Friday, October 6, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI SEHEMU YA ( 6 )

HADITHI hii inaletwa kwa hisani kubwa ya Kampuni ya mabasi ya FREYS COACH ifanyayo safari zake Tanga, Moshi, Arusha, Babati na Singida kila siku, na hufanya safari zake hizo kutoka Singida na Tanga kila siku, kwa mawasiliano 0622 292990

MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI 6

ILIPOISHIA

Kijana huyo aliyeonekana kuwa na wasiwasi alikaa kwenye kiti taratibu kama vile aliogopa kukiumiza.

“Unaitwa nani?”

“Naitwa Ramadhani Stambuli”

“Unaishi wapi?”

“Ninaishi Mbezi, hivi unavyoniona ninatoka Mbezi. Nilikodi teksi”

“Msichana mwenye namba niliyokupigia ni nani wako?”

“Ni rafiki yangu au niseme ni mpenzi wangu kwa muda mrefu”

“Sawa. Anaitwa nani?”

“Anaitwa Pili”

“Pili nani?”

“Pili Amrani”

“Anaishi wapi?”

“Anaishi hapa hapa Kinondoni”

SASA ENDELEA

“Mliwahi kukutana kwa siku ya leo?”

“Tulikutana jana usiku. Leo hatukuwahi kukutana”

“Kwanini msikutane, si umesema ni mpenzi wako?”

“Tuwapenzi, sawa lakini kila mmoja anaishi sehemu yake. Yeye anaishi Kinondoni, mimi ninaishi Mbezi. Mara nyingi tunakutana usiku kwa sababu mchana tunakuwa makazini. Na kwa usiku wa leo hatukukutana. Sikujua alikuwa amekwenda wapi na hakujibu sms zangu”

“Yeye anafanya kazi wapi?”

“Ni mpishi wa Waziri Mkuu”

Inspekta Alex akagutuka.

“Ala kumbe yule msichana ni mpishi wa Waziri Mkuu!”

“Ndiyo”

“Alitoka kazini muda gani?”

“Sijui kwa leo alitoka muda gani”

“Kwani kwa kawaida anatoka kazini saa ngapi?”

“Hana muda maalum. Wakati mwingine anatoka mapema, wakati mwingine anachelewa hadi saa tatu usiku”

“Sasa nikwambie kitu…”

“Ndiyo”

“Kama masaa mawili hivi yaliyopita tuliarifiwa kuwa kuna msichana ametupwa katika eneo la shule ya msingi ya Kinondoni…” Alex alimueleza mkasa mzima uliotokea.

Kijana huyo alishituka na kutikisa kichwa. Kwa sekunde kadhaa akawa ameduwaa akimtazama Inspekta Alex mdomo wake ukiwa wazi.

“Sikutaka kukueleza ukweli huo kwenye simu, nilitaka ufike hapa ndio nikueleze” Alex alimwambia.

“Pili ameuawa?” Kijana huyo akauliza kama aliyekuwa akiiuliza nafsi yake mwenyewe.

“Ndiyo ameuawa”

“Moyo wangu hautaki kukubali mpaka nisadikishe kwa macho yangu. Naomba kama inawezekana nikamuone mwenyewe huko hospitali” Kijana huyo akasema kwa unyonge.

“Utakwenda kumuona asubuhi. Unadhani ni kina nani waliofanya kitendo hiki?”

“Kwa kweli siwezi kujua, sikuwa naye wakati huo” Kijana huyo alijibu kwa kusikitika.

“Unaweza kukisia au kutueleza watu unaowashuku”

Kijana huyo akatikisa kichwa.

“Kwa kweli sina mtu yeyote ninayemfikiria kuwa anaweza kufanya kitendo hicho”

“Sawa. Sasa kuna kitu kingine ambacho wewe ndio utatusaidia, kuipata familia yake”

“Mimi nitawaonesha nyumbani kwao”

“Basi tunakutaka ufike hapa kituoni  kesho asubuhi ili utupe ushirikiano wako”

“Sawa. Nitafika hapo kesho asubuhi”

Siku iliyofuata Ramadhani Stambuli aliwasili kituoni hapo saa moja na nusu asubuhi. Macho yake yalikuwa mekundu yaliyovimba, hali iliyoonesha kuwa hakuwa amelala usiku uliopita.

Alipoondoka kituo cha polisi usiku alirudi nyumbani kwake ambako alikesha akiwaza huku akiomboleza hadi kunakucha.

Licha ya kufika mapema kituoni hapo alikutana na Inspekta Alex saa mbili na nusu asubuhi. Alikuwa amesubiri kwa saa nzima hadi inpekta huyo alipotokea.

