Uchambuzi huu wa magazeti unaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya kituo cha Elimu Cha Candle Education Centre Tanga, Kituo kinaongoza kufaulisha wanafunzi kidato cha pili hadi cha sita kwa wanaorisiti na wale wanaojiendeleza. Kituo pia kinatoa kozi ya Kiingereza na Computer. Wapo Tanga mkabala na Bank ya CRDB simu 0715 772746
JAMBOLEO
Mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la
Matata Sheba mkazi wa Tungi Manispaa ya Morogoro amenyofolewa sehemu za
siri na kuliwa na mambo wakati akioga mtoni.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo
Diwani wa kata ya Tungi, Deogratius Mzeru alisema Sheba alikwenda mtoni
kuoga gafla alitokea mamba na kumg’ata.
Alisema wakati Sheba akijaribu kujiokoa
kwa kupiga kelele za kuomba msaada alifanikiwa kutoka kwenye maji wakiwa
wanavutana na mamba na kelele zilipozidi zilimshtua mamba na kumg’ata
korodani na kurudi majini.
“Juzi jioni wakati Shebe anaoga mara
alitokea mamba anayeishi katika mto huo na kutaka kummeza lakini katika
purukushani alifanikiwa kutoka nje ya maji lakini alikuwa ameng’atwa
sehemu zake za siri ”Mzeru.
Alisema baada ya taarifa hizo kumfikia aliamua kutafuta usafiri wa kumpeleka hospitali ambapo hali yake ilikuwa mbaya.
Mganga mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa wa
Morogoro Rita Lyamuya alisema hali ya mgonjwa imekuwa ikiimarika ingawa
bado ana maumivu.
MWANANCHI
Serikali imetishia kuanza kutekeleza
sheria inayodhibiti asasi za kijamii na kidini, ikizitaka taasisi hizo
kuacha mara moja kutoa matamko yanayolenga kuwashawishi waumini wao
waikatae Katiba Inayopendekezwa na pia kuwapangia nini cha kufanya
katika Uchaguzi Mkuu ujao na kusema watakaobainika watachukuliwa hatua
kali.
Katika kuzipiga ‘kufuri’ taasisi hizo,
Serikali imesema kuanzia Aprili 20 itazifuta taasisi zote zilizosajiliwa
na Wizara ya Mambo ya Ndani ambazo havifuati matakwa ya kisheria ya
kuwasilisha taarifa zao za mwaka za ukaguzi wa hesabu na kulipa ada za
kisheria.
Hata hivyo, viongozi wa dini ya Kikristo
na Kiislamu waliozungumza na gazeti hili jana kuhusu kauli hiyo,
wamesema taasisi zao zinawakilisha watu, na hivyo zina haki ya kikatiba
na kisheria kupinga jambo lolote zitakaloona linakwenda kinyume na
maslahi ya Taifa na kwamba ziko tayari kukaguliwa.
Waziri wa Mambo ya Ndani, Mathias
Chikawe alisema jana kuwa kazi hiyo ya kupitia usajili wa vyama hivyo
itaanza kwa vyama vilivyopo jijini Dar es Salaam, baadaye kuendelea nchi
nzima.
Vyama vyote vitakavyofutiwa usajili vitawekwa katika tovuti ya wizara hiyo na havitaruhusiwa kuendelea na shughuli zake.
“Matukio ya aina hii yanapofanyika
yanaashiria kuvuruga amani na utulivu nchini. Kazi ya Serikali ni
kuhakikisha usalama wa watu wote unaimarishwa ili shughuli zote za
kisiasa, kidini, kijamii na kiuchumi, zinatekelezwa kwa misingi ya
kisheria,” alisema Chikawe.
Uamuzi huo umekuja wakati Jukwaa la
Wakristo likiwa limetoa tamko la kuwataka waumini wake kujiandikisha kwa
wingi katika Daftari la Kudumu la Wapigakura, kuisoma Katiba
Inayopendekezwa na kujitokeza kuikataa kwa kupiga kura ya hapana.
Jukwaa hilo, linaloundwa na Jumuiya ya
Kikristo Tanzania (CCT), Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki Tanzania
(TEC) na Umoja wa Kanisa la Pentekoste Tanzania (CPCT), linadai kuwa
Serikali imewaahidi Waislamu kuwapa Mahakama ya Kadhi ili waipigie
Katiba Inayopendekezwa kura ya ndiyo. Jambo ambalo limesema
litasababisha mgawanyiko.
