Monday, October 16, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI, SEHEMU YA 16

HADITHI

MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI 16

ILIPOISHIA

Baada ya hapo ndipo mke wa Waziri Mkuu alipomsafisha Monica ile damu na kuliweka vizuri lile jaraha ili lisioneshe athari ya meno.

“Mimi naona tuweke plasta hapa watakaomuosha wataiondoa watajua alijiumiza mwenyewe” Mke wa Waziri Mkuu alishauriana na mume wake ambaye limkubalia.

Baada ya kuushughulikia mwili wa Monica ndipo Waziri Mkuu alipotoa taarifa ya kifo cha mwanawe usiku ule ule.

Viongozi wa serikali wakaanza kumiminika nyumbani kwa Waziri Mkuu. Raisi mwenyewe pia alifika usiku huo huo baada ya kupata habari ya kifo hicho.

Waziri Mkuu alikuwa akitoa maelezo ya uongo aliyokuwa ameyapanga na mke wake juu ya kifo cha binti yao.

Kwa vile kifo hicho kilikuwa kimetokea ghafla, watu wengi walipatwa na mshangao waliposikia taarifa ya Waziri Mkuu.

SASA ENDELEA

Asubuhi kulipokucha maombolezo yakaanza nyumbani kwa Waziri Mkuu. Wakati wote mke wa waziri Mkuu na Vero, binti yao wa kwanza, walikuwa sambamba na Sofia. hawakumpa nafasi ya kuwa peke yake kwa sababu yakutomuamini.

Hatimaye mwili wa Monica uliagwa  kwa heshima za viongozi wa Serikali na wananchi waliofurika  mchana kabla ya kusafirishwa kijijini kwao Morogoro kwa ajili ya mazishi.

Baada ya mazishi ya Monica ndipo Waziri Mkuu na mke wake walipokaa chini kulizungumzia suala la Sofia.

“Sasa itabidi uende naye Nairobi kama ambavyo tulipanga” Waziri Mkuu alimwambia mke wake.

“Niende naye lini?”

“Hatuna muda wa kupoteza, yasije yakatokea mengine. Utakwenda naye kesho kwa ndege”

“Umeshatayarisha mipango yote?”

“Mipango iko tayari. Kinachohitajika ni safari tu”

“Sawa”

Siku iliyofuata Sofia na mama yake wakapanda ndege kuelekea Nairobi nchini Kenya. Walitua katika uwanja wa Jommo  Kenyatta wakapanda teksi iliyowapeleka katika hospitali ya magonjwa ya akili iliyokuwa nje kidogo ya jiji la Nairobi.

Siku ile ile vipimo vya akili ya Sofia vilichukuliwa na siku ile ile matokeo yake yalipatikana. Sofia aligunduliwa alikuwa mzima kabisa wa akili. Matokeo hayo yalimshangaza mama yake.

Akaona ampigie mume wake kumjulisha.

Waziri Mkuu alipoambiwa hivyo na mke wake naye alishangaa.

“Hawakugundua tatizo lolote?” akamuuliza.

“Ripoti yake inaonesha kuwa hana tatizo lolote la akili”

“Umewaeleza kuhusu vitendo ambavyo amevifanya”

“Siwezi kuthubutu kufanya hivyo”

“Ni kweli. Sasa jaribu kuchukua vipimo vya malaria”

“Itabidi twende katika hospitali nyingine. Hii ni ya magonjwa ya akili peke yake”

“Mnaweza kwenda”

Sofia na mama yake wakapanda tena teksi iliyowapeleka katika hospitali nyingine iliyokuwa katikati ya jiji.

Sofia alifanyiwa uchunguzi wa damu yake kuangalia vimelea vya malaria lakini jibu lililotoka ni kuwa Sofia hakuwa akiugua malaria.

Mama yake alimpigia tena simu mume wake akamjulisha kuhusu matokeo hayo.

“Mh! Ni mambo ya ajabu!” Waziri Mkuu akasema.

