Wednesday, October 11, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI SEHEMU YA 12

HADITHI hii inaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya Kampuni ya mabasi ya abiria FREYS LUXURY COACH  yanayofanya safari zake Tanga hadi Singida kupitia Moshi, Arusha na Babati kila siku, na hufanya hivyo kutoka Singida kwenda Tanga kila siku, kwa mawasiliano, 0622 292990

MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI 12

ILIPOISHIA

“Angerudi na angeniaga kuwa anakwenda sehemu, ningewambia”

“Unadhani atakuwa amekwenda wapi?”

Msichana huyo akabetua mabega yake.

“Kwa kweli siwezi kujua. Pili alikuwa mtulivu sana, hakuwa mtu wa kutokatoka sana anaporudi nyumbani. Mimi mwenyewe nilishangaa kwa kutomuona ile jana usiku.

“Hakuwahi kukueleza kama kulikuwa na mtu ana ugomvi naye?”

“Hakuwahi kunieleza. Pili mwenyewe alikuwa mpole sana. Sidhani kama alikuwa na ugomvi na mtu yeyote”

“Hakuwa na tabia ya kwenda kwa waganga wa kienyeji ambao labda watakuwa ndio waliomfyonza damu”

“Mh!” Msichana aliguna kisha alisema.

“Sijui. Kama alikuwa anakwenda kwa waganga wa kienyeji basi ilikuwa siri yake. Mimi hakuwahi kuniambia hata siku moja”

“Kwa hiyo huna tetesi tetesi zozote ulizozipata zinazohusiana na kuuawa kwake?”

SASA ENDELEA

Msichana akatikisa kichwa.

“Kwa kweli sijapata tetesi zozote”

“Tunakushukuru sana kwa maelezo yako ambayo ingawa hayakutusadia sana lakini yametupa mwanga kidogo”

“Na mimi pia nawashukuru, karibuni tena”

Wakati huo Kombo alikuwa ameshainuka, wenzake nao wakanyanyuka.

“Haya kwaheri mama” Mzee Amrani akamuaga.

“Jamanai karibuni sana”


Msichana huyo aliwasindikiza wageni wake hadi nje. Kombo na wenzake wakajipakia kwenye gari. Walimrudisha mzee Amrani nyumbani kwake kisha wakaelekea kituo cha polisi cha Kinondoni.

“Maelezo ya Waziri Mkuu na ya baba wa marehemu yanapingana sana” Kombo alimwambia Inspekta Alex.

“Hata mimi nimepata utata kidogo”

“Waziri Mkuu ametuambia kuwa marehemu aliondoka kazini kwake saa kumi na moja jioni baada ya kujisikia kuumwa kichwa na inawezekana kuwa alielekea hospitali. Lakini baba wa marehemu anasema mwanawe aliendelea kuwa kazini hadi saa moja na nusu usiku”

“Labda urudi tena kwa Waziri Mkuu akupe ufafanuzi zaidi” Alex alimwambia Kombo.

Kombo akanyamaza kimya. Aliona kurudi kwa Waziri Mkuu ili ampe ufafanuzi ilikuwa ni kama kumtuhumu kuwa alisema uongo.

“Hatuwezi kwenda kwa Waziri Mkuu kama tunaokwenda nyumbani kwa mtu mwingine” Kombo alisema baada ya ukimya. Akaongeza.

“Suala lenyewe ni muhimu sana kueleweka”

“Ni muhimu kwa sababu kinachotakiwa ni kujua marehemu alitoka saa ngapi kazini na alipotoka alikwenda wapi”

Baada ya Alex kusema hivyo palipita ukimya mwingine. Kombo alikuwa bado akiendelea kuwaza.

Alimuamini sana Waziri Mkuu kuwa hawezi kuongopa katika suala kama hilo lakini pia alimuamini yule mzee ambaye alimuonesha ushahidi wa meseji ambayo marehemu alimtumia saa moja na nusu usiku kumjulisha kuwa bado alikuwa kazini. Sasa nani atakuwa amesema uongo kati ya Waziri Mkuu na baba wa marehemu?

“Huu uchunguzi sasa umeanza kuingia utata!”  Kombo alisema na kuutanzua ukimya uliokuwepo.

“Afande mimi naona suala ni la kurudi kwa Waziri Mkuu ili atoe ufafanuzi!”

Msisitizo huo wa Alex ulimkera Thabit Kombo kwa vile mtu aliyemtaja alikuwa mheshimiwa. Lakini mbali ya kukereka huko Kombo aliona kauli ya Alex ilikuwa ya ukweli na ya maana.

“Nitajadiliana na wakubwa” Kombo alisema huku macho yake yakitazama mbele ya kioo. Uso wake ulionesha kuwa alikuwa amezama kwenye mawazo.

“Hilo pia ni wazo zuri, unaweza kwenda kumhoji mheshimiwa Waziri Mkuu ukajikuta unalaumiwa”

“Ninajua. Kazi zetu zinakwenda kwa sheria lakini pia kwa amri”

Kombo alimuacha Alex kituo cha polisi cha Kinondoni akaelekea makao ya polisi.