Mbali na jukwaa hilo, pia Jumuiya na
Taasisi za Kiislamu liliwataka waumini wake kuikataa Katiba
Inayopendekezwa iwapo Serikali itashindwa kuwasilisha bungeni muswada wa
Mahakama ya Kadhi ili chombo hicho kitambulike kisheria. Muswada huo
uliondolewa baada ya kuibuka kwa mvutano mkali katika mkutano wa 19 wa
Bunge uliomalizika Aprili Mosi, mwaka huu.
Katika siku za hivi karibuni viongozi
mbalimbali wa dini wamekuwa wakitaja wazi sifa na hata majina ya watu
wanaopaswa kugombea urais katika Uchaguzi Mkuu ujao, na wakati fulani
vikundi vya wachungaji na masheikh kwa nyakati tofauti vilienda nyumbani
kwa kada wa CCM, Edward Lowassa mjini Dodoma kumshawishi atangaze nia
ya kugombea urais.
“Kauli za viongozi wa dini kuhusu
masuala ya Katiba au Uchaguzi Mkuu ujao zinakiuka sheria za usajili wa
taasisi zao. Viongozi ambao tayari wameshatoa matamko ya aina hiyo
tunawapa onyo kwa sasa, wasirudie tena,” alisema Waziri Chikawe.
Alisema waumini wana haki ya kuamini
mafundisho ya dini zao, lakini wanapaswa kutekeleza masuala yao ya
kisiasa na kijamii kwa utashi wao bila ya kushawishiwa na mtu yeyote,
kama sheria za nchi zinavyotaka.
MWANANCHI
Huenda Watanzania wanaougua magonjwa ya
moyo wakaepuka kusafiri nje ya nchi kwa ajili ya matibabu baada ya tiba
ya kuzibua mishipa ya moyo iliyoziba kufanyika kwa mara ya kwanza
nchini.
Asilimia kubwa ya Watanzania wamepoteza
maisha kutokana na magonjwa ya moyo yanayosababishwa na mtindo wa maisha
ikiwamo mshtuko wa moyo na kuharibika kwa valvu za moyo.
Akizungumza wakati timu ya madaktari
ikiendelea na tiba hiyo katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH)
jana, Mkuu wa Idara ya Tiba na Upasuaji wa Moyo, Profesa Mohamed
Janabi alisema hayo ni mapinduzi makubwa na yenye tija katika sekta ya
afya.
“Tanzania imeandika historia ya pekee na
huenda kasi ya kupeleka wagonjwa nje ya nchi ikapungua kwa kiasi
kikubwa kwa sababu wale wote wenye matatizo haya watapatiwa tiba hapa
hapa,” alisema.
Idara ya Tiba na Upasuaji itashirikiana
na wataalamu kutoka Marekani na India kuhakikisha wanafanya uchunguzi,
kutoa tiba kwa wagonjwa wa moyo na kufundisha madaktari wa nchini.
Akielezea jinsi matibabu yanavyofanyika,
Profesa Janabi ambaye pia ni Daktari Bingwa wa magonjwa ya Moyo
alisema, tiba hiyo inatumia kifaa maalumu kiitwacho ‘stent’ ambacho
huingizwa hadi kwenye moyo na kuzibua mishipa ya damu iliyoziba.
Alieleza kuwa, mtambo maalumu uitwao
‘Cath Lab’ huingizwa mwilini mwa mgonjwa na kusaidia kuona iwapo kuna
tatizo la moyo kabla ya kuweka kifaa hicho cha kuzibua mishipa ya
kusambaza damu kwenye moyo.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali
ya Taifa ya Muhimbili, Hussein Kidanto alisema, ujio wa tiba hiyo una
manufaa makubwa kwani Watanzania.
Kwa upande wake, Daktari Bingwa wa
Upasuaji wa Moyo kutoka Kituo cha Afya cha Virginia, Marekani, Peter
O’Brien alisema, fursa ya kuwafunda madaktari wa Kitanzania ni ya muhimu
kwake kwani inampa ujuzi zaidi hata kujifunza jinsi nchi nyingine
zinavyotoa tiba ya moyo.
“Watanzania hawana budi kuacha tabia
hatarishi zinazosababisha magonjwa haya kama vile, kuvuta sigara, kula
vyakula vya kusindikwa na vyenye mafuta mengi, pia wafanye mazoezi,”
alisema.
