Saturday, June 3, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 34

ZULIA LA FAKI
 
NILIKIONA CHA MTO URITHI WA BABU 34
 
ILIPOISHIA
 
“Mwenzako amekudanganya. Amekwambia mimi ni mbaya kwa maana yake. Alikuleta huku ili akuue. Ile dawa aliyokupa kwenye kikombe haikuwa dawa. Ilikuwa ni sumu. Kama  ungekunywa ungekufa pale pale! Mimi ndiye niliyekibeta kile kikombe”
 
Hapo ndipo nilipogutuka.
 
“Kumbe alikuwa ananipa sumu?”
 
“Alikuwa anakupa sumu akuue. Ukishakufa alitaka  anichukue mimi  niwe  mke wake ili apate utajiri”
 
“Ndiyo maana aliniambia  tuje huku shamba!”
 
“Sasa ndiyo ujue kuwa ulichofanya kilikuwa ni upuuzi. Kwanini ulikuja kumueleza siri ya mimi na wewe?”
 
“Nilikuja kumtaka ushauri, ndio akaniambia kuwa wewe ndiye uliyemuua babu yangu na utaniua na mimi. Kwa hiyo alitaka akuondoe”
 
“Shiit…! Mimi nimuue babu yako kwa kosa gani wakati nilimchunuka mwenyewe.  Babu yako alikufa kwa sababu alikuwa mzee. Angeendelea kuishi hadi lini?”
 
SASA  ENDELEA
 
 
“Basi alinaimbia umemuua wewe”
 
“Yale yalikuwa maneno ya uchochezi yenye lengo la kutaka unichukie mimi na ukatae kunirithi” Maimun aliniambia kwa huzuni kisha akaongeza.
 
“Ni mganga mwenye roho mbaya sana. Kama mimi ni mbaya mbona alinitaka yeye?”
 
Nikanyamaza kimya nikifikiria kwamba kama si mwanamke huyo ningekuwa nimeshauawa kwa sumu.
 
“Unajua hukupaswa kuwaeleza watu kila kitu. Babu yako alikuwa msiri sana. Hakuwa  na mtu  yeyote aliyejua kama alikuwa na mke jini. Hata yule mganga wake hakumwambia”
 
“Ni kweli nilikosea”
 
“Sasa acha  tabia ya kuwaeleza watu habari zangu. Utakuja kuuawa bure”
 
“Yule mganga sitamuamini tena”
 
“Kwani nani alikwambia kwamba ataamka tena?”
 
Nikashituka.
 
“Hataamka tena?”
 
“Ile ndiyo safari. Nilikubeba wewe kile kikombe kisha nikampiga kibao. Alijiona anapigwa lakini  hajui anapigwa na nani. Hataamka  tena. Ile ndiyo  safari!”
 
“Niloimuona amekakamaa”
 
“Hivi ndivyo ninavyomfanya mtu mpumbavu. Kama ni mganga kweli mwenye majini, mbona  hawakunizuia nisimpige? Yule hawezi kunichukua mimi. Mimi ni jini wa kweli kweli. Sio vijini vyake ochwara!”
 
Kikapita kimya cha sekunde  kadhaa nikiyawazia maneno ya Maimun.
 
“Sioni haja ya kusubiri ujiandae au ufikirie. Unajiandaa kwa lipi au unafikiria nini?  Leo utanirithi na ninakuwa mke wako. Sasa twende madukani tukanunue nguo kwa ajili ya sherehe yetu ya usiku” Maimun akaniambia ghafla.
 
“Tutakuwa na sherehe leo usiku” nikamuuliza.
 
“Ndiyo, sherehe ya kuoana kwetu”
 
“Itafanyika wapi?”
 
“Itafanyika nyumbani kwako usiku”
 
“Itakuwa ni sherehe ya namna gani?”
 
“Sherehe kama sherehe yoyote ya ndoa. Nitawaalika wageni wangu kutoka kwetu lakini wewe usialike mtu. Itakuwa sherehe ya majini”
 
“Kwani haitaki maandalizi?”
 
