Sunday, June 4, 2017

SIMULIZI, NILIKIONA CHA MOTO URITHI WA BABU SEHEMU YA 35

ZULIA LA FAKI
 
NILIKIONA CHA MTO URITHI WA BABU 35
 
ILIPOISHIA
 
Nikamtajia jina langu.
 
“Nikilitaja jina lako utaitikia labeka”
 
“Sawa”
 
Mzee huyo akaniita. Nikamuitikia “labeka”
 
“Ninakuozesha Maimun binti Hashhash kwa mahari mliyokubaliana. Unakubali?”
 
“Nimekubali”
 
“Sema nimekubali kumuoa Maimun binti Hashhash kwa  mahari tuliyokubaliana”
 
Nikasema kama vile alivyonifundisha. Akarudi kunaimbia hivyo mara tatu.
 
Hapo hapo nikasikia sauti za wanawake waliokuwa wamekaa  ukumbini ziking’ara kwa vifijo.
 
Yule mtu aliyekuwa amenichukua kutoka mlango wa chumbani kwangu, akaniambia niinuke. Nilipoinuka akanirudisha chumbani kwangu. Nilipoingia nilikuta chumba hicho kimebadilishwa.
 
SASA ENDELEA
 
Hakikuwa kile chumba changu kabisa. Kitanda kilikuwa kimewekwa kingine. Kabati lilikuwa jingine na mapazia  pia  yalikuwa mengine. Kwa kweli kilikuwa kimependeza sana. Hata taa zizokuwa zinawaka zilikuwa  ni za rangi mbali mbali.
 
Nikamkuta Maimun binti Hashhash amekaa kwenye kitanda. Pale  kwenye kitannda palikuwa pametandazwa maua ya mawarisi,  asmini, vilua, mlangilangi na vitu vingine ambavyo vilikuwa vikitoa  harufu nzuri mle chumbani.
 
Maimun alikuwa amepambwa na kupendeza kama malkia wa Habesh. Alikuwa akinukia manukato ya kila aina. Mwili wake ulikuwa umejaa mapambo ya dhahabu. Kuanzia kwenye shingo yake ambapo palikuwa na mkufu mzito wa thamani. Masikioni mwake alikuwa amewekwa vipuli vilivyokuwa vikimeremeta. Kwenye mikono yake alikuwa amevaa aina ya bangili za dhahabu.
 
Kadhalika katika mguu wake wa kulia alikuwa amefungwa mkufu mwembamba uliokuwa ukimeremeta.
 
Kwa kweli alikuwa amependeza na kutamanisha.
 
Alikuwa amefunikwa mtandio uliokuwa unaonya. Hivyo niliweza kuyaona macho yake yaliyokuwa yamepakwa wanja mzito mweusi huku yakiwa na kope ndefu mithili ya kope za bandia.
 
Nyusi zake pia zilikuwa zimeongezewa msitari wa wanja uliopinda juu ya macho yake mithili ya pindi za mvua.
 
Aliniomba nimfunue ule mtandio, nikaushika kwa uoga na kuufunua. Akaniambia.
 
“Asalaam alaykum mume wangu” Wakati akinipa salaam hiyo alikuwa akinipa mkono.
 
“Wa alayka salaam” nikamjibu na kushikana naye mkono.
 
Mkono wake ulichorwa maua kwa kutumia piku na hina. Ulikuwa umeota malaika marefu yasiyo ya kawaida.
 
“Salaam yako ina kasoro, sikuipenda” Maimun akaniambia wakati tumeshikana.
 
“Kwanini?”  nikamuuliza.
 
“Nimekusalimia asalaam alaykum mume wangu. Ulipaswa kujibu wa alayka salaam mke wangu”
 
“Samahani. Ni kweli nimekosea”
 
“Sasa  nijibu kwa usahihi”
 
“Wa alayka salaam mke wangu”
 
Maimun akakibusu kiganja cha mkono wangu kisha akaniambia.
 
“Karibu chumbani”
 
“Asante” nikamjibu.
 
