Thursday, October 26, 2017

RIWAYA, KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI SEHEMU YA 9

KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI 9

ILIPOISHIA

“Nikwambie ukweli tatizo lako ni gumu. Kama nitajidai kuwa naweza kukusaidia ninaweza kupata matatizo kwani hao majini wanaokalia hizo pesa ni majini hatari. Ni majini wa jamii ya Subiani. Sisi huwaita Subiani Damisi au jini maiti. Wanaweza kukukata mara moja”

Ustaadhi huyo aliponiambia hivyo alinitisha. Uso wangu ulifadhaika hapo hapo.

Hapo nikaona nimuhadithie kile kisa cha yule mganga aliyetandikwa bakora.

Utaadhi huyo alipokisikia kisa hicho aliangua kicheko.

“Huyo mganga alipata tamaa. Alitaka kuzichukua pesa hizo akiamini kuwa alikuwa na majini wanaoweza kumlinda. Lakini huyo jini wa baba yako alipomfuata, majini wa huyo mganga walisambaratika. Ni bahati yake alitandikwa bakora. Angeweza kumuua kabisa”

“Kwa hiyo utanisaidiaje” nikamuuliza tena mganga huyo huku sauti yangu ikiwa imenywea.

“Sikufichi, hakuna mganga yeyote atakayeweza kukusaidia kwa tatizo hilo labda akudanganye tu”


SASA ENDELEA


“Una maana kwamba mke wangu naye atafanywa taahira”

“Hilo ni lazima muda wake ukiwadia”

“Mpaka dakika hii sioni faida ya zile pesa kwa sababu zimeshagharimu maisha ya mama yangu na mwanangu na bado zitagharimu maisha ya mke wangu. Ni afadhali niende nikazitupe, zisiwe mikononi mwangu”

“Hao majini wa pesa hizo hawatakubali uzitupe kwa sababu baba yako alikwenda kuzitafuta huko Zanzibar na alikubali masharti aliyopewa”

“Lakini ni yeye aliyezifuata huko Zanzibar na mwenyewe ameshakufa. Mimi hazinihusu”

“Zinakuhusu kwa sababu baba yako alikutaja kama mrithi wake na ndio maana zilikuja kwako”

Ustaadhi huyo alizidi kunichanganya, nikainamisha kichwa changu na kukitikisa.

“Baba yangu atakuwa na hatia kubwa mbele ya Mungu” nikajisemea kwa hasira.

“Wakati wewe unasema hivyo, wako watu wanaozitafuta pesa hizo kwa udi na uvumba lakini hawajafanikiwa kuzipata”

“Hawajali kuwapoteza wake zao na watoto wao?”

“Mbele ya pesa hawajali”

“Sasa huu ulimwengu unakwenda wapi!”

“Unajua binaadamu tuna roho tofauti. Pesa zimewabadili watu na zimeubadili ulimwengu wetu mpaka umekuwa hivyo”

“Sasa sijui niende wapi?”

“Pata muda wa kutafakari zaidi”

Ustaadhi aliponiambia hivyo nikainuka. Kwa kweli nilikuwa nimechnaganyikiwa na kuchoka.

“Nimeshatafakari vya kutosha. Lengo langu ni moja tu kumuokoa mke wangu na kumkomboa mama yangu na mwanangu” nikamwambia huku nikitoka nyumbani kwake bila kumuaga.

Ni vizuri nikiri kuwa nilikabiliwa na mtihani mgumu katika maisha yangu. Kulikuwa na kila dalili kuwa nisingeweza kushinda mtihani huo.

Lilikuwa ni tatizo lililohitaji elimu ambayo sikuwa nayo. Waganga ambao ndio niliokuwa nikitegemea wanipe msaada wao walikuwa wananikatisha tamaa.

Wakati natoka nyumbani kwa yule mganga, akilini mwangu niliunda picha ya mama yangu na mwanangu wakienelea kuteseka kwenye lile pango hadi wanakufa kwa dhiki.

Vile  vile niliunda picha ya mke wangu niliyekuwa nikimpenda naye akichukuliwa kafara na kuwekwa katika pango hilo.

Kama hali itakuwa hiyo, nilijiambia. Sitaweza tena kurudi kazini kwangu. Nitalazimika kubaki hapo hapo Korogwe nimhudumie mke wangu hadi naye atakapokufa.

Na bila shaka, nikaendelea kujiambia, hivyo ndivyo wanavyofanya watu wanaomiliki pesa za majini kama alivyokuwa baba yangu. Wanaendelea kuwahudumia watu wao waliowatoa makafara huku wakifurahia pesa za bure walizopewa na majini.

Hili jambo halikuingia akilini mwangu kabisa. Niliona sawa na kumfanyia unyama binaadamu mwenzako ilimradi tu umiliki pesa.

Mtu unapomlaumu jambazi kuwa anatumia bunduki kuua watu na kupora fedha, akumbuke kuna na huyu jambazi mwingine anayemtoa kafara mke wake ili apate pesa.

Nilipofika nyumbani niliingia chumbani kwangu nikajilaza kitandani na kuendelea kuwaza.

Nilikuwa mtu wa kuwaza tu wakati wote. Nikiwa hapo kitandani niliwaza sana lakini licha ya kupoteza muda mwingi sikuwa nimepata ufumbuzi wowote.

Pengine utashangaa kuwa niliwaza kila kitu lakini wazo la kuwa tajiri halikupita akilini mwangu kabisa. Nilitaka niendelee kuishi nikiwa masikini vile vile na nife nikiwa masikini. Mshahara wangu ninaolipwa kila mwezi na jeshi ulitosha kabisa kuendesha maisha yangu.

