Friday, September 23, 2016

HADITHI, YAMENIKUTA SALAMA MIE

SIMULIZI ZA FAKI A FAKI
 
YAMENIKUTA SALMA MIE  6
 
ILIPOISHIA
 
“Wangu mimi hatugombani, ni mgumu tu. Kila siku yeye hana pesa lakini biashara anafanya. Sijui pesa zake zinakwenda wapi!”
 
“Basi ana mwanamke nje, ndiye anayemla. Mwenzangu wala chuya, mchele waliwa na mwenzio!”
 
Rita aliponiambia hivyo alinicheka na mimi nikajidai kucheka lakini moyo wangu ulipata fadhaa sana nilipohisi kuwa inaweza kuwa ni kweli mume wangu akawa na msichana  wa nje anayekula pesa zake.
 
Siku ile niliwaza sana yale maneno aliyoniambia shoga yangu.
 
Mume wangu aliporudi jioni nilijaribu kumwambia.
 
“Mume wangu huninunulii hata pikipiki na mimi”
 
“Unataka pikipiki ya nini mke wangu?”
 
“Pikipiki ya nini? Watu wananunuliwa magari, wewe unasema pikipiki ya nini?”
 
“Kama ni gari si hili tunalo”
 
“Hilo ni la kwako. Mimi nataka pikipiki”
 
“Tuombe Mungu, kazi zangu zikienda vizuri nitakununulia”
 
“Utaninunulia lini?”
 
SASA ENDELEA
 
“Si nimekwambia ufanye subira. Mambo yakiwa mazuri utapata pikipiki, hata gari”
 
“Yako ni hayo tu kila siku. Wanaume wengine hawapendi hata kuwapendezesha wake zao!”
 
“Salma usiige mambo ya watu. Kwa vile umemuona jirani yako ana gari na wewe unataka ununuliwe gari. Wewe unajua mume wake anafanya kazi gani?”
 
“Wala sio hivyo. Mimi nina akili zangu na naangalia maisha yangu. Siigi mtu mimi. Kama ninataka pikipiki ninaitaka kwa shida yangu. Tatizo ni kuwa kila ninachokwambia mume wangu lazima ukipinge”
 
Ibrahim akajidai kucheka.
 
“Si kweli. Mbona vitu vingi nakununulia. Nguo nakununulia pamoja na kukutimizia  mahitaji mengine. Sema wewe sasa unataka makubwa”
 
“Haya basi nayaishe. Naona labda kuna mwenzangu wa pembeni maana siku hizi umebadilika sana”
 
Siku ile nilijaribu tu kumpima mume wangu ili nione atanijibu nini. Lakini jibu lake lilikuwa ni la kukatisha tamaa. Sikamini kabisa kuwa kwa kipato cha mume wangu angeshindwa kuninunulia pikipiki.
 
Pia sikuamini kuwa mwaname huyo angeshindwa kunitimizia mahitaji yangu mengine ninayotaka kama anavyofanyiwa shoga yangu na mume wake.
 
Pegine ulikuwa ni ugumu au roho mbaya inayotokana na mila zilizopitwa na wakati zinazowadharaulisha wanawake kwa wanaume.
 
Baada ya siku ile sikumuuliza kitu tena Ibrahim lakini ndani ya moyo wangu nilishaamua kama tabia ya Ibrahim itaendelea kuwa  ile nisingeweza kupata maendeleo kama wanawake wenzangu.
 
Nilikaa kama siku tatu hivi nikiwaza, siku ya nne yake nikaenda kwa yule rafiki yangu. Nilimkuta amekaa sebukeni akitizama filamu kwenye televisheni yake.
 
“Vipi shoga?” akaniuliza.
 
“Ah mambo ya mume wangu yananichokesha!” nikamwambia huku nikiketi kwenye kochi.
 
Shoga yangu Rita akanicheka.
 
“Yamekuchokesha vipi shoga?”
 
“Ugumu shoga! Mume wangu ni mgumu sana. Juzi nilijaribu tu kumuomba aninunulie pikipiki, eti anajidai kuniuliza pikipiki ya nini…gari si hili tunalo”
 
“Labda hana pesa”
 
“Sio kutokuwa na pesa, sema ni mgumu. Pesa anazo lakini ana dharau, hataki maendeleo yangu. Nimeshamuona yule si mume ni gume gume”
 
Shoga yangu akacheka tena lakini mimi sikucheka nilijifanya nimekasirika.
 
“Kweli nakwambia shoga…yule si mume ni gume gume”
 
“Siku ile nilikwambia mwendee kwa songoma ukaleta gozi gozi. Si unamuona huyu mume wangu nimemnyoosha, haoni wala hasikii, nikikohoa tu ananiuliza wataka nini mke wangu?”
 
“Na hilo la songoma ndilo lililonileta, nataka unipeleke na mimi nikamtengeneze, awe kama mume wako. Nikimuona amekaa sawa, namwambia anijengeee nyumba”
 
Mimi na shoga yangu tukacheka pamoja.
 
