Monday, September 19, 2016

HADITHI, YAMENIKUTA MIE SALAMA SEHEMU YA 3

HADITHI Inaletwa kwenu kwa hisani kubwa na Kampuni ya Usafirisji abiria kutokea Tanga, Moshi, Arusha, Babati hadi Singida kila siku na pia kutokea Singida kuja Tanga kila siku 0622 292990
 
NDOA YA SALMA 3
 
ILIPOISHIA
 
Nilimuandikia namba  yangu ya simu na kumuachia. Kwa vile yeye hakuwa na simu, sikuwa na haja ya kuomba namba yake.
 
Baada ya hapo nilitoa shilingi elfu hamsini nikampa.
 
“Hizi zitakusaidia kwa matumizi madogo madogo ukiwa hapa hospitalini” nikamwambia.
 
Msichana alipokea pesa hizo na kunishukuru.
 
“Asante kaka”
 
Yule muufuzi aliondoka na kutuacha.
 
“Hivi kaka ile baskeli niliyokuwa naendesha uliiona?”
 
“Baskeli yako itakuwa imechukuliwa na polisi. Ukitoka hapa unaweza kuifuata kituo cha polisi cha Mabawa”
 
“Asante kaka”
 
Baada ya hapo niliagana na yule msichana. Nilimuahidi kumtembelea tena siku itakayofuata.
 
Wakati natoka nje ya hospitali niliona polisi wa usalama barabarani wakisimamisha gari lao. Nikajua walikuwa wamemtembelea yule msichana.
 
Nikajipakia kwenye gari langu na kuondoka.
 
SASA ENDELEA
 
 
Zilipita siku tatu, sikufika kule hospitali kutokana na kubanwa na majukumu yangu. Siku ya nne yake nikafika kumjulia hali yule msichana.
 
Lakini nilikuta kitanda kikiwa na mgonjwa mwingine.  Kulikuwa na muuguzi aliyekuwa akimpa dawa mgonjwa huyo.
 
Nikawasalimia wote wawili kisha nikamuuliza yule muuguzi kuhusu yule majeruhi wa ajali ya gari.
 
“Unamuulizia Salma?” Muuguzi huyo akaniuliza lakini kabla sijamjibu akaniambia.
 
“Salma alishapewa ruhusa tangu jana”
 
“Kumbe…!”
 
Nikaduwaa kidogo kisha nikamuaga muuguzi huyo na kuondoka.
 
“Kama amepata nafuu ndivyo nilivyokuwa ninamuombea” nikajiambia huku nikijipakia kwenye gari langu.
 
Nililiwasha moto na kuondoka.
 
Ikapita wiki nzima. Nilikuwa ninaendesha gari langu nikitokea gereza la Maweni ambako nilikwenda kuchukua hundi ya malipo yangu, simu yangu iliyokuwa kwenye mfuko wa shati langu ilipoita.
 
Nilitumia mkono wangu wa kushoto kuitoa na kutazama namba iliyokuwa inanipigia. Sikuweza kuitambua. Ilikuwa namba ngeni.
 
Nikajiuliza haraka haraka ni nani? Sikupata jibu. Nikabonyeza kiwambo cha kupokelea na kuiweka simu karibu na sikio.
 
“Hello!”
 
“Hello! Bila shaka nazungumza na Ibrahim Amour?” Sauti laini ya kike ikaniuliza kwenye simu.
 
Nikajikuta nazungusha akili yangu kujiuliza alikuwa nani.
 
“Ndiye mimi, nani mwenzangu?” nikamjibu.
 
“Naitwa Salma Aboud!”
 
Kusema kweli moyo wangu ulishituka.
 
Hapo hapo nikamkumbuka msichana aliyekuwa amegongwa na gari wiki moja iliyopita.
 
“Wewe ndiye yule msichana uliyepata ajali?” nikamuuliza.
 
“Ndiye mimi. Nilishapewa ruhusa hospitali, samahani kwa kuchelewa kukujulisha. Najua huenda ilikusababishia usumbufu kidogo…”
 
“Ni kweli, nilifika hospitali nikaambiwa kuwa uliondoka jana yake. Vipi hali yako?”
 
“Kwa sasa sijambo kidogo”
 
“Unaendelea vizuri?”
 
