Wednesday, October 18, 2017

RIWAYA, KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI , SEHEMU YA 2



RIWAYA

KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI 2

ILIPOISHIA

Baada ya sekunde chache nikisikia sauti ya mke wangu kwenye simu. Alikuwa bado analia.

“Hebu nyamaza kwanza tushauriane. Shemeji ameniuliza kuhusu mazishi lakini sikuwa na jibu”

“Mimi nitakuja kesho asubuhi. Msizike mpaka nifike” Mke wangu alijikaza akaniambia.

“Kama utaondoka asubuhi, kila ilivyo utafika huku usiku. Kwa hiyo tutazika usiku utakapofika”

“Nadhani nitakuja peke yangu. Huku baba amezidiwa tena. Kaka atabaki”

“Sawa”

“Basi ni hivyo”

“Vizuri, nakutakia safari njema”

SASA ENDELEA

Baada ya kuzungumza na mke wangu nilimueleza baba kuwa tutazika usiku wa kesho yake baada ya mke wangu kuwasili kutoka Dodoma.

“Amekwambia atawasili saa ngapi” akaniuliza.

“Atafika usiku huo huo”

“Watu wengi wananiuliza kuhusu mazishi lakini nimekuwa sina jibu, sasa nitawaeleza kuwa mazishi yamepangwa  kufanyika kesho usiku”

“Waeleze hivyo. Na tumeyapanga muda huo kwa sababu ya kumsubirisha mama yake, vinginevyo tungeweza hata kuzika kesho mchana”

Ilipofika saa tano usiku, mke wangu alinipigia simu tena akaniuliza kilichokuwa kinaendelea nikamueleza. Akaendelea kunisisitiza kuwa tusizike  mpaka atakapowasili.

“Tumeshapanga kuwa mazishi yatafanyika baada ya wewe kufika”

“Sawa. Mimi nimeshajiandaa, kesho asubuhi naondoka” mke wangu akaniambia.

Usiku wa siku ile hatukulala. Mimi na baba tulikuwa tukitafakari kuhusu msiba ule uliotutokea ghafla.

Asubuhi kulipokucha tuliendelea kupokea wageni waliokuja kuomboleza kwenye msiba huo. Baadhi ya watu walitoka katika vijiji vingine vya karibu.

Matayarisho ya mazishi yaliendelea hapo nyumbani hadi jioni. Mke wangu alifika na basi lililowasili saa moja usiku. Alinipigia simu kunijulisha kuwa alikuwa ameshawasili. Nikawaagiza wifi zake waende wakampokee.

Wakaenda kumpokea na kuja naye lakini walipofika tu hapo nyumbani kilio kikaanza upya. Mke wangu alianza kulia na wifi zake nao wakalia pamoja naye..

“Mwanangu umepatwa na nini…mwanangu umepatwa na nini…mbona mwanangu umenitoka ghafla…” Ndiyo maneno aliyokuwa akimtamka mke wangu.

Ndugu na jamaa walijaribu kumnyamazisha. Akanyamaza na kuingia katika chumba kilichokuwa na mwili wa marehemu lakini alipouona mwili wa mwanawe akaanza tena kulia.

Kwa vile tulipanga atakapofika mke wangu, mwili wa marehemu utolewe kwa ajili ya kwenda kuzikwa, shughuli hiyo ikafanyika.

Mpaka inafika saa tatu usiku, jeneza lilikuwa limeshafikishwa makaburini. Baada ya mazishi tukarudi nyumbani.

Mke wangu aliendelea kubaki hapo Korogwe kwa wiki nzima kabla ya kurudi tena Dodoma.

Hazikupita hata wiki mbili baba yangu naye akapatwa na homa ghafla. Nilimpeleka hospitali nikidhnani alikuwa na malaria lakini baada ya kuchukuliwa vipimo aligundulika hakuwa na malaria. Hata hivyo alipewa tembe za kwenda kumeza nyumbani.

Baada ya kutumia tembe hizo alipata nafuu kidogo lakini zilipita  karibu wiki mbili baba alikuwa ndani akijiuguza.

Usiku mmoja akaniita na kuniambia.

“Mwanangu naona kiza mbele yangu. Kuna kitu nataka kukwambia”

Aliponiambia hivyo nilishituka nikamkazia macho na kumuuliza.

“Unataka kuniambia nini baba?”.

“Cha kwanza ninachotaka kukwambia ni kuwa endapo nitafumba macho siku yoyote, urithi wako uko chini ya mvungu wa kitanda nilicholala” akaendelea kuniambia huku akielekeza mkono wake chini ya mvungu wa kitanda.

Mimi nilikuwa nimenyamaza nikimsikiliza kwa makini.

“Sasa kuna majukumu ambayo nataka nikukabidhi lakini si hapa. Itabidi tutoke usiku huu twende mahali fulani”

Hapo nikamuuliza.

“Ni majukumu gani hayo baba na hapo mahali unapotaka twende usiku huu ni wapi?”

“Nifuate tu”

Baba alikuwa ameshainuka kwenye kitanda. Kitu ambacho kilinishangaza ni kuwa alipoinuka alikuwa na nguvu mpka nikahisi kuwa alikuwa amepona.

Nikapata matumaini. Na mimi nikanyanyuka na kumwambia.