Utajiri ule wa pesa zilizokuwa chini ya kitanda nilichokuwa nimekilalia wakati ule, sikuuhitaji. Ni kweli kuwa hakuna mtu asiyetaka utajiri lakini utajiri wa kuangamiza maisha ya watu haukuwa utajiri. Ni sawa na ujambazi tu.

Baada  ya kuwaza kwa muda mrefu, usingizi ulinipitia hapo hapo nikalala. Wakati nimelala nikaota ndoto. Niliota nimesafiri na boti kwenda Pemba. Nikafika katika kijiji kinachoitwa Giningi. Nikakuta kisima kilichochimbwa miaka mingi iliyopita.

Wakati nakishangaa kile kisima nilisikia sauti ya mwanamke ikiita jina langu.

Nilipogeuka niliona mwanamke amesimama kando ya mti akiniashiria kwa mkono nimfuate pale. Nikamfuata. Nilipofika karibu yake nikagundua kuwa alikuwa ni yule mwanamke wa kijini aliyekuwa mke wa baba yangu.

“Umefuata nini huku?” akaniuliza.

“Nimekuja kumtafuta yule mzee aliyempa pesa baba yangu”

“Nyumba yake ile pale”

Mwanamke huyo akanionesha nyumba iliyokuwa mbali kidogo na mahali tulipokuwa.

Wakati naitazama ile nyumba akaendelea kuniambia.

“Lakini hivi sasa hayuko amekwenda shamba”

“Na wewe unafanya nini hapa?” nikamuuliza na yeye.

“Hapa ndipo nilipotoka mimi. Na mzee uliyemuuliza ndiye baba yangu. Nataka nikukumbushe kitu, karibuni mama yako atakufa nimekuja kuchukua idhini kwa baba yangu ili tumtoe kafara mke wako achukue nafasi ya mama yako”

Maneno hayo yakanishitua.

“Sisi tunataka kuondoka kurudi Dar, mke wangu huwezi kumpata”

“Hamuwezi kuondoka tena, mtabaki pale pale Korogwe. Mke wako ataishi kwenye pango na ni wewe utakayemuhudumia”

“Likizo yangu ikiisha nitatakiwa kazini”

“Hatutakuruhusu uendelee na kazi yako kwa sababu tumeshakupa utajiri”

Ndoto yangu ikaishia hapo hapo. Nikajikuta nimezinduka kutoka usingizini. Kumbe kilichonizindua zilikuwa kelele za simu yangu iliyokuwa inaita. Si unazijua simu hizi za kichina zilivyo na sauti kali.

Nikaitoa simu hiyo kwenye mfuko wa shati langu na kutazama skirini ya simu. Nikaona aliyekuwa akinipigia alikuwa mke wangu. Sikujua ni kwanini moyo wangu ulishituka ukawa unanienda mbio.

Nikaipokea ile simu.

“Hello!”

“Ulikuwa  umelala?” Sauti ya mke wangu ikauliza.

“Simu yako ndiyo imeniamsha”

“Naisikia sauti yako umekuwa nzito kama una mafua”

“Nilikuwa nimelala. Hamjambo?”

“Hatujambo. Nataka kukujulisha kuwa kesho nakuja huko”

Nikaduwaa kwa sekunde kadhaa kabla ya  kujibu chochote. Akilini mwangu niliwaza kwamba mke wangu akija Korogwe tu amekwisha.

“Kwani hali ya baba inaendelea vizuri?”

“Ndiyo, yuko vizuri. Yeye ndiye anayenihimiza nirudi kwa mume wangu. Ameniambia nimekaa kwake kwa muda mrefu”

Nilishindwa kumwambia mke wangu kuwa asije, angeniuliza sababu na nisingekuwa na jibu kwa wakati ule.

“Mume wangu mbona umenyamaza, hutaki nije huko?” Sauti ya mke wangu ikauliza.

“Hapana. Nilikuwa nameza dawa. Kichwa kinaniuma. Wewe njoo tu” nikajisemea baada ya kushutumiwa.

“Au una mwenzangu huko, niambie tu usinifiche”

“Hapana mke wangu.Mimi niko kwenye msiba wa baba, nitafute mwanamke wa nini!”

“Naona tangu jana nikikwambia suala la kuja huko unasitasita”

“Sijasitasita ila wasiwasi wangu upo kwenye hali ya mzee. Kama unasema hivi sasa anaendelea vizuri basi unaweza kuja tu”

“Nitumie nauli”

“Nitakutumia”

“Ni hapo kesho tutakapokutana”

“Mungu akituweka hai”

Mke wangu akakata simu. Badala ya kuwa na furaha ya kuzungumza na mke wangu, moyo wangu ukajaa machungu.

Kile nilichokuwa nikikihofia sasa kilikuwa kinakaribia kutokea.

Mke wangu umeng’ang’ania kuja huku lakini huku kuna matatizo ambayo siwezi kukuambia kwa sasa, nikajikuta nikisema peke yangu.

Nikajiambia kama mke wangu atakuja hapo kesho huenda huo ukawa ndio mwisho wake.

Licha ya kutambua bayana  madhara ambayo yangeweza kumkuta mke wangu nilishindwa kumzuia asije. Mwenyewe ameshaanza shutuma zisizo na msingi, hajui jinsi dakika zake zilivyokuwa zinakaribia.

Wakati nikiwaza hivyo kichwa changu kilikuwa kipo kwenye mchakato wa haraka haraka kutafuta ufumbuzi wa suala hilo. Nikakumbuka ile ndoto niliyoiota kwamba nilikwenda Pemba mahali panapoitwa Giningi na kukutana  na yule mwanamke wa kijini.

Je nini kitatokea? Usikose kuwa nami kesho hapahapa kumekucha.com

No comments:

Post a Comment