Monday, October 30, 2017

RIWAYA, KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI SEHEMU YA 10

RIWAYA

KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI  10

ILIPOISHIA

Mke wangu akakata simu. Badala ya kuwa na furaha ya kuzungumza na mke wangu, moyo wangu ukajaa machungu.

Kile nilichokuwa nikikihofia sasa kilikuwa kinakaribia kutokea.

Mke wangu umeng’ang’ania kuja huku lakini huku kuna matatizo ambayo siwezi kukuambia kwa sasa, nikajikuta nikisema peke yangu.

Nikajiambia kama mke wangu atakuja hapo kesho huenda huo ukawa ndio mwisho wake.

Licha ya kutambua bayana  madhara ambayo yangeweza kumkuta mke wangu nilishindwa kumzuia asije. Mwenyewe ameshaanza shutuma zisizo na msingi, hajui jinsi dakika zake zilivyokuwa zinakaribia.

Wakati nikiwaza hivyo kichwa changu kilikuwa kipo kwenye mchakato wa haraka haraka kutafuta ufumbuzi wa suala hilo. Nikakumbuka ile ndoto niliyoiota kwamba nilikwenda Pemba mahali panapoitwa Giningi na kukutana  na yule mwanamke wa kijini.

SASA ENDELEA

Nilikuwa nikifahamu kuwa  jini huyo alichukuliwa na baba yangu kutoka  mahali hapo ambapo ndipo alipopatia utajiri wake. Nikakumbuka kuwa yule jini alinieleza kuwa hapo Giningi kuna mzee mmoja anayeitwa Habib Sultani ambaye ndiye anayewauzia watu majini wanaozalisha pesa.

Hao majini wanamuita mzee huyo “baba.”, yaani wanamfanya kama baba yao na ndiye huyo ambaye katika ile ndoto niliambiwa amekwenda shamba.

Nikapata wazo moja. Wazo hilo lilikuwa ni kwenda Pemba kumtafuta mzee huyo na kumueleza hali halisi kuhusu matatizo yaliyokuwa yananikabili. Ikiwezekana nimrudishie pesa zake na yeye achukue majini wake.

Wazo hilo likanipa nguvu, nikaona ndio wazo pekee ambalo litanipatia ufumbuzi wa matatizo yangu.

Sasa kama nataka kusafiri kwenda Pemba, nikajimbia, muda ulikuwa ndio ule. Sikuwa  na muda tena wa kupoteza kwani mke wangu angefika kesho yake.

Nikiianuka kwenye kitanda nikaenda bafuni kuoga. Nilipomaliza nilirudi ndani nikavaa nguo nyingine za safari. Nilichukua begi langu nikatia nguo mbili za akiba nikatoka na kufunga mlango wa nyumba.

Sikumuaga mtu yeyote nikaanza safari ya miguu kuelekea stendi ya mabasi. Nilipofika nilipanda basi la kwenda Tanga.

Wakati nimo safarini kuelekea tanga likanijia wazo jingine kuwa endapo sitampata huyo mzee nitafanya nini. Kwa kweli hapo sikuwa na jibu lakini waswahili wanasema “Mfa maji hushika maji” Na mimi kwa vile nilikuwa mfa maji nikaamua kushika maji.

Nilipofika Tanga nilikwenda kwenye duka la mkazi mmoja wa Pemba ambaye nilikuwa nikimfahamu, nikamuulizia kuhusu usafiri wa kwenda Pemba. Akaniambia maneno ya kunikatisha tamaa.

“Usafiri wa kwenda Pemba unafanyika kwa wiki mara moja, inabidi ukae hadi jumamosi ndio utapata usafiri wa Pemba” Mtu huyo akaniambia.

Siku ile ilikuwa ni jumatano. Kwa maneno yake ni kwamba nilipaswa kukaa hadi siku ya jumamosi ndipo niondoke kwenda Pemba wakati nilihitaji kufika Pemba siku ile ile.

Hapo nikagwaya. Jasho lilikuwa linanitoka kwenye uso wangu.

“Kwani wewe ulihitaji kwenda lini?” mtu huyo akaniuliza.

“Nilihitaji kufika leo”

“Labda uende Pangani. Kule kuna usafiri wa kila siku wa kwenda Pemba na Unguja”

“Si kitu, naweza kwenda Pangani”

“Lakini usafiri wa huko ni wa majahazi. Utaweza kusafiri kwenye jahazi?”

“Nitaweza. Acha jahazi hata kwa dau nitakwenda”

Mpemba huyo akacheka.

“Kwani una dharura kubwa sana?” akaniuliza.

“Nina dharura kubwa, ni muhimu nifike leo”

“Basi wewe nenda Pangani. Mabasi ya Pangani yapo wakati wote”

Kutokana na muongozo wa rafiki yangu huyo sikuhangaika tena kwenda bandarini kuulizia usafiri wa Pemba, nikaenda katika kituo cha mabasi nikapanda basi la Pangani. Nililikuta basi hilo limejaa na lilikuwa tayari kuazna safari. Ikanibidi nisimame baada ya kutopata siti.

Mpaka nafika Pangani ilikuwa saa tisa alasiri. Nilikuwa na matumaini madogo sana ya kufika Pemba kwa siku ile.

Ile ilikuwa ndio mara yangu ya kwanza kukanyaga katika mji huo wa kihistoria niliokuwa nikiusikia na kuusoma kwenye ramani. Nilikuwa na shauku ya kwenda kupaona mahali palipokuwa na soko la watumwa ambapo pamekuwa ni kivutio kikubwa cha watalii lakini muda haukuniruhusu.

Nilishuka pwani nikakuta kulikuwa na majahazi kibao.

