Monday, October 2, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI SEHEMU YA ( 2 )

HADITHI

MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI 2

ILIPOISHIA

“Unajisikia kuumwa?” Lazaro akaendelea kumuuliza.

“Nasikia kichwa kinagonga kwa mbali”

“Hukuuma mtu?”

Sofia akatikisa kichwa.

“Sijauma mtu”

“Wewe si ulikuwa umekwenda jikoni baada ya kuondoka kwenye chakula?”

Sofia alifikiri kisha akajibu.

“Ndiyo nilikwenda jikoni kuchukua pilipili”

“Ulimkuta Pili?”

“Ndiyo nilimkuta”

“Halafu nini kilitokea?’

Sofia alivuta kumbukumbu kisha akatikisa kichwa.

SASA ENDELEA

“Sikumbuki. Kichwa kinaniuma sasa”

Lazaro akashusha pumzi ndefu. Akamtazama mke wake.

“Inawezekana ana malaria na imepanda kichwani” alimwambia mke wake.

“Inawezekana” Vicky alisema huku hofu na wasiwasi vikisomeka wazi usoni kwake.

“Sijui yule msichana amemfanya nini. Mwenyewe hakumbuki kitu”

“Naona kama amemng’ata”

Wakati Waziri Mkuu Dastan Lazaro na mke wake Vicky wakisemeshana, Sofia alikuwa akiwasikiliza na kuwatazama kwa mshangao.

“Nimemng’ata nani?” akawauliza.

“Pili, mpishi wetu” Lazaro akamjibu.

Sofia akatikisa kichwa.

“Hapana, sijang’ata mtu”

“Umemng’ata na ndio sababu una damu midomoni”

Mama yake naye akaongeza.

“Hicho kipande cha kitambaa ulichokuwa umeshika ni cha nguo aliyovaa. Ulikichana wakati umemshika lakini mwenyewe ulikuwa hujijui”

Mshangao wa Sofia sasa ulionekana waziwazi usoni kwake.

Lazaro alimshika mkono mke ake wakatoka mle chumbani.

“Unadhani kitu gani kimesababisha kifo cha yule msichana?” Lazaro akamuuliza mke wake.

Walikuwa wamesimama kando ya mlango.

“Labda alimkaba koo”

“Sidhani”

Sofia akawafuta kusikiliza walichokuwa wanazungumza. Wakaliona tumbo lake, lilikuwa limejaa kama mja mzito. Wakati akiondoka kwenye meza ya chakula, tumbo lake halikuwa hivyo.

“Mbona tumbo limejaa Sofia?” Mama yake akamuuliza.

Sofia akalitazama tumbo lake na kulishika.

“Limejaa kweli mama, na nateuka ladha ya damu tupu”

Lazaro na mke wake wakatambua kwamba Sofia alikuwa amemfyonza damu yule msichana na ndiyo iliyokuwa imejaa kwenye tumbo lake.

“Subiri upelekwe hospitali mwanangu” Lazaro akamwambia.

“Nitakuwa nina malaria baba?”

“Bila shaka”

Lazaro alitoa simu yake akampigia dereva wa mke wake ambaye muda ule alikuwa amesharudi nyumbani.

“Hebu njoo, kuna tatizo kidogo” Lazaro alimwambia dereva huyo kwenye simu.

“Sawa, mzee ninakuja”

“Unaweza kukodi teksi ikulete mara moja, tutailipia”

“Sawa mheshimiwa”

Lazaro akakata simu.

“Mtayarishe mwanao, dereva anakuja umpeleke hospitali”

Mke wa Waziri Mkuu akamtazama Sofia.

“Nenda chumbani mwako ubadili nguo kisha usukutue mdomo wako” alimwambia.

“Sawa mama”

Sofia akaondoka.

“Sofia ndio amemuua yule mpishi wetu” Lazaro akamnong’oneza mke wake.

“Sasa tutafanyaje” Vicky akauliza kwa tashiwishi.

