Sunday, October 15, 2017

HADITHI, MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI SEHEMU YA 15

HADITHI hii inaletwa kwenu kwa hisani kubwa ya Kampuni ya mabasi isafirishayo abiria kati ya Tanga hadi Singida kila siku na kutoka Singida kwenda Tanga kupitia, Babati, Arusha hadi Moshi, ofisi kwa Tanga zipo barabara ya 12 Ngamiani, kwa mawasiliano, 0622 292990

MBIO ZA SAKAFUNI HUISHIA UKINGONI 15

ILIPOISHIA

Hakupata jibu. Akasogea kwenye kitanda ambako Sofia alikuwa amelala akamtazanma kwa makini. Maswali matatu yakamjia  tena akilini.

Kwanini Sofia ana damu midomoni?

Damu ile imetoka wapi?

Na kwanini tumbo take limejaa?

Moyo wake ukiwa umeshituka, mke wa Waziri Mkuu alitoka haraka akashuka ngazi na kumfuata mume wake aliyekuwa chumbani.

“Hebu twende ukawaone wale watoto” alimwambia kwa sauti ya kutaharuki.

Waziri Mkuu naye alishituka.

“Wana nini?” akamuuliza.

“Hebu twende ukawaone mwenyewe”

Mke wa Waziri Mkuu alikuwa ameshatangulia kutoka. Waziri Mkuu akamfuata nyuma.

SASA  ENDELEA

Walipanda ngazi na kuingia katika chumba walichokuwemo Sofia na Monica.

“Hebu watazame”

Waziri mkuu akawatumbulia macho mabinti zake wawili, mmoja akiwa kitandani na mwingine akiwa chini.

“Uliwakuta wakiwa hivi hivi?”

“Niliwakuta hivyo hivyo, Monica yuko chini ana michirizi ya damu shingoni na Sofia yuko kitandani, mdomoni ana damu na tumbo lake limejaa…!”

Waziri Mkuu akiwa ameshituka alichutama akamtazama Monica.

“Monica! Monica! Monica!” alimuita mara tatu.

Monica hakuitika wala kugeuka. Mke wake alijaribu kumshika na kumuinua. Monica alikuwa baridi na alikuwa amelegea kama mnyoo. Akamrudisha chini na kuweka mkono kifuani kwake kusikiiza mapigo ya moyo wake.

Wakati akifanya hivyo Waziri Mkuu alikuwa akimtazama.

“Moyo unapiga?” akamuuiza.

Mke wake akatikisa kichwa.

“Sina hakika kama mwanangu yuko hai” akasema.

“Isije kuwa lile tukio la mpishi wetu limejirudia kwetu?”

Waziri mkuu naye aliuweka mkono wake kwenye pua ya Monica kuona kama alikuwa anapumua, hakuhisi dalili yoyote kuwa Monica alikuwa anahema.

Hapo hapo akaguna. Uso wake ukasawijika. Alikuwa kama mtu ambaye alitaka kulia.

Akanyanyuka na kusogea kunako kitanda, akamtazama Sofia. Kwa kumtazama kwa macho tu aligundua kuwa Sofia alikuwa akipumua tena alikuwa akipumua kwa nguvu kama alikuwa anakabwa pumzi.

Tumbo lake lililokuwa limejaa kuliko kawaida lilikuwa likienda juu na kurudi chini. Tembe za jasho zilikuwa zikiendelea kutanda kwenye paji la uso wake.

Midomo yake alikuwa ameichanua. Damu nyeusi ya mtu mwenye afya njema ilionekana kwenye papi za midomo hiyo. Meno yake yalionekana. Yalikuwa mekundu kwa damu.

“Sofia!” Waziri Mkuu alimuita.

Sofia aliendelea kupumua tu kama mtu aliyekuwa kwenye usingizi mzito.

Mke wa Waziri Mkuu alisogea karibu na kitanda akamshika mkono Sofia na kumuita.

“Sofia!”

Sofia akashituka, akafumbua macho na kuwatazama mama yake na baba yake kwa macho makali. Macho yenyewe yalikuwa mekundu yakionesha kuwa alikuwa katika usingizi mzito.

Sofia alipozinduka aliduwaa kwa sekunde kadhaa kabla ya kuinuka na kujifuta midomo yake. Aliifuta ile damu kisha akaitazama damu hiyo kwenye mikono yake.

“Hii ni damu!” akasema peke yake na kuuliza.