Kusema kweli nilikuwa nimenywea kama vile kile chumba hakikuwa changu.
 
Yule mtu aliyenisindikiza mle chumbani akaniambia.
 
“Kama umeshaonana na mke wako, mimi nakwenda zangu”
 
“Wewe nenda, muache” Maimun akanijibia.
 
Yule mtu alipotoka Maimun akajilaza kitandani na kuniambia.
 
“Huu ni wakati wako. Karibu tujipumzishe…..”
 
                                                **********
 
Mkono wenye ngozi laini kama ya mtoto mchanga uliokuwa ukipapasa kifua changu ndio ulioniamsha kutoka usingizini.
 
Nikafumbua macho yangu  na kuisikia sauti ya Maimun ikiniambia.
 
“Amka  mume wangu, kumekucha”
 
Maimun alikuwa amesimama kando ya kitanda mkono wake ukiwa kwenye kifua  changu. Sikuweza kujua alikuwa ameondoka muda gani hapo kitandani lakini wakati ule ananiamsha kulikuwa kumeshakucha.
 
“Amka ukaoge, nimeshakuandalia kifungua kinywa” akaniambia.
 
Nikaitenga shuka na kushuka kitandani.
 
“Utaoga maji ya moto?” Maimun akaniuliza.
 
“Hapana, ninaoga maji baridi tu”
 
Niliingia naye bafuni tukaoga pamoja. Baada ya kuoga Maimun akanikaribisha mezani nipate kifungua kinywa alichokuwa ameniamndalia. Ile vurugu pale nyumbani haikuwepo tena.
 
Nyumba ilikuwa kimya na hakukuwa na mgeni yeyote aliyekuwa amebaki. Sikuweza kujua wageni wale waliokuwepo usiku waliondoka saa ngapi.
 
Kitu kilichoonesha kuwa usiku uliopita kulikuwa na sherehe ni mapambo yaliyopambwa mle ndani ambayo bado yalikuwepo.
 
Baada ya kupata kifungua kinywa pamoja na Maimun tulirudi chumbani ambapo Maimun alifungua kabati. Hilo kabati lilikuwa moja ya vitu vilivyoletwa usiku uliopita. Halikuwa lile kabati langu.
 
Maimun alipolifungua kabati hilo, upende mmoja  ulikuwa umepangwa nguo zake, upande mwingine ulipangwa nguo zangu.
 
Katika sehemu ya chini ya kabati hilo kulikuwa na sanduku la chuma. Maimun akanipa funguo na kuniambia nilifungue   sanduku hilo. Nikalifungua na kupatwa na mshituko.
 
Sanduku hilo lilikuwa na tabaka tatu. Tabaka ya kwanza ilikuwa imepangwa maburungutu ya noti nyekundu za Kitanzania. Zilikuwa noti nyingi na mpya zilizozonesha kama zilitoka benki kwani bado zilikuwa zimefungwa mfungo ule  ule wa kibenki.
 
Tabaka la pili lilikuwa limejaa mapambo ya dhahabu, mikufu, bangili, vipuli na vitu vngine.
 
Tabaka la tatu lilikuwa na maburubgutu  ya noti lakini hazikuwa za Kitanzania. Zilikuwa ni dola za Kimarekani.
 
Nikamtazama Maimun kwa mshangao.
 
“Hizo ni za kutumia hapa nyumbani. Zikiisha ninaweka zingine” Maimun akaniambia.
 
Nikageuza tena uso wangu na kuzitazama zile noti nilizoambiwa kuwa ni za kutumia.
 
“Bado kuna pesa za miradi ambazo nitakupa” Manuna aliendelea kuniambia.
 
Akilini mwangu niljiambia kuwa nimeshakuwa tajiri.
 
“Chukua kiasi unachotaka uweke mfukoni mwako”
 
“Nichukue dola au hizi za Kitanzania?’
 
“Chukua unazotaka”
 
“Kuna miradi mingi ambayo ninataka kuianzisha”
 
 
ITAENDELEA kesho hapahapa Usikose

No comments:

Post a Comment