Monday, October 9, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI SEHEMU YA 9

HADITHI hii inaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya Kampuni ya usafirishaji abiria ya FREYS LUXURY COACH Tanga hadi Singida kila siku, na Singida Tanga kupitia Moshi, Arusha na Babati, Tanga wasiliana na simu no, 0622 292990

MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI 9

ILIPOISHIA

Kamanda wa polisi alianza kubabaika. Alibabaika kutokana na ukweli kuwa hakuwa amepata taarifa yoyote wakati alikuwa ndiye kamanda wa polisi wa mkoa huo.

“Sijapata bado” akasema kwa sauti ya wasiwasi.

“Kwanini?”

“Leo wamenicheleweshea taarifa”

“Eh! Mpishi wa Waziri Mkuu ameuawa jana usiku, wewe huna taarifa. Sasa sisi tumuulize nani?”

Kamanda wa polisi alionesha kuhuzunika waziwazi.

“Hawa jamaa wananicheleweshea taarifa na nilikwisha waeleza taaarifa za mauaji waniwasilishie haraka. Sasa acha niwaulize halafu nitakupigia”

“Inaonekana katika ofisi yako mambo hayaendi sawa!”

“Tatizo ni ucheleweshwaji tu wa taarifa. Hilo tatizo nitalirekebisha lisitokee tena”

SASA ENDELEA

Waziri wa Mambo ya Ndani alikuwa ameshakata simu.

Kamanda wa polisi alipogundua simu ilikuwa imeshakatwa alimpigia haraka afisa wa chini yake ambaye ni afisa upelelezi wa mkoa.

“Nini kinaendelea hapo ofisini kwako?” akamuuliza. Sauti yake ilikuwa tulivu lakini ilikuwa ya hasira.

“Afande nimepata taarifa za mauaji sasa hivi kutoka kwa OCD wa Kinondoni” Sauti ya afisa upelelezi ilisikikika kutoka simu ya upande wa pili.

“Ulikuwa unasubiri nikupigie ndio uniarifu?”

“Hapana afande, taarifa yenyewe nimeipata muda huu”

“Ni mauaji ya nani?”

“Nimeelezwa kwamba ni ya msichana mwenye umri wa miaka ishirini na tisa anayeitwa Pili, mkazi wa Kinondoni na ni mpishi wa Waziri mkuu”

“Aliuawa saa ngapi, aliuawa na nani na tukio lilitokea wapi?”

“Nimeelezwa kwamba aliuawa mahali pasipojulikana lakini maiti yake ilikwenda kuachwa katika kiwanja cha shule ya Msingi ya Kinondoni saa nane usiku”

“Ameuawa kwa kitu gani?”

“Taarifa ya uchunguzi wa mwili wa marehemu imeonesha kuwa marehemu alifyonzwa damu kupitia mshipa wake wa shingo na kusababisha kifo chake”

“Mh! Alifyonzwa na nani?”

“Uchunguzi umeonesha kuwa amefyonzwa na binaadamu lakini hajajulikana ni nani, kwa hiyo polisi ndio wanaendelea na uchunguzi”

“Ni nani ambaye aliuoana mwili wa marehemu ulipoachwa hapo kiwanjani?”

“Ni mlinzi wa ile shule”

“Ninahitaji kupata taarifa kamili”

“Ninakuja nayo ofisini kwako afande”

“Niletee sasa hivi” 

 Baada ya robo saa hivi, afisa upelelezi akaingia ofisini mwa kamanda wa polisi akiwa ameshika jalada.

Aliketi kwenye kiti kisha akampa jalada hilo kamanda wa polisi.

“Taarifa kamili niliyoletewa imo humu, unaweza kuisoma” Afisa upelelezi huyo akamwambia kamanda wa polisi.

Kamanda alipolitwaa jalada hilo alilifungua na kulisoma. Zilimchukua dakika kumi hivi kuyapitia maelezo yote haraka haraka. Akauinua uso wake na kumtazama Afisa upelelezi.

“Hilo gari mtalipataje?”

“Tatizo ni kuwa magari aina ya Toyota Land Cruisser ya rangi nyeupe ni mengi hapa Dar, ni afadhali kama yule mlinzi angeona namba zake za usajili. Tungeweza kulipata kwa urahisi”

“Unadhani ni akina nani watakuwa wamefanya unyama huu?”

