Friday, October 20, 2017

RIWAYA , KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI SEHEMUA YA 4

RIWAYA

KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI 4

ILIPOISHIA

Pia nilikuta chupa ambayo ndani yake mlikuwa na yai zima lililoandikwa maandishi ya kiarabu kwa wino mwekundu. Pia mlikuwa na talasimu iliyokuwa na picha ya mtu. Sikuweza kujua lile yai liliingia vipi ndani ya ile chupa wakati mdomo wa chupa ulikuwa na uwazi mdogo sana.

Mbali ya ile chupa kulikuwa na kipande cha ubao mweusi uliokuwa na maandishi ambayo sikuweza kutambua yalikuwa ya lugha gani, Kigiriki si Kigiriki, Kichina si Kichina! Pia kulikuwa na vikorokoro vingine ambavyo sikuweza kuvielewa. Vitu hivyo kwa kweli vilinishangaza.

Baada ya kuviangalia kwa dakika kadhaa nilivirudisha ndani ule mkoba.

Nilichukulia kwamba wazee  wa zamani walikuwa na vikorokoro vingi vya kiasili walivyokuwa wanavihifadhi kwa imani mbalimbali. Na kwa kweli nisingeweza kujua baba yangu alikuwa amehifadhi vitu vile kwa sababu gani.

Nikaamua kuurudisha ule mkoba mvunguni nilikoutoa. Mkoba huo haukushughulisha sana akili yangu. Akili yangu ilikuwa imeshughulishwa zaidi na zile pesa. Nilipotoka pale chumbani nilitaka kurudi tena chumbani mwangu nizitazame tena zile pesa kwenye lile sanduku la chuma lakini nikajizuia. Niliona kama nilikuwa ninafanya jambo la kitoto.

SASA ENDELEA

Kwa vile sikuwa na kazi nyingine ya kufanya nikaamua kukaa barazani mwa ile nyumba yetu na kupanga mambo yangu. Jambo la kwanza nililolipanga ni jinsi ya kuondoka na zile pesa kwenda nazo Dar.

Utata ulikuwa ni namna nitakavyoweza kusafiri kwenye basi nikiwa  na sanduku hilo zito bila watu kujua kama lilikuwa na kiasi kingi cha pesa.

Nilijiambia kwa vyovyote vile lazima ningetiliwa mashaka na abiria wenzangu na kama sanduku hilo litafikishwa polisi na kufunguliwa, polisi wangeshuku kuwa nilikuwa jambazi kwani wasingeamini kuwa pesa zile nimezirihi kutoka kwa baba yangu.

Nikazidi kujiambia kuwa hata kama nitafika Dar na pesa hizo, nisingeweza kuzihifadhi benki kwani nisingeweza kujieleza nimezipata wapi. Mwisho wake ningeangukia mikononi mwa polisi na kutakiwa nijieleze vizuri.

Usiku ulipowadia nilikwenda kula kwa mama lishe kwa vile nyumbani nilibaki peke yangu. Baada ya kula chakula nikarudi nyumbani kulala.

Hata huo usingizi wenyewe haukunijhjia. Nilikuwa nikiwaza zile pesa tu. Nakumbuka nilitazama saa yangu na kuona ilikuwa
saa nane usiku nikatoka uani kujisaidia kisha nikarudi kulala. Safari hii nilipofumba macho yangu tu usingizi ukanichukua hapo hapo.

Vile napata usingizi tu ikanijia ndoto ya ajabu. Nilimuota mwanamke mmoja wa kiarabu amekaa kwenye kiti kilichokuwa mle chumbani.

Alikuwa mzuri sana. Mavazi yake ndiyo yaliyonishitua. Alikuwa amevaa shuka nyeupe tupu huku miguu yake ikiwa pekupeku. Kichwani alikuwa amejifunga kilemba cha rangi nyekundu.

Wakati namtazama huku nikijiuliza mwanamke yule ametokea wapi, aliniuliza.

“Unanijua mimi?”

“Sikujui” nikamjibu.

“Mimi ndiye niliyekuwa mke wa baba yako. Mimi ni mwanamke wa kijini. Jina langu ni Maimuna. Kwetu ni Kisima cha Giningi Zanzibar”

Akaendelea kuniambia.

“ Baba yako alifika mahali hapo kutafuta fedha za majini. Akakutana na Baba yetu aliyekuwa akitufuga, mzee Habibu Sultani wakakubaliana kwamba ili baba yako apate fedha za majini aozeshwe mke wa kijini miongoni mwa majini wanaokalia mali”

Huku nikimsikiliza kwa makini mwanamke huyo aliendelea.

