Tuesday, October 10, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI SEHMU YA 10

HADITHI hii inaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya Kampuni ya mabasi ya usafirishaji abiria Tanga hadi Singida kila siku kupitia Arusha, Babati na hufanya hivyo kutoka Singida kwenda Tanga, kwa mawasiliano , 0622 292990

MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI 10

ILIPOISHIA

“Mimi nimeogopa sana yule polisi niliyezungumza naye kwenye simu aliponiambia sababu ya kifo cha Pili ni kufyonzwa damu. Ina maana Sofia alimfyonza damu nyingi”

“Halafu ile nguvu ya kumdhibiti yule mwanamke aliipata wapi. Ukiwatazama Pili na Sofia, Pili ana nguvu zaidi. Alimzidi vipi mpaka akaweza kumfyonza damu na kumuua?”

“Kisha unajua kuwa mpaka muda huu Sofia hajui alichotenda. Ina maana kwamba jana usiku alikuwa amerukwa na akili!”

“Inabidi tuendelee kumfanyia uchunguzi zaidi wa akili yake…”

Waziri Mkuu akakatizwa na mlio wa simu yake ya mkononi iliyokuwa kwenye mfuko wa koti lake. Hakuwa na tabia ya kutoa simu kwa haraka inapoita lakini siku ile aliitoa haraka ili kujua ni nani aliyekuwa akimpigia.

SASA ENDELEA

Akaona jina la waziri wa Mambo ya Ndani Jackson Maro.

Akapokea simu.

“Hello Maro…!”

“Mheshimiwa nilitaka kukufahamisha kuwa uchunguzi wa mauaji ya mpishi wa nyumbani kwako Pili  Amrani unaendelea. Nimearifiwa kuwa polisi wanataka kuja nyumbni kwako kuchukua maelezo”

Waziri Mkuu alishituka.

“Ni maelezo gani wanayoyataka?”

“Ni malezo yanayohusiana na uchunguzi wao”

“Sidhani kama tuna maelezo yanayoweza kuwasaidia kwa sababu Pili aliondoka hapa nyumbani mapema. Alituambia alikuwa anajisikia kuumwa. Sasa kilichoendelea huko alikokwenda hatukijui”

“Sawa. Mtawaeleza hali halisi. Kuna maswali ambayo watawahoji”

“Watakuja saa ngapi?”

“Watakuja muda huu”

Baada ya kusita kidogo Waziri Mkuu alisema.

“Sawa waache waje?”

“Nashukuru mheshimiwa”

Waziri Mkuu akaiweka simu juu ya stuli ndogo ya kioo iliyokuwa mbele yake.

“Ni nani?” Mke wake akamuuliza akiwa amekunja uso.

“Ni Jackson Maro Waziri wa Mambo ya Ndani”

“Anataka nini?”

“Ameniambia kuna  askari watakuja hapa kwa ajili ya uchunguzi wa mauaji ya Pili”

“Wanashuku kwamba ameuliwa hapa?”

“Hapana. Wanakuja kutuhoji tu kwa sababu inaonekana Pili aliuawa baada ya kuondoka hapa”

‘Sasa tutawaeleza nini hao polisi?”

“Itabidi tupange jinsi ya kuwaeleza”

Waziri Mkuu akajiweka sawa na kumuelekea mke wake.

“Sasa sikiliza, hawa jamaa wakija tuwe na kauli moja. Kwanza tusiwahusishe wale watoto. Tuwambie hawakuweko. Mimi na wewe ndio tutazungumza. Umenielewa?”

“Ndio”

“Kwa hiyo tutawambia kuwa Pili aliondoka saa kumi na moja jioni baada ya kudai kuwa kichwa kinamuuma, tukamruhusu aende hospitali”

“Labda wanaweza kuuliza aliondoka kwa usafiri gani kama alikuwa anaumwa?’

“Hatujui. Tutawambia kwamba hatujui. Hapa nyumbani aliondoka kwa miguu yake. Sasa huko nje hatujui alitumia usafiri gani”

“Sawa. Tutawambia hivyo. Sidhani kama watakuwa na maswali mengine”

“Wanaweza kuwa nayo lakini tutatumia akili kuyajibu”

Mke wa Waziri Mkuu akabaki kimya.

Ilikuwa ni baada ya saa moja Waziri Mkuu alipofahamishwa na mlinzi wa nyumbani kwake kuwa kulikuwa na makachero watatu waliokuwa wakihitaji kuonana naye.

Waziri Mkuu akatoa ruhusa makachero hao waingie ndani. Sekunde chache baadaye makachero hao wakakakaribishwa sebuleni na Waziri Mkuu mwenyewe.

Hawakupoteza muda. Mrakibu wa polisi kutoka idara ya upelelezi makao ya polisi Thabit Kombo alijitambulisha na kuwatambulisha wenzake Inspekta Alex na mwenzake Inspekta Temba.

“Mheshimiwa kuna hili tukio la mauaji ya Pili Amrani yaliyotokea Kinondoni jana usiku, ndio limetuleta hapa” Thabit Kombo alianza kumwambia Waziri Mkuu.

“Nimeshaarifiwa kuwa mtakuja. Hili tukio kwa kweli limenisikitisha sana” Waziri Mkuu alijidai kusikitika.