“Imetoka wapi?”

Alijipangusa tena kisha akaitazama damu hiyo.

“Ninatoka damu midomoni” alisema kisha akateuka.

Wakati huo wote baba yake na mama yake walikuwa wakimtazama.

“Inatoka wapi hiyo damu?” Baba yake akamuuliza.

Sofia akabetua mabega.

“Sijui baba, kinywa chote kimejaa harufu ya damu. Hapa nilipoteuka nimeteuka damu halafu naona tumbo langu limejaa”

Wakati Sofia akisema hivyo Baba yake na mama yake walikuwa wakitazamana kwa mshangao.

“Monica yuko wapi?” baba yake akajaribu kumuuliza.

“Nilikuwa naye hapa kitandani tunazungumza halafu usingizi ulinipitia. Labda ameondoka”

Waziri Mkuu akamtazama mke wake.

“lazima kuna tatizo” akasema.

“Kwani mwanangu unajisikiaje?” Mke wa Waziri Mkuu akamuuliza Sofia.

“Najisikia kichwa kinaniuma” Sofia alisema.

“Hebu toka naye” Waziri Mkuu akamwambia mke wake.

Mwanamke huyo alimshika mkono Sofia akamwambia ashuke kwenye kitanda.

“Monica si huyu hapa amelala chini!” Sofia alisema alipomuona Monica, lakini hakukuwa na yeyote aliyemjibu.

Alitoka na mama yake.

Waziri Mkuu alisali kisha akaubeba mwili wa Monica na kuuingiza katika chumba cha wageni, akaulaza kwenye kitanda.

Hapo ndipo alipomchunguza Monica kwa makini. Mbali ya kuthibitisha kuwa Monica alikuwa ameshakufa aligundua pia jaraha la meno kwenye shingo ya Monica, pale pale palipokuwa na michirizi ya damu.

Akashusha pumzi ndefu. Aliketi pembeni mwa kile kitanda akawa anajiuliza, mwanawe Sofia alikuwa amepatwa na nini?

Alishagundua kuwa Sofia alikuwa amemfyonza damu mwenzake hadi kumuua. Alifahamu pia kuwa wakati Sofia akifanya hivyo hakuwa akijitambua na baada ya hapo akapitiwa na usingizi mzito kama ilivyotokea siku ile kwa Pili.

Baada ya muda kidogo mke wake aliingia mle chumbani. Alisimama mbele ya kitanda kilicholazwa mwili wa Monica na kuangua kilio.

“Hapana, usilie mke wangu. Tatizo limeshatokea tunatakiwa tupange tutafanya nini. Kwanza Sofia yuko wapi?”

Mke wake alijifuta machozi.

“Sofia nimemuacha sebuleni anaangalia tv”

“Sasa hebu keti hapa tupange”

Mke wake akaketi kwenye pembe ya kitanda karibu na mume wake.

“Monica ameshakufa na ameuawa na Sofia, amemfyonza damu kama alivyomfyonza yule mpishi wetu” Waziri Mkuu alimwambia mke wake ambaye aliposikia maneno ya mume wake alianza tena kulia.

“Nimekwambia usilie, jikaze kwanza. Sofia atakuwa na matatizo ya akili. na matatizo yake ni makubwa kuliko ya mwendawazimu anayevua nguo”

“Si ndio tulipanga tumpeleke Nairobi kesho kutwa akafanyiwe uchunguzi, sasa leo tatizo limejitokeza tena”

“Tulichelewa. Lakini si kitu. Sasa huyu binti yetu aliyekufa tutasema ameuawa na nini?”

“Tutasema alikufa mwenyewe”

“Ana jeraha kwenye shingo yake!”

“Tumfute ile damu tumuweke sawa, tusimpeleke hospitali kuchunguzwa. Mtu anapokufa si lazima apelekwe hospitali”

“Ni sawa. Labda tuseme kuwa aliumwa ghafla”

“Ndio. Tunaweza kusema alidai kuwa alikuwa anajisikia vibaya baya. Wakati tunamuandaa kumpeleka hospitali akafariki ghafla”

“Itatosha”

“Hakuna atakayetuhoji chochote. Kifo ni kitu cha kawaida”

“Tukishamzika ndio tutashughulikia suala la Sofia”


ITAENDELEA kesho Usikose uhondo huu nini kitatokea na kufuatia.

No comments:

Post a Comment