“Lingekuwepo moja kati ya malaria au ugonjwa wa akili tungeelewa”

“Sasa tuseme ana tatizo gani?”

“Tatizo lake halijulikani”

“Halijulikani lakini lipo. Lazima tatizo liwepo”
 
“Sisi tunalala leo tunarudi kesho”

Waziri Mkuu akanyamaza kimya.

“Mbona umenyamaza?”

“Ninafikiria. Tegemeo langu kubwa lilikuwa huyo mtoto atakutwa na matatizo kichwani mwake…”

“Hayakukutwa. Sasa unashaurije?”

“Basi mnaweza kurudi hapo kesho”

Usiku wa siku ile walilala katika hoteli moja jijini humo asubuhi yake wakapanda ndege kurudi Dar.

Waziri Mkuu alituma gari kwenda kuwapokea kiwanja cha ndege. Gari hilo liliwapeleka nyumbani. Siku iliyofuata Sofia na mama yake walikwenda kwao Morogoro.

Mke wa waziri Mkuu akaenda kwa mganga mmoja kijijini kwao na kumuelezea kuhusu matatizo ya mwanawe.

“Inawezekana ana matatizo lakini hatuwezi kuyajua mpaka nipige ramli” Mganga akamwambia.

“Tunataka tuyajue na uyatibu, piga ramli”

Mganga akapiga ramli yake ya kuchungulia tunguri. Alikuwa akichungulia kwenye tundu ya tunguri kisha anaeleza alichokuwa anakiona.

“Ramli yangu inanionesha mbali sana” Mganga akasema.

“Mbali, wapi?”

“Ramli inakwenda kwa baba yake”

“Amefanya nini?”

“Huyu ndiye amemdhuru mtoto…”

“Eti nini, baba yake ndio amemdhuru binti yetu? Amemdhuru kivipi?”

“Hebu nieleze wewe mke wake, kabla ya mumeo kuwa Waziri Mkuu alifanya nini?”

Mke wa Waziri Mkuu akabetua mabega.

“Sijui”

“Hakuna sehemu ambayo alikwenda kutambika au kufanya maombi?”

“Ndiyo nakumbuka. Alikwenda kwa bibi mmoja kijijini kwao wakaenda kwenye mzimu”

“Walikwenda kwenye huo mzimu kwa madhumuni gani?”

“Mh! Ni kwa mambo yao haya  ya kisiasa”

“Yapi, hebu nieleze”

“Mimi aliniambia alikwenda kutambikiwa na kuweka nadhiri kwenye mzimu wa kwao kuwa endapo atateuliwa kuwa Waziri Mkuu atapeleka ng’ombe kwenye ule mzimu”

“Je alipoteuliwa kuwa Waziri Mkuu alitimiza nadhiri aliyoweka?”

“Mh! Sijui sasa…”

“Nenda kamuulize alipeleka yule ng’ombe?”

“Kwa hiyo kama hakupeleka linaweza kuwa ndio tatizo?”

“Ndio”

“Sasa ngoja nirudi Dar, niende nikamuulize Jibu atakalonipa nitakuja kukuambia”

“Utakuja lini tena?”

“Nitakuja kesho”

“Utanikuta”

Mke wa Waziri Mkuu akarudi Dar pamoja na Sofia. Wakati wa usiku akamueleza mumewe kuwa alikwenda kwa mganga wa kienyeji na kuelezwa aliyoelezwa.

Waziri Mkuu alipoyasikia maelezo ya huyo mganga akashituka. Mawazo yake yakarudi nyuma miaka kadhaa iliyopita, wakati huo akiwa Waziri wa Nchi ofisi ya Makamu wa Rais.

Chama chake kilikuwa kimeshinda uchaguzi. Rais alikuwa anasubiri kuapishwa ili aunde serikali  yake. Kulikuwa na watu watatu waliokuwa wakitajika kupewa wadhifa huo, mmojawapo akiwa yeye.

ITAENDELEA kesho kesho Usikose Uhondo huu nini kitafuatia

No comments:

Post a Comment