“Vile vile ni tukio ambalo limetushangaza polisi. Mara kwa mara mauaji yanatokea lakini si ya aina hii ya kuuawa kwa kufyonzwa damu”

“Inawezekana labda ni mnyama amemfyonza baada ya kuuawa”

“Hapana. Uchunguzi wa madaktari umebainisha kuwa aliuawa kwa kufyonzwa damu na aliyemfyonza ni binaadamu”

Waziri Mkuu akajifanya anatikisa kichwa kusikitika.

“Sijui huu ulimwengu hivi sasa unaelekea wapi!” alisema.

“Sasa mheshimiwa tumekuja kukusumbua kidogo. Tunahitaji maelezo kutoka hapa nyumbani kwako ambako yule msichana alikuwa anafanya kazi”

“Maelezo ya aina gani?”

“Kwanza tungependa kujua huyu marehemu jana aliondoka hapa saa ngapi?”

Waziri Mkuu akajifanya anafikiria.

“Kwa kweli jana aliondoka majira ya saa kumi na moja jioni”

Kombo alikuwa amefungua jalada alilokuwa ameliweka mapajani. Akaanza kuandika maelezo ya Waziri Mkuu.

“Alikuwa amewahi au ndio muda wake wa kawaida?”

“Yeye alikuwa ni mpishi wetu. Sasa kazi ya upishi si kama kazi ya ofisini, ikifika saa kumi unaondoka. Yeye kuondoka kwake ni mpaka amalize kazi. Wakati mwingine anaondoka usiku, wakati mwingine anawahi kuondoka”

“Anapotoka kazini anatumia usafiri gani kurudi nyumbani?’

“Usafiri unakuwa ni juu yake mwenyewe isipokuwa kuna siku tunamrudisha nyumbani kama ni usiku na kuna siku tunamfuata nyumbani kwake na gari”

“Kwa hiyo anapoondoka anatumia usafiri wake?’

“Hapa nyumbani anaondoka kwa miguu, sasa huko nje anajua yeye mwenyewe atapanda nini. Siku hizi kuna usafiri mwingi, kuna bodaboda, kuna teksi, kuna daladala”

“Mheshimiwa imeelezwa kuwa mwili wa marehemu ulitupwa katika eneo la shule usiku wa jana kutoka katika gari aina ya Toyota Land Cruisser ya rangi nyeupe…”

Waziri Mkuu alishituka.

Akanyamaza kimya kumsikiliza kachero huyo ili ajue angesema nini.

“Katika upelelezi wetu pia tunataka kulitambua hili gari ili liweze kukamatwa, je hapa nyumbani kwako kuna gari la aina hiyo?” Thabit Kombo akamuuliza.

Moyo wa Waziri Mkuu ukaanza kwenda mbio.

Kwanza alishukuru kwamba gari hilo halikuwepo pale nyumbani muda ule. Kama lingekuwepo na makachero hao wangeliona wangelitilia mashaka.

Alitumia kama sekunde tatu kujiuliza ajibu nini. Akubali kwamba analo gari hilo au akatae. Akajiambia endapo atakubali anaweza kuingia katika kashifa ya mauaji itakayopelekea sio tu kujiuzulu cheo chake bali pia kukabiliwa na mashitaka ya mauaji.

Akaona ni bora akatae kwamba hana gari hilo. Aliendelea kujiambia kwamba hata kama gari hilo litaonekana barabarani lisingeweza kushukiwa kwa vile jiji hilo lilikuwa na maelfu ya magari ya aina hiyo yenye rangi nyeupe.

Waziri Mkuu baada ya kuwaza alitikisa kichwa.

“Hapa nyumbani hatuna gari hilo” akasema.

Kachero Kombo aliandika kwenye jalada. Alipomaliza kuandika alimwambia Waziri Mkuu.

“Tunakupa pole kutokana na msiba huu. Tutaendelea kulitafuta hili gari na waliohusika katika tukio hili, ili wafikishwe katika vyombo vya sheria”

“Na mimi ninawaomba mjitahidi kuhakikisha kuwa watu hao wanakamatwa”

“Asante sana mheshimiwa. Tutajitahidi kwa kadiri ya uwezo wetu”

Makachero hao walimuaga Waziri Mkuu na kunyanyuka. Waziri Mkuu aliwasindikiza hadi nje ya nyumba yake. Makachero hao wakajipakia kwenye gari na kuondoka.

Mara tu Waziri Mkuu aliporudi ndani mke wake alimuuliza.

“Umesema huna gari hilo, je kama watalikamata barabarani na dereva akasema ni la kwako, huoni kama umejitia mwenyewe katika hatia”

“Na ni kwanini likamatwe gari langu wakati jiji hili lina maelefu ya  magari ya aina ile ya rangi nyeupe?”

“Polisi wanaweza kufanya msako wa kuyakamata”

“Watakamata magari mangapi na watakwenda kuyaweka wapi. Mimi nikisikia kuna msako huo nitawazuia. Nitawambia zoezi hilo litasumbua wananchi”

“Si itaonekana unazuia upelelezi?”

“Hapana. Sasa tujiandae twende huko kwenye msiba tuwape pole na pia tutoe ubani wetu”

“Sawa”

Baada ya kumaliza kula chakula cha mchana Waziri Mkuu na mke wake walikuwa kwenye magari mawili tofauti huku wakiongozwa na gari la polisi lililokuwa na kimulimuli.

Walifika Kinondoni nyumbani kwa wazazi wa Pili ambako tayari watu walikuwa wamejaa na vilio vilikuwa vimetawala.


ITAENDELEA kesho hapahapan usikose, KUMEKUCHA UPYA

No comments:

Post a Comment