“Na huyo songoma mwenyewe akikufanyia dawa zake utakuja kuniambia. Lazima mumeo atakujengea nyumba” Rita akaniambia na  kuzidi kunipa moyo.
 
“Sasa utanipeleka lini shoga?”
 
“Siku yoyote utakayotaka, mimi niko tayari”
 
“Nataka unipeleke kwa huyo huyo aliyekufanyia wewe”
 
“Na ndiko huko huko nitakakokupeleka”
 
“Na itachukua siku ngapi hadi matokeo yaonekane?”
 
“Si siku nyingi. utamuona akibadilika kidogo kidogo”
 
Nilinyamaza kidogo kufikiri kisha nikamuuliza.
 
“Tunaweza kwenda kesho?”
 
“Tunaweza lakini iwe asubuhi, mpaka saa sita twe tumerudi”
 
“Na mimi pia muda wangu mzuri ni wa asubuhi, yule bwana akienda kazini. Najua akiondoka harudi mpaka jioni”
 
“Harudi mchana kuja kula?”
 
“Zamani ndio alikuwa anarudi kula lakini siku hizi akiondoka ndio mpaka jioni. Sijui anakula kwa huyo mke mwenzangu!”
 
“Yote utayajua huko huko kwa  huyo mganga”
 
“Kama ana mwanamke atanieleza?”
 
“Atakueleza yote”
 
“Nataka nijue, uwezekano huo wa kwa na mwanamke upo”
 
“Sasa basi wewe jiandae, nikikupigia simu kesho asubuhi unakuja, tunakwenda zetu”
 
“Ni mbali sana”
 
“Mganga mwenyewe yuko Kisosora”
 
“Si tutakwenda na gari yako”
 
“Tutakwenda na gari yangu, usijali. Hapo Kisosora hata lita moja ya petroli haimaliziki”
 
“Tutatia lita moja”
 
“Mbona mume wangu ananitilia ya kutosha. Ananiwekea mafuta ya wiki nzima”
 
“Acha mambo yaende vizuri, na mimi keshokutwa nitakuwa na gari langu. Mwanaume pesa anazo lakini ni mgumu sana. Hataki hata nijue katika akaunti yake ya benki ana shilingi ngapi”
 
“Tena nakwambia ukimuweka sawa, hata jina la akaunti yake ya benki anaweka la kwako?”
 
“Acha shoga! Kwani wewe mume wako ameweka jina lako kwenye akaunti yake?”
 
“Mimi amenifungulia akaunti yangu kabisa, ananiwekea pesa kila mwezi”
 
“Na mimi itakuwa hivyo hivyo. Nitamwambia anifungulie akanti benki”
 
Siku ile nilirudi nyumbani kwangu nikiwa na furaha na ndoto za kupata tajiri. Kama mume wangu atanijengea nyumba, ataninunulia gari, atanifungulia akaunti benki, nitajiona  kama nimeshakuwa tajiri.
 
Mume wangu aliporudi nyumbani jioni nilimchangamkia sana kuliko kawaida yangu kwa vile nilishajua mahali ambapo nitakwenda kumnyoosha.
 
Kwa vile ingekuwa ni mara yangu ya kwanza kwenda kwa waganga, siku ile sikupata usingizi kwa mawazo.
 
Mawazo yangu yalikwenda mbali nikawa nawaza wakati mume wangu akiwa bwege langu akinitii kwa kila kitu.
 
Nilijiambia wakati huo maisha yangu yatakuwa mazuri sana. Fedha za mume wangu nitakuwa nakaa nazo mimi.
 
Asubuhi kulipokucha nilianza kufanya usafi wa nyumbani kwangu. Sikushughulika kubandika chai mapema kwa sababu mume wangu alikuwa akiondoka asubuhi bila kunywa chai. Ananywea huko huko, yeye na mdogo wake.
 
Muda wao wa kutoka ulipowadia Ibrahim alinifuata uani akaniaga.
 
“Nimekuachia pesa za sokoni kitandani” akaniambia.
 
“Hizo ni pesa au visenti. Pesa utakuja kuniachia nitakapokutengeneza” nikamjibu kimoyomoyo.
 
Alipoondoka na mdogo wake nikaenda bafuni kuoga. Nilipomaliza nilivaa. Nikaenda kuketi sebuleni kwangu kusubiri Rita anipigie simu.
 
Nilipoona kimya na muda unakwenda nikampigia mimi.
 
“Shoga habari ya asubuhi?” nikamuuliza alipokea simu.
 
“Nzuri shoga, mume wangu ndio ameondoka sasa hivi. Nilikuwa nataka kukupigia kukwambia jitayarishe”
 
“Nimeshajitayarisha shoga”
 
“Basi njoo, mimi najiandaa”
 
Nikarudi chumbani kwangu kuchukua baibui langu nikalivaa na kupachika mkoba wangu begani, nikatoka.
 
ITAENDELEA kesho usikose je, Salama afikapo kwa Mganga nini kitatokea?

No comments:

Post a Comment