Thursday, October 5, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI SEHEMU YA ( 5 )

HADITHI

MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI 5

ILIPOISHIA

Kwa mtu mwenye uzoevu mdogo tu wa vitendo vya uhalifu ilikuwa kazi ndogo tu kuutupa mwili wa Pili na kukimbiza gari kuondoka mahali hapo. Lakini kwa afisa wa serikali aliyezoea kukaa ofisini na kutoa amri kwa maneno, ilikuwa kazi kubwa sana.

Kitendo kile cha kufumwa na mlinzi kilimfanya ataharuki na kuamsha mapigo yake ya moyo. Ingawa alifanikiwa kufika nyumbani kwake salama hakuamini kwamba ilikuwa salama. Alijiambia huenda mlinzi aliziona namba za gari lake wakati akikimbia na atawatajia polisi.

Karibu  njia nzima alikuwa akilaani na kujiona alikuwa amefanya kitendo cha kizembe.

Wakati analizima moto gari hilo alishusha pumzi ndefu kisha akafungua mlango na kushuka. Mke wake alikuwa amesimama kwenye mlango wa nyumba yake akimsubiri.

“Vipi?” akamuuliza.

Waziri Mkuu hakumjibu kitu, aliingia ndani. Aliketi sebuleni akauweka mguu wake juu ya mwingine. Kitendo hicho kilikuwa ni cha mazoea ya ukwasi tu, hakikuwa cha kujinafasi katika muda ule wa taharuki.

SASA ENDELEA

“Umefanikiwa?” mke wake alimuuliza tena alipomuona yuko kimya.

“Nimefanikiwa lakini…”

Mke wake akashituka kidogo.

“Kumetokea nini?”

“Unajua nilikwenda kumtupa kinondoni karibu na eneo la shule. Nikadhani hapakuwa na mtu”

Vicky alianza kutikisa kichwa.

“Enhe. Nini kilitokea?”

“Wakati nataka kuuweka chini ule mwili, mlinzi wa ile shule aliniona akaja haraka na kunimulika tochi.

Mke wa Waziri Mkuu akapiga mluzi.

“Alikuona?”

“Sijui lakini nadhani hakunitambua. Nikautupa ule mwili chini na kukimbilia kwenye gari ili asinitambue. Alikuwa ameshika sime…”

“Enhe..?’

“Sasa sijui huko nyuma nini kilitokea. Mimi niliondoka na gari haraka”

“Lakini nadhani hakukutambua”

“Ndiyo imani yangu”

“Habari zaidi tutazipata hapo asubuhi”

                           *******************

Land Rover ya polisi wa kituo cha Kinondoni ilisimama pembeni mwa barabara karibu na uwanja wa shule ya msingi.

Polisi aliyekuwa amesimama na mlinzi alilifuata gari hilo kwa hatua za hima.

Polisi wemzake walipomuona walishuka kwenye gari. Walikuwa polisi wanne akiwemo Inspekta Alex.

Alimpigia saluti Inspekta Alex kisha akamwambia.

“Tukio limetokea sehemu ile”

Alimuonesha kwa kidole mahali hapo.

Dereva wa gari hilo alilielekeza gari mahali walipooneshwa na kumulika taa. Mwili wa msichana ulionekana waziwazi pamoja na mlinzi wa shule aliyekuwa amesimama kando yake.

Walikwenda mahali hapo na kuukagua mwili huo.

“Hebu tueleze nini kilitokea?” Inspekta Alex akamuuliza mlinzi wa shule.

“Nilikuwa nimekaa mbele ya jengo la shule nikiendelea na shughuli zangu za ulinzi, nikaona gari linasimama hapa…” Mlinzi alieleza huku akionesha mahali liliposimama gari hilo.

“Lilikuwa gari la aina gani”

“Ni hizi Toyota Land Cruiser”

“La rangi gani?”

“Nyeupe”

“Namba zake za usajili uliziona?”

“Namba sikuwahi kuziona”

“Enhe. Gari hilo liliposimama hapa nini kilitokea?”

“Niliona mtu mmoja akishuka akafungua mlango wa nyuma na kumtoa huyu mtu. Alikuwa amemmbeba kwenye mikono yake. Hapo nikashituka na kumfuata haraka. Aliponiona akanirushia huyu mtu, akaanguka kando yangu. Yeye mwenyewe akaimbilia kwenye gari na kulipiga moto”

Mlinzi alisita kidogo akavuta pumzi kisha akaendelea.

“Ilikuwa kidogo anikanyage kwa sababu nilikuwa namfuata ili anieleze ni kwanini amemtupa huyu mtu hapa”

“Nadhani atakuwa ameshakufa. Vaeni gloves zenu mumpakie kwenye gari” Inpekta Alex aliwambia polisi wenzake.