MWANANCHI
Jumuiya ya Umoja wa Ulaya EU imeachia
Serikali shilingi bilioni 107 kati ya trilioni 1 za bajeti
zilizoshikiliwa kwa muda kutokana na sakata la ufisadi katika akaunti ya
Tegeta Escrow.
Taarifa iliyotolewa jana na mkuu wa
kitengo cha siasa na habari cha EU, Luena Reale alisema hatua hiyo
imefikiwa baada ya wahisani wa maendeleo kukubaliana kuziachia kabla ya
mwaka wa fedha 2014/15 kuisha.
“EU imeridhishwa na hatua za Serikali ya
Tanzania na taasisi nyingine zilizoshiriki katika kushughulikia suala
la Escrow’ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Mwaka jana baada ya sakata hilo kupamba
moto, jumuiya ya wahisani wa maendeleo waliitaka Serikali kuchukua hatua
dhidi ya waliohusika.
Mwenyekiti wa wahisani hao ambao ni
ambao ni balozi wa Finland Sininka Antila alitangaza uamuzi huo wa
kusitisha fedha hizo mwaka jana, akisema wataziachia pindi ripoti ya
uchunguzi itakapotolewa na CAG na hatua kuchukuliwa.
NIPASHE
Wanafunzi sita wa shule ya msingi,
wamefariki dunia kwa kupigwa na radi na wengine 15 wamejeruhiwa miongoni
mwao vibaya kufuatia mvua kubwa iliyoambatana na upepo mkali na radi
kunyesha katika Manispaa ya Kigoma/Ujiji jana.
Tukio hilo lilitokea jana saa 5:00 asubuhi katika Shule ya Msingi Kibirizi iliyopo kwenye manispaa hiyo.
Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya
Mkoa wa Kigoma ya Maweni, Dk. Fadhili Kibaya, alisema alipokea maiti za
watu wanane zikiwamo za wanafunzi sita wa Shule ya Msingi Kibirizi na
moja ya mwalimu wao jana saa 6:00 mchana.
Alisema maiti nyingine ni ya mwanaume mkazi wa Bangwe katika manispaa hiyo. Alisema mbali ya maiti, pia alipokea majeruhi 15.
Aidha, alisema wengine watano wako
kwenye chumba cha uangalizi maalum (ICU) na wengine walitibiwa na
kuruhusiwa kurudi nyumbani kwao.
Kwa upande wake, Mwalimu wa Shule ya
Msingi Kibirizi, Emmanuel Wilbert, alisema mwalimu aliyefariki dunia
alitoka darasa la tatu na kuingia ofisi ya walimu na kukaa akiendelea na
shughuli zake kama kawaida.
Wilbert alisema baada ya muda mvua kubwa
iliyoambatana na upepo mkali na radi huku walimu wengine wakiwa
madarasani wakiendelea na vipindi, ilipiga radi iliyosababisha kifo cha
mwalimu na wanafunzi hao waliokuwa madarasani.
Alisema baada ya tukio hilo, wanafunzi
na walimu walikimbia ovyo na mwalimu mwingine Merina Serilo, alipigwa na
radi na kujeruhiwa.
NIPASHE
Asasi zisizo za kiserikali 53
zimemwandikia Rais Jakaya Kikwete, barua ya kumuomba asisaini Sheria ya
Takwimu ya 2015 na Sheria ya Makosa ya Mtandaoni zilizopitishwa na Bunge
hivi karibuni ili kuruhusu kufanyiwa marekebisho kwanza.
Kwa majibu wa barua hiyo iliyosainiwa na
asasi 53 na mtandao wa asasi za kiraia ambayo zinataka sheria hizo
zirudishwe bungeni kuondoa vifungu vinavyokwenda kinyume na Katiba ya
Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977 na haki za binadamu kwa ujumla.
“Tunashauri kabla ya kutia saini sheria
hizi upate muda wa kusikiliza kilio cha jamii juu ya ubaya wa sheria
hizi kwa mustakabali wa taifa.
Sheria hizi zikipitishwa katika utawala
wako zitatia doa dhamira yako nzuri ya kuongeza wigo na uhuru wa habari
na ushiriki wa wadau katika maendeleo ya kitaifa,” alisema.
Barua hiyo imeeleza sababu za kumtaka
Rais kutosaini sheria hizo kuwa ni, malengo ya Sheria ya Takwimu siyo tu
kuratibu takwimu za kitaifa, bali umetoa madaraka makubwa kwa Ofisi ya
Taifa ya Takwimu (NBS) kama kitovu cha utoaji wa takwimu nchini.