“Nashukuru Mungu, ninaendelea vizuri”
 
“Nakumbuka  uliniambia unaishi Chumbageni, ndipo ulipo hivi sasa?”
 
“Ndiyo niko nyumbani Chumbageni”
 
“Ile baskeli yako uliipata?”
 
“Sijakwenda kituo cha polisi kuifuatilia”
 
“Natumaini itakuwa bado iko. Siku ukipata nafasi unaweza kwenda kuichukua”
 
“Sawa kaka. Asante. Kwa mara nyingine nakushukuru sana kwa msaada wako. Ukipata nafasi unaweza kunitembelea nyumbani, mama yangu atafurahi sana atakapokuona. Nilimueleza jinsi ulivyonisaidia”
 
“Vizuri. Nitatafuta siku ya kuja kukuona”
 
“Sawa. Asante sana kaka”
 
“Asante”
 
Msichana akakata simu.
 
Nikairudisha simu mfukoni..
 
“Salma bado ananikumbuka” nikajiambia kimoyomoyo wakati nikikata kona kuelekea benki.
 
Siku zikaendelea kupita.
 
Kulikuwa na siku nilikuwa nikiendesha gari langu mitaa ya Chumbageni. Kulikuwa na jamaa niliyekuwa nimemfuata. Sasa wakati narudi ofisini kwangu nikamkumbuka Salma ambaye aliniambia alikuwa anaishi Chumbage. Nikaliegesha gari langu pembeni mwa barabara kisha nikatoa simu yangu na kumpigia.
 
“Hello Salama!” nikasema mara tu simu ilipopokelewa.
 
“Kaka Ibrahim. Nimefurahi kuwa leo umenipigia”
 
“Niko maeneo ya Chumbageni, nataka nikujulie hali?”
 
“Oh! Uko upande upi?”
 
‘Niko hapa karibu na shule ya chekechea”
 
Salma akanielekeza nyumba  yao ilipo. Haikuwa mbali sana na pale. Nikafika.
 
Nilishuka kwenye gari. Nilimkuta amesimama mlangoni akinisubiri.
 
“Oh karibu” alliniambia huku akitabasamu.
 
Nilikwenda kwenye mlango, Salma akanikaribisha ndani.
 
Nilipita ndani. Upande wa kushoto wa nyumba hiyo kulikuwa na sebule pana iliyokuwa imepambwa vizuri.
 
“Karibu ukae” Salma akaniambia. Tabasamu lilikuwa likiendelea kuchanua usoni kwake.
 
Nikakaa kwenye kochi mojawapo.
 
“Ngoja nimuite mama, anataka kukuona”
 
Salma aliingia ndani. Nikabaki nikiyazungusha macho yangu kwenye sebule hiyo.
 
Punde tu Salama alirudi akiwa amefuatana na mwanamke mmoja. Kwa mimi mwenyewe nisingeweza kuamini kama yule alikuwa ni mama yake kwani alionekana bado msichana. Na walionekana kama mtu na mdogo wake.
 
“Mama yule kaka aliyenisaidia siku ile kunipeleka hospitali na kunitolea damu ndiye huyu hapa” Salama alimwambia mama yake.
 
“Baba unajisikiaje hali yako?” Mama huyo akaniuliza kwa furaha.
 
“Sijambo mama. Shikamoo”
 
“Marahaba. Habari za siku”
 
“Ni nzuri, sijui nyinyi hapa”
 
“Sisi hatujambo. Tunashukuru Mungu”
 
“Kaka Ibrahim, huyu ndiye mama yangu” salma akaniambia huku akiketi.
 
“Nimefurahi kumuona”
 
“Leo umeamua kututembelea…” mwanamke huyo aliendelea kuniambia. Alikuwa bado amesimama na hakuonesha dalili yoyote kuwa angeketi.
 
Baada ya kuulizana  naye hali akatuambia.
 
“Haya endeleeni kuzungumza, mimi niko huko uani nina kazi kidogo”
 
“Asante, hata hivyo sitakaa sana. Nimekuja mara moja  tu kumjulia hali mgonjwa wangu kisha nitaondoka”
 
ITAENDELEA

No comments:

Post a Comment