoni. Nilipomchunguza vizuri nikagundua kuwa alikuwa na jeraha ambalo sikuweza kujua ni la kitu gani.
“Nikaondoka pale pale kumfuata yule msichana aliyetoka mle ofisini ili nimuulize nini kilitokea ndio hapo nilipomuona Waziri Mkuu na mke wake wamesimama mbele ya mlango wakinitazama. Waziri Mkuu akaanza kunishutumu kuwa nimemfyonza damu muuguzi wangu jambo ambalo si kweli”
“Sofia binti wa Waziri Mkuu alikuwa amefuata nini ofisini kwako?” Thabit kembo, mmoja wa makachero waliokuwa wakimhoji Dk Deo alimuuliza.
“Sijui”
“Je wewe ulikutana na Waziri Mkuu alipofika hospitalini kwako?’
“Sikukutana naye na wala sikuwa na taarifa kuwa waziri Mkuu anakuja hospitalini kwangu”
“Baada ya Waziri Mkuu kukwambia kwamba amekuona umemfyonza damu muuguzi wako, alichukua hatua gani?’
“Aliita polisi wanikamate na hakunipa nafasi ya kujitetea”
 
ITAENDELEA kesho hapa hapa kumekucha.com