“Maana yake ni kwamba taasisi zote za
serikali, mashirika binafsi, taasisi za elimu ya juu, vyuo vikuu na
taasisi za utafiti hazitakuwa na uhuru wa kutoa matokeo ya tafiti
wanazozifanya bila ya kibali au ridhaa ya NBS” ilisema barua hiyo.
NIPASHE
Wanafunzi wa vitivo vya Sayansi ya Afya
wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Kampala-tawi la Dar es Salaam (KIU),
wamegoma kuendelea na masomo baada ya kubaini kuwa kozi wanazosoma
katika chuo hicho hazijasajiliwa katika bodi mbalimbali kama taratibu na
sheria zinazoelekeza.
Walianza mgomo huo tangu Ijumaa
iliyopita baada ya kugundua kuwa kozi wanazofundishwa hazijasajiliwa
katika Bodi ya Mafamasia, Bodi ya Maabara na Baraza na Madaktari.
Walisema jana chuoni hapo kuwa wamekuwa
wakiendelea na masomo bila kugundua kama kozi wanazochukua
hazijasajiliwa katika bodi hiyo huku uongozi wa chuo ukikaa kimya.
Waziri wa Afya wa Serikali ya Wanafunzi
(KIUSO), Kenedy Murunya, alisema walibaini kuwa kozi wanazosoma
hazijasajiliwa baada ya kwenda katika ofisi za bodi na kuelezwa kuwa
hazijasajiliwa.
Wanafunzi waliokumbwa na tatizo hilo ni wale wanaochukua Shahada za maabara, udaktari na upasuaji.
“Wanafunzi walipokwenda Tume ya Vyuo
Vikuu (TCU) waliambiwa kuwa tume imeshafanya asilimia 50 ya usajili wa
chuo hicho na asilimia 50 nyingine zilizobaki zinatakiwa zishughulikiwe
na bodi husika za usajili,” alisema.
Alisema Septemba, 2014 walikwenda Wizara
ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa lengo la kumuona Waziri, Dk. Shukuru
Kawambwa, lakini hawakumuona hivyo kumwandikia barua ili awape majibu
ambayo hadi sasa hawajapatiwa.
Alisema wanaendelea kulipa ada kubwa
japokuwa serikali ilikiagiza chuo hicho kushusha ada cha kushangaza
Baraza la KIU ambalo lipo Uganda lilikataa maagizo ya serikali.
Alisema wanafunzi wa udaktari mwaka wa
pili wanalipa Sh. milioni 8 wakati wa mwaka kwanza wanatozwa Sh. milioni
6.7, maabara sh. milioni 4.8, Famasia milioni 5.4 huku wa mwaka
wakilipa sh. milioni 3.8.
MTANZANIA
Jeshi la Polisi nchini, limesema
Watanzania 866 wamefariki dunia katika kipindi cha miezi mitatu,
kutokana na ajali za barabarani.
Akizungumza na waandishi wa habari
jijini Dar es Salaam jana, Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani,
Mohammed Mpinga alisema kuanzia Januari hadi Machi mwaka huu, ajali
2,116 zimetokea katika maeneo mbalimbali nchini.
Alisema katika ajali hizo, watu 866 wamepoteza maisha na wengine 2,363 kujeruhiwa, ambao baadhi yao wamepata ulemavu.
Hata hivyo nje na kipindi hicho, ajali
nyingine zilizotokea kuanzia Machi 11 hadi April 12, mwaka huu
zimesababisha vifo vya watu wengine 103 na hivyo kufanya idadi ya watu
walipoteza maisha katika kipindi cha miezi mine kuwa 969.
Akizungumzia sababu za ajali hizo,
Kamanda Mpinga alisema ni mwendo kasi usiozingatia alama za barabarani
na kufutika kwa baadhi ya michoro barabarani.
Alisema sababu nyingine, ni baadhi ya
wamiliki wa vyombo vya moto kuhamasisha mwendo kasi kwa madereva wao,
abiria kushabikia na baadhi ya wadau wa usalama barabarani kutowajibika
ipasavyo.
Kamanda Mpinga, alisema uzembe wa
madereva, ubovu wa barabara na uoni hafifu kwa baadhi ya madereva ni
miongoni mwa sababu zinazochangia ajali nyingi kutokea..
Kuhusu hatua, Kamanda Mpinga, alisema
madereva wote waliosababisha ajali za hivi karibuni watachukuliwa hatua,
ikiwa ni pamoja na kunyang’anywa leseni zao.