Alipofika alikwenda moja kwa moja kwenye ofisi ya afisa upelelezi wa mkoa.

“Afande nimekwenda nyumbani kwa Waziri Mkuu kuchukua maelezo yake na pia nimekwenda nyumbani kwa wazazi wa marehemu, nako pia nimepata maelezo kutoka kwa baba wa marehemu” Kombo alimwambia afisa upelelezi.

“Je umegundua nini katika upelelezi wako?”afisa upelelezi akamuuliza.

“Nimegundua kwamba kuna utata kati ya maelezo ya Waziri Mkuu na maelezo ya baba wa marehemu”

“Umegundua utata gani?”

“Maelezo yamepishana kidogo. Waziri Mkuu alitueleza kwamba marehemu aiondoka kazini kwake jana saa kumi na moja jioni. Aliondoka mapema kwa sababu alikuwa anaelekea hospitali baada ya kueleza kuwa kichwa kilikuwa kinamuuma”

“Ndio”

“Baba wa marehemu ametuambia kwamba aliwasiliana na mwanawe saa moja usiku akiwa bado yuko kazini. Alituonesha meseji ambayo marehemu alimtumia baba yake kumjulisha kuwa muda huo alikuwa bado yuko kazini. Na vile vile baba wa marehemu hakuwa na taarifa yoyote kuwa mwanawe alikuwa anaumwa”

“Naam. Huo utakuwa ni utata”

“Sasa tufanyeje?”

“Itabidi urudi tena nyumbani kwa waziri Mkuu ili atuweke sawa. Nitamfahamisha hilo Mkurugenzi wa Upelelezi”

“Sawa”

“Inawezekana alighafilika au inawezekana baba wa marehemu ndiye aliyeghafilika lakini vizuri umfahamishe ili atuweke sawa”

“Nimekuelewa afande”

                                        ******************

Toyota Land Cruiser la rangi nyeupe la mheshimiwa  Wazirui Mkuu lilikuwa linatoka Kibaha. Dereva wa gari hilo alikuwa ametumwa na mheshimiwa kwenda kukagua shughuli zilivyokuwa zikiendelea katika shamba lake lililoko nje kidogo ya mji wa Kibaha.

Shamba hilo lililokuwa na zaidi ya hekta mia moja lilikuwa na ng’ombe mia tatu wa mheshimiwa Waziri Mkuu na lilikuwa na wafanyakazi wasiopungua thelathini.

Dereva wa gari hilo Kidas Athumani alikuwa eneo la Kimara akielekea nyumbani kwa Waziri Mkuu. Aliona lori linataka kumpita akabana kushoto. Mbele yake kulikuwa na gari jingine dogo alilokuwa amelikaribia sana.

Kwa vile gari la Waziri Mkuu lilikuwa kwenye kasi, dereva Kidasi aligusagusa breki ili kuzuia gari lisiligonge gari la mbele yake kwa nyuma. Moyo wake ulishituka alipogundua kuwa breki haikutii agizo lake. Gari lilikuwa limefei breki!

Kutahamaki akajikuta ameligonga kwa nyuma gari la mbele yake!

Kwa sababu gari hilo lilikuwa limefeli breki liliendelea kulibamiza gari hilo hadi liliposimama.

Kidasi alifungua mlango na kushuka haraka. Alikwenda mbele ya gari hilo na kulitazama gari aliloligonga. Lilikuwa limebonyea sehemu ya nyuma upande wa kushoto ambapo taa yake ilikuwa imevunjika.

Mwenye gari hilo ambalo lilikuwa limesimama, naye alikuwa ameshuka akilitazama gari lake lilivyoharibiwa.

“Unaona!” alimwambia Kidasi kwa hasira.

“Samahani. Gari langu lilifeli breki”

Watu wakaanza kumiminika katika eneo hilo. Polisi wa usalama barabarani waliokuwa karibu wakajisogeza mahali hapo. Walishaona kilichokuwa kimetokea.

“Umemgonga mwenzako kwa nyuma, ni kosa kubwa sana” Polisi mmoja alimwambia Kidasi.

“Ni kweli gari langu lilikuwa limefeli breki” Kidasi aliwambia. Uso wake tayari ulishajaa tembe za jasho. Alitoa kitambaa akajifuta.

Polisi hao walilikagua gari lake kisha wakamwambia atoe leseni yake waione.

Kidasi aliwapa leseni yake. Polisi mmoja akaikagua.

“Lete kadi ya gari lako”

Kidasi aliwatolea kadi hiyo na kuwapa.

Baada ya kuikagua kadi hiyo polisi huyo alimuuliza Kidasi.

“Gari hii ni ya nani?”

“Ni ya mheshimiwa Waziri Mkuu”

Polisi hao walishituka.

“Wewe ni dereva wake?” Polisi mmoja akamuuliza.

“Ndiyo”

Walimrudishia leseni yake na kadi ya gari.

“Umesema gari ilifeli breki?”

“Ndiyo”


itaendelea kesho hapahapa tangakumekuchablog Usikose KUMEKUCHA UPYA

No comments:

Post a Comment