Thursday, October 19, 2017

RIWAYA, KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI SEHEMU YA 3

RIWAYA

KAMA UNATAKA FEDHA ZA MAJINI 3

ILIPOISHIA

Baada ya kukaa na kuwaza nikiwa pembeni mwa kitanda nilichoulaza mwili wa baba, nikayakumbuka yale maneno ya baba aliyoniambia.

“Cha kwanza ninachotaka kukwambia ni kuwa endapo nitafumba macho siku yoyote, urithi wako uko chini ya mvungu wa kitanda nilicholala”

Nikajiambia baba yangu alishajua kuwa atakufa leo ndio maana aliniita na kunieleza maneno hayo.

Lakini shauku ya kutaka kujua kile alichoniambia ni urithi wangu kilichoko chini ya mvungu ikanipata. Nikachutama na kumulika taa chini ya mvungu wa kitanda chake.

Nikaona mfuko wa ngozi kisha nikaona sanduku la chuma. Shauku yangu ikawa kwenye lile sanduku la chuma.

Nikatia mkono mvunguni na kulivuta. Lilikuwa zito. Ikabidi nitumie mikono miwili, nikalitoa kwenye mvungu.

Lilikuwa llimefungwa kwa kufuli kubwa ya shaba. Nikafikiria niivunje ile kufuli ili nitazame kilichomo ndani lakini nikakumbuka baba yangu alikuwa na tabia ya kutembea na funguo nyingi anazozifunga kiunoni.

SASA ENDELEA

Nikajua lazima kutakuwa na funguo ya kufuli ile.

Nikainuka na kumtazama kiunoni. Nikaziona zile funguo alizozifunga kwenye mkanda wake. Nikazitoa.

Zilikuwa karibu funguo tano. Nikawa natafuta ufunguo unaokubaliana na ile kufuli. Nikagundua funguo mbili. Kwa vile sikujua ni funguo ipi itakayofungua ile kufuli, nilizijaribu zote. Moja ilikataa hata kuingia kwenye tundu ya kufuli. Nyingine ikakubali na ndiyo iliyofungua kufuli hiyo.

Kufuli ilipofunguka niliichomoa nikaufungua mlango wa sanduku hilo. Nilipotupa macho ndani nilishituka nikajiuliza kama kweli baba yangu alikuwa na utajiri wa kiasi kile!

Noti nyekundu za elfu kumi kumi zilikuwa zimejaa ndani sanduku hilo hadi juu! Wakati ninazitazama niliona kama ninachanganyikiwa kwa sababu sikuwahi kuona fedha nyingi kiasi hicho.

“Baba yangu alizipata wapi pesa hizi?” nikajiuliza kwa mshangao lakini sikupata jibu akilini mwangu.

Nikaona nizitoe zile pesa na kuzihesabu. Nilifanya ile kazi usiku kucha! Mpaka kunaanza kupambazuka sikuwa nimemaliza kuzihesabu noti zote.

Nikaona nizirudishe kwenye lile sanduku. Nikalifunga na kutia ile kufuli kisha nikalibeba na kwenda nalo katika chumba nilichokuwa ninalala mimi. Nikalitia mvunguni.

Nikarudi tena katika chumba cha baba. Nikaufunika mwili wake kwa shuka yake aliyokuwa akijifinika. Nikaamua nikae kwenye kiti nisubiri kuche ili nitoe taarifa kwa majirani kuwa mzazi wangu amefariki usiku.

Ilipofika saa kumi na mbili asubuhi nikampigia simu mke wangu na kumjulisha kuwa babamkwe wake amefariki usiku.

Mke wangu alishituka sana akaniambia angefanyaje wakati baba yake naye alikuwa katika hali mbaya.

“Wewe mshughulikie mzazi wako kwanza, huku tutazika tu” nikamwambia.

Akanipa pole nyingi na kuniambia kuwa alikuwa ananisikitikia hasa vile ambavyo nilikuwa peke yangu. Baada ya mazungumzo yetu nikakata simu na kuwapigia ndugu na jamaa waliokuwa pale Korogwe.

Baada ya hapo nikatoka nje. Muda huo baadhi ya watu walikuwa wanakwenda mashamba na wanawake walikuwa wakifanya usafi nje ya nyumba zao.

Watu wa kwanza kuwaarifu walikuwa ni wale majirani zetu wa karibu. Baada ya kuwapa taarifa na wakafika nyumbani kwangu. Kuna waliojitolea kusambaza habari zile kwa majirani wa mbali zaidi.