MTANZANIA
Shirikisho la Vyama Vya Wafanyakazi
Tanzania (TUCTA), linatarajia kuitisha mgomo wa wafanyakazi nchi nzima,
endapo Mamlaka ya Usimamizi wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (SSRA)
haitaondoa kanuni mpya ambayo inaruhusu watumishi watakaostaafu kwa
hiari yao kukatwa asilimia 18 ya mafao yao.
Kanuni hiyo mpya itaanza kutumika Julai mwaka huu ambapo watumishi watakaostaafu kwa hiari watalazimika kukatwa kiasi hicho.
Ili kuhakikisha suala hilo
linashughulikiwa ndani ya muda mwafaka, TUCTA imeazimia kuitisha mkutano
mkuu unaotarajiwa kufanyika Aprili 23 na 24, mwaka huu ili kujadili
suala hilo.
Rais wa shirikisho hilo, Gratian Mukoba
alisema kanuni hiyo ni kandamizi na inawanyima haki watumishi kwa sababu
kulipwa mafao ni haki ya mtumishi aliyestaafu, ingawa pia wakati
wanajadili kuipitisha hawakushirikishwa.
“Tutawahamasisha watumishi kugoma nchi nzima ili kuishinikiza SSRA kubadili kanuni hii kwa sababu ni kandamizi kwa mtumishi.
“Bila ya kufanya hivi, Serikali
itaendelea kutunga kanuni nyingine ambazo zinaweza kutoa nafasi kwa
watumishi kuendelea kufanya kazi hadi miaka 70 ili wakifariki kabla ya
muda huo wawe wamepoteza mafao yao, kutokana na hali hii, hatutakubali
na tunataka iondolewe mara moja,”alisema Mukoba.
Alisema kutokana na hali hiyo, shirikisho hilo linasubiri majibu ya barua hiyo na endapo hawasikilizwa watafanya mgomo huo.
MTANZANIA
Naibu Waziri wa Sayansi, Teknolojia na
Mawasiliano, Januari Makamba ametajwa kuwa mwanasiasa bora kijana na
taasisi ya Tanzania Awards International, jijini Dar es Salaam juzi.
Makamba ameshika nafasi hiyo akiwapita
wanasiasa wengine vijana ambao ni pamoja na Kiongozi wa chama cha ACT
Wazalendo, Zitto Kabwe, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye,
Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, Naibu Waziri wa Fedha
Mwigulu Nchemba, Wabunge Vick Kamata, Esther Bulaya, David Kafulila na
Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Mboni Mhita.
Katika tuzo za mwanasiasa mtu mzima
ushindi umechukuliwa na aliyekuwa Waziri wa Nishati na katika kundi
hilo, Profesa Muhongo alishindanishwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda,
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbrod Slaa, Waziri Sheria na Katiba, Dk.
Asha Rose Migiro na Waziri wa Nchi Katika Ofisi ya Makamu wa Rais,
Muungano, Samia Suluhu.
Wengine ni Mwenyekiti wa NCCR Mageuzi,
James Mbatia, Waziri wa Ujenzi Dk. John Magufuli, Waziri wa Ushirikiano
wa Afrika Mashariki, Dk. Harrison Mwakyembe, Waziri wa Kilimo, Chakula
na Ushirika, Steven Wasira na Balozi wa Tanzania nchini Marekani,
Liberata Mulamula.
Tuzo ya jamii ilichukuliwa na Mwenyekiti Mtendaji wa Makampuni ya IPP, Reginald Mengi.
Waliopewa tuzo za heshima katika jamii ni Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Nyerere na Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Hayati Nelson Mandela.
Waliopewa tuzo za heshima katika jamii ni Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Nyerere na Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Hayati Nelson Mandela.
Si Makamba, Profesa Muhongo wala Mengi waliohudhuria shughuli hiyo badala yake waliwakilishwa na ndugu zao.
Hata hivyo sherehe za kutoa tuzo hizo
zilidororora hasa kwa kuwa Rais Jakaya Kikwete aliyepangwa kuwa mgeni
rasmi hakuhudhuria na aliwakilishwa na mkuu wa mkoa lakini naye
aliwakilishwa na Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Raymond Mushi.
Akitoa ufafanuzi wa tuzo hizo, Mratibu
wa Taasisi hiyo, Amani Mwaipaja alisema zilikuwa katika vipengele vitano
ambavyo ni tuzo ya jamii 2015, tuzo za jamii ya heshima, tuzo jamii
katika haki za binadamu, tuzo ya mwanasiasa kijana na tuzo ya mwanasiasa
mzee.
