Wednesday, November 1, 2017

RIWAYA, KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI SEHEMU YA 13

RIWAYA

KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI 13

ILIPOISHIA

Kichwa changu kilikuwa kimeshavurugika. Nilijiambia  kama mke wangu atakwenda Korogwe, anaweza kupata madhara kwa vile sikuwa nikijua lile tatizo langu lingekwishaje usiku ule.

Kwa vile sikutaka yule mzee ajue kuwa nilikuwa nimefadhaika, tukaanza kuzunguma.

Tulizungumza mengi kuhusu kile kisima cha Giningi. Aliniambia yeye alizaliwa wakati wa utawala wa sultani na hicho kisima allikikuta hivyo hivyo.

“Haijulikani ni nani alikichimba na kilichimbwa wakati gani” aliniambia.

“Huenda kilichimbwa miaka mingi iliyopita. Baba yangu aliniambia alikikuta hivyo hivyo” akaongeza.

“Unadhani hapo kilipochimbwa kilichimbwa kwa madhumiuni gani?” nikamuuliza ili kupata undani wa kisima  hicho.

“Nafikiri kilichimbwa na wenyeji wa wakati huo ili kupata maji ya kutumia”

“Mpaka hii leo watu wanateka maji?”

“Hivi sasa hakitumiki tena”

SASA ENDELEA

“Sasa imekuwaje mahali hapa pakawa panatumika katika mambo haya?”

Hapo nilikusudia mambo yale ya uchawi na majini.

“Tangu sisi tunainukia tulikuta watu wakifanya matambiko na mambo mengine ya kijadi”

“Unafikri ni kwanini?”

“Hiki kisima ni cha miaka mingi. Kitakuwa kinakaliwa na majini na kuna miujiza mengi iliyowahi kutokea mahali hapa.

“Kama ipi?”

“Kulikuwa na watu waliokuwa wakionekana nyakati za usiku wakikusanyika mahali hapa. Watu hao walikuwa ni majini. Wakati mwingine  huonekana moto lakini haijulikani ni nani aliyeuwasha. Hizi zote ni ishara kuwa hili eneo lina wenyewe”

“Sasa tukirudi kwenye hii shughuli yangu, unadhani itafanikiwa?”

“Tutamsikiliza mwenyewe maalim atakapotuita usiku”

“Kwani inaweza ikashindikana?”

“Kwa vile amekwambia atakushughulikia usiku, nafikiri itawezekana. Kushindikana si aghalabu sana” Mzee akaniambia na kunipa  chembe ya matumaini.

“Mzee sitakuficha, hofu yangu kubwa ni kwa mke wangu. Hivi sasa yuko Dodoma lakini amesema kesho atanifuata Korogwe na mimi sikumwambia kuwa ninakuja huku”

“Kwanini hukumwambia?”

“Sikumwambia kwa sababu niliogopa kumtia waiwasi. Yule jini aliniambia mama yangu atakufa hivi karibuni na mke wangu ndiye atakayechukua nafasi yake. Sasa sikutaka aje pale Korogwe mpaka hili suala nilipatie ufumbuzi”

Nilipomwambia hivyo yule mzee hakunijibu kitu, alinitazama tu kama vile aliniona nilikuwa mgeni sana katika mambo yale ya mtu kutolewa kafara wakati yeye aliona yalikuwa ya kawaida.

Tukaendelea kuzungumza lakini ghafla niliona mwenzangu akianza  kusinzia.

Alipogutuka akaniambia twende tukalale. Tukaingia ndani ya kile kibanda na kulala. Mimi nililala na nguo zangu hivyo hivyo.

Kusema kweli sikulala usingizi. Muda wote nilikuwa nikiwaza tu na niliyekuwa nikimuwazia sana alikuwa mke wangu. Hofu yangu ilikuwa kwenye ile safari yake ya kwenda Korogwe.

Niliwaza kwamba anaweza kufika Korogwe kabla ya mimi na hivyo akahatarisha maisha yake.

“Yule jini anaweza kumchukua” nilikuwa nikijiambia.

Wakati nikiendelea kuwaza, muda nao ulikuwa ukienda. Sikutambua kama ulikuwa usiku mwingi niliposikia hatua za mtu zikisogea pale kwenye kibanda tulichokuwemo. Moyo wangu ukashituka, nikatega masikio yangu kusikiliza.

Ghafla nilisikia mlango wa kibanda hicho ukibishwa.

“Bwana Hanzuruni…Bwana Hanzuruni….” Nikaisikia sauti ya yule maalim ikiita.

Nikainuka na kukaa.

“Bwana Hanzuruni!” Sauti ikaendelea kuita.

Nilitaka nimuamshe yule mzee aliyekuwa amelala lakini akawahi kuamka mwenyewe.

“Labeka maalim” akasema huku akiinuka.

Alinishika mguu kisha akanitazama.

“Alah! Kumbe umeshaamka!” akaniambia.

“Mimi nimeshaamka, nilikuwa nataka kukuamsha wewe”

“Maalim huyo ameshakuja”

“Nilifikiri sisi ndio tutakwenda kwake”

“Amekuja mwenyewe kutuamsha labda alijua tumepitiwa na usingizi”

Nikaitazama saa yangu na  kuona ilikuwa saa nane ikikaribia kuwa na nusu.

Tukanyanyuka na kutoka kwenye kile kibanda.

“Wakati umewadia twendeni” Maalim huyo akatuambia. Alikuwa ameshika tochi mkononi.