“Ni mapema mno kudhani, upelelezi wetu ndio utatoa jibu. Tukio kama hili ndio mara ya kwanza kutokea hapa Dar”

“Sasa ni lazima vijana wako wachunguze kujua huyu msichana jana alitoka kazini saa ngapi na alipotoka kazini alikwenda wapi. Kama alirudi nyumbani kwake, alitoka tena saa ngapi na alikwenda wapi. Vile vile ni muhimu kujua kwa mara ya mwisho alikuwa na nani”

“Sawa afande, nitalishughulikia hilo suala”

Afisa upelelezi akainuka kwenye kiti na kutoka.

Alipotoka tu, kamanda wa polisi akainua simu na kumpigia Waziri wa Mambo ya ndani.

Baada ya kumueleza tukio zima, waziri alimuuliza.

“Ni uchunguzi gani ambao umefanyika hadi sasa?”

“Kitu cha kwanza kilikuwa ni kupata taarifa ya uchunguzi wa mwili wa marehemu. Hatua ya pili ilikuwa ni kuwapata jamaa wa marehemu ambao pia hawakuwa na taarifa yotote.

“Hatua ya tatu itakuwa kutuma vijana kwenda nyumbani kwa mheshimiwa Waziri Mkuu  kujua marehemu aliondoka kazini saa ngapi jana na pia kwenda nyumbani kwake kujua kama alirudi nyumbani alipotoka kazini na kama alirudi aliondoka saa ngapi na alikwenda wapi”

“Ninachowaomba ni kwamba chochote ambacho mtagundua mnifahamishe haraka” Waziri akamwambia kamanda huyo wa polisi.

“Tutakufahamisha”

“Sawa”

Waziri alitangulia kukata simu kabla ya kamanda wa polisi.aliyekuwa amempigia.

Haikutimia hata dakika moja Mkuu wa Jeshi la Polisi akampigia kamanda wa polisi  kumuulizia kuhusu tukio hilo.

“Ni kweli tukio hilo limetokea, polisi wanaendelea na uchunguzi” Kamanda huyo alimjibu.

“Uchunguzi huo umefikia wapi?”

“Kwa sasa hivi sina maelezo ya kutosha lakini mpaka saa kumi jioni nitakuwa na taarifa kamili’

“Utanijulisha”

“Sawa afande”

Mkuu wa Jeshi la polisi akakata simu na kamanda wa polisi akaurudisha mkono wa simu mahali pake.

Waziri Mkuu alirudi nyumbani kwake saa saba mchana. Alimkuta mke wake akiwa na fadhaa.

“Karibu” Mwanamke huyo alimkaribishaWaziri Mkuu huyo sebuleni. Sauti yake haikuwa na uchangamfu wa kawaida.

Dastan Lazaro aliketi kwenye kochi. Kama kawaida yake aliuweka mguu mmoja juu ya mwingine akamtazama mke wake.

Vicky alipoona mume wake anamtazama akamuuliza.

“Je?”

“Nimekuwa nikijiuliza swali lakini sipati jibu, Sofia amepatwa na tatizo gani?” Waziri Mkuu akamuuliza mke wake.

“Si rahisi kujua. Kama vipimo vya hospitali vinasema ni mzima, sisi tutawezaje kujua kilichompata”

“Mimi kwanza nilidhani ni malaria imempanda kichwani lakini malaria yenyewe haikuonekana”

“Mimi nimeogopa sana yule polisi niliyezungumza naye kwenye simu aliponiambia sababu ya kifo cha Pili ni kufyonzwa damu. Ina maana Sofia alimfyonza damu nyingi”

“Halafu ile nguvu ya kumdhibiti yule mwanamke aliipata wapi. Ukiwatazama Pili na Sofia, Pili ana nguvu zaidi. Alimzidi vipi mpaka akaweza kumfyonza damu na kumuua?”

“Kisha unajua kuwa mpaka muda huu Sofia hajui alichotenda. Ina maana kwamba jana usiku alikuwa amerukwa na akili!”

“Inabidi tuendelee kumfanyia uhunguzi zaidi wa akili yake…”

Waziri Mkuu akakatizwa na mlio wa simu yake ya mkononi iliyokuwa kwenye mfuko wa koti lake. Hakuwa na tabia ya kutoa simu kwa haraka inapoita lakini siku ile aliitoa haraka ili kujua ni nani aliyekuwa akimpigia.

Akaona jina la waziri wa Mambo ya Ndani Jackson Maro.

Akapokea simu.

“Hello Maro…!”

“Mheshimiwa nilitaka kukufahamisha kuwa uchunguzi wa mauaji ya mpishi wa nyumbani kwako Pili  Amrani unaendelea. Nimearifiwa kuwa polisi wanataka kuja nyumbni kwako kuchukua maelezo”


ITAENDELEA kesho usikose uhondo huu hapahapa tangakumekuchablog, KUMEKUCHA UPYA

No comments:

Post a Comment