Wednesday, June 7, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 37

ZULIA LA FAKI
 
NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU 37
 
ILIPOISHIA
 
Siku nilipogundua hilo nilimuuliza.
 
“Hivi  wewe Maimun hulali usiku?”
 
“Sisi majini hatulali, tunakuwa macho tu” akanijibu.
 
“Kwaninini?”
 
“Ndiyo  maumbile yetu”
 
“Kumbe usiku nalala peke  yangu?”
 
“Ukilala mimi nakulinda”
 
Kuna siku moja aliniamsha saa nane usiku akaniambia nichukue shepe kisha nitoe gari. Baada ya kulitia shepe kwenye gari nililitoa gari. Maimun akajipakia na kukaa kando yangu.
 
“Twende Kigamboni” akaniambia.
 
“Kuna  nini?” nikamuuliza.
 
“Wewe twende tu”
 
Nilikwenda kukutana na maajabu ambayo sitayasahau katika maisha yangu.
 
SASA ENDELEA
 
Tulifika Kigamboni kama saa nane na nusu hivi. Ilielekea Maimun alikuwa akilijua vizuri eneo hilo kwani aliniongoza hadi sehemu ambayo ilikuwa na pori.
 
Akaniambia niingize gari katika pori hilo. Sikumuelewa halafu pia nilipata hofu kidogo. Nikafunga breki na kumuuliza.
 
“Kwani tunakwenda wapi?”
 
“Wewe twende tu”
 
“Lakini huku unakoniambia twende hakuna njia”
 
“Mimi pia nina macho, ninaona kuwa hakuna njia. Ingiza gari hivyo hivyo”
 
“Unataka tutokee wapi?”
 
“Kassim mbona mbishi sana?”
 
“Mahali kuna pori, unaniambia niende! Njoo uendeshe wewe”
 
“Kumbe huniamini?”
 
“Ninakuamini. Tatizo nini kuwa siwezi kuendesha gari kwenye pori na pia sijui tunakwenda wapi”
 
“Kwahiyo turudi?”
 
“Tusirudi. Nimekwambia njoo uendeshe wewe”
 
“Inaelekea wewe ni muoga sana!”
 
Hapo sikumjibu. Nikanyamaza kimya kwani ukweli ni kuwa uoga pia nilikuwa nao.
 
“Shuka unipishe hapo kwenye sukani” Maimun akaniambia.
 
Nikafungua mlango na kushuka.
 
Kulikuwa na gari ambayo ilikuwa nyuma yetu ikatupita na kusimama mbele yetu.
 
Wakati ule nafungua mlango nikaona ninavamiwa na mtu mmoja miongoni mwa wanne waliotoka kwenye lile gari. Mtu huyo alinishikia bastola na kunitia kabari kwa nyuma. Mtu mwingine alifungua mlango wa upande aliokuwa Maimun akamwambia.
 
“Shuka haraka!”
 
Maimun akashuka kwenye gari.
 
“Mnataka nini?” Maimun akiwauliza.
 
Mimi nilikuwa nimeshadhibitiwa. Mkono ulionitia kabari ulikuwa ukinikaza na kunifanya nisifurukute hata kidogo. Mdomo wa bastola ulikuwa ukitekenya shavu langu la kulia.
 
Sikuweza kujua watu wale walikuwa kina nani na walikuwa wanataka nini.
 
Kulikuwa na watu wengine wawili ambao walikuwa wamefungua milango ya ile gari kama vile walikuwa wakitafuta kitu.
 
“Mnakwenda wapi?” Yule mtu aliyemtoa Maimun kwenye gari akamuuliza Maimun.
 
“Nyinyi ni majambazi sio?” Maimun akawauliza.
 
Yule mtu alitaka kumpiga Maimun kibao, bila shaka kwa vile alivyowambia ni majambazi. Maimun akatoweka ghafla mbele  yake. Kibao kikakata hewa. Maimun akaibuka tena mahali pale pale. Nikamsikia akitoa mlio kama wa fataki inayopaa juu huku na yeye akirefuka kwenda juu.
 