“Mimi mwenyewe nitaandaa kila kitu”
 
Nikabaki nimeduwaa. Ningemjibu nini Maimun anayeua watu kwa vibao?  Ilibidi nimkubalie kila alichosema.
 
Nikampitisha katika maduka makubwa ya nguo. Akanunua vitu pamoja na nguo zake na zangu. Alijaza masanduku mawili ya nguo zenye thamani na kuyapakia kwenye gari. Pesa  zilizomtoka zilikuwa karibu shilingi milioni ishirini na tano!
 
Ile ‘shopping’ ilinitisha hata mimi. Kununu nguo zenye thamani kubwa kiasi kile kwa wakati  mmoja halikuwa jambo dogo. Niliamini kuwa kweli yule mwanamke alikuwa na utajiri, si mchezo.
 
Tulirudi  nyumbani kwangu na yale masanduku. Maimun akaniambia siku ile nisiondoke kwenda popote. Nikatii agizo lake nikashinda nyumbani hadi jioni lakini yeye aliondoka. Usiku nilitoka mara moja kwenda kula chakula halafu nikarudi kulala.
 
Yapata saa nae usiku, mlango wa chumba changu  ukabishwa. Nikasikia sauti za watu ukumbini.  Sikupata hofu kwa vile Maimun aliniambia sherehe zitafanyika usiku. Nikaamka na kwenda kufungua mlango.
 
Niliona wasichana wawili waliokuwa mbele ya mlango. Sikuwa  na shaka kwamba wasichana hao walikuwa majini kwani walikuwa wazuri sana.
 
“Wakati umewadia. Unatakiwa uoge uvae joho lako alilokununulia dada, ujifunge na kilemba halafu ujitie manukato” Mmoja wa wasichana hao wakaniambia.
 
Nikarudi chumbani na kuingia bafuni. Nilioga na nilipomaliza nilitoka  nikavaa ‘Panjabi’ aliyoninunulia Maimun kisha nikajitia manukato.
 
Nikatoka bila kuvaa kilemba kwani nilishindwa kukifunga. Nilikuwa nimekishika mkononi.
 
Wale wasichana wawili walikuwa bado wako kando ya mlango kama maaskari. Waliponiona  ninatoka, mmoja alinishika mkono akanirudisha chumbani.
 
“Usitoke hivi hivi, dadada atagomba” akaniambia na kunifunga kile kilemba.
 
Baada ya kufungwa kilemba hicho nilijitazama kwenye kioo. Nilijiona nilikuwa kama ‘Mpakistani’ anayejiandaa kwanda kuswalisha.
 
Nyumba yangu ilikuwa imepambwa vilivyo. Mapazia yalikuwa yamewekwa mengine. Taa zilikuwa zimebadilishwa na kuwekwa taa za rangi  mbalimbali na zisizo na mwanaga mkali.
 
Niliona  watu mbalimbali, wake kwa waume, wakishughulika. Maimun aliniambia mchana kuwa ataalika wageni kutoka kwao. Nikahisi wageni wenyewe ndio wale niliowaona hapo.
 
Nikapelekwa sebuleni. Sebule ilikuwa imebadilishwa. Makochi yangu yaliondolewa na kuwekwa makochi mengine ya chini chini. Nilikuta watu wawili, mmoja akiwa mzee mwenye ndevu nyeupe ambaye alikuwa amevaa joho na kilemba cheupe.
 
Pembeni yake palikuwa na chetezo kilichokuwa kinafuka  moshi uliokuwa unanukia ubani uliochanganya na udi wa mawaridi, wengine huuita udi wa Unguja.
 
Sebule nzima ilikuwa ikinukia udi wa mawaridi.
 
“Kaa hapa” yule mzee aliyekuwa amevaa joho akaniambia akinionesha sehemu iliyokuwa mbele yake.
 
Nilipokaa tu akaniambia.
 
“Lete mkono wako”
 
Nikampa mkono.
 
“Unaitwa nani?” akaniuliza.
 
 ITAENDELEA kesho Usikose Uhondo huu

No comments:

Post a Comment