Wednesday, December 3, 2014

Kumekucha blog, Handeni

Handeni,KERO ya upatikanaji wa maji Wilayani Handeni Mkoani Tanga bado limekuwa  likiwasumbua wakazi wake na hivyo kuitaka Serikali kama iko na dhamira ya kweli ya kulipatia ufumbuzi kuanza mchakato wake.

Wakizungumza wakati wa kongamano la vijana na Maendeleo jana, walisema wagonjwa wengi katika vituo vya afya wanaugua magonjwa ya kichocho na matumbo na kushindwa kufanya kazi za kujiletea  maendeleo.

Walisema kwa miaka mingi viongozi wa Serikali na wa vyama wamekuwa wakitoa matumaini ya kulimaliza tatizo hilo lakini hakuna dalili zozote na hivyo kutaka kuangaliwa kwa jicho la huruma ili kulinda afya za wananchi.

“Serikali imekuwa ikipiga nara ya kampeni yake ya kilimo kwanza----mimi nasema maji kwanza kwani bila ya maji huwezi kufanya jambo lolote na hata huko maofisini hakutakalika” alisema Rajab Shamte

“Naiomba Serikali kubadilisha kauli mbiu yake na kusema maji kwanza na sio kilimo kwanza----bila ya maji huwezi kulima hata bustani majumbani” alisema Shamte

Vijana hao wamesema wamekuwa wakishirikishwa katika makongamano mbalimbali kuzungumzia kero ya maji na kutumika pesa za wananchi  lakini hakuna linaloendelea zaidi ya malalamiko hayo kuishia katika makaratasi.

Kwa upande wake mkazi wa Misima, Farijala Said. Aliwataka vijana wenzake kuutumia vyema uchaguzi wa Serikali za mitaa kwa kuwachagua viongozi ambao watakuwa na uchungu na wananchi.

Alisema vipindi vya kampeni za uchaguzi ni wakati wa kuwachagua watu ambao watakuwa na moyo wa kuitumikia jamii na kuwasikiliza ikiwa na pamoja na kuzifikisha kero zao katika ngazi husika.

Alisema vipindi vya uchaguzi wamekuwa wakizuka wagombea na kutoa  ahadi kemukemu na kushindwa kuzitekeleza jambo ambalo wananchi wanatakiwa kuwa makini na watu hao.

“Nawaomba vijana wenzangu kipindi hiki cha kampeni za uchaguzi wa Serikali za mitaa kuwa makini na wagombea-----hii ni kutokana na kuzoea kudanganywa” alisema Said

Aliwataka vijana kujitokeza kwa wingi siku ya uchaguzi wa viongozi na kuchagua wanaofaa ambao watakuwa bega kwa bega na wananchi walio katika kuharakisha maendeleo yao.

                                         Mwisho

No comments:

Post a Comment