Kumekucha blog
Korogwe, MKUU wa Wilaya ya Korogwe, Mrisho
Gambo, amewataka wenyeviti wa mitaa na vitongoji Wilayani humo ifikapo
Julay mwakani kuhakikisha kila kijiji inasajili kaya 200 kujiunga na Mfuko wa
Bima ya Afya (NHIF).
Agizo hilo amelitoa jana wakati akifungua kituo cha zahanati
kijiji cha Kalalani kata ya Kigwase Wilayani Korogwe kilichojengwa kwa msaada
wa Hifadhi ya Taifa Mkomazi na kusema kuwa kiongozi yoyote ambaye atashindwa
kufanya hivyo atawajibishwa.
Alisema agizo hilo limekuja baada ya kuonekana wananchi wengi wanashindwa kumudu gharama za
matibabu kufuatia kupanda kwa maisha hivyo kuwataka kutoa elimu ya nyumba kwa
nyumba na kusajili wanachama ambao watapata matibabu bure mwaka mzima kwa kuchangia shilingi
elfu tano.
“Natoa agizo viongozi wote wa kijiji, mtaa na kitongoji
kusajili kaya mia mbili kujiunga na mfuko wa bima ya afya---na ifikapo mwezi wa
saba mwakani ambaye hajakamilisha kufanya hivyo bora aachie ngazi” alisema
Gambo
“Wananchi hawana uelewa wa mifuko ya bima ya afya hivyo ni
wajibu wenu kuhakikisha munatoa elimu ya nyumba kwa nyumba ili kila mmoja
atambue umuhimu wa mfuko huo na kuchangia kiasi kidogo cha pesa na kupata
matibabu bure mwaka mzima” alisema
Mkuu huyo wa Wilaya aliwataka wajawazito vipindi vya
kujifungua kwenda katika vituo vya zahanati na kuepuka kujifungulia katika
sehemu ambazo sio salama ili kuepusha matatizo wakati wa kujifungua.
Alisema wajawazito wengi wamekuwa wakipata matatizo yakiwemo
kupoteza damu nyingi na uhai wa mtoto kwa kwenda sehemu ambazo sio salama na hivyo
kuwataka vipindi vya ujauzito kuhudhuria vituo vya afya.
Awali akisoma risala fupi mbele ya mgeni rasmi, Mrisho
Gambo,Meneja Ujirani Mwema Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Ahmed Mbugi,alisema
mradi huo hadi kukamilika kwake umetumia
zaidi ya shilingi milioni 97 ambapo mchango wa wananchi ni milioni 19.
Alisema hifadhi ya Taifa ya Mkomazi kwa kuthamini ushirikiano wa wananchi na
hifadhi hiyo na kuona kero ya kufuata matibabu zaidi ya kilometa 30 ikaona ni
vyema kuwajengea kituo cha afya ikiwa ni moja ya sera za hifadhi hiyo.
“Sera ya hifadhi ya taifa kwa wananchi walioko kandokando ni
kuwapatia huduma muhimu zakiwemo za elimu na afya----kwa muda mrefu tulikuwa
tunaumiza vichwa ni jambo gani muhimu tulifanye kwa wakazi hawa” alisema Mbugi
“Tuliwaita viongozi wa Serikali ya kijiji na Wilaya na
tukapeleka wazo la kutaka kujenga kituo cha afya hapa Kalalani na kwa kweli
tuliungwa mkono na wananchi nao wakalipokea kwa mikono miwili” alisema
Aliwataka kukitunza kituo hicho na kuwa msaada kwa wakazi wa
eneo hilo na jirani na kuwataka kuwa na mashirikiano kwa jambo lolote na kusema
kuwa Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi itashirikiana nao kwa hali na mali.
Alisema kituo hicho kitakuwa mkombozi wa mama wajawazito na
wazee na kuondokana na kero ya kufuata
matibabu kwa zaidi kilometa 30 jambo ambalo baadhi ya vipindi wajawazito
walikuwa wakijifungulia njiani.
No comments:
Post a Comment