Sunday, April 30, 2017

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 16

ZULIA LA FAKI
 
NILIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 18
 
ILIPOISHIA
 
“Maana yake mtu amekufa halafu anakuja  kuonekana tena”
 
“Sasa yule si mtu yule yule”
 
“Ni nani sasa?”
 
“Kwanza mtu akifa hawezi kuonekana tena”
 
“Mbona mimi nimemuona Ummy?”
 
“Uliyemuona si Ummy”
 
“Ni yeye. Licha ya  kunielekeza kwao alinipa  namba ya simu yake na nilimuonesha ndugu yake pale nyumbani kwao akasema ni namba  ya Ummy kweli”
 
“Kwani ulifika kwao kumuulizia?’
 
“Ndiyo, nilifika jana”
 
“Wakakuambia nini?”
 
“Wakaniambia hivyo hivyo kwamba Ummy alikufa”
 
“Si ndiyo nilivyokueleza mimi?”
 
SASA ENDELEA
 
Nilihisi kwamba maelezo ya Mzaramu badala ya  kunisaidia yalizidi kunichanganya. Mzaramu hakutaka  kukubaliana na miimi kwamba niliyemuona alikuwa ni Ummy wakati nilikuwa na imani kuwa niliyekutana naye alikuwa  ni Ummy Nasri.
 
Kitu muhimu kilichonifanya niamini kuwa niliyemuona  ni Ummy Nasri  aliyedaiwa kufa ni ile picha ya Ummy niliyooneshwa na baba yake huku mdogo wake akikiri kwamba namba ya simu niliyopigiwa na Ummy ilikuwa namba  ya Ummy kweli. Mdogo wake  huyo alikuwa ameikariri.
 
Sasa kulikuwa na vitu viwili vilivyonitia mawazo. Kwanza ni yale maelezo ya Mzaramu kwamba Ummy kabla ya kufa alikuwa na uhusiano na mzee mmoja  ambaye Mzaramu alinithibitishia kuwa ndiye yule niliyemuonesha katika  picha iliyokuwa kwenye simu yangu.
 
Picha  hiyo  ilikuwa ni ya babu yangu marehemu mzee Limbunga. Hivyo maelezo ya Mzaramu yalionesha kwamba babu yangu alikuwa na uhusiano na Ummy.
 
Kitu cha pili kilichoniitia  mawazo ni maelezo ya Ummy kwamba anazijua siri za  malli ya babu yangu.  Inawezekana kweli anaijua siri ya mali ya babu yangu kwa vile alikuwa na uhusiano naye. Ila kinachotatanisha hapo ni kuwa Ummy mwenyewe anadaiwa kuwa alishakufa.
 
Yakanijia mawazo yale yale kwamba niliouona ulikuwa mzuka wa Ummy, yaani iliwezekana kuwa Ummy alishakufa kweli lakini nilichokutana nacho kilikuwa kivuli chake. Nilishasikia hadithi nyingi za watu waliokufa kuonekana tena ikidaiwa kuwa ni mizuka  ya watu hao.
 
Lakini mara nyingi mizuka hiyo  inapotokea inakuwa na sababu.
 
Sasa nikajiambia labda nijaribu kutafuuta sababu ya kutokea kwa mzuka wa Ummy ambaye aliwaua watu wote waliokuwa wakidaiwa na  babu yangu na kusababisha nisilipwe pesa ambazo ningelipwa na watu hao.
 
Nikajiuliza kama Ummy alikuwa mzuka ni kwanini aliwaua  watu hao  halafu aniambie kuwa anaijua siri ya mali ya babu yangu na kutaka nikutane naye?
 
Kwa kweli kila  nilivyowaza  niliona sivyo na kila nilivyojiuliza sikupata jibu. Hapo ndipo nilipozidi kuchanganyikiwa.
 
“Mbona umeduwaa rafiki yangu?”  Mzaramu akaniuliza akiwa hajui yaliyokuwa  yanapita akilini mwangu.
 
Nikazinduka kutoka katika mawazo yangu na kumwambia.
 
“Nilikuwa nafikiria  hadithi uliyonieleza”
 
“Kahawa imekutosha?” akaniuliza.
 
“Imetosha. Ni kiasi gani?”
 
“Sijakuuzia, nimekupa kiurafiki kwa  vile siku nyingi hatujaonana”
 
“Asante, nakushukuru sana. Naona nikuage, tutaonana siku nyingine”
 
Nilipoondoka kwa Mzaramu nilikusudia nipite pale nyumbani kwa kina Ummy na kama nitakutana na yule mzee nisalimiane naye.
 
