Sunday, April 12, 2015

VISHOKA WAZIDI KUIUMIZA KICHWA TANESCO, LUSHOTO

Tangakumekuchablog

Lushoto, SHIRIKA la umeme Tanzania (Tanesco) Wilayani Lushoto Mkoani Tanga limefanikiwa kugundua kusimikwa nguzo nne za umeme na watu wanaoaminika kuwa ni vishoka  ambazo zilikuwa katika hatua za mwisho za  kuunganishwa  umeme  na kuingizwa majumbani.

Hatua hiyo imekuja baada ya operesheni saka vishoka iliyofanywa kwa siku tatu katika maeneo mbalimbali Wilayani humo na kufanikiwa kugundua wizi wa umeme katika nyumba pamoja na usimikaji wa nguzo za umeme kinyume na taratibu.

Akizungumza katika eneo la tukio kijiji cha Baga na  Mtae ziliposimikwa nguzo hizo, Kaimu meneja wa Shirika la umeme Tanesco Lushoto, Daudy Kupaza, alisema kugundulika huko kulikuja baada operesheni saka vishoka ambayo wameifanya kwa siku  tatu mfululizo.

Aliwataka wateja ambao wanataka kuunganishiwa  umeme majumban  kufuata taratibu kwa kufika katika ofisi za shirika hilo na kuepukana na vishoka ambao huwatapeli .

“Tunatambua kuwa kuna watu ambao ni vishoka kwa kujifanya wafanyakazi wa shirika la umeme-----watu hawa wamekuwa wakitusumbua sisi na wateja wetu” alisema Kupaza na kuongeza

“Katika operesheni yetu saka vishoka tumegundua kusimikwa kwa nguzo nne kinyume cha sheria---na sasa tunamtafuta huyo alieziweka na tuko katika uchunguzi na mara tutakapomgundua itakuwa fundisho kwa wengine” alisema

Kwa upande wake mkazi wa kijiji cha Bagai, Shaban Juma, amelitaka shirika la umeme kuwaelimisha wateja wao wanaotaka kufungiwa umeme hasa wa vijijini ili kuepuka kutapeliwa na mafundi vishoka.

Alisema wateja wa vijijini ambao umeme bado haujafika ni vyema shirika hilo kutoa elimu  ya kujua  namna ambavyo  taratibu za kupatiwa umeme zinavyofuatwa  na kuepuka kutapeliwa na vishoka.

“Kama shirika la umeme halitokuwa na utaratbu wa kuwaelimisha wateja wake hasa yale maeneo ya vijijini  ambayo wanataka kupeleka umeme  mafundi vishoka hawataisha” alisema Juma

“Kuna vishoka wengine wanadiriki hata kuwa na vitambulisho feki vinavyowatambulisha kama wafanyakazi wa shirika la umeme----na hii inaleta uaminifu wanapokuja kwetu na pale wanapotutapeli ndio tunashtuka” alisema

Alisema ili kuweza kutokomeza vishoka ni vyema shirika la umeme Tanzania Tanesco kuweka sheria kali za kuwabana vishoka na kuweza kulitokomeza tatizo hilo ambalo limeota mizizi kila kona.

                                                          Mwisho

No comments:

Post a Comment