Tulikwenda kando ya kile kisima. Maalim akaniambia.

“Unaouna ule mti” Alinionesha mti wa mkuyu uliokuwa mbali kidogo na sisi.

“Nauona” nikamjibu.

“Sasa nenda chini ya mti ule utaje jina la baba yako na jina lako halafu umuite Maimuna binti Ibilisi. Umuite mara tatu. Kuna kivuli kitakuja pale utakiambia shida yako. Hicho kivuli ni cha jini aliyemiliki kisima hiki. Umenielewa?” Maalim aliniambia haraka haraka.

“Yaani niende peke yangu?” nikamuuliza kwa hofu kwani mahali penyewe palikuwa mbali kidogo na palikuwa panatisha usiku ule. Isitoshe pia nilitishika kukutana na hicho kivuli nilichoambiwa ni cha jini aliyemiliki kisima kile.

“Unataka uende na nani? Mwenye shida ni wewe au sisi?” Maalim akaniuliza.

“Ni mimi”

“Basi wewe ndiye unayetakiwa kwenda hata baba yako alikwenda pale pale muda kama huu, ndio akapewa huyo jini, sasa na wewe unatakiwa uende pale pale”

“lakini sitapata tatizo lolote?”

“Tatizo kama lipi?”

Hapo nikashindwa kujibu. Badala yake  nikatoa hoja nyingine.

“Mzee hawezi kunisindikiza mpaka pale karibu karibu?” nikamwambia yule mzee.

Maalim akaja juu.

“Unajua tumeacha usingizi wetu kwa ajili yako wewe!”

“Sawa. Sasa nilikuwa na swali moja”

“Swali gani?”

“Nikishasema shida yangu ndio itakuwaje”

“Atakupa jibu, utakuja kutuambia”

“Kwa hiyo nieleze kwamba mimi sitaki zile pesa nilizorithi kwa baba yangu na pia simtaki yule jini…”

“Wewe zungumza utakavyoweza. Eleza kama ulivyotueleza sisi. Useme kwamba hizo pesa zirejee hapa pamoja na huyo jini aliyekuwa mke wa baba yako”

Nikashusha pumzi ndefu kabla ya kuyapeleka tena macho yangu kweye ule mti. Bado nilikuwa nikiushauri moyo wangu niende mahali pale nikazungumze na kivuli ambacho sikujua kilikuwa kikoje.

Nilihisi huo ulikuwa ni mtihani mwingine uliokuwa umenikabili. Lakini nilipowaza kuwa matatizo yaliyokuwa yakinikabili mimi mwenyewe, mke wangu, mwanangu na mama yangu waliokuwa kwenye pango, nilijikuta nikipiga hatua za kiaskari kuelekea kwenye mti huo.

“Kitakachotokea na kitokee, potelea mbali!” nikajiambia kimoyomoyo.

Kwa vile bahari haikuwa mbali sana na mahali hapo, upepo wa baridi ulikuwa ukinipulizia lakini niliendelea kutembea kwa hatua za ukakamavu kuelekea kwenye mti huo.

Kama sijakosea ulikuwa kama mwendo wa hatua mia moja hivi hadi nilipokifikia kivuli cha mti huo. Chini ya mti palikuwa na kichaka lakini hakikuwa kikubwa. Juu ya mti huo kunguru walikuwa wakirukaruka na kupiga kelele.

Kwa mbali nilisikia sauti ya bundi anayelia. Nilipofika hapo ilibidi nitazame nyuma ili niwaone wale watu. Walikuwa wamesimama mbali kidogo wakinitazama.

Sikutaka kuingia kwenye kile kichaka usiku ule kwa sababu sikujua kama palikuwa salama. Nikasimama mwanzo wa kichaka hicho na kuusemea ule mti.

Kwa vile yule Maalim aliniambia niseme shida yangu, nikazungumza kwa sauti ya kusikika kile kilichokuwa moyoni mwangu. Nilieleza kwamba baba yangu ambaye kwa wakati ule ni marehemu alifika mahali hapo na kutaka apate pesa za majini.

Nikaendelea kueleza kwamba marehemu  alipatiwa mke wa kijini  na alipata utajiri kama alivyotaka lakini inasemekana alinitaja mimi kama mrithi wake bila kunishauri mwenyewe.

“Sasa baba mwenyewe amekufa, yule jini pamoja na zile pesa za majini vimekuja kwangu. Kilichonileta hapa ni kuwa mimi sizitaki zile pesa kwa sababu siye niliyeziomba na pia simtaki yule mke wa kijini, nataka arudi kwao” nikasema.

Lakini sikuishia hapo tu, niliendelea kuzungumza kuwa baba alimtoa kafara mke wake pamoja na mjukuu wake ambaye ni mwanangu mimi ili kutimiza masharti ya kupata utajiri.

“Sasa nataka mama yangu pamoja na mwanangu wawe wazima kama zamani. Na pia yule jini ameniambia kuwa mke wangu naye atatolewa kafara. Mimi sitaki atolewe kafara kwa sababu sitaki utajiri wa pesa zile” nikasema.

Nikamalizia kwa kueleza.

“Kwa hiyo nataka yule jini arudi kwao na zile pesa zirudi huku huku na mama yangu na mwanangu wawe wazima”

Nilipomaliza nilisubiri kwa dakika moja, sikuona kitu chochote. Nikageka na kurudi kwa wale watu.


Je nini kitatokea? ungana nani hapahapa kumekucha.com

No comments:

Post a Comment