SIMULIZI
KISIWA CHA HARISHI (10)
ILIPOISHIA TOLEO LILILOPITA
Tulikula pilau ikiwa ndani ya
kapu. Tukashiba na kupata nguvu.
“Nimesahau kuwachukulia maji
ya kunywa” Yasmin akatuambia.
“Na maji tuliyokuwa nayo
yamekwisha” nikasema.
“Lakini kwa leo Harishi
hatarudi, mnaweza kuja nyumbani” Yasmin akatuambia.
“Mh!. Nyumbani kwako
kunaogopesha” nikamwambia Yasmin.
“Tunaweza kwenda mnywe maji
halafu mtarudi huku huku”
Tukajadiliana na Yasmin,
mwisho tukaamua turudi katika lile jumba. Tukarudi.
Tulipofika alitupatia maji ya
kunywa. Tukamshukuru kwa wema wake.
“Bado mna wasiwasi?” Yasmin
akatuuliza.
“Kuwa na wasiwasi ni lazima”
nikamjibu na kuongeza. “Tunajiona kama tuko kwenye vita”
“ Kwa leo msiwe na wasiwasi.
Yule jini hatarudi tena. Kama ni kurudi ni
kesho. Tunaweza kukaa tukaongea hadi usiku mkaenda zenu”
Tukashauriana na kukubaliana
tukae hadi usiku kwa vile mwenyeji wetu ameshatuhakikishia kuwa tutakuwa
salama. Pia tulikuwa tunamuhurumia Yasmin aliyekuwa mpweke katika jumba lile.
Tukaona tukae tumchangamshe.
Tukakaa kwenye ule ukumbi
pamoja na Yasmin na kuanza kuzungumza.
“Yasmin alitupa hadithi ya
jinsi alivyofikishwa katika jumba lile na jinsi alivyokuwa akilia katika siku
za mwanzo mwanzo.
ITAENDELEA
.
“Lile jini hata ukilia,
halijali. Linakwambia utazoea tu. Na ni kweli kadiri siku zilivyokwenda
nilijikuta nikizoea” Yasmin aliendelea kutuhadithia.
“Sasa mnaishije, wakati wewe
ni mtu na yule ni jini?” Mwenzetu mmoja akamuuliza.
“Tunaishi kama mke na mume
ingawa mwenzangu ni jini lakini ndio nimeshamzoea. Ameshaniambia kwamba nitaishi
naye hadi kufa kwangu”
“Je kama akifa yeye?”
nikamuuliza.
“Amesema yeye hatakufa
haraka. Umri wa majini ni mrefu sana.
Pale alipo ana miaka mia tatu na anaweza kuishi hadi miaka mia tano”
“Loh!. Wewe utakufa, yeye
ataendelea kuishi kwa miaka mingi sana”
Mtu mmoja akamwambia Yasmin.
“Lakini mimi ningependa kujua
hisia zako. Unajisikiaje unapohisi kuwa utaishi ndani a jumba hili hadi ufe
wakati bado ni msichana mdogo” Mimi nilimuuliza Yasmin swali hilo.
Yasmin akabetua mabega.
“Nasikia vibaya lakini
nitafanyaje sasa. Nimelia nimechoka, sasa silii tena”
“Kwa hiyo ndio unaishi
ukisubiri kifo chako kitokee humu humu ndani?” Mtu mwingine alimuuliza.
Lilikuwa si swali zuri. Sikulipenda. Lakini Yasmin alimjibu.
“Wakati mwingine najidanganya
kwamba iko siku yaweza kutokea miujiza nikaokolewa kwa namna nisiyoijua.
“Na tangu uishi humu
hakujatokea watu kama sisi wakaingia katika
jumba hili?” nikamuuliza.
“Nyinyi ndio watu wa kwanza
kuwaona tangu nianze kuishi katika jumba hili”
Tukaendelea kuzungumza na
Yasmin hadi alipotuambia kuwa anakwenda kupika chakula cha usiku.
Tukabaki sisi peke yetu na kuendelea
kuzungumza na kujadiliana kuhusu maisha ya Yasmin na maisha yetu wenyewe.
Jua lilipokuwa limekuchwa
nilimfuata Yasmin jikoni nikamwambia kwamba tunaondoka.
“Kwanini…subirini mle
chakula. Nimepika chakula kingi kwa ajili yenu” Yasmin akaniambia
“Giza linaingia. Tuna hofu yule jini anaweza
kutokea. Acha tuondoke tu”
“Jamani mkiwepo
mnanichangamsha na mimi. Sasa mnataka kwenda wapi?”
“Tunarudi kule kule
ulikotukuta”
“Kwanini jamani? Nimewambia
Harishi hawezi kurudi leo labda kwa kesho. Mnaweza hata kulala hapa na mkawa
salama. Muhimu ni kuamka kabla hakujapambazuka mwende zenu”
“Unajua tuna hofu na
wasiwasi, wenzetu wawili wameshauawa humu humu ndani”
“Sasa kule mtakaaje usiku huu
na baridi? Je mvua ikinyesha usiku huu mtafanyaje. Si bora mlale hapa hapa”
“Ngoja nikawashauri wenzangu”
nikamwambia Yasmin na kurudi kule ukumbini. Yasmin naye akanifuata.
“Yasmin amesema tusubiri
chakula na pia tunaweza kulala hapa hapa” nikawambia wenzangu.
“Tulale hapa hapa?” Mtu mmoja
akaniuliza kwa mshituko.
“Hakuna neno. Mnaweza kulala
tu ilimradi muamke alfajiri kabla ya kupambazuka mwende zenu” Yasmin akawambia.
“Una hakika kwamba Harish
hatakuja usiku huu?’
“Hatakuja tena kwa leo ila
kesho anaweza kuja. Sasa kwa vile sijui atakuja saa ngapi ndio maana nninawambia
muondoke alfajiri”
Yasmin alipoona wenzangu
wameduwaa wakitazamana kutafakari yale maneno yake akatuambia.
“Jamani kuweni na mimi. Hivi
nashukuru kupata wenzangu wa kunichangamsha. Harish hatakuja tena leo”
“Mimi naona tumsikilize
mwenyeji wetu, acha tukae” Nikawambia wenzangu kwa kumuonea huruma Yasmin.
Pia huko tulikotaka kwenda
hakukuwa salama. Tungeweza kushambuliwa na wanyama usiku ule au kunyeshewa na
mvua.
Tukakubaliana kuwa tubaki na
Yasmin.
“Hakuna lolote litakalotokea,
kaeni kwa roho moja. Mimi ndiye ninayejua kawaida na nyendo za Harishi.
Mnachotakiwa ni kujihimu wakati wa alfajiri muondoke humu ndani ili kama kesho atatokea asiwakute” Yasmin akatusisitizia
kabla ya kurudi jikoni.
Baada ya muda kidogo
alituletea chakula, tukala pamoja na yeye.
Tulipomaliza kula Yasmin
aliondoa vyombo. Aliporudi tena alikuwa ameshika karata. Akaketi na kutuambia.
“Sasa tuchezeni karata, tukichoka tunakwenda kulala”
ITAENDELEA KESHO
USIPITWE NA KISA HIKI CHA KUSISIMUA KESHO NINI KITATOKEA WAKATI WA KUCHEZA KARATA
No comments:
Post a Comment