Tuesday, October 10, 2017

SIMULIZI, TAMAA MBELE MAUTI NYUMA SEHEMU YA 1

HADITHI hii inakuja kwa hisani kubwa ya kampuni ya mabasi ya Abiria ya Raqeeb Luxury Coach ifanyayo safari zake kati ya Tanga na Arusha kila siku, siku mara 6 kuanzia saa 2 hadi saa 6, ofisi zao zoko barabara ya 12 Ngamiani Tanga mkabala na kituo cha mafuta cha Tapco, unaweza kuwasaliana nao kwa simu no, 0655 902929

TAMAA MBELE, MAUTI NYUMA…  (1)

NA FAKI A FAKI

Mbinguni kuna nyota tatu zilizofuatana katika mstari mmoja. Ukitazama angani wakati wa usiku unaweza kuziona. Wahenga wanasema nyota hizo zinaashiria kuwa tamaa kwa binaadamu iko mbele, mauti yako nyuma na binaadamu yuko katikati.
Wakati binaadamu anaikimbiza tamaa na yeye anakimbizwa na mauti!
Nyota hizo zinawakilisha ukweli kwamba siku zote binaadamu anaongozwa na tamaa. Lakini amesahau kuwa mauti nayo yako nyuma yake!

SASA ENDELEA.

Shangwe Mpya ilikuwa moja ya hoteli maarufu jiji Tanga. Haikuwa maarufu kwa sababu ya mandhari yake ya kupendeza au kuwa katika mtaa ambao ni maarufu, ilikuwa maarufu kwa sababu ilikuwa hoteli ya miaka mingi.

Ilikuwa hoteli ya ghorofa moja tu iliyokuwa katika barabara ya Eckenford. Pengine ilikuwa hoteli ambayo haikuvutia wageni kwani idadi ya wageni waliofika katika hoteli hiyo haikuwa kubwa.

Hoteli ya Shangwe Mpya ilivutia zaidi wenyeweji wa Tanga. Sababu kubwa ni kuwa kulikuwa na vyakula vya kiasili na bei yake ilikuwa nafuu sana. Pengine hilo ndilo lililofanya hoteli ya Shangwe Mpya kuwa maarufu sana.

Saa moja usiku Dastan Seseko aliisimamisha pikipiki yake mbele ya hoteli ya Shangwe. Akaiegesha kwenye eneo la kuegesha pikiki na kuelekea kwenye mlango wa kuingia hotelini humo.

Ilikuwa kawaida yake kwenda kula chakula cha jioni kila ifikapo saa mbili usiku lakini usiku huo aliwahi kufika. Alikuwa na sababu moja kubwa iliyomfikisha mapema mahali hapo.

Kwa siku tatu mfululizo kila alipofika hotelini hapo alikuwa akikutana na msichana mmoja aliyekuwa akienda kula chakula cha jioni. Lakini mara zote hizo Dastan anapofika, msichana huyo huwa ameshamaliza kula na kutoka.

Hivyo usiku huo Dastan alifika mapema zaidi kuliko muda wake ili aweze kumuona vyema msichana huyo.

Dastan aliingia katika eneo la wazi la hoteli ambalo lilitapakaa viti na meza kwa ajili ya wateja.

Kwanza alizungurusha macho katika eneo hilo ambalo halikuwa na watu wengi muda huo. Baada ya kutomuona msichana aliyekuwa akimtaka alitafuta meza ya pembeni na kwenda kuketi.

Aliagiza nyama choma na juisi kisha akayaelekeza macho yake kwenye mlango wa kuingia katika eneo hilo.

Aliamini kuwa msichana aliyesababisha afike mahali hapo mapema angewasili wakati wowote.

Dastan alikumbuka siku ya kwanza alipomuona msichana huyo alistushwa na umbile lake pamoja na sura yake jamali. Akajiambia hakuwahi kukutana na msichana aliyeugusa moyo wake kiasi kile kama ilivyokuwa kwa msichana huyo.



Siku ya pili alimuona tena akitoka. Alipomtazama alijiridhisha kuwa mawazo yake yalikuwa sahihi. Msichana huyo alikuwa mrembo na mwenye mvuto.

Siku ya tatu alikutana  naye tena. Bahati mbaya siku zote hizo hakupata muda wa kutosha angalau wa kumsalimia.

Ulikuwa ni upumbavu ambao ungeweza kumnasa mwanaume yeyote anayekutana na msichana mrembo. Dastan alitaka kuzungumza naye na amueleze kuwa alikuwa amempenda.

Wakati Dastan analetewa nyama choma aliyoagiza pamoja na bilauli ya juisi akamuona msichana huyo akiingia. Moyo wake ulishituka kidogo akaacha kuitazama sahani ya nyama choma na kumuangalia msichana huyo huku vyakela vyote alivyoagiza akivipiga pindu na kumwagika chini.

Alitamani aende akaketi katika meza aliyoketi yeye lakini ilikuwa sivyo. Msichana alikwenda kukaa katika meza nyingine.

Wakati Dastan akiendelea kumtazama huku akisifia uzuri wake alijiambia baada ya muda kidogo ataamisha makazi kwenye meza ya msichana huyo ili aweze kuzungumza naye.

Msichana aliletewa nyama choma na ndizi za kuchoma. Wakati anaanza kula, kuna jamaa aliingia na kwenda kukaa katika meza aliyokaa msichana huyo. Kitendo hicho kilimkera Dastan na kumfanya ajilaumu kwa kuchelewa kwenda kuketi yeye.

Baada ya muda kidogo aliwaona wawili hao wameingia katika mazungumzo. Dastan alikuwa akiumia kimoyomoyo huku akienndelea kujilaumu.

Lakini baadaye kidogo alipata shaka kwamba watu hao huenda walikuwa  wanajuana kwani baada ya kumaliza kula waliondoka pamoja.

Dastan alikuwa amemaliza kula kitambo baada ya kuagiza mlo mwengine baada ya ule wa awali kuupiga pindu. Baada ya kulipa bili yake aliinuka na kuwafuata nje.

Aliwaona wakijipakia kwenye gari la msichana na kuondoka.

Kihoro kilikuwa kimemshika Dastan. Na yeye akawasha pikipiki yake na kuwafuata.

Gari hilo lilikamata barabara ya Eckenford, baadaye lilikata kushoto likaingia eneo la Bombo. Dastan alikuwa bado akiwafuata nyuma.

Walilivuka daraja la Mkwakwani kisha wakakata kulia. Dastan naye alikata kulia. Gari hilo baada ya kuumaliza mtaa huo, lilikata kushoto na kusimama mbele ya nyumba moja iliyokuwa upande wa kulia wa barabara.

Dastan alilipita gari hilo na kwenda kusimama mbele, mahali ambapo palikuwa na kiza kilichotokana na mti wa muarubaini uliokuwa umeota pembeni mwa barabara.

Ili aweze kuwaona vizuri, aliigeuza pikipiki yake ielekee upande ule aliotokea na kuendelea kuwatupia macho watu hao.

Aliwaona wawili hao wakishuka kwenye gari na msichana akafungua mlango wa ile nyumba na kuingia ndani pamoja na mtu huyo.

Dastan aliendelea kusubiri kuona kama wangetoka tena. Ukapita muda mrefu. Wakati inakaribia kuwa saa tano usiku, Dastan aliona taa ya mbele ya nyumba hiyo ikizimwa, kukawa kiza. Lakini kulikuwa na mwanga hafifu uliotoka katika nyumba za jirani.

Baadaye Dastan alimuona yule msichana ametoka peke yake. Akaangalia kila upande. Mtaa huo ulikuwa kimya na hakukuwa na mtu yeyote aliyekuwa akipita.

ITAENDELEA kesho hapahapa tangakumekucha, KUMEKUCHA UPYA

No comments:

Post a Comment