“Sijui mke wangu. Kuliripoti tukio hili ni sawa na kumwaga petroli kwenye moto, linaweza kumpa matatizo Sofia na kuniweka mimi katika wakati mgumu japokuwa najua Sofia alifanya hivyo akiwa hajitambui lakini haitaonekana hivyo”

“Ninajua. Kuna mambo mengi yataangaliwa na kusemwa”

“Ninaweza pia kutakiwa kujiuzulu uwaziri mkuu kwa sababu tukio limetokea nyumbani kwangu na itaonekana nimeshindwa kulizuia’

“Sasa tutafanyaje” Viccky alirudia swali lake.

“Ile maiti tuihifadhi kwanza, tungoje vipimo vya Sofia”

“Sawa. Ngoja nikamuandae. Dereva akija twende naye”

Mke wa Waziri Mkuu akamfuata Sofia. Lazaro akawaita wanawe wengine Vero na Monica.

“Nataka tukio hili liwe siri ya humu ndani, lisitoke nje. Mmenielewa?”

Wasichana hao walikubali kuwa wamemuelewa.

“Sofia ana malaria na imempanda kichwani, bila kujielewa amemng’ata yule msichana mpishi wetu na kumfyonza damu hadi amemuua. Kwa sasa sitaki habari hii ifike kwenye vyombo vya dola wala uraiani”

“Sasa ile maiti tutaipeleka wapi?’ Vero akamuuliza baba yake.

“Tutaihifadhi humu humu ndani tukisubri Sofia apelekwe hospitali. Nimeshamuita dereva. Sasa twendeni tukasaidiane kuiondoa kule jikoni’

Lazaro na wanawe wakashuka ngazi na kuingia jikoni.

“Tumbebe tukamuweke stoo kwa muda” Lazaro akawambia wanawe.

Waliubeba mwili wa Pili na kwenda kuulaza stoo. Baada ya kumlaza, Lazaro aliichunguza ile sehemu ya shingoni iliyokuwa inatoka damu. Akagundua kuwa ilikuwa imepigwa meno na ilikuwa na tundu mbili za meno.

Wakati Waziri na wanawe wanatoka stoo, mke wa Waziri na
Sofia walikuwa wanashuka ngazi. Sofia alikuwa ameshabadili nguo.

“Sisi tuko tayari” Mke wa waziri alimwambia mume wake.

Waziri Dastan alimtazama Sofia. Safari hii alimuona tofauti kidogo. Alikuwa amechangamka na alionekana wa kawaida.

“Mumsubiri dereva awapeleke”

“Sijui atakuja saa ngapi?”

Hapo hapo mlinzi akampigia simu waziri. Waziri alipoipokea aliambiwa.

“Dereva ameshafika”

“Mwambie asubiri afunguliwe geti”

Waziri akakata simu na kumwambia mke wake.

“Dereva ameshafika, yuko nje”

“Ngoja nikamfungulie geti” Alikuwa Vero ambaye alitoka kwenda kufungua geti. Dereva akaingia.

Waziri na mke wake pamoja na Sofia walikuwa wametoka na kusimama karibu na banda la gari.

“Wapeleke hospitali, Sofia anaumwa” Waziri akamwambia dereva huyo.

“Nichukue gari lipi?’

“Chukua gari langu binafsi” Waziri alimwambia huku akimpa funguo.

Dereva alizipokea funguo za gari akaingia ndani ya gari hilo na kuliwasha.

Alilitoa kwenye banda akalisimamisha. Mke wa waziri na Sofia wakajipakia katika siti za nyuma. Walipofunga milango gari likaondoka. Lilitoka kwenye geti na kukamata barabara.

“Tunakwenda hospitali gani?” dereva akauliza.

“Tupeleke hospitali ya H.B.M” mke wa waziri akamjibu.


Fuatilia hadithi hii katika blogy hii hapo kesho

KUMEKUCHA UPYA

No comments:

Post a Comment