Wakati ule mmojawao, alikuwa ameshajipakia kwenye gari kwenye siti ya dereva. Nikahisi walitaka kutupora lile gari.
 
Lakini kitendo cha Maimun kurefuka kiliwashitua. Maimun aliendelea kurefuka akafikia kimo cha mnazi!
 
Nikawasikia wale watu wakisema kwa fadhaa. “Ha! Ha1 Ha!”
 
Yule aliyenitia kabari aliniachia akakimbilia kwenye gari lao. Yule aliyetaka kuendesha lile gari letu alitoka kwenye gari na kukimbia lakini yule aliyetaka kumpiga Maimun kibao alinata pale pale.
 
Wale waliokimbilia kwenye gari walikwama baada ya Maimun kupiga hatua moja na kutinga mbele ya gari hilo. Mtu mmoja alianguka hapo hapo. Wengine wakakimbia kwingine na kuliacha gari.
 
Baada ya tukio hilo nikauona mwili wa Maimun umerudi vile vile kama ulivyokuwa mwanzo.
 
Akaja kwenye gari letu upande wa dereva na kuniambia.
 
“Ingia garini twende”
 
Nikazunguka kwenye mlango wa upande wa pili na kujipakia. Yule mtu aliyenata alikuwa bado amesimama pale pale, mkono wake mmoja akiwa ameunyoosha mbele kama vile anampiga mtu kibao.
 
Maimun alikuwa ameshaingia kwenye gari akaliondoa na kuliingiza kwenye pori.
 
Kile kitendo cha Maimun kujirefusha, hata mimi kilinishitua kwani katika maisha yangu sijawahi kuona mtu akirefuka kwenda juu akafikia kimo cha mnazi.
 
Mpaka wakati ule nilikuwa bado nikitweta.
 
“Umewaona wapumbavu wale?” Maimun akaanza kuniambia akionekana alikuwa amekasirika.
 
“Nimewaona lakini sikujua walikuwa ni kina nani”
 
“Wale  ni majambazi, walitaka kulipora hili gari. Walitufuata kuanzia mbali sana. Nilishawaona lakini sikukwambia”
 
“Kwa hiyo walitaka watuue?”
 
“Sasa kama walitutolea bastola, unadhani walikuwa wana maana gani nyingine?”
 
“Lakini wametishika!”
 
“Walivyonuona ninakuwa mrefu sio?”
 
“Ndiyo. Hata mimi nimetishika”
 
“Wewe mume wangu pia unatishika?”
 
“Sijawahi kukuona ukiwa vile!”
 
“Acha vile naweza kujirefusha mpaka ukawa hujui  nimefikia wapi!”
 
“Sasa unafanyaje?”
 
“Ni namna yetu. Naweza pia kujigeuza mnyama kama vile punda au joka kubwa”
 
“Lakini sitapenda ufanye hivyo mbele yangu”
 
“Nikifanya mbele yako ndipo utakaponizoea”
 
“Eh! Nitaogopa sana”
 
“Utazoea tu. Utaogopa mwanzo, mwisho utakuwa huogopi tena”
 
“Sasa yule mtu aliyetaka kukupiga kibao, ataendelea kubaki pale hadi lini?”
 
“Atajua mwenyewe, achana naye”
 
Maimuna aliendesha gari huku akikata kona ndani ya msitu hadi tukatokea mahali ambapo palikuwa na mawe makubwa sana yaliyotokea ardhini.
 
Akalisimamisha gari na kuniambia tushuke.  Tukashuka. Palikuwa ni mahali panapotisha usiku huo lakini kwa vile nilikuwa na Maimun sikuwa na hofu sana. Nilijua kama kutatokea tatizo atanisaidia.
 
“Toa lile shepe nyuma ya gari” akaniambia.
 
 
 ITAENDELEA kesho hapahapa Usikose uhondo huu

No comments:

Post a Comment