Sunday, October 22, 2017

RIWAYA, KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI SEHEMU YA 5

RIWAYA

KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI 5

ILIPOISHIA

Vile naingia tu, zile sauti zikazidi. Nikamuona mama yangu na mwanangu wamewekwa chini kama walemavu wakilia njaa. Walikuwa weusi kama waliopakwa lami na walikuwa wamekonda sana kiasi kwamba walikuwa wanatisha na kuonekana kama vinyago.

Walikuwa wamenikodolea macho huku wamefungua midomo yao kuashiria kuwa walikuwa wanataka kula. Kwa kweli walinitia huruma sana. Mambo yale yalifanywa na baba yangu aliyekuwa ameshakufa lakini kama angekuwa hai ningekwenda kumpiga sime nikamuua kwa hasira.

Baada ya kumuona mama yangu na mwanangu wanavyolalamikia njaa, nikakumbuka kwamba nilikwenda kizembe mahali hapo. Sikuwachukulia chakula chao nilichoagizwa. Nikageuka na kutoka mbio.

Nilirudi nyumbani nikawatayarishia uji wa mapumba  ya mahindi kama nilivyoagizwa kisha nikautia uji huo asali ya nyuki. Sikuona vibaya kuwapelekea uji wa mapumba ya mahindi kwa sababu ni mzuri na mimi mwenyewe niliwahi kuunywa mara nyingi.

Uji ulipoiva niliutia kwenye chupa ya chai nikachukua vikombe viwili na kutoka  mbio kurudi kule pangoni.

Niliingia kwenye lile pango nikawamiminia uji kwenye vile vikombe na kuwapa. Walikuwa hawawezi kunywa wenyewe. Walikuwa kama watu waliopooza. Ilibidi niwanyweshe. Uji ulikuwa moto lakini walikunywa hivyo hivyo kwa sababu ya njaa.

SASA ENDELEA

Kila mmoja alikunywa vikombe vinne. Sasa nikahisi kuwa walikuwa wakijsikia vyema. Hata hivyo hawakuwa watu wa kuzungumza chochote. Walikuwa wameduwaa tu huku wakitoka ute.

Wakati nawatazama, machozi yalianza kunitoka. Nikajiuliza ni kwanini baba yangu alikuwa katili kiasi kile. Hivi watu wanaodaiwa kumiliki pesa za majini wanakuwa katili kiasi hiki?

Nikaendelea kujiuliza kama kulikuwa na umuhimu wa kuendelea kuzifurahia zile pesa za marehemu baba yangu wakati zimekatisha uhai wa mama yangu na mwanangu wa pekee ambao sasa wamekuwa mazezeta wasiojielewa?.

Sasa fikira zangu zikawa katika kuwaokoa viumbe hao waliokuwa katika mateso mazito. Sikuhitaji tena zile pesa ambazo kwa wakati ule niliziona kama sumu iliyokuwa inanyemelea kunimaliza mimi mwenyewe.

Nikawa nafikiria jinsi ya kuwaokoa viumbe hao ili warudi katika uhai wa kawaida na mimi mwenyewe niweze kuyanusuru maisha yangu.

Nikajiuliza nifanye nini wakati yule jini alishaniambia kuwa ni lazima nitii na nifuatishe maagizo yake kwa vile ndio makubaliano yake na marehemu baba yangu.

Upande mmoja wa akili yangu uliniambia kuwa hatua yoyote nitakayochukua kwenda kinyume na maagizo niliyopewa, inaweza kuyagharimu maisha yangu.

Nikaondoka katika lile pango nikiwa na chupa yangu niliyokuwa nimeitilia uji. Wakati natoka nilimuona mama yangu na mwanangu wakinitazama. Walikuwa wakinitazama bila kujielewa lakini nilihisi kama vile walikuwa wakiniambia nisiwaache pale lakini hawakuwa na uwezo wa kutamka maneno.

Nikatembea taratibu kurudi nyumbani huku nikiwaza. Picha ile mama yangu na mtoto wangu ilikuwa imekaa katika akili yangu wakati wote. Ilikuwa picha ambayo sikuipenda hata kidogo.

Nilipofika nyumbani niliketi kwenye kigoda huku nikiendelea kuwaza.

Wazo la kutolewa kafara kwa mke wangu nalo liknijia akilini. Nikaona kama sitaharakisha  kuchukua hatua stahiki, nitamkosa mke wangu ingawa sikujua ingekuwa ni lini.

Hapo nikapata wazo jingine la kwenda kwa mganga. Nikajiambia kwenda kwa mganga lilikuwa ndilo suala sahihi kwa matatizo yaliyokuwa yananikabili.

Sasa nikawa nafikiria niende kwa mganga gani. Kulikuwa na waganga kadhaa pale kijijini kwetu. Nikagundua kulikuwa na mganga mmoja aliyekuwa maarufu zaidi ambaye alikuwa akiishi kijiji cha pili. Nikaamua kwenda kwa mganga huyo nikiamini kwamba angeweza kulipatia ufumbuzi tatizo langu.

Nilipopata wazo hilo sikutaka kukaa tena, nikaondoka kwenye kigoda nikatoka na kufunga mlango. Nilikwenda kwenye kituo cha bodaboda. Nikapakiwa kwenye pikipiki na kuelekea katika hicho kijiji kilichokuwa na huyo mganga.

Kijana wa bodaboda alinishusha mbele ya nyumba ya mganga huyo. Uzuri wa waganga wa vijijini ni kwamba hata kama ni hodari kiasi gani huwezi kukuta msururu mrefu wa watu nyumbani kweke. Muda ule niliofika nilikuta watu watatu tu waliokuwa wakisubiri kuingia kwa mganga huyo.

Niliposhuka kwenye bodaboda nilikwenda barazani mwa nyumba hiyo nikawasalimia watu hao niliowakuta kisha nikakaa kwenye foleni.

Yalipita karibu masaa mawili hadi ilipofika zamu yangu. Niliingia kwenye ukumbi wa mganga huyo uliokuwa umetandikwa jamvi. Mganga mwenyewe alikuwa ameketi karibu na ukuta akiwa amevaa kaniki na shati jeupe.

Kando yake kulikuwa na chetezo kilichokuwa kinafuka moshi uliokuwa unanukia harufi ya udi.

Mbele yake kulikuwa na na rundo la vitabu vilivyokuwa vimewekwa chini. Juu ya ukuta aliokuwa ameegemea kulikuwa na tunguri kadhaa zilizokuwa zimepachikwa.

“Karibu, kaa hapo” Mganga aliniambia huku akinionesha mahali pa kukaa. Nikakaa chini mbele yake.

“Naweza kukusaidia” akaniambia.

“Nina shida. Naomba msaada wako”

“Shida gani?”

Nikamueleza tatizo lililokuwa limenipeleka pale. Mganga akashituka aliposikia kuwa ninamiliki sanduku la pesa za majini.

“Pesa za majini zina matatizo” Mganga akaniambia na kuongeza.

“Matatizo yake ni kama hayo. Mimi namfahamu baba yako lakini sikuwa nikijua kama alikuwa akimili pesa za majini. Kumbe alimtoa mhanga mke wake na mjukuu wake. Mwenyewe amekufa na siri imefichuka!”

“Sasa naomba msaada wako”

“Ulitaka nikusaidieje?”

“Kwanza uwaokoe mama yangu na mwanangu ambao wanateseka kule mapangoni. Na pili ninataka kuepukana na zile pesa. Mimi sizitaki tena”

Mganga akacheka.

“Kwanini huzitaki?”

“Masharti yake ni magumu kwangu. Yule jini aliniambia niende nikamzini makaburini. Sitaweza”

“Lakini baba yako aliyaweza yote hayo”

“Kosa alilofanya ni kunifanya  mimi kuwa mrithi wake wa pesa zile na kwa hivyo ninatakiwa nimrithi na yule jini wake jambo ambalo siitaliweza. Baya zaidi ni kuwa ninatakiwa nimtoe kafara mke wangu ili mama yangu akifa pawepo na mtu mwingine”

“Kwa kweli ni tatizo. Lakini kuna watu wengine wanazitaka hizo pesa za majini na wako tayari kuwatoa kafara ndugu zao au wazazi wao pamoja na watoto wao”

“Ni kweli watu hao wapo na mmojawapo ni huyo marehemu baba yangu. Hakujali kumtoa kafara mke wake na mjukuu wake ili apate pesa”

“Nikwambie kweli kuwakomboa mama yako na mwanano litakuwa ni tatizo kwa sababu yule jini anayehusika hivi sasa unaye wewe”

Aliponiambia hivyo nilishituka.

“Mimi siko naye” nikamwambia na kuongeza.

“Sijakubaliana naye”

“Makubaliano ni yale ya jini huyo na baba yako kwamba atakapokufa yeye mrihi utakuwa ni wewe. Kwa hiyo baada ya baba yako kufa, wewe ndio umemrithi huyo jini!”

Nikajishika kichwa na kukitikisa kusikitika.

“Huu ni upuuzi. Ushirikina wao utanihusu nini mimi? Huyu baba alikuwa mtu wa aina gani!” nikajisemea kisha nikamuuliza yule mganga.

“Yaani haitawezekana kuwakomboa mama yangu na mwanangu?”

“Haitawezekana”

“Haitawezekana hata kama sizitaki zile pesa zao, wachukue wenyewe?”

Niliporudia kutaja pesa yule mganga alitulia kimya. Nikamuona kama alikuwa akiwaza kitu.

“Una uhakika kwamba hizo pesa huzihitaji?” akaniuliza baada ya ukimya mfupi.

“Sizihitaji. Namuhitaji mama yangu na mwanangu!?” nilimwambia kwa sauti kali ili aweze kunielewa vizuri..

“Na una uhakika kwamba hujazitumia hata kidogo?”

“Sijazitumia na sitazitumia”

“Sasa sikiliza, niletee mimi hizo pesa kama huzihitaji. Mimi nitajua jinsi ya kuzifanya”

“Lakini nakuomba  uzingatie tatizo la msingi!”

“Tatizo la msingi ni lipi?’

“Ni kuwapata mama yangu na mwanangu”

“Mama yako na mwanano utawapata kwa sababu hizo pesa utakuwa umezitoa kwa mtu mwingine. Mimi ndiye nitakaye beba jukumu hilo”

“Na lile jini litakuja kwako?”

“Hilo jini linakuwa na mtu anayemiliki hizo pesa. Kama wewe umezitoa halitakaa kwako tena”

“Mimi nitakuwa huru?”

“Ndiyo. Wewe utakuwa huru”

“Sawa. Sasa hizo pesa ziko kwenye sanduku la chuma. Kulileta kwako muda huu haitawezekana lakini kama tutasaidiana kulibeba wakati wa usiku, tunaweza kulileta hapa kwako”

“Una maana kwamba limejaa pesa hadi juu?”

“Limejaa mpaka pomoni na ni nyekundu tupu!”

Mganga alitoa ulimi akaupitisha kwenye mdomo wake wa juu kwa tamaa. Akaniambia.

“Tufuatane sasa hivi hadi nyumbani kwako, niende nikaziangalie”

“Twende”

Hapo hapo mganga akainuka.

“Nisubiri kidogo”

Je nini kitatokea? Usikose kuwa nami kesho hapahapa

No comments:

Post a Comment