Wednesday, October 18, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI, SEHEMU YA 17

HADITHI

MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI 17

ILIPOISHIA

Kwa sababu ya kiherehere, aliamua kwenda kijijini kwao kuwaona wazee. Kulikuwa na bibi mmoja ambaye alikuwa mganga maarufu kijijini kwao akampeleka kwenye mzimu wa kwao na kumfanyia maombi ya kishirikina kwenye mzimu huo.

Akamuombea kupata uwaziri mkuu.

Baada ya maombi kukamilika, bibi huyo alimtaka Dastan Lazaro wakati huo akiwa si waziri mkuu, kuweka nadhiri kwenye mzimu huo kuwa endapo atateuliwa kuwa waziri mkuu atapeleka ng’ombe kwenye mzimu huo.

“Hilo ni sharti. Ukiteuliwa kuwa waziri mkuu kama unavyotaka, uje uchinje ng’ombe hapa” Bibi huyo alimsisitizia Lazaro.

“Hilo jambo dogo sana”

“Sawa. Kazi yetu imekwisha, turudi”

Waziri Mkuu alikumbuka kwamba alipoteuliwa kushika wadhifa huo alisahau kutimiza nadhiri aliyoiweka.

Kuna siku mke wake alimkumbusha. “Mume wangu unakumbuka kwamba uliniambia uliweka nadhiri kwenye mzimu kwamba utapaleka ng’ombe.?”

“Mke wangu huo ni ushirikina”

SASA ENDELEA

“Lakini si ulikwenda mwenyewe ukakubali kuweka nadhiri wewe mwenyewe”

“Nilimfuatisha tu yule bibi lakini sikuwa nikiamini”

“Kwa hiyo umeamua uache?”

“Unadhani naweza kufanya upuuzi ule? Si nitaharibu hata heshima yangu”

Dastan Lazaro akapuuza sharti alilopewa na mganga. Mzimu aliopelekwa ulikuwa maarufu na watu mbalimbali walikuwa wakifika kwenye mzimu huo kwa dharura zao za kishirikina.

Eneo hilo lilikuwa likikaribisha fisi waliokuwa wakifuata mizoga ya wanyama waliokuwa wakitolewa makafara kwenye mzimu huo. Kijiji kilipopanuka mzimu huo ukawa upo karibu na makazi ya watu, ndipo Waziri Mkuu alipoamuru uondolewe.

Magreda ya halmashauri yalipelekwa kwenda kuung’oa mzimu huo, ukawa haupo tena. Eneo hilo lilisafishwa likawa jeupe. Ziara za kuzuru mzimu huo zikawa hazipo tena. Baadaye mahali hapo palikuja kujengwa shule ya kijiji.

Baada ya Waziri Mkuu kuvuta kumbukumbu hiyo alimtazama mke wake.

“Mganga alikwambia uje uniulize kama nilitimiza ile nadhiri?” akamuuliza

“Ndio aliniambia nije nikuulize kisha niende nikamjibu”

“yeye alijuaje kama nilikwenda kuweka nadhiri kwenye mzimu ule?”

“Alijua baada ya kupiga ramli”

“Sio kwamba wewe ndio ulimueleza?”

“Hapana. Sikumueleza. Yeye ndiye alinieleza mimi”

“Alikuwa na maana kwamba kutotimiza ile nadhiri ndio kumemsababishia mtoto wetu matatizo aliyonayo?”

“Ndivyo alivyonieleza”

“Kivipi?”

“Alitaka kwanza nikampe jibu ndio atanieleza”

“Nenda kamwambie kwamba sikutimiza ile nadhiri. Sasa mtoto amedhurika kivipi?”

“Kesho nitakwenda kumueleza”

Asubuhi yake, mke wa Waziri Mkuu pamoja na Sofia wakaenda Morogoro. Wakiwa kijijini kwao Vicky, yaani mke wa Waziri Mkuu alimuacha Sofia nyumbani kwao, akaenda peke yake kwa yule mganga.

Alipofika alimueleza kuwa baada ya mume wake kuupata uwaziri mkuu hakutimiza ile nadhiri aliyoweka kwenye mzimu.

“Hilo ndilo lililoleta tatizo kwa binti yenu” Mganga akamwambia.

“Limeleta tatizo kivipi?”

“Ule mzimu uliahidiwa damu, yaani yule ng’ombe angechinjwa kwenye ule mzimu na mzimu ungepata damu. Sasa baada ya mume wako kutotimiza ahadi yake mzimu ule ulimuingia binti yenu, sasa unafyonza damu za watu”

Mke wa Waziri Mkuu alishituka.

“Kumbe ule uliompata mwanangu ni mzimu?” akauliza kwa mshangao.

“Ni mzimu”

“Kwani ulitaka ng’ombe wangapi?”

“Ng’ombe mmoja tu alioahidi mume wako”

“Sasa mbona ameshafyonza damu watu wawili?”

“Na utaendelea kufyonza watu zaidi”

“Kwanini sasa?”

“Ni kwa sababu mmeufanyia dharau. Mmeuahidi kitu halafu hamkutimiza”

“Si mimi, ni baba yake”

“Ndio unawakomoa nyote”

Vicky akatikisa kichwa kusikitika.

“Sasa hauna tiba?”

“Hauna tiba nyingine”

“Isipokuwa?”

“Mume wako atimize ile nadhiri yake?”

“Akitimiza ndio itakuwa tiba yake?”

“Ndio”

Vicky akarudisha jibu kwa mume wake.

“Mume wangu ulikosea sana kwenda kuweka nadhiri kwenye mzimu kisha ukapuuza”

“Mganaga amekwambiaje?”

“Ameniambia baada ya kuacha kupeleka yule ng’ombe, ule mzimu umemuingia mtoto wetu, sasa unafyonza damu za watu ukiwa mwilini mwake”

Waziri Mkuu akashituka.

“Mpaka lini?”

“Mpaka utimize ile nadhiri yako”

“Ngoja kesho nitakwenda kwa yule bibi niliyekwenda naye wakati ule. Tutakwenda kuyamaliza huko huko”

Siku iliyofuata Waziri Mkuu akaenda Morogoro. Alikwenda kijijini kwao na kufika nyumbani kwa yule bibi aliyekwenda naye kwenye ule mzimu.

“Yule bibi alikufa tangu mwaka jana?” Mwanamke mmoja alimwambia Waziri Mkuu alipomuuliza mwanamke huyo.

Waziri Mkuu akashusha pumzi ndefu.

“Kumbe yule bibi alikufa?”

“Alikufa, hatuko naye tena”

“Hivi hakuna mtu mwingine aliyechukua kazi zake?”

“Yule bibi hakuwa na mtoto wala mjukuu”

“Na wale wasaidizi wake wako wapi?”

“Msaidizi wake alikuwa mmoja tu na ndiye aliyetangulia kufa”

Waziri Mkuu hakuwa na jingine isipokuwa kuaga na kuondoka. Aliporudi nyumbani kwao alimuuliza ndugu yake kama alikuwa anamfahamu mganga yeyote wa kienyeji aliye hodari.

“Namfahamu”

“Kama namuhitaji unaeza kumleta hapa muda huu?”

“Naweza”

“Hebu nenda kamlete, nina shida naye”

Ndugu huyo wa Waziri Mkuu aliondoka na gari lake. Baada ya nusu saa tu alirudi akiwa na mtu mwingine ambaye alimpeleka kwa Wazi Mkuu.

“Mganga mwenyewe ndiye huyu” akamwambia

“Karibu sana” Waziri Mkuu alimwambia mganga huyo.

“Asante”

Ndugu wa Waziri Mkuu aliondoka na kuwaacha. Waziri Mkuu akamueleza mganga huyo tatizo la binti yake na jinsi walivyoambiwa na mganga wa awali kwamba tatizo hilo linatokana na nadhiri aliyoweka kwenye mzimu.

“Ni kweli kwamba uliweka nadhiri hiyo?” mganga akamuuliza Waziri Mkuu.

“Ni kweli niliiweka lakini sikuwahi kuitimiza kwa sababu ya shughuli kuwa nyingi”

itaendelea kesh hapao usikose Uhondo huu hapa

No comments:

Post a Comment