Wednesday, October 4, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI SEHEMU YA { 4}

HADITHI

MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI 4

ILIPOISHIA

Waziri alijiambia  hatua aliyochukua ambayo aliiona ilikuwa ya maana ya kuutupa mwili huo mahali hapo, ilikuwa ya kipumbavu. Hakuwa amefanya uchunguzi sahihi na kugundua kuwa mahali hapo palikuwa salama.

Wazo la kuwa eneo hilo litakuwa na mlinzi halikuwemo katika akili yake.

Waziri alijuta. Alijiambia siku ya kuumbuka na kukatwa katwa mapanga ndiyo ile.

Wakati mlinzi akiendelea kumfuata kwa mwendo wa haraka akiwa ameipunga sime yake, waziri alimrushia ule mwili ukaanguka karibu yake kwa kishindo.

Mlinzi akasita na kukitazama kitu kilichokuwa kimetupwa mbele yake. Alipourudisha uso wake kwa waziri, waziri hakuwepo.

Alikuwa ametimua mbio kuelekea kwenye gari lake. Kwa vile mlango aliuacha wazi alikaa kwenye siti haraka. Alishukuru kwamba gari hakuwa amelizima moto. Akatia gea  ya kwanza  na kuliondoa.

Mlinzi alikuwa kikimbia kulifuata gari hilo.

“Simama wewe, umetupa nini pale?” Mlinzi huyo alimwambia waziri akiwa ametinga mbele ya gari hilo.

SASA ENDELEA

Waziri alimkwepa. Ilibaki kidogo tu angemgonga. Mlinzi mwenyewe pia aliruka kando kulikwepa gari hilo. Gari likampita na kutokea barabarani.

Waziri aliposhika barabara alikanyaga mafuta. Gari lilikimbia kwa kasi!

Mlinzi alikuwa ametaharuki baada ya kukoswa kuswa na gari la waziri. Alikuwa amesimama akilitazama gari hilo likikata mbuga!

Hakuweza kujua gari hilo lilikuwa likiendeshwa na nani na kile kiu alichorushiwa kilikuwa kitu gani. Akarudi sasa kiukiangalia vizuri.

Aliumwilika tochi mwili wa Pili. Mlinzi akashituka alipogundua kuwa ni mtu tena wa jinsia ya kike. Aligeuza tena uso akatazama upande ule lilikoelekea gari la waziri kisha akachutama na kuutazama vizuri mwili huo.

Kwanza alihisi mwanamke huyo alikuwa amelewa chakari kiasi kwamba hakuwa akijiweza lakini akajiuliza aliyelewa hapumui na macho yake hayapepesi?

Akaguna kisha akanyanyuka. Akaanza kutimua mbio kuelekea kituo kidogo cha polisi kilichokuwa jirani na pale. Alipofika aliwakuta polisi wawili waliokuwa wakisinzia. Akawaamsha.

“Kitu gani?” Polisi mmoja akamuuliza kwa kutaharuki baada ya kuamshwa usingizini.

“Mimi ni mlinzi wa ile shule ya msingi pale. Kuna mtu alikuja na gari akatupa mtu tena mwanamke…” Mlinzi huyo aliwambia.

“Hebu tueleze vizuri, ni mtu gani aliyetupwa hapo?” Polisi mmoja akamuuliza.

“Sijui. Hebu twendeni mkamuone”

“Huyo mtu yuko katika hali gani?”

“Sijui amekufa…sijui ni mzima…kwa maana hapumui!”

“Ni mwanamme au mwanamke?”

“Ni mwanamke”

Polisi mmoja akamwambia mwenzake afuatane na yule mlinzi akamuone huyo mtu.

Polisi na mlinzi huyo walipofika mahali hapo, mlinzi aliumulika tochi mwili wa Pili.



Polisi huyo baada ya kuutazama mwili huo alisema.

“Sijui amepigwa au amebakwa. Kwenye shingo yake kuna damu”

“Unaona tairi za gari lenyewe hizi hapa” Mlinzi alimwambia polisi huyo huku akizimulika alama za tairi za gari la waziri zilizokuwa kwenye michanga.

“Lilitokea upande gani?”

“Lilitokea upande huu, mimi nilikuwa nimekaa pale ninaangalia tu. Gari hilo lilipofika hapa ndipo mtu mmoja akashuka, nikaona anatoa kitu. Mimi nikaja haraka. Aliponiona akanitupia huu mwili na kukimbia kwenye gari…”

“Walikuwa watu wangapi?”

“Mimi niliona mtu mmoja tu labda wenzake walikuwa kwenye gari”

“Ina maana walikuja kuutupa huu mwili?”

“Labda”

Polisi huyo akatoa simu ya mkononi na kumpigia mwenzake aliyemuacha kituoni.

“Aisee kuna mtu hapa…sijui ameuawa au amezimia…ametupwa katika uwanja wa shule” Polisi huyo alimwambia mwenzake alipopokea simu.

“Anaonekanaje…amepigwa au…?” Sauti ya mwenzake ilisikika ikiuliza.

“Katika shingo yake kuna damu iliyoganda…sasa sijui amenyongwa shingo au vipi…!”

“Ni mwanamke au mwanaume?”

“Ni mwanamke. Inawezekana walimbaka kwanza ndio wakaamua kuja kumtupa hapa”

“Sasa kata simu niwapigie polisi wa kituo kikuu walete gari”

“Sawa”

Polisi huyo akakata simu.

Polisi aliyekuwa kituoni akawapigia simu polisi wa kituo cha Kinondoni.

“Nini kimetokea hapo?” Inspekta Alex aliyekuwa katika zamu ya usiku kiuoni hapo alimuuliza.

“Kuna tukio limetokea sasa hivi. Mlinzi wa shule ya msingi ya Kinondoni ametuletea taarifa kwamba kuna mwanamke ametupwa karibu na eneo la shule”

“Nyinyi mmefika kumuona?”

“Aliyekwenda ni constebo Faustus na amenipigia smu”

“Amesemaje?’

“Amemuona huyo mwanamke na hana uhakika kwamba ameuawa au yuko hai”

“Hao waliomtupa ni kina nani?”

“Ni watu waliofika na gari. Walimshusha wakamtupa na kukimbia na gari”

“Kuna watu walioliona hilo gari?”

“Mlinzi aliliona”

“Sawa. Subiri tunakuja”

                                            *************

Waziri Mkuu alipofika nyumbani kwake aliliingiza gari ndani ya geti akaliegesha katika banda la kuegesha magari. Alipolizima gari aligundua kuwa alikuwa akihema kama aliyekuwa akikimbia kwa miguu.

ITAENDELEA usikose kwani KUMEKUCHA UMPYA

No comments:

Post a Comment