“Haya twende”

Nikatoka naye pale nyumbani. Nakumbuka ilikuwa saa saba usiku.

“Ni usiku huu, chukua silaha” akaniambia.

“Kwani ni mbali sana baba?”

“Ni mbali kidogo”

“Kwanini tusiende kesho”

“Mimi nataka twende leo”

Nikarudi ndani na kuchukua sime. Nilipotoka, nikamwambia.

“Haya twende”

Tukaanza safari.

“Acha mimi niwe mbele yako” Baba akaniambia wakati tunakwenda.

Nikamuacha atangulie mbele yangu. Njia tuliyokwenda ilikuwa ikielekea lilikokuwa shamba lake. Nikahisi tulikuwa tunakwenda shambani kwake. Lakini tulipolikaribia shamba hilo tuliliacha shamba upande wa kushoto tukashika njia ya upande wa kulia.

Kimoyomoyo nilikuwa nikijiuliza, baba alikuwa ananipeleka wapi usiku ule. Kwa mbali tulikuwa tukisikia milio ya fisi pamoja na ya wanayama wengine.

Kile kitendo ch baba kuwa mbele yangu kilinizuia nisimuulize maswali mengi yaliyokuwa yakipita akilini mwangu.

Baada ya muda kidogo tukawa tumeingia kwenye njia iliyoelekea kwenye pori. Ilikuwa njia nyembamba ya kupita kwa miguu.

Sehemu yenyewe ilikuwa inatisha lakini baba alikuwa akitembea bila kuonesha wasiwasi wa aina yoyote. Mimi niliyekuwa nyuma yake nikiwa nimeshika sime mkononi ndiye niliyekuwa nikitazama kila upande kwa wasiwasi.

Wakati tunazidi kutokomea katika pori hilo, ghafla nilimuona baba akianza kusita sita. Kasi yake ya kutembea ilipungua. Mwisho akawa aamesimama akielekeza mkono upande wangu kama aliyekuwa akihitaji msaada.

Nikaushika mkono wake na kumuuliza.

“Nini baba?”

Nikamuona kama aliyekuwa anataka  kuanguka, nikamshika vizuri.

Niliuona uso wake. Alikuwa kama aliyekuwa akisikia maumivu.

Hakuweza kusema kitu hadi nilipomlaza chini kichali chali.

Kwanza alinyoosha kidole chake kuelekea ule upande tuliokuwa tunakwenda.

“Kule mbele kuna mti wa mkuyu. Utakuta katika moja ya matawi yake nimening’iniza kitambaa chekundu na cheusi...utakata kushoto utakuta kichaka kikubwa. Ukiingia ndani ya kichaka hicho utakuta pango…” akaniambia lakini huo ulikuwa ndio mwisho wa maelezo yake.

“Ni pango gani baba?” nikamuuliza haraka.

“Safari yangu itaishia hapa…wewe nenda tu…” akaniambia.

“Sijakuelewa baba. Unasema….?”

Kabla hata sijamaliza kumuuliza nilichotaka kumuuliza alivuta pumzi ndefu kisha akazishusha. Akawa kimya.  Hapo hapo nikajua kuwa baba yangu alikuwa ameshakufa.

Alikuwa ameniacha njia panda. Sikujua baba alikuwa ananipeleka wapi huko alikoniambia kuna pango. Na pia sikujua alikuwa anakwenda kunionesha nini usiku ule.

Nilichofanya hapo ni kumbeba begani na kurudi naye nyumbani. Kwa vile nilitembea naye mwendo mrefu, hadi tunafika nyumbani nilikuwa nimechoka.

Nilimuingiza chumbani kwake nikamlaza kitandani kisha nikammulika taa kumtazama usoni kwake. Kwa kweli mzee alikuwa ameshakufa!

Likizo yangu ile ilikuwa ya balaa. Nilipofika tu hapo Korogwe alikufa mwanangu, siku ile tena mzee wangu naye ananiaga katika mazingira ya kutatanisha.

Baada ya kukaa na kuwaza nikiwa pembeni mwa kitanda nilichoulaza mwili wa baba, nikayakumbuka yale maneno ya baba aliyoniambia.

“Cha kwanza ninachotaka kukwambia ni kuwa endapo nitafumba macho siku yoyote, urithi wako uko chini ya mvungu wa kitanda nilicholala”

Nikajiambia baba yangu alishajua kuwa atakufa leo ndio maana aliniita na kunieleza maneno hayo.

Lakini shauku ya kutaka kujua kile alichoniambia ni urithi wangu kilichoko chini ya mvungu ikanipata. Nikachutama na kumulika taa chini ya mvungu wa kitanda chake.

Nikaona mfuko wa ngozi kisha nikaona sanduku la chuma. Shauku yangu ikawa kwenye lile sanduku la chuma.

Nikatia mkono mvunguni na kulivuta. Lilikuwa zito. Ikabidi nitumie mikono miwili, nikalitoa kwenye mvungu.

Lilikuwa llimefungwa kwa kufuli kubwa ya shaba. Nikafikiria niivunje ile kufuli ili nitazame kilichomo ndani lakini nikakumbuka baba yangu alikuwa na tabia ya kutembea na funguo nyingi anazozifunga kiunoni.

Je nini kitatokea? Usikose kuwa nami hapo kesho hapahapa

No comments:

Post a Comment