Wednesday, October 7, 2015

EU YAFANYA OPERESHENI BAHARINI

EU kuzuia meli za wahamiaji baharini

Sophia
Muungano wa Ulaya EU umeanzisha operesheni mpya ambayo itahusisha kuzuiwa kwa meli zinazowasafirisha wahamiaji wanaotaka kufika Ulaya zikiwa kwenye bahari ya Mediterranean.
Chini ya operesheni hiyo kwa jina Sophia inayoshirikisha meli sita za kijeshi, wanajeshi wa majini watakuwa na ruhusa ya kuabiri meli, kupekua, kukamata na kuelekeza kwingine meli zinazoshukiwa kutumiwa kusafirisha watu.
Hadi sasa, EU ilikuwa imeangazia tu kufuatilia meli baharini na uokoaji.
Mwaka huu, zaidi ya wahamiaji 130,000 wameingia Ulaya kutoka Afrika kaskazini. Zaidi ya 2,700 wamekufa maji.
Hata hivyo, wahamiaji wengi na wakimbizi, hasa wanaotoroka mapigano Syria, wanafika Ulaya kwa kuvuka na kuingia Uturuki kwa miguu kabla ya kutumia bahari kuingia Ugiriki ambayo ni mwanachama wa Muungano wa Ulaya. Wengi wanataka kwenda Ujerumani.
Mzozo wa wahamiaji unatarajiwa kuwa moja ya masuala makuu yatakayozungumziwa Chansela wa Ujerumani Angela Merkel na Rais wa Ufaransa Francois Hollande watakapofanya hotuba nadra ya pamoja kwa Bunge la Ulaya mjini Strasbourg baadaye Jumatano.
Mara ya mwisho viongozi wa mataifa hayo kutoa hotuba kama hiyo ilikuwa 1989 wakati Francois Mitterrand alipokuwa akiongoza Ufaransa naye Helmut Kohl Ujerumani.
Hata hivyo, kuna mambo ambayo operesheni hiyo ya EU haitaweza kuyafanya. Meli za kivita lazima ziheshimu mipaka ya kimataifa baharini, hii ikiwa na maana kwamba haziwezi kuingia eneo la maili 12 kutoka pwani ya Libya.
Chanzo BBC
Kwa habari, matukio na michezo ni hapahapa tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment