Saturday, November 4, 2017

RIWAYA, KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI SEHEMU YA 15

RIWAYA

KAMA UNATAKA FEDHA ZA  MAJINI 15

ILIPOISHIA

“Umesikia, umeambiwa kama unataka kuwakomboa mama yako na mwanao utoe ngo’ombe dume mweusi”

“Nimtoe wapi?” nikamuuliza.

“Umtoe hapa hapa” Ile sauti ndiyo iliyojibu.

“Yaani utuletee ng’ombe mweusi kabla hujarudi kwenu” Maalim akanifafanulia.

“Utanionesha wanapouzwa. Nitanunua mmoja nimlete”

“Kama mmekubaliana mimi naondoka” Ile sauti ikatuambia na hapo hapo kile kivuli kikatoweka.

“Basi twende zetu, tumeshapata ufumbuzi” Maalim akaniambia.

Tukaondoka na Maalim. Tulipofika kwa yule mtu mwingine Maalim alimwambia.

“Asubuhi utampeleka huyu mtu akanunue ng’ombe dume mweusi, mje naye hapa”

“Sawa”

SASA ENDELEA

Baada ya hapo Maalim akaenda zake na sisi tukarudi kwenye kile kibanda.

Kusema kweli ile nilioiona kwenye ule mti ilikuwa miujiza mikubwa kwangu. Niliamini kweli pale mahali palikuwa pa hatari.

Asubuhi kulipokucha nilimuuliza yule mzee, ng’ombe anauzwa kiasi gani pale kijijini kwao.

“Hapa kijijini kwetu ng’ombe wanauzwa kuanzia shilingi laki nne hadi laki tano. Ni ghali sana” Mzee huyo akanijibu.

Nikanyamaza kidogo. Nilinyamaza kufikiria kwamba mfukoni kwangu sikuwa na kiasi hicho cha fedha na awali sikufikiria kama bei ya ngombe ingekuwa kubwa kiasi hicho kwa vile pale palikuwa ni kijijini.

“Mbona umenyamza?” Yule  mzee akaniuliza.

“Nilikuwa nafikiria. Pesa nilizokuja nazo ni chache sana mpaka niende nikachukue benki”

“Hapa kijijini kwetu hakuna benki mpaka uende mjini”

“Si kitu, nitakwenda mjini kwenye ATM nikatoe”

“Kwa hiyo tukusubiri?’

“Ndiyo mnisubiri, sitachelewa kurudi”

Nilifanikiwa kupata mahali palipokuwa na ATM katika mji wa chake chake. Ilikuwa kwenye hoteli moja ya kitalii ambako nilikuta wazungu wengi.

Kwa vile kadi yangu ya benki nilikuwa nayo, nilitoa shlingi milioni moja ambayo ilikuwa akiba yangu iliyokuwa benki. Baada ya kupata pesa hizo niliingia hotelini humo kupata kifungua kinywa.

Wakati nakunywa chai, nilijiambia nitakapomaliza shughuli nzima niliyoagizwa kule Kisima cha Giningi, hapatakuwa na cha kuniweka tena pale Pemba.

Ilinibidi niharakishe kurudi Tanga ili kumuepushia usumbufu mke wangu atakapokuja Korogwe.

Kwa upande mwingine nilifurahi lile suala langu kupata ufumbuzi kwani licha ya kumuokoa mke wangu, mama yangu na mwanangu watasalimika na kuwa wazima.

Nilijiambia nitakuwa na furaha kumuona mama yangu na mwanangu wakiwa wazima.

“Najua watu watawashangaa kwa sababu mama yangu na mwanangu walishakufa lakini nitawambia watu kuwa hawakuwa wamekufa bali walichukuliwa msukule na sasa wamerudi” nikajiambia.

“Najua wako watakaoamini na wako ambao hawataamini lakini jibu langu litakuwa hilo” niliendelea kujiambia.

Baada ya kumaliza kifungua kinywa, nilitoka nikatafuta usafiri wa kunirudisha Kendwa. Muda wa saa moja nikawa nimeshafika katika kijiji hicho. Kijana wa bodaboda akanipakia kwenye baskeli na kunipeleka huko kilikokuwa Kisma cha Giningi.

Nilipokwenda katika kile kibanda nikamkuta yule mzee.

“Umesharudi?” akaniuliza kwa uchangamfu.

“Ndiyo mzee, nimerudi”

“Umefanikiwa kupata pesa?”

“Ndiyo nimepata, sasa twende tukanunue huyo ng’ombe”

“Sawa. Twenzetu”

Tukaondoka na yule mzee kuelekea katika kijiji kingine ambako aliniambia ng’ombe anayehitajika angeweza kupatikana.

Tukiwa  njiani tukitembea kwa miguu nilimwambia mzee huyo kuwa nilitaka ile shughuli ikamilike mapema ili niwahi kurudi Korogwe.

“Unaharakisha nini?” akaniuliza.

“Si nilikwambia mke wangu atakuja Korogwe kutoka Dodoma. Nilipendelea nisipishane naye sana”

“Sasa kuwahi kwako kurudi itategemea kumalizika hii shughuli”

“Unadhani inaweza kuchukua muda gani?”

“Siwezi kujua. Anayejua ni Maalim mwenyewe”

“Kama nitalazimika kulala tena huku itakuwa ni mtihani kwangu”

Nilipomwambia hivyo mzee huyo alinitazama tu bila kuniambia kitu. Jambo lile lilinipa ishara kwamba huenda shughuli iliyobaki ikawa ndefu kiasi cha kunilazimisha kulala tena Pemba.

