Kumekucha blog
Tanga,WANAHARAKATI na wadau mbalimbali
wanaopiga vita vitendo vya Ukatili wa kijinsia Tanga, wamedai kuongezeka kwa Maambukizi ya Virusi vya
Ukimwi Mkoani humo ni kutokana na baadhi ya wanaume kuwalazimisha wanawake
kufanya vitendo vya ngono na usagaji kwa wanawake.
Akizungumza katika kilele cha siku 16 za kupiga vita vitendo vya
ukatili wa kijinsia jana, Afisa Mradi mwandamizi wa Asasi ya Kiraia ya Tree of
Hope, Goodluck Malilo, alisema kuongezeka kwa maambukizi ya virusi vya Ukimwi
ni kutokana na wanaume kuwalazimisha
wanawake kufanya vitendo vya ngono bila ridhaa.
Alisema jamii kama haitopiga vita vitendo vya ukatili wa
kijinsia kwa wanawake na watoto, maambukizi ya virusi vya Ukimwi havitopungua
na hivyo kuitaka kukemewa kwa nguvu zote.
“Leo tunaadhimisha siku kumi na sita za kupiga vita vitendo
vya ukatili wa kijinsia----tumeona maambukizi badala ya kupungua yanazidi
kuongezeka kwa kasi” alisema Malilo na kuongeza
“Kuna baadhi ya watu wanaojitambua wamekuwa wakiwalazimisha
iwe ni wanaume au wanawake kufanya vitengo vya ngono zembe huku wakijijua kuwa
wako na maambukizi---kwa pamoja tupige vita na tuishinde” alisema
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Asasi ya Tree of Hope,
Fourtunata Manyeresa, amewataka wanawake na wasichana mashuleni kutoa taarifa
za vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia kwa walimu wao .
Alisema kuna baadhi ya wanawake na wasichana mashuleni
wamekuwa wasiri baada ya kufanyiwa vitendo vya ukatili wa kijinsia na kudhani
kuwa kusema itakuwa aibu na fedheha kwa
jamii.
Alisema hali hiyo pia imekuwa ikitokea majumbani ambapo
wanawake wamekuwa wakifanyiwa ukatili wa kijinsia kwa waume zao na hivyo
kuwataka kuwa na moyo wa ujasiri kwa kutoa taarifa katika madawati na vyombo
vya sheria.
“Kampeni bado inahitajika majumbani na mashuleni pamoja na
kutoa elimu katika sehemu za wazi hii ni kutokana na watu kumezea baada ya
kuogopa kusema juu ya vitendo wanavyofanyiwa iwe ni waume zao au marafiki wa
kiume na wa kike” alisema Manyeresa
Katika kuadhimisha siku 16 za kupiga vita vitendo vya ukatili
wa kijinsia Asasi hiyo ya Tree of Hope ilienda sambamba na kampeni ya Tunaweza
iliyolenga kusajili wanamabadiliko wanaume kwa wanawake watakaokuwa mstari wa
mbele kukemea na kupiga vita vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa kupita mitaani
kuhamasisha kujisajili.
No comments:
Post a Comment