Wednesday, October 14, 2015

VITUKO KATIKA KAMPENI VYAPAMBA MOTO KILA SIKU, SIKIA HII

Tangakumekuchablog

Tanga,MGOMBEA Udiwani kata ya Mnyanjani kwa tiketi ya ACT, Wazalendo, Suleiman Khafidh haachi vituko vyake na mara hii amesema endapo atachaguliwa kuwa Diwani nyumba zote za makuti zilizoko ndani ya kata yake ataziweka bati moja baada ya nyengine  kwa kutumia mshahara wake.

Mgombea huyo kijana machachari ameyasema hayo leo uwanja wa mabatini na   amekuwa kivutio kila apandapo jukwaani kwani haachi kutoa vituko jambo ambalo limekuwa likiwavutia watu wengi.

Alisema anatambua kuwa hakuna mtu anaependa kuishi katika nyumba ya makuti lakini ni kutokana na umasikini na hivyo kusema kuwa  wakimchagua  mshahara wake wa kila mwezi atakuwa akinunua bati na kutoa nyumba mmoja baada ya nyengine.

“Ndugu zangu wananchi napatwa na uchungu kuona wazee wangu na ndugu zangu wakiishi katika nyumba za makuti----natambua kuwa hakuna anaependa hali hii hivyo nichagueni niwaekeeni bati kupitia pesa za mshahara wangu” alisema Khafidh na kuongeza

“Nikishuka katika jukwaa hili  nitaanza kuzihesabu nyumba mmoja mmoja ili kupata idadi kamili ---lengo nikupata tathmini ili mshahara wangu nikipokea tu nakimbilia dukani” alisema

Mgombea huyo wa Udiwani aliwataka wananchi wa kata hiyo kutofanya makosa kwa kumchagua diwani mwengine kwa madai kuwa yeye yuko na uwezo wa kuibadilisha kata hiyo na kuwa kama posta Dar es Salaam.

Alisema kitu ambacho atakipa kipaumbele mara baada ya kuutwaa Udiwani ni kuhakikisha anaweka miundombinu ya kutiririsha maji kuelekea baharini pamoja na kumwaga kifusi katika mabwawa  ili kumaliza  mazalia ya mbu na malaria.

Alisema kata hiyo iko na kero ya mazalia ya mbu wakati wa mvua kunyehs kutokana na maji hayo kutokuwa na njia ya kupitisha na hivyo kutoa ahadi ya kulimaliza kero hiyo.

“Vipaumbele vyangu nikiwa ni diwani wenu kwanza nitachimba mfereji wa kupitisha maji ya mvua na majumbani yaelekee baharini----vipindi vya mvua hapa kwetu ni sawa na ziwa Victoria” alisema Suleiman


Alisema ili kuweza kuja maendeleo ya kweli ni kuhakikisha kura zote za udiwani zinakuja kwake pamoja na kumpigia  mgombea Rais wa chama chake ili kuweza kuwabadilishia  katika mfumo wa maisha duni  wa sasa .
                                                        Mwisho

No comments:

Post a Comment