Nikajiambia kama mke wangu atakuja korogwe kama alivyoniambia, huenda akakutana na matatio kwa vile yule jini aliyetaka kumtoa kafara mke wangu alikuwa bado yuko nyumbani.

Nilipoona mzee amenyamaza na mimi nikanyamaza. Tulipofika katika kijiji hicho tulifanikiwa kupata ng’ombe dume mweusi kwa gharama  ya shilingi laki tano. Wakati natoa kile kitita cha noti niliona yule mzee amezikodolea macho zile pesa huku macho yake yakimwekamweka.

Baada ya kumnunua ngombe huyo tulimkabidhi kwa watu wanaoswaga ng,ombe ili waende naye katika kile kijiji tulichotoka.

Mimi na yule mzee tukatangulia kurudi kwa miguu. Tukiwa njiani nilimuuliza yule mzee kama ile kazi ingekuwa na gharama yoyote.

“Utamuuliza Maalim mwenyewe” Mzee akanijibu.

Kwa vile alikuwa amechoka kwa mwendo nilitoa noti mbili za shilingi elfu kumi kumi nikampa ili kumtia nguvu.

“Mzee na wewe chukua hizi, umenisaidiaa sana”

Mee huyo alizipokea pesa hizo na kunishukuru.

“Ondoa wasiwasi, utafanikiwa tu” akaniambia.

“Unaamini kwamba matatizo yangu yatakwisha kabisa?” nikamuuliza kwa matumaini.

“Yatakwisha tu. Yule jini atarudishwa kwao na wewe utakuwa salama”

“Kwa hiyo mke wangu hatadhurika?”

“Na mama yako pamoja na mtoto wako pia watasalimika kwa vile umezikataa zile pesa za majini. Zile pesa zina taabu lakini watu hawajui tu”

Tuliporudi pale kijijini tulikwenda kwa Maalim na kumjulisha kuwa tumeshanunua huyo ng’ombe aliyetakiwa.

“Mmekuja naye?” Maalim akatuuliza.

“Analetwa na mswagaji wa ng’ombe” Mzee akamwambia.

Tukasubiri mpaka saa tisa, ng’ombe huyo alipoletwa pale kijijini. Maalim alipomuona aliuliza.

“Ng’ombe mwenyewe ndiye huyu?”

“Ndiye huyo” Mzee akamjibu.

“Haya. Sasa shika kamba yake uende naye ukamfunge pale kwenye ule mti” Maalim akaniambia akinionesha ule mti tuliokwenda usiku wa jana yake.

“Nimfunge tu kisha nimuache?” nikamuuliza.

“Mfunge umuache hapo hapo”

Nikaishika kamba ya ng’ombe huyo na kuanza kumkokota kuelekea katika ule mti. Kwa vile sikuzoea kukokota ng’ombe kazi hiyo haikuwa rahisi. Ng’ombe alikuwa mbishi na mara kwa mara nililazimika kumvuta.

Nilipofika kwenye huo mti nilimfunga ng’ombe huyo kwenye mti huo kisha nikarudi.

“Nimeshamfunga” nikamwambia yule Maalim.

“Sasa unaweza kwenda zako” akaniambia. Kwa kweli nilifurahi.

“Kwa hiyo nikifika nitawakuta wale watu wameshakuwa wazima?” nikamuuliza nikimaanisha mama yangu na mwanangu.

“Umeshawafanyia kafara lao, watakuwa wazima tu”

“Na mke wangu hatadhurika tena?”

“Mke wako hawezi kupata madhara”

“Nashukuru sana. Sasa je zile pesa nizipeleke wapi?”

Maalim alinipa jibu lililonishangaza.

“Wewe achana nazo na usitumie hata senti moja. Watajua majini wenyewe. Na si pesa tu, kila kilichonunuliwa kwa pesa hizo achana nacho. Si mali yako tena”

“Mimi sijui ni kitu gani na gani kimenunuliwa kwa pesa hizo”

“Ukirudi Korogwe utajua. Kile ambacho kimenunuliwa kwa pesa za majini watakichukua wenyewe”

“Sawa. Ninachotaka mimi ni mama yangu na mwanangu kuwa wazima”

“Hilo halina shaka, wamekuhakikishia wenyewe”

“Nitashukuru kama itakuwa hivyo. Pia nataka kujua ninatozwa kiasi gani kwa kazi hii”

“Hapa hatutozi mtu gharama ila chochote utakachopenda kunipa kitakuwa kama sadaka yako”

“Sawa”

Nikatia mkono mfukoni na kutoa shilingi laki moja nikampa. Maalim alinishukuru sana.

Baada ya hapo tukaagana nikaondoka. Wakati niko njiani kwenda kupanda bodaboda nilikutana na watu watatu, wawili wanaume, mmoja mwanamke. Nilishuku tu kuwa walikuwa wakielekea kule Kisima cha Giningi.

Watu hao walioonekana kuwa wageni walinisalimia na mmojawapo akaniuliza.

“Eti bwana, huku tunakoelekea ndiko kilipo Kisima cha Giningi?”

“Ndiyo huko huko” nikamjibu.

Je nini kitatokea? ungana nami kesho hapahapa kumekucha.com

No comments:

Post a Comment