Thursday, December 4, 2014

Walemavu wataka Chuo Kikuu



Kumekucha blog
Tanga,JAMII ya walemavu Mkoa wa Tanga wameitaka Wizara ya Elimu na Mafunzo Ustadi (Veta) kujenga chuo kikuu  maalumu kwa walemavu ili kutoa hamasa kwao katika kusoma na kujiendeleza kimasomo  shuleni.
Akizungumza mara baada ya kumalizika kongamano la walemavu wa viungo na wasiona jana, Mratibu wa Walemavu Wasiona Tanga (TLB), Jumaa Mwakachalika, alisema kuwepo kwa chuo hicho itakuwa chachu kwa jamii ya walemavu kielimu.
Alisema changamoto hiyo pia itawasukuma wazazi wenye watoto walemavu kuwabidiisha watoto katika elimu kwa kuelewa kuwa ataweza kusoma masomo ya juu Chuo Kikuu baada ya kuwepo kwa misingi ya kumfikisha huko.
“Kama walemavu watajengewa chuo kikuu maalumu kwa ajili yao ni wazi kabisa wazazi na watoto wenyewe watakuwa na misukumo ya kujibidiisha darasani----na hii ni kutambua kuwa iko siku atasoma chuo kikuu” alisema Mwakachalika
“Hii sio kuwa ni ubaguzi bali tutaka kuongeza changamoto katika ushindani wa kielimu nchini---kuna dhana kuwa walemavu hawawezi kufika masomo ya juu kama walivyo wengine jambo ambalo tunataka kufuta msemo huo” alisema
Kwa upande wake mlemavu wa viungo, Mwanahawa Tuwa, ameitaka Serikali kuwalazimisha wajenzi wa majengo ya huduma za umma kukumbuka kuweka miundombinu ya walemavu.
Alisema majengo mengi yahana miundombinu hiyo na badala yake wamekuwa wakijenga njia ya kupita kwa  gorofa ya kwanza chini na hivyo kushindwa kuzifikia huduma nyengine  majengo yenye zaidi ya gorofa moja.
“Majengo mengi hayana miundombinu ya walemavu na hata yale ambayo yako nayo wamejenga sehemu ndogo tu ya kuingia katika jengo-----zaidi ya hapo huna ofisi nyengine ambayo unaweza kufika” alisema Tuwa
Alisema hali hiyo imekuwa ikiwasababishia walemavu wengi kushindwa kupata huduma kwa wakati na usahihi baada ya baadhi ya mambo kutumishia hata jambo ambalo ni siri.
Alishauri Serikali kuzuia vibali vya ujenzi kwa wakandarasi ambao hawana michoro ya miundombinu ya walemavu ikiwa na pamoja kuweka sheria  ujenzi wa majengo ya Serikali na umma.
                                                        Mwisho


No comments:

Post a Comment