Wakati nipo barabarani nikitembea kwa miguu kuelekea upande ule ilikokuwa nyumba ya mzee Nasri, nikakutana na mdogo wake Ummy akitokea dukani.
 
Msichana huyo aliponiona akasimama.
 
“Kaka wewe ndiye uliyekuja nyumbani jana ukatuambia kuwa ulimuona dada?”  akaniuliza.
 
“Ndiye mimi”
 
“Jana ulitutia wasiwasi sana. Ilibidi mama aende kwa mganga kumueleza kuhusu kuonekana kwa Ummy ambaye alishakufa. Mganga akamwambia kwamba huyo aliyeonekana alikuwa Ummy kweli, amechukuliwa msukule”
 
“Amechukuliwa msukule na nani?” nikamuuliza.
 
“Huyo mganga alimwambia amechukuliwa msukule  na mwanamke mmoja ambaye aliwahi kugombana  naye”
 
“Waligombania nini?”
 
“Huyo mwanamke alikuwa akidai kuwa marehemu alikuwa anatembea na mume wake”
 
Nikayakumbuka yale maelezo ya Mzaramu. Nikafikiri kidogo  kisha nikamuuliza.
 
“Kama alichukuliwa msukule mbona yuko vizuri tu, anaongea kwenye simu na nilikutana naye Botswana, Zimbabwe na Afrika Kusini. Mtu aliyechukuliwa msukule anapanda ndege?”
 
“Hayo ni maelezo ya huyo mganga lakini baba alipoelezwa amesema hataki mambo ya kishirikina, anachojua yeye ni kuwa mwanawe amekufa, huyo aliyeonekana siye mwanawe”
 
“Mimi pia hayo madai ya kuchukuliwa msukule sikubaliani nayo. Waganga wengine wanakisia tu”
 
“lakini wewe una hakika kuwa ulimuona dada?”
 
“Nilimuona  na ni yeye aliyenielekeza nije kwenu. Mimi nilikuwa sijui kwamba amekufa”
 
“Na tangu jana hajakupigia simu?”
 
“Hajanipigia bado”
 
“Na wewe hujampigia?”
 
“Sijampigia”
 
“Ungempigia umuulize vizuri”
 
“Kusema kweli nimetishika  baada ya kusikia kuwa alishakufa”
 
“Hebu jaribu kumpigia sasa hivi?”
 
Nikatoa simu na kuitafuta namba ya Ummy, nilipoipata nikampigia.
 
Simu ikaita. Nikajua itapokelewa ili nimpe mdogo wake azungumze naye lakini simu haikupokelewa. Ilipokata nikapiga tena.
 
“Hapokei simu?” nikamwambia yule msichana.
 
“Labda alikudanganya tu?”
 
ITAENDELEA kesho hapahapa Usikose Uhondo huu nini kitatokea, je simu itapokelewa na mdogo wake atazungumza nini na dada yake ambaye anauhakika ameshafariki?
 

MICHE YA MIKOROSHO MKANYAGENI MUHEZA TANGA



Mkulima wa zao la korosho shamba la Mkanyageni Wilayani Muheza Mkoani Tanga, Kurwa Joseph, akiichukua miche katika kitalu chake na kwenda kuipanda . Wakulima hao huuza korosho kwa bodi ya korosho Tanzania kwa shilingi 1,800 kwa kilo.
Imeelezwa kuwa Tanga zao la korosho linaweza kuwakomboa wakulima badala ya kung'ang'ania kilimo kimoja ambacho ni cha msimu.





SUNDERLAND YASHUKA DARAJA, DEFOE KUCHEZA MCHANGANI

Mshambuliaji wa Sunderland Jermain DefoeKipindi cha miaka kumi cha klabu ya Sunderland katika ligi ya Uingereza hatimaye kimekwisha baada ya kushindwa na Bournemouth nyumbani.
Matokeo hayo pamoja na yale ya sare kati ya Hull City na Southampton yanamaanisha timu hiyo ya David Moyes ina pointi 14 ikiwa imesalia mechi nne.
Joshua King wa Bournemouth alifunga bao la pekee ikiwa imesalia dakika 2 na kuipa ushindi timu yake.
Raia huyo wa Norway pia karibu afunge katika dakika ya 20 lakini shambulio lake lilipiga mwamba wa goli na kurudi katika mikono ya kipa Pickford.
Hiyo ni mara ya 23 ya Sunderland kupoteza ,hatua inayomaanisha timu hiyo ya Black Cat imeshushwa dajara kutoka ligi ya Uingereza kwa mara ya nne.