Ndugu wa upande wa baba walipofika tulikubaliana kuwa marehemu tumzike mchana wa siku ile ile kwa vile hakukuwa na cha kungoja.

Tuliita walimu waliokuja kuuandaa mwili wa marehemu kwa ajili ya mazishi ikiwa ni pamoja  na kufanya visomo vilivyohitajika. Hadi inafika saa sita mchana, kila  kitu kikawa tayari. Mwili wa marehemu ulitiwa kwenye jeneza na kutolewa kwa ajili ya kupelekwa msikitini kuswaliwa.

Baada ya marehemu kuswaliwa alitolewa kupelekwa makaburini tayari kwa ajili ya mazishi.

Tulipomaliza kuzika tulirudi ntumbani ambako baada ya kufanyika dua ya mwisho ya kumuombea marehemu, nilitoa hutuba fupi kuwashukuru ndugu jamaa na majirani walioshirikiana na mimi katika msiba huo.

Kama ilivyo kawaida katika mazishi yoyote yale, niliuliza kama marehemu alikuwa akimdai mtu yeyote au kama alikuwa anadaiwa na mtu yeyote yule.

Sikupata jibu. Nikataoa angalizo kama kutatokea mtu yeyote ambaye anadaiwa na marehemu au anamdai marehemu anifuate mimi na kunifahamisha anachodai ili niweze kumlipa  na kama anadaiwa yeye anilipe mimi.

Baada ya hapo niliwashukuru tena watu wote na kuwapa ruhusa ya kuondoka. Watu wakatawanyika na kurudi katika shughuli zao.

Tulibaki ndugu watupu tukaweka vikao vyetu. Baada ya vikao hivyo ndugu hao nao wakatawanyika. Nyumbani kulibaki wanawake wachache ambao walikaa kwa siku tatu kukamilisha mila zetu. Siku ile ya tatu walioga maji na kuondoka.

Nikabaki peke yangu kwenye nyumba ile. Mara tu baada ya watu kuondoka nilijifungia chumbani mwangu nikalitoa lile sanduku la pesa. Nililifungua nikatoa zile pesa na kuzimwaga kwenye godoro. Zilienea godoro lote.

Nikaanza tena kuzihesabu ili nijue zilikuwa ni kiasi gani. Siku ile ya kwanza nilipozihesabu niliziacha nusu. Sasa nikaamua kuzihesabu zote.

Kwa vile pesa zenyewe ziliwekwa katika vitita vya shilingi milioni moja moja. Ilinirahisishia kazi ya kuzihesabu.

Zile pesa nilizozihesabu nilikuwa ninazirudisha mle mle kwenye sanduku.

Nilianza kuhesabu kutoka saa tatu asubuhi, hadi inafika saa sita mchana sikuwa nimezimaliza pesa zote. Kulikuwa na kiasi kikubwa ambacho kilikuwa kimebaki.

Nikaendelea kuhesabu ili nikimalize kiasi hicho lakini kila nilivyoendelea niliona kama vile zile pesa zilikuwa haziishi. Nikaanza kupata wasiwasi.

Sanduku lilikuwa linakaribia kujaa lakini pesa zilizobaki zilikuwa nyingi kuliko zile nilizozihisabu na kuzitia kwenye sanduku hilo.

“Pesa zote hizi si zilitoka kwenye sanduku hili hili?” nikawa najiuliza.

“Mbona sasa zinaonekana ni nyingi?” nikaendelea kujiuliza.

Ile kazi ya kuhesabu ikaanza kunitia uvivu. Sasa nikataka nizirudishe zile pesa zote kwenye sanduku nione kama zitajaa na kubaki.

Baada ya kufanya hivyo nikaona maajabu. Pesa hizo ambazo sikuwa nimezihesabu ambazo niliona zilikuwa nyingi kuliko zile nilizozitia kwenye sanduku, nilipozirudisha kwenye sanduku hilo ziliingia zote bila kubaki.

Kwa kweli nilipata wasiwasi. Nikazitazama pesa hizo kisha nikalifunga lile sanduku na kulirudisha mvunguni.

Nikakaa kitandani na kujiuliza, baba yangu alipata wapi pesa zile wakati mwenyewe alikuwa masikini.

