Monday, January 5, 2015

WAZAZI WALALAMIKIA WATOTO KUTUMIKISHWA KATIKA MIGODI YA MAWE



Kumekucha blog
Pemba, WAZAZI na walezi Micheweni Wilaya ya Kaskazini Pemba wameitaka Serikali na wadau wa elimu kukemea tabia ya makampuni ya uchimbaji mawe na kokoto kuwaajiri watoto wadogo wenye umri wa kwenda shule kufanya kazi za uchimbaji na ubanguaji wa kokoto.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti baada ya mwandishi wa habari hizi kuwahoji wazazi wa kijiji cha Maziwang’ombe kuwepo kwa taarifa za watoto wao kujishughulisha na kazi za uchimbaji wa mawe na kokoto, wamedai ugumu wa maisha umepelekea wazazi kuwacha huru.
Walisema watoto wengi wenye umri wa kwenda shule wamekuwa wakijishughulisha na uchimbaji wa mawe katika migodi na kupata pesa jambo ambalo limekuwa likiwasahaulisha  umuhimu wa kwenda shule pamoja na wazazi wao
“Tatizo la watoto wetu kujishughulisha na kazi ya uchimbaji wa mawe na kokoto lipo zamani na halikomeshwi---vijana wengi wamekuwa wakikatisha masomo na wengine hawajaenda kabisa na kutojua kusoma wala kuandika” alisema Makame Shaame
“Jambo la kushangaza ni kuona hakuna taasisi wala wadau wa elimu kuhoji watoto wadogo kufanya kazi ya uchimbaji wa mawe na ubanguaji wa kokoto wakiamini kuwa muda huo ni wa kuweko shule” alisema
Kwa upande wake mkazi wa Mapofu, Ali Sheha, amewalaumu wazazi kuwaacha watoto wao kujishughulisha na majukumu ambayo hawana ulazima nao yakiwemo ya kufanya kazi ya kuchimba mawe na kuendesha magari ya mizigo.
Alisema wazazi wengi wamekuwa wakiwapa majukumu watoto  yakiwemo pia ya kuendesha magari ya ng’ombe kwa ajili ya kubeba mizigo na hivyo kuwataka kuwabidiisha na masomo.
“Ni sisi wazazi na walezi wenye kulaumiwa kwa kuwaacha vijana wetu huru na kuacha kuwafuatilia maendelo ya masomo yao mashuleni----ndio utaona wengi wako mitaani na barabarani” alisema Sheha
Alisema ili kuweza kuwasaidia watoto hao ni jukumu la kila mzazi na mlezi kuhakikisha vijana wao wanapata elimu stahiki na kuwa na utaratibu wa kuwafuatilia maendeleo shuleni na kuwa msaada wa maisha yao ya baadae.
                                                      Mwisho

No comments:

Post a Comment