Saturday, April 29, 2017

BIASHARA, MATIKITI MAJI SOKO LA MGANDINI TANGA


Mfanyabiashara wa matikiti maji soko la Mgandini Tanga wakisubiri wateja kuwauzia matunda yao. Tikiti moja lilikuwa likiuzwa 3,000 hadi 5,000 kulingana na ukubwa wake.
Kipindi hiki cha msimu wa matunda wafanyabiashara wengi wamekuwa wakitafuta masoko na kulalamika kukosa soko la uhakika hivyo kuuza kwa wateja mmoja mmoja jambo ambalo wamedai kuogopa kuwaozea mikononi.




Friday, April 28, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URUTHI WA BABU SEHEMU YA 15

ZULIA LA FAKI
 
NILIKIONA CHA MTO URITHI WA BABU 15
 
ILIPOISHIA
 
Nikajiambia kama  hatakuwa shetani atakuwa ni mzuka. Lakini sikuelewa ni kwanini mzuka huo uliwaua wale watu na kwanini  uliniambia kuwa unajua siri za mali za babu yangu.
 
Kwa vile suala la msichana huyo lilikuwa limenipa dukuduku, nilipofika  nyumbani nikapata wazo moja. Wazo hilo lilikuwa ni kufanya  utafiti ili kumjua huyo Ummy niliyemabiwa kuwa alikufa, alikuwa msichana wa aina  gani. Alikuwa  akifanya kazi  gani na pia nijue kama alikuwa na uhusiano na marehemu babu yangu.
 
Sikutaka tena kumpigia simu Ummy kwa sababu huenda angeipokea na kunieleza maneno ya kunitisha.
 
Ili kuanza upelelezi wangu niliona niende katika mtaa ule ule aliokuwa anaishi Ummy nitafute mtu aliyekuwa anamfahamu nifanye  naye  urafiki na kisha nianze kumhoji kuhusu maisha ya Ummy mpaka kufa kwake.
 
Ule mtaa nilikuwa mgeni nao, nilijua isingekuwa kitu rahisi kumpata rafiki wa kunipa habari za Ummy lakini  nilijiambia ni lazima nijitahidi kwa kadiri ya uwezo wangu nimpate mtu ambaye ataweza kunifumbulia kitendawili  cha Ummy Nasir.
 
SASA ENDELEA
 
Siku ile yule msichana hakunipigia simu na mimi sikumpigia. Mimi sikumpigia kwa hofu niliyoipata baada ya kuelezwa kuwa msichana huyo alishakufa. Na kama alishakufa na nimekuja kukutana naye, basi atakuwa ni mzuka.
 
Asubuhi ya siku ya pili yake  nikaenda katika ule mtaa niliyokwenda jana yake kumuulizia  Ummy.  Safari hii sikwenda na  gari langu. Nilipanda daladala.
 
Sikutaka kufika tena pale nyumbani kwa mzee Nasir. Nilizuga zuga katika nyumba zilizokaribiana na nyumba  yake nikitafuta mtu ambaye ningeweza kufanya naye urafiki  na kumuuuliza kuhusu marehemu Ummy.
 
Katika kutupatupa macho nikaona  sehemu iliyokuwa na meza ya  kahawa na kashata.  Kulikuwa na mabenchi matatu ya kukalia.  Muuza kahawa aliyekuwa amevaa kofia kubwa lililosukwa kwa minyaa kama la mvuvi  wa samaki, alikuwa amekaa upande wa pili wa meza yake akiwa na ndoo mbili, jiko na birika la kahawa lililokuwa likifuka  moshi jikoni.
 
Muda ule kulikuwa na mtu mmoja tu aliyekuwa amekaa akinywa kahawa. Nikaona  niende nikakae mahali hapo ili nifikirie la kufanya.
 
Mara tu nilipoketi akaja mtu mwingine. Tukawa watu watatu.
 
Muuza kahawa akatutilia kahawa bila hata kutuuliza. Ukishakaa kwenye benchi lake maana yake ni kuwa unataka kahawa.
 
Nilichomsikia  akiuliza ni.  “Nikutilie tangawizi?”
 