Lakini kulikuwa na matukio ya wakati wa nyuma ambayo yalinifikirisha. Ile nyumba tuliyokuwa tunakaa pale kijijini ilikuwa ni ya gharama kubwa na aliijenga marehemu baba yangu. Hakukuwa na mtu yeyote ambaye alijua baba yangu alipata wapi pesa za kujengea nyumba ile wakati raslimali yake ilikuwa ni shamba dogo tu.

Pia nilikumbuka kuwa aliwahi kufungua duka kubwa halafu akalifunga. Hakukuwa na aliyejua alipata wapi pesa za kufungulia duka lile. Pia alinunua gari la thamani akaliendesha kwa siku chache tu kisha akaliuliza.

Wakati ule sikupata akili ya kumuuliza baba alipata wapi pesa za kufungua duka au kununua gari, nilipata akili ya kumuuliza kwanini alilifunga lile duka na kwanini aliuza lile gari.

Jibu lake lilikuwa alilifunga lile duka kwa sababu wachawi wakiona ana mali watamuandama sana.

Na kuhusu gari aliniambia ameliuza kwa kuogopa fitina za watu.

Sasa niligundua kuwa baba yangu alikuwa na pesa lakini hakutaka kutambulika. Alihofia kwamba endapo angejulikana kuwa ni tajiri angeuawa kwa mujibu wa mtazamo wake.

Kwa vile hakutaka ajulikane kuwa alikuwa na pesa aliishi kama masikini. Na hata mimi mwanawe nilijua kuwa baba yangu alikuwa masikini.  Lakini kumbe hakuwa masikini.

Lakini kitu ambacho kiliumiza akili yangu kukifikiria ni jinsi baba yangu alivyopata pesa zile. Baba yangu hakuwa na raslimali yoyote zaidi ya shamba, alipata wapi pesa hizo?

Wakati ninajiuliza swali hilo likanijia swali jingine, kwanini pesa hizo zinaonekana kama zina miujiza fulani. Wakati wa kuzihesabu zinaonekana kuwa ni nyingi na huwezi kuzimaliza?

Labda swali hilo ndilo ambalo lilinipa utata zaidi kwa sababu lilikuwa halina jibu.

Baada ya kutopata jibu nilitoka mle chumbani nikaingia katika chumba cha marehemu baba yangu. Nilichutama chini ya kitanda nikatia mkono na kutoa ule mkoba ambao niliuona mvunguni.

Niliutoa na kuona ulikuwa umejaa vumbi. Nikaukung’uta kisha nikaketi kitandani na kuufungua.

Ndani ya mkoba huo, niliona kitabu kidogo kilichokuwa na maandishi ya kiarabu. Nilikuta pete ya fedha ambayo baba yangu alikuwa akipenda kuivaa. Ilikuwa na kito cha rangi ya bahari kilichowekwa alama ya nyota na mwezi.

Pia nilikuta chupa ambayo ndani yake mlikuwa na yai zima lililoandikwa maandishi ya kiarabu kwa wino mwekundu. Pia mlikuwa na talasimu iliyokuwa na picha ya mtu. Sikuweza kujua lile yai liliingia vipi ndani ya ile chupa wakati mdomo wa chupa ulikuwa na uwazi mdogo sana.

Mbali ya ile chupa kulikuwa na kipande cha ubao mweusi uliokuwa na maandishi ambayo sikuweza kutambua yalikuwa ya lugha gani, Kigiriki si Kigiriki, Kichina si Kichina! Pia kulikuwa na vikorokoro vingine ambavyo sikuweza kuvielewa. Vitu hivyo kwa kweli vilinishangaza.

Baada ya kuviangalia kwa dakika kadhaa nilivirudisha ndani ule mkoba.

Nilichukulia kwamba wazee  wa zamani walikuwa na vikorokoro vingi vya kiasili walivyokuwa wanavihifadhi kwa imani mbalimbali. Na kwa kweli nisingeweza kujua baba yangu alikuwa amehifadhi vitu vile kwa sababu gani.

Nikaamua kuurudisha ule mkoba mvunguni nilikoutoa. Mkoba huo haukushughulisha sana akili yangu. Akili yangu ilikuwa imeshughulishwa zaidi na zile pesa. Nilipotoka pale chumbani nilitaka kurudi tena chumbani mwangu nizitazame tena zile pesa kwenye lile sanduku la chuma lakini nikajizuia. Niliona kama nilikuwa ninafanya jambo la kitoto.

Je nini kitatokea? Usikose kuwa nami kesho hapahapa tangakumekuchablog

No comments:

Post a Comment