Polisi hao walitoa mipira ya kuvaa mikononi kutoka mifukoni mwao na kuivaa mikononi kisha wakaubeba mwili wa Pili na kwenda kuupakia kwenye gari.

“Na wewe utakuja asubuhi kituoni uandikishe maelezo yako. Wewe ndiye shahidi pekee uliyeona tukio hili” Inpekta Alex alimwabia mlinzi.

“Sawa. Nitafika kituoni asubuhi”

Alex alitoa notibuku yake mfukoni na kalamu.

“Unaitwa nani?” alimuuliza mlinzi.

“Naitwa Mrisho Rajab”

“Shule unayolinda inaitwaje?”

“Ni shule ya msingi ya Kinondoni”

“Okey”

Alex aliirudisha notibuku yake mfukoni.

“Tuonane hapo kesho” alimwambia mlinzi huyo.

“Sawa afande”

Inspekta Alex alilifuata gari la polisi lilipokuwa limesimama akajipakia na gari hilo likaondoka. Kwanza walikwenda kituo cha polisi cha Kinondoni.

Mwili wa Pili ulipekuliwa, ulikutwa na simu moja ya bei mbaya na saa ya mkononi iliyokuwa imevunjika kioo.

Vitu hivyo vilihifadhiwa mikononi mwa polisi kisha mwili huo ukapelekwa hospitali ya Muhimbili.

Daktari aliyeupokea mwili huo baada ya kuuchunguza kwa dakika chache alimwambia Inspekta Alex.

“Huyu ameshakufa”

“Labda utueleze alikufaje, aliuawa? Na kama aliuawa aliuawa kwa kitu gani? Na pia utueleze kama aliwahi kubakwa”

“Tutatoa majibu kesho baada ya uchunguzi kamili”

“Kwa hiyo tuje kesho kufuatia majibu”

“Ndiyo mje kesho majira ya saa nne, tutakuwa tumekamilisha uchunguzi wetu”

“Sawa dokta, kwaheri”

Alex na polisi wenzake wakaondoka.

Walirudi kituoni. Alex akaingia ofisini kwake na kuanza kuipekua simu ya Pili.

Ilikuwa imeseviwa majina ya watu wengi. Majina mengine yaliwekwa kwa herufi moja au mbili. Alex akazingatia jina moja lililokuwa na herufi mbili za ML. Jina hilo lilionekana katika meseji nyingi za mapenzi zilizokuwa ndani ya simu hiyo.

Alex akahisi kwamba aliyewakilishwa kwa herufi hizo ndiye aliyekuwa mpenzi wa marehemu na kwamba kama atapatikana ataweza kuwaeleza, msichana aliyeuwa alikuwa nani, alikuwa anaishi wapi na pia kuisaidia polisi katika uchunguzi.

Alex akampigia simu kwa kutumia simu ileile.

Simu ikaita kwa muda mrefu kisha ikapokelewa. Sauti nzito ya mtu aliyetoka usingizini ikauliza.

“Unanipigia saa hizi, ulikuwa wapi?”

Kauli ile peke yake ilitosha kumpa imani Alex kuwa mtu huyo aliyempigia hakuwa akifahamu chochote kuhusiana na tukio lililomtokea marehemu.

“Kuna tatizo limetokea hapa” Alex akamwambia.

“Na wewe ni nani?”

“Mimi ni afisa wa polisi, niko kituo cha Kinondoni. Kuna tatizo limemtokea huyu msichana. Tunakuomba ufike mara moja”

“Mh! Tatizo gani tena?”

“Huyu msichana ameshambuliwa na watu wasiofahamika. Tumekuta namba yako kwenye simu yake, tunajua mnafahamiana”

“Ndiyo tunafahamiana”

“Sasa hebu njoo mara moja hapa kituoni”

“Umeniambia ameshambuliwa, ameshambuliwa na nani?”

“Nimekwambia kwamba ameshambuliwa na watu wasiojulikana”

“Hebu mpe simu nizungumze naye”

“Hawezi kuzungumza, ndio sababu nimekupigia mimi”

“Loh! Aisee umenishitua sana. Subiri nakuja”

“Tunakusubiri.”

Alex akakata simu.

Baada ya nusu saa tu teksi ilisimama nje ya kituo cha polisi. Kijana mmoja mtanashati aliyekuwa amevaa vizuri alishuka kwenye teksi na kuingia katika kituo hicho cha polisi.

Alijitambulisha kaunta akapelekwa katika ofisi aliyokuwemo Inspekta Alex.

Alex akamtazama kabla ya kumwambia.

“Kaa kwenye kiti?”


Itaendelea kesho hapahapa usikose kwani KUMEKUCHA UPYA

No comments:

Post a Comment