Ili nijue taratibu za usafiri wa hapo nilimfuata mtu mmoja nikamuulizia kuhusu usafiri wa Pemba.

“Muulize mtu yule pale”

Mtu huyo naye akanielekeza kwa mtu mwingine aliyekuwa amekaa pembeni chini ya mti akivuta sigara.

Jinsi alivyokuwa amevaa alionesha alikuwa mmoja wa manahodha wa zile jahazi. Nikamfuata.

Wakati namkaribia nilianza kusikia kupuo la harufu ya bangi. Yule mtu alikuwa akizidi kupuliza moshi. Nilipofika karibu yake nikagundua kuwa sigara aliyokuwa akivuta ilikuwa bangi.

Alikuwa akivuta kwa uhuru bila kujali kuwa alichokuwa akivuta kilikuwa haramu. Mpaka ninamfikia hakuonekana kushituka. Alikuwa akiendelea kuvuta.

“Habari ya saa hizi?” nikamsalimia mtu huyo aliyekuwa na mwili mfupi uliokakamaa.

Alikuwa na macho madogo yaliyoiva kwa bangi.

Mtu huyo akanitazama kisha akanijibu.

“Nzuri”

“Nilikuwa naulizia usafiri wa kwenda Pemba”

“Wewe ndiye unayetaka kwenda Pemba?” akaniuliza.

“Ndiyo.

“Jahazi ile pale, tutaondoka sasa hivi”

Alinionesha jahazi moja iliyokuwa baharini ambayo tayari ilikuwa  imejaa watu.

“Kwa hiyo niende nikajipakie”

“Lipa nauli kwanza”

“Ni kiasi gani?”

“Elfu saba”

Niliona kilikuwa kiasi kidogo sana. Nikatoa kiasi hicho na kumpa.

Nilimpompa pesa hizo alizima bangi yake. Kipisi kilichobaki alikitia mfukoni kisha akainuka.

“Haya twende” akaniambia.

Nikafuatana naye kuelekea baharini.

“Sega suruali yako isiingie maji” akaniambia.

Nikasega suruali yangu. Tukaenda kupanda jahazi pamoja. Kumbe alikuwa akisubiriwa yeye avute bangi kwanza ndipo jahazi liondoke.

Nilitafuta mahali nikakaa na kuanza kuitafakari safari hiyo ambayo ilishaanza kunitia mashaka.

Nahodha mwenyewe ameshavuta bangi, jahazi limejaa abiria na mizigo na bahari ilionekana haikuwa shwari.

Lakini kutokana na umuhimu wa safari yenyewe ilibidi niende tu. Ingawa mimi nilipata hofu kidogo lakini usafiri huo ndio unaotumiwa siku zote na baadhi ya abiria kwa vile unapatikana kila siku na nauli yake ni nafuu.

Yule mtu alikuwa ndiye nahodha. Akiwa kwenye ile jahazi alikuwa na lugha chafu na alikuwa mkali kama pilipili.

Dakika chache  tu baada ya kujipakia sisi safari ikaanza. Jahazi iliondoka polepole, tukaanza kuiacha pwani ya Pangani. Baada ya masaa mawili mji wa Pangani hatukuuona tena.

Ghafla upepo mkali ukaanza kuvuma tukawa tunakutana na mawimbi makubwa makubwa. Nikaona baadhi ya  abiria wanawake wakianza kupiga kelele. Huku baadhi wakitapika hasa watoto.

Chombo chetu kilikuwa kikiinuliwa na mawimbi na kisha kurudishwa chini kwa kishindo. Abiria mmoja ambaye nilikuwa nimekaa naye akaanza kutapika.

Nahodha alikuwa amesimama ameshikilia kamba. Kazi yake ilikuwa ni kulielekeza jahazi kulielekea wimbi linapotokea. Sikujua ilikuwa ni kwanini alifanya vile. Mimi niliona ilikuwa  vyema kulikwepa wimbi na sio kulifuata.

Wakati anapolielekea wimbi ndipo jahazi linapoinuliwa na kisha kurudishwa chini na hapo ndipo watu wanapotapika na  kupiga kelele.

Hali ilizidi kuwa mbaya mpaka mimi mwenyewe nikaona matumbo yamenichafuka. Nikasikia baadhi ya abiria wakipiga kelele kumwammbia nahodha.

“Rudisha chombo bandarini!  Rudisha chombo bandarini! Hali si shwari”

Wengine walikuwa wakisema.

“Nahodha utatuua wewe, kuna watoto humu!”

“Alikuwa akivuta bangi, huyo hana akili!” Mwanamke mmoja alisema kwa hasira.

Pamoja na kelele zote hizo nahodha huyo hakumsikiliza mtu yeyote, aliendelea kukielekeza chombo hicho kwenye mawimbi. Ile dharuba iliyokuwa ikitupiga haikumtia hofu hata chembe.

Pale ndipo nilipogundua sababu ya baadhi ya manahodha kuvuta bangi, ni kutaka kupata uwezo wa kiakili wa kukabiliana na ile hali endapo itatokea.

Yule mtu alionekana kama mwehu. Wimbi linapokuja linatutosa. Na yeye alitota chapa chapa lakini hakuonesha kupata hofu wala kujali. Siku ile niliapa kuwa sitasafiri tena na jahazi na sikujua kama tungefika salama Pemba.

Yale mawazo ya kufa yakanifanya nimkumbuke mke wangu. Nikakumbuka kwamba nilimuahidi kumtumia nauli na nikahisi kwamba angenipigia simu kuniulizia tena.

Nikatoa simu yangu na kuizima ili akipiga simu asinipate.

Je nini kitatokea? tukutane kesho hapahapa kumekucha.com

No comments:

Post a Comment