KUMEKUCHA BLOG
Tanga,WAKATI jeshi la polisi likiumiza
vichwa kuwabaini wafanyabiashara wa kusafirisha wahamiaji haramu kwa kutumia mipaka
na nchi jirani ya Kenya , polisi Mkoani Tanga imefanikiwa kumkamata mtu
anaedaiwa kuwa kinara wa usafirishaji.
Mtu huyo alietajwa kuwa ni Ali Mbukuzi (27) mkazi wa
kijiji cha Chongoleani kata ya Zingibari Wilayani Mkinga Mkoani hapa, anadaiwa
kuwa kinara wa kusuka mipango na kuwasafirisha kupitia njia za panya ikiwemo
misitu ya Horohoro na Handeni.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana,
kamanda wa polisi Mkoani hapa, Freisser Kashai, alisema tukio hilo lilitokea
jana saa 8 usiku wakati polisi wakiwa katika doria katika vijiji na msitu wa
Horohoro unaopakana na nchi jirani ya Kenya.
Alisema polisi ilitaarifiwa kuwepo kwa kundi la
wahamiaji haramu ambao walikuwa wamefichwa katika nyumba kijiji cha Zingibari
Wilayani Mkinga wakitokea nchi jirani ya Kenya.
“Tumemkamata mtu ambaye tunadhani ndie kinara wa
kusafirisha na kusuka mipango ya kusafirisha wahamiaji haramu----kwa muda mrefu
tulikuwa tunamtafuta na alikuwa akikwepa mitego yetu” alisema Kashai na
kuongeza
“Tulivamia banda lililoko porini na kumkuta akiwa
amelala usingizi na wahamiaji haramu wa Kiethopia na aliposhtuka hakuweza
kukimbia---tunamuhoji ili kuujua mtandao mzima” alisema Kashai
Akitoa wito kwa wananchi wanaokaa kandokando na mpaka
wa Mombasa , kamanda Kashai, aliwataka kuacha kushirikiana na watu
wanaosafirisha wahamiaji haramu pamoja na magendo na kusema kuwa msako
utafanywa usiku na mchana.
Alisema tatizo kubwa kwa wananchi wanaokaa karibu na
mipaka wamekuwa wakiogopa kutoa taarifa za kihalifu na za kimagendo na hivyo
kuwataka kuwasiliana na polisi kwa kutoa taarifa.
“Tatizo kubwa kwa wakazi wa mipakani wamekuwa wasiri
na hofu ya kutoa taarifa za kihalifu----huenda wana maslahi nayo ndio maana
wanawaficha----dhamira yetu ni kuharibu mitandao yote ya magendo na
usafirishaji binadamu” alisema Kashai
Alisema hatua kali zitachukuliwa mtu yoyote ambaye
atabainika kwa namna moja au nyengine kushirikiana na wahalifu na hivyo
kuwataka kuwa makini na zoezi hilo litafanyika muda wowote.
No comments:
Post a Comment