Walipokutana, Stambuli aliambiwa asuburi. Alisubiri hadi saa tatu ambapo Inspekta Alex alimpakia kwenye gari.

“Sasa tunakwenda hospitali ya Muhimbili”

“Sawa”

Wakati gari likiwa katika mwendo Alex alimuuliza Stambuli.

“Mpaka sasa hujaweza kuwafikiria watu ambao wanaweza kuwa wamemuua Pili?”

“Sidhani kama watakuwa  watu ninaowafahamu. Nadhani watakuwa ni wahuni tu”

“Ndio sababu polisi tunahimiza sana juu ya ulinzi shirikishi jamii katika maeneo yetu. Ulinzi huu unasaidia sana kuzuia uhalifu mdogo mdogo na hata uhalifu mkubwa”

Stambuli akanyamaza kimya. Mawazo yake yalikuwa mbali sana.

“Unajua ni kwanini ninasema hivyo, ni kwa sababu uhalifu kama huu wa mauaji utazuilika kwa vile maeneo yetu yatakuwa na ulinzi wa wana jamii wenyewe. Na kama kwa bahati mbaya tukio kama hili linatokea basi ni rahisi wahalifu hao kujulikana au kukamatwa” Alex aliendelea kumueleza Stambuli.

“Ni kweli” Stambuli alimkubalia bila kuzingatia alichoambiwa.

Alex alipoona mwenzake alikuwa amefadhaika akanyamaza hadi alipolisimamisha gari kwenye maegesho ya hospitali ya Muhimbili.

Walishuka wakaingia ndani ya majengo ya hospitali hiyo. Dakika chache baadaye Mganga Mkuu alimpa Alex taarifa ya uchunguzi wa mwili wa maremu Pili iliyokuwa imetiwa kwenye bahasha.

Alex hakuisoma hapo hapo, aliomba kuuona mwili wa marehemu. Yeye na Stambuli wakapelekwa mochwari.

Walioneshwa mwili wa Pili ambao mara tu baada ya Stambuli kuuona aliangua kilio hapo hapo.

“Nyamaza bwana, wewe mwanaume!” Alex alimwambia akimpiga piga mabegani.

Stambuli aliendelea kulia.

“Jikaze rafiki yangu”

Walitoka hapo hospitali huku Stambuli akiendelea kulia. Lakini alinyamaza baadaye walipoingia kwenye gari.

“Najua inatia uchungu sana kwa sababu marehemu alikuwa mpenzi wako lakini jikaze kiume uweze kutusaidia” Alex alimwambia wakati akiliondoa gari.

Stambuli alijifuta machozi yake kwa kitambaa kabla ya kushukuru.

“Uhalifu umekuwa ni mwingi sana siku hizi katika jiji hili. Tunazidiwa kwa sababu polisi ni wachache”

Baada ya hapo hawakuzungumza chochote hadi walipofika kituoni.

Wakiwa ofisini mwa Alex ndipo inspekta huyo alipoisoma taarifa ya uchunguzi wa mauaji hayo.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa uchunguzi wa madaktari katika mwili wa marehemu umebaini chembe chembe za mate ya binaadamu katika eneo la shingo mahali ambapo unapita mshipa wa damu. Kuna kijaraha cha kung’atwa na meno katika mshipa huo ambapo damu ilifyonzwa mwilini kupitia mshipa huo na kusababisha kifo cha marehemu.

Taarifa hiyo ilikuwa  ndefu iliyoandikwa kitaalamu. Alex alipomaliza kuisoma aliiweka karatasi hiyo kwenye meza. Akamtazama Stambuli.

“Taarifa ya uchunguzi wa madaktari inaeleza kuwa marehemu aling’atwa katika mshpa wa shingo na kufyonzwa damu jambo ambalo limesababisha kifo chake” Alex akamwambia Stambuli.

“Alifyonzwa damu na binaadamu au mnyama?” Stambuli akamuuliza.

“Madaktari wamegundua chembe chembe za mate ya binaadamu, itakuwa aling’atwa na kufyonzwa damu na binaadamu”

“Ah! Binaadamu anamfyonza damu binaadamu mwenzake?”

“Ndio uchunguzi ulivyoonesha”

“Hakuuawa?’

“Ameuawa lakini ameuawa kwa njia hiyo”

Stambuli akatikisa kichwa kisha akawa kama anajiuliza peke yake.

“Sasa ni nani aliyefanya unyama huu?”

Alex akamjibu.

itaendelea kesho hapa hapa usikose KUMEKUCHA UPYA

No comments:

Post a Comment