“Tumeangalia vigezo kadhaa ikiwa pamoja
na uadilidu, uaminifu, utii katika sheria, kuwa na maono, mikakati na
mipango,” alisema Mwaipaja.
HABARILEO
Serikali imesema inafuatilia kwa karibu
maelezo yanayotolewa na Mtanzania Rashid Mberesero (20) aliyekamatwa
Kenya akidaiwa kufanya ugaidi katika Chuo Kikuu cha Garissa
uliosababisha vifo vya watu 148.
Aidha, Serikali imewatoa hofu Watanzania
na kuwaambia kuwa nchi iko salama katika suala la ugaidi. Hayo
yamebainishwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe
jijini Dar es Salaam jana alipozungumzia mustakabali wa nchi kuelekea
kura ya maoni kuhusu Katiba Inayopendekezwa na Uchaguzi Mkuu.
Chikawe alisema wizara yake inafuatilia
kwa makini kile anachozungumza Mtanzania huyo katika mahojiano nchini
Kenya ili kuweza kubaini kama kuna Watanzania wanaoshirikiana naye.
“Kwa sasa amefikishwa mahakamani, lakini
kama serikali tunafuatilia kila anachokizungumza kwenye mahojiano na
wenzetu wa Kenya ili kuweza kuwabaini kama kuna Watanzania wanaohusika
ambao wapo nchini,” alisema.
Mtanzania huyo anadaiwa kukamatwa baada
ya kujificha kwa saa nane akiwa amejichanganya na maiti, lakini baadaye
alipanda na kujificha darini akiwa na mabomu.
Chikawe alisema tatizo la ugadi ni la
kidunia, lakini aliwataarifu Watanzania kuwa nchi iko salama. “Ugaidi ni
tatizo la kidunia, sehemu nyingi kuna matatizo kama hayo, napenda
niwaambie Watanzania nchi yenu iko salama, tuko salama,” alisema.
Aidha, Chikawe alisema Serikali
itachukua hatua kali kwa watu binafsi, vyama vya siasa na taasisi za
dini zitakazobainika kuvuruga usalama na utulivu wa nchi.
Alisema uzoefu unaonesha kila ifikapo
wakati wa kuelekea kufanya chaguzi mbalimbali kumekuwa kukitokea matukio
yanayoashiria uvunjifu wa usalama na utulivu.
Alisema ili kukabiliana na hali hiyo, ni
vyema wananchi, vikundi zikiwemo taasisi za dini kuepuka kushiriki
katika vitendo vinavyoashiria kuvuruga amani na utulivu na kuwa serikali
itachukua hatua za kisheria kudhibiti hali hiyo.
“Kazi ya serikali ni kuhakikisha kuwa
usalama wa watu wote unaimarishwa ili shughuli zote zikiwa ni za
kisiasa, kidini, kijamii na kiuchumi zinatekelezwa kwa misingi ya
kisheria,” alisema.
Chikawe ameonya viongozi wa taasisi za
dini kutoendelea kutoa matamko yanayoashiria kuingilia masuala ya
kisiasa kinyume na sheria ya vyama na katiba zinazosimamia uendeshaji wa
taasisi hizo.
Alitolea mfano tamko lililotolewa na
viongozi wa taasisi za dini wakilenga kuwashawishi waumini wao wafuate
maelekezo yao kuhusiana na masuala ya Katiba Inayopendekezwa na kuhusu
uchaguzi mkuu ujao.
Alisema viongozi wa taasisi za dini wana
haki ya kushiriki katika masuala ya kisiasa kama watu binafsi ila ni
kinyume cha sheria kutumia uongozi wao kushawishi waumini wao watekeleze
matakwa yao ya kisiasa.
“Mfano mwingine ni pale kiongozi au
viongozi wa dini wanapochangisha fedha na kuandamana au kukutana na
wanasiasa kwa kile kinachoelezwa kuwa ni kuwashawishi kugombea nafasi
mbalimbali za uongozi. Hii si kazi ya taasisi za dini na ni kinyume cha
sheria,” alisisitiza.
Tangakumekuchablog inakuletea uchambuzi wa magazeti kila siku , usikose uhondo huu nkujua yote yaliyoandikwa katika magazeti ya Tanzania, ni hapa hapa www.tangakumekucha.blogspot.com
No comments:
Post a Comment