Alikuwa akimtazama yule mwenzangu aliyekuja baada ya mimi.
 
“Ndiyo tia” Mtu huyo  akamjibu.
 
“Na wewe?” akaniiuliza mimi.
 
Wakati  ananitazama, sura yake ikanijia akilini mwangu. Zilinichukua  kama nukta tatu hivi kumkumbuka  Selemeni Mzaramu.
 
Wakati  namkumbuka, yeye alishanikumbuka zamani.
 
“Ah! Kasim Fumbwe… kumbe  ni wewe?” akaniuliza  kwa mshangao.
 
“Mzaramu!  Bado upo Dar hii!” nikamuuliza.
 
“Twende wapi ndugu yangu. Tunabangaiza humu humu. Makamba alituambia tutabanana hapa hapa”
 
Tukacheka.
 
“Nikuwekee tangawizi?’  akaniiuliza tena.
 
“Ndiyo niwekee”
 
Selemani Mzaramu alikuwa rafiki yangu wa miaka mingi. Nilisoma naye shule ya msingi hadi darasa la saba. Wakati  mimi  naendelea na masomo ya sekondari, mwenzangu hakuchaguliwa. Na baada ya hapo sikuwahi kukutana  naye tena hadi siku ile nilipomuona  amevaa kofia la minyaa akiuza kahawa.
 
Mzaramu alinisogezea kikombe cha  kahawa akaniuliza.
 
“Uko wapi Kasim?”
 
“Mimi niko hapa hapa  Dar. Nilikuwa Morogoro , maisha yakanishinda, nikarudi hapa  Dar”
 
“Unafanya kazi  wapi,  nije  unipe kibarua?”
 
“Bado nipo  nipo tu, sifanyi kazi popote. Nilikuwa na duka Morogoro, duka likafa, nikarudi Dar baada ya babu yangu kufariki. Na ndiyo nimeamua niendelee kuwa hapa”
 
“Mimi baada ya masomo nilihangaika na malori mpaka yamenitia kilema. Sasa  nipo  hapa?”
 
“Alah! Umepata ulemavu?”
 
“Mguu wangu ulivunjika  mara tatu. Mfupa ulisagika vibaya. Nimeokolewa na vyuma…”
 
Mzaramu alinionesha mguu  wake wa kushoto  baada  ya kuisega suruali yake. Mguu huo ulikuwa hautazamiki kwa mishono!
 
“Nje unaouna ni mguu lakini  ndani  ni vyuma vitupu, yaani ulikuwa ukatwe lakini kaka  yangu alijitahidi sana kunipeleka hospitali za pesa ambako niliwekewa vyuma. Nikasema sasa malori basi”
 
“Loh! Pole sana rafiki yangu. Ulikuwa dereva?”
 
“Nilikuwa taniboi. Basi nilikaa hospitali karibu mwaka  mzima”
 
Nikatikisa kichwa changu kumsikitikia.
 
“Pole sana rafiki yangu lakini kama unapata riziki yako na maisha yanakwenda, shukuru Mungu”
 
“Nashukuru.  Nimeoa na nina watoto  wawili lakini mke wangu alinikimbia aliposikia nitakatwa mguu. Kaniachia watoto lakini nimewalea mwenyewe na hivi  sasa wanasoma”
 
“Kumbe  ulipata  mkasa mkubwa rafiki yangu….”
 
“Kula kashata” Mzaramu akaniambia.
 
Nikaokota kashata moja na kuing’ata.
 
“Unazitengeza  mwenywe?” nikamuuliza.
 
“Nazitengeza mwenyewe usiku.  Asubuhi nakuja  nazo”
 
“Kwani unaishi wapi??’
 
“Naishi hapa  hapa  Mwananyamala”
 
“Mtaa huu?”
 
“Ndiyo  naishi mtaa huu huu lakini ni kule mwisho”
 
“Umeishi mtaa  huu kwa miaka mingapi?’
 
“Nina miaka  kumi na mitano  sasa”
 
Nikajiambia kimoyomoyo kuwa atakuwa anamjua Ummy ambaye alikufa  miaka mitano tu iliyopita.
 
“Katika mtaa huu alikuwa akiishi msichana mmoja  aliyekuwa akiitwa Ummy Nasri…”
 
“Nyumba  yao ile paleee lakini huyo msichana alikwisha  kufa  zamani ila namfahamu sana”
 
ITAENDELEA kesho Usikose