HADITHI
KISIWA CHA HARISHI (11)
ILIPOISHIA TOLEO LILILOPITA
Akagawa karata, tukacheza
hadi usiku mwingi. Wenzangu wengine walikuwa wameshaanza kusinzia. Tukavunja
mchezo na kwenda kulala.
Tuliingia katika vyumba
viwili. Chumba kimoja waliingia watu wawili na chumba kingine waliingia watu
watatu. Mmoja aliweka godoro chini. Mimi nilikuwemo katika kile chumba
walichongia watu watatu. Nililala kitandani. Na mwenzetu mmoja ndio alilala
chini.
Licha ya Yasmin kututoa
wasiwasi kuwa Harishi hatatokea usiku ule, hatukulala kwa raha. Mara kwa mara
nilikabiliwa na hofu. Nilipolala kidogo nilijikuta ninagutuka na kutupa macho
huku na huku.
Wakati inakaribia kuwa
alfajiri ndipo nilipopata usingizi wa uhakika. Nikalala moja kwa moja.
Sikuzinduka mpaka kumekucha. Kilichonizindua ni hisia zangu. Niliona kama mlango
wa mle chumbani unafunguliwa na mtu aliyekuwa nje.
Nilipofumbua macho niliona
kweli mlango unafunguliwa na kulikuwa kumeshakucha ingawa Yasmin alituambia
tuamke alfajiri na kuondoka.
Nikajiuliza ni nani
anayefungua mlango. Nikaona kanzu yenye madoa ya damu ikiingia ndani.
Alikuwa harishi!
SASA ENDELEA
Nilishituka sana nilipogundua kuwa aliyefungua ule mlango
alikuwa ni jini Harishi. Tulipaswa kujilaumu kwa uzembe wetu wa kulala hadi
muda ule wakati Yasmin alituambia tuondoke kabla hakujapambazuka.
Na kwa kweli haukuwa uzembe
bali tulipitiwa na usingizi, tena wakati mimi nazinduka wenzangu wote walikuwa
bado wamelala.
Harishi aliingia ndani ya
kile chumba. Sasa niliweza kuuona vizuri uso wake. Alikuwa na macho makubwa
yenye makengeza.
Nikajifanya kama nimelala
lakini nilikuwa nikimuangalia kwa pembeni na kwa makengeza huku mwili wangu ukitetemeka kwa
hofu.
Pengine ni kutokana na ale
makengeza yake, Harishi alipoingia mle chumbani macho yake yalikwenda kwa yule
mtu aliyelala chini.
Mara moja aliinama na kumshika
shingo yake kisha akamuinua na kutoka naye ukumbini.
Nikaisikia sauti ya Harishi
akiuliza.
“Hii nyumba ni yako?”
Sikusikia jibu bali
nilimsikia mwenzetu akipiga ukulele mmoj tu.
“Jamani nakufa!”
Halafu sikusikia kitu tena.
Hapo nilijua mwenzetu huyo
alikuwa ameshatoolewa utosi na alikuwa
akifyonzwa damu.
Ule ukulele aliopiga
ulimuamsha mwenzangu niliyelala naye. Akainuka na kuketi kitandani.
“Kitu gani?” akaniuliza.
Nikaweka kidole changu cha
shahada kwenye midomo yangu kumkataza asitoe sauti.
“Nini kwani?” Sasa sauti yake
ilikuwa ya chini. Uso wake ulikuwa umeanza kushituka.
Nilishuka kitandani
nikamnong’oneza “Harishi!”
Akagutuka. Uso wake
ukabadilika na kuvamiwa na hofu.
“Yuko wapi?” akauliza
kipumbavu
Sikumjibu. Nikamwambia
“Tuingie mvunguni mwa kitanda”
Akakurupuka na kujiingiza
kwenye mvungu huku akiburuza shuka aliyokuwa amejifinika. Tulipoingia kwenye
mvungu huo tukanyamaza kimya.
Tuliamua kujificha humo
japokuwa hatukuwa na uhakika kuwa tutapona. Bada ya muda kidogo tuliona mlango
unafunguliwa tena.
Nilimuona mwenzangu anatikisa
kichwa kwa hofu. Tuliona miguu ya Harishi ikiingia. Ilikuwa miguu mikubwa
iliyochafuka na yenye vidole vyenye kucha ndefu. Ilikuwa pekupeku.
“Kumbe alikuwa ni yule peke
yake!” Tukamsikia akisema Peke yake.
Ile shuka ya mwenzangu
aliyokuwa akiiburuza ilitokeza nje ya mvungu wa kitanda. Harishi akaiona!
Tukaona mkono wake ukishika
ncha ya shuka na kuivuta. Jamaa akaiachia. Shuka yote ikavutwa na kuchukuliwa
na Harishi.
“Hizi ni shuka zangu
ninazoziiba kwa Wahindi. Imewekwa na nani huku mvunguni?’ akajiuliza mwenyewe
kisha akaitupa chini.
Tukaona miguu inageuka na
kutoka. Alipotoka tulishukuru. Mimi nilitambaa hadi kwenye mlango, nikaufungua
na kumchungulia.
Nilimuona akiinama na
kuushika mguu wa mwenzetu aliyemuua, akamburuza kuelekea kwenye mlango wa
kutokea.
Mwenzangu alikuwa amebaki
mvunguni akinitazama. Nikaufunga mlango taratibu kisha nikarudi mle mvunguni.
“Mwenzetu ameuawa”
nikamwambia mwenzangu. “Harishi amemburuza na kutoka naye”
“Alimuona wapi?”
“Mara ya kwanza aliingia
ndani, wewe ulikuwa umelala, Akamsomba pale kwenye godoro na kutoka naye kwenda
kumuua. Ndio pale ulipoamka”
“Kumbe Yasmin alitaka tufe
alipotuambia tulalae humu?”
“Ni makosa yetu sisi. Yasmin alituambia tutoke
Alfajiri, sisi tumelala hadi saa hizi kumekucha”
“Lakini ni kweli”
Wakati tunazungumza kwenye
mvungu, Yasmin akaingia.
Tulipoona miguu yake tulitoka mvunguni.
“Jamani niliwambia nini?”
akatuuliza kwa kutaharuki.
ITAENDELEA KESHO NINI KITATOKEA, kumekucha blog
No comments:
Post a Comment