“Mzee Sultani akaniozesha mimi kwa baba yako baada ya baba yako kukubaliana na masharti yetu. Masharti yetu yalikuwa kwa kunioa mimi yeye atapata fedha za majini na atakuwa tajiri lakini lazima amtoe kafara mke wake aliyekuwa naye awe dondocha. Na baada ya miaka kumi amtoe kafara mtoto wake au mjukuu wake naye pia awe dondocha”

Wakati nikielezwa hayo nilikuwa nimeduwaa nikimsikiliza mwanamke huyo ambaye aliendelea kunieleza.

“Sharti letu jingine lilikuwa lazima amtaje mrithi wake ili nimjue mapema. Baba yako akakutaja wewe na ndio sababu alipokaribia kufa alikwambia urithi wako uko mvunguni mwa kitanda.

“Zile pesa zilizomo kwenye lile sanduku ni pesa zangu. Kila siku zinaongezeka. Zile hazizishi, utatumia mpaka unakufa. Baada ya baba yako kutimiza  masharti yetu nilianza kumuingizia zile pesa kwenye sanduku mpaka hivi sasa limejaa. Alimfanya mke wake dondocha na juzi juzi tu alimfanya dondocha mjukuu wake, yaani mtoto wako”

“Ninavyojua mimi ni kuwa mama yangu alikufa na mwanangu pia alikufa mwenyewe” nikamwambia mwanamke huyo.

“Hivyo ndivyo ilivyoonekana kuwa watu hao wamekufa lakini hawakufa, wako hai. Ni kama vile wamechukuliwa msukule. Mama yako na mwananao wako kule kwenye pango ambako baba yako alitaka kukupeleka siku ile usiku lakini akafikwa na umauti.

“Watu hao wapo hai, wanaishi katika pango lakini si wazima. Wote wawili ni mataahira wanaohitaji kuhududumiwa kwa chakula. Chakula chao ni uji wa mapumba ya mahindi uliochanganywa na asali ya nyuki. Baba yako alikuwa akiwapelekea uji huo saa nane usiku kila siku. Wanakula usiku tu”

Mwanamke huyo alinyamza akanitazama kabla ya kuendelea.

“Kwa vile wewe umerithi zile pesa utanirithi na mimi na utawarithi na wale madondocha, yaani utakuwa unawatazama wewe na kuwapa chakula chao kila siku.

“Na mimi kila wiki utakuwa unaniingilia kimwili kama mke wako. Siku unayopenda utakwenda kwenye kaburi lolote utavua nguo na kubaki uchi saa nane usiku halafu mimi nitakuja hapo”

“Je kama nitakataa?” nikamuuliza yule jini baada ya maelezo yake kunitia hofu.

“Huwezi kukataa. Hayo ndiyo masharti ya sisi na baba yako. Lazima urihi zile pesa na ni lazima ukubaliane na yote niliyokueleza” Mwanamke huyo aliniambia na kuongeza.

“Kingine nilichotaka kukueleza ni kuwa kama vile ambavyo baba yako alimtoa kafara mke wake na wewe utatakiwa umtoe kafara mke wako ili mama yako aweze kufa kwa sababu muda wake umekwisha”

Loh! Yalikuwa maneno yaliyonitisha sana. Nimtoe kafara mke wangu awe dondocha? Na ni kwa sababu gani hasa? Kama ni pesa za majini aliyezitaka ni baba yangu ambaye ameshakufa, mimi zinanihusu nini?

Hapo nikatikisa kichwa kukataa.

“Sikubaliani na mashrti hayo. Mimi siwezi kumtoa kafara mke wangu, siwezi kufanya ukatili huo”

“Huwezi nini, wakati hayo ni makubaliano ya sisi na baba yako. Baba yako alituambia wewe utarithi pesa zile na utatimiza mashrti tutakayokupa” Mwanamke huyo akaniambia kwa mkazo.

Nikaendelea kutikisa kichwa.

“Huwezi kukataa kitu hapa. Kama umerithi zile pesa lazima utimize masharti hayo. Kama utakataa tutamchukua wenyewe mke wako. Sasa nenda kawape chakula wale madondocha, hawajakula tangu baba yako alipokufa”

Hapo hapo nikashituka usingizini.. Nikatazama huku na huku, sikumuona  yule mwanamke aliyekuwa akiniambia maneno hayo.

Jasho lilikuwa limenisambaa mwili mzima. Nikanyanyuka na kuketi kitandani.

Nikagundua kuwa nilikuwa ninaota lakini huenda ndoto yenyewe ilikuwa  na ukweli unaotisha.

Kwa ndoto ile niligundua marehemu baba yangu alikuwa akiishi na yule jini mwanamke ambaye alitaka nimrithi.

Pia niligundua kuwa baba yangu alikwenda eneo la Kisima cha Giningi huko Zanzibar kutafuta pesa za majini ndipo alipokutana na Habib Sultan ambaye alimmilikisha yule jini pamoja na kumpa masharti ya kupata utajiri.

Kumbe baba yangu alikuwa akimiliki pesa za majini! Na pia alikuwa akiishi na mke wa kijini! Ndio maana baada ya kufa mama yangu, baba hakuoa mke mwingine hadi mwenyewe alipofariki.

Lakini habari nyingine iliyonishitua ni kuhusu kuwa hai kwa mama yangu na mwanangu Abdul. Nilichokuwa ninakifahamu na kila mtu anakifahamu ni kuwa mama yangu alikufa, tena alikufa baada ya kuugua kwa muda mrefu.

Na kuhusu mwanangu ni hivyo hivyo. Nilichokuwa ninakifahamu ni kuwa mwanangu alikufa.

Sasa ile habari kuwa watu hao wako hai wamegeuzwa madondocha, ilinishitua sana.

Lakini wakati nafikiria zile pesa, nikakumbuka kwamba mke wangu naye alikuwa kwenye hatari ya kufanywa dondocha bila kutaka mimi mwenyewe.

Pesa zilikuwa tamu lakini masharti yake yalikuwa  magumu. Sikuweza kujua marehemu baba yangu aliupata wapi ujasiri wa kuyakubali masharti yale.

Kusema kweli baada  ya kuamka sikulala tena hadi asubuhi kulipokucha. Baada  ya kuoga na  kuvaa nilichukua sime nikatoka kuelekea kule kwenye pango ambako niliambiwa mama yangu na mwanangu walikuwa wamewekwa.

Nilifika hadi pale mhali ambapo baba  yangu alianguka na kufa nikaendelea kwenda hadi nikaona ule mti ambao baba yangu aliniambia. Nikakata kushoto. Baada ya mwendo mfupi nikakuta kichaka ambacho nilishuku ndio kile nilichoambiwa kuwa ndani yake kuna pango.

Kitu kilichonipa moyo na kuona kuwa mahali hapo palikuwa na watu nilisikia sauti za watu wanaolalamika. Nikaingia ndani ya kile kichaka, nikaona pango.nililokuwa limezibwa kwa jiwe kubwa. Sauti nilizokuwa ninazisikia zilikuwa zinatoka ndani ya pango hilo.

Nikaliondoa lile jiwe na kulisukuma kando. Mlango wa pango ukawa wazi. Nikashika sime yangu mkononi na kuingia. Mwanga wa jua ulikuwa umejipenyeza hadi ndani ya pango hilo na hivyo niliweza kuona vyema.

Vile naingia tu, zile sauti zikazidi. Nikamuona mama yangu na mwanangu wamewekwa chini kama walemavu wakilia njaa. Walikuwa weusi kama waliopakwa lami na walikuwa wamekonda sana kiasi kwamba walikuwa wanatisha na kuonekana kama vinyago.

Walikuwa wamenikodolea macho huku wamefungua midomo yao kuashiria kuwa walikuwa wanataka kula. Kwa kweli walinitia huruma sana. Mambo yale yalifanywa na baba yangu aliyekuwa ameshakufa lakini kama angekuwa hai ningekwenda kumpiga sime nikamuua kwa hasira.

Baada ya kumuona mama yangu na mwanangu wanavyolalamikia njaa, nikakumbuka kwamba nilikwenda kizembe mahali hapo. Sikuwachukulia chakula chao nilichoagizwa. Nikageuka na kutoka mbio.

Nilirudi nyumbani nikawatayarishia uji wa mapumba  ya mahindi kama nilivyoagiwa kisha nikautia uji huo asali ya nyuki. Sikuona vibaya kuwapelekea uji wa mapumba ya mahindi kwa sababu ni mzuri na mimi mwenyewe niliwahi kuunywa mara nyingi.

Uji ulipoiva niliutia kwenye chupa ya chai nikachukua vikombe viwili na kutoka  mbio kurudi kule pangoni.

Niliingia kwenye lile pango nikawamiminia uji kwenye vile vikombe na kuwapa. Walikuwa hawawezi kunywa wenyewe. Walikuwa kama watu waliopooza. Ilibidi niwanyweshe. Uji ulikuwa moto lakini walikunywa hivyo hivyo kwa sababu ya njaa.

Je nini kitatokea? Usikose